Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha Hisi Yako ya Uharaka

Dumisha Hisi Yako ya Uharaka

Dumisha Hisi Yako ya Uharaka

“Lihubiri neno, fanya hivyo kwa bidii.”—2 TIM. 4:2.

JE, UNAWEZA KUELEZA?

Kwa nini Wakristo wa karne ya kwanza walihubiri wakiwa na hisi ya uharaka?

Tunawezaje kudumisha hisi yetu ya uharaka?

Kwa nini kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme ni ya haraka sasa kuliko wakati mwingine wowote ule?

1, 2. Ni maswali gani yanayotokea kuhusu ‘kufanya kazi yetu ya kuhubiri kwa bidii,’ au kwa haraka?

KWA kawaida, watu ambao kazi yao ni kuokoa uhai wanafanya kazi hiyo wakiwa na hisi ya uharaka. Kwa mfano, wazima-moto wanakimbia wanapoitwa kwa dharura; wanajua kwamba uhai wa watu uko hatarini.

2 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunajitahidi kuwasaidia watu ili waokolewe. Kwa sababu hiyo, tunachukua kwa uzito kazi yetu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Bila shaka, hatukimbii huku na huku bila kufikiri. Basi, Paulo alimaanisha nini alipotoa himizo hili: “Lihubiri neno, fanya hivyo kwa bidii,” au kwa haraka? (2 Tim. 4:2) Tunawezaje kuhubiri tukiwa na hisi ya uharaka? Na kwa nini kazi yetu ni ya haraka sana?

KWA NINI KAZI YETU YA KUHUBIRI NI YA HARAKA?

3. Matokeo yanaweza kuwa nini watu wakikubali au kukataa ujumbe wa Ufalme?

3 Unapofikiria jinsi kazi yetu ya kuhubiri inavyoweza kuokoa uhai wa watu, huenda unahisi kwamba kuna uhitaji wa haraka wa kuwahubiria wengine habari njema. (Rom. 10:13, 14) Neno la Mungu linasema hivi: “Ninapomwambia mwovu: ‘Hakika utakufa,’ naye kwa kweli ageuke na kuiacha dhambi yake na kuendelea kutenda haki na uadilifu, . . . hakika ataendelea kuishi. Yeye hatakufa. Hakuna yoyote kati ya dhambi zake alizozitenda itakayokumbukwa juu yake.” (Eze. 33:14-16) Kwa kweli, Biblia inawaambia hivi wale wanaohubiri ujumbe wa Ufalme: “Utajiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.”—1 Tim. 4:16; Eze. 3:17-21.

4. Kwa nini uasi-imani ulifanya kazi ya kuhubiri iwe ya haraka katika karne ya kwanza?

4 Ili uthamini kwa nini Paulo alimhimiza Timotheo ahubiri kwa uharaka, chunguza muktadha wa andiko letu la msingi. Tunasoma hivi: “Lihubiri neno, fanya hivyo kwa bidii katika majira yanayofaa, katika majira yenye taabu, karipia, kemea, himiza, kwa ustahimilivu wote na ufundi wa kufundisha. Kwa maana kutakuwa na kipindi cha wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe; nao watageuza masikio yao kutoka kwenye kweli.” (2 Tim. 4:2-4) Yesu alitabiri kwamba kungekuwa na uasi-imani. (Mt. 13:24, 25, 38) Kwa kuwa uasi-imani huo ulikuwa karibu kutokea, lilikuwa jambo la haraka kwa Timotheo ‘kuhubiri neno’ hata ndani ya kutaniko ili Wakristo wasidanganywe na mafundisho ya uwongo. Uhai wa watu ulikuwa hatarini. Namna gani leo?

5, 6. Ni mawazo gani yaliyoenea ambayo tunaweza kupata katika huduma yetu?

5 Uasi-imani kutoka katika ibada ya kweli umekua na kuenea sasa. (2 The. 2:3, 8) Ni mafundisho gani ya uwongo ambayo yanafurahisha masikio ya watu leo? Katika maeneo mengi, fundisho la mageuzi limeenezwa kwa bidii kama fundisho la kidini. Ingawa kwa kawaida lugha ya kisayansi inatumiwa ili kueleza fundisho la mageuzi, ni kana kwamba fundisho hilo limekuwa dini ambayo inaathiri maoni ya watu juu ya Mungu na watu wengine. Fundisho lingine ambalo limeenea ni lile la kwamba Mungu hapendezwi nasi; na hivyo, sisi pia hatuhitaji kupendezwa naye. Kwa nini mafundisho hayo yanavutia sana hivi kwamba yanawafanya mamilioni ya watu walale usingizi wa kiroho? Mafundisho yote mawili yanakufanya uamini kwamba ‘Unaweza kufanya jambo lolote unalotaka kwa sababu hutatozwa hesabu.’ Kwa kweli huo ni ujumbe ambao umefurahisha masikio ya watu wengi.—Soma Zaburi 10:4.

6 Lakini kuna njia nyingine ambazo zinatumiwa ili kufurahisha masikio ya watu. Watu fulani ambao bado wanaenda kanisani wanapenda walimu ambao wanawaambia hivi: ‘Hata utende jambo gani, Mungu anakupenda.’ Mapadri na makasisi wanafurahisha masikio ya wengine kwa kuwasadikisha kwamba sherehe, Misa, sikukuu za kidini, na sanamu zinakubaliwa na Mungu. Huenda watu hao wanaoenda kanisani wasitambue kwamba wako katika hali ya hatari. (Zab. 115:4-8) Hata hivyo, tukiwaamsha kiroho ili waelewe ujumbe wa kweli wa Biblia, wanaweza kufaidika kutokana na Ufalme wa Mungu.

KUHUBIRI TUKIWA NA HISI YA UHARAKA KUNAMAANISHA NINI?

7. Tunaweza kuonyeshaje hisi yetu ya uharaka?

7 Daktari aliye makini ni lazima akazie fikira kazi yake bila kukengeuka kwa sababu uhai uko hatarini. Katika huduma yetu ya Kikristo, tunaweza kuonyesha hisi ya uharaka kwa kukazia fikira kazi yetu, yaani, kutafakari juu ya matatizo, maswali, au habari zinazoweza kuwapendeza watu tunaokutana nao. Hisi ya uharaka inaweza pia kutuongoza kurekebisha ratiba yetu ili tuwatembelee watu wanapokuwa tayari zaidi kutusikiliza.—Rom. 1:15, 16; 1 Tim. 4:16.

8. Kwa kawaida kutenda kwa uharaka kunatia ndani nini?

8 Kuwa na hisi ya uharaka kunatia ndani pia kupanga mambo ya kutanguliza. (Soma Mwanzo 19:15.) Kwa mfano, wazia kwamba baada ya kupata matokeo ya uchunguzi wa afya yako, daktari anakuita katika ofisi yake na kukwambia kwa uzito hivi: “Unahitaji kutibiwa kwa haraka. Una mwezi mmoja tu wa kushughulikia ugonjwa wako.” Bila shaka, inaelekea hutatoka haraka katika ofisi yake kama wazima-moto ambao wameitwa kwa dharura. Lakini huenda utamwomba akupe mapendekezo yake, utarudi nyumbani, na kufikiria kwa uzito mambo unayohitaji kufanya kwanza.

9. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Paulo alihubiri kwa hisi ya uharaka alipokuwa Efeso?

9 Tunaweza kujifunza kuhusu hisi ya uharaka ya Paulo kwa kusoma yale aliyowaambia wazee wa Efeso kuhusu kazi yake ya kuhubiri habari njema katika wilaya ya Asia. (Soma Matendo 20:18-21.) Tangu siku ya kwanza alipofika, Paulo alishughulika sana kuwahubiria watu habari njema nyumba kwa nyumba. Isitoshe, kwa muda wa miaka miwili alifuata kwa ukawaida ratiba ya ‘kutoa hotuba nyingi kila siku katika jumba la shule ya Tirano.’ (Mdo. 19:1, 8-10) Kwa wazi, hisi ya uharaka ya Paulo ilikuwa na uvutano juu ya mambo aliyofanya. Kusudi la himizo la kwamba ‘tufanye huduma yetu kwa bidii’ au kwa haraka si kutufanya tuhisi tumelemewa na kazi nyingi. Hata hivyo, tunapaswa kutanguliza kazi ya kuhubiri maishani mwetu.

10. Kwa nini tunafurahi kwamba Wakristo walitenda kwa uharaka miaka 100 hivi iliyopita?

10 Mfano wa kikundi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia ambao kabla ya mwaka wa 1914 walianza kuhubiri habari njema unaonyesha maana ya kuwa na hisi ya uharaka. Ingawa walikuwa maelfu machache tu, walitambua uharaka wa nyakati na kwa shauku walianza kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Walichapisha hotuba mbalimbali katika mamia ya magazeti na kuonyesha programu iliyoitwa “Photo-Drama of Creation” iliyokuwa na picha za rangi na sinema. Kwa njia hiyo, waliwahubiria mamilioni ya watu habari njema. Ikiwa hawangekuwa na hisi ya uharaka, ni wangapi kati yetu wangesikia ujumbe wa Ufalme?—Soma Zaburi 119:60.

JIHADHARI USIPOTEZE HISI YAKO YA UHARAKA

11. Kwa nini wengine walipoteza hisi yao ya uharaka?

11 Mambo yanayokengeusha fikira yanaweza kumfanya mtu asione umuhimu wa kazi ya kuhubiri. Mfumo wa Shetani unakusudiwa kutuchochea ili tufuatie mambo ya kibinafsi na mambo yasiyo na maana. (1 Pet. 5:8; 1 Yoh. 2:15-17) Baadhi ya wale ambao wakati fulani walitanguliza utumishi wao kwa Yehova walipoteza hisi ya uharaka. Kwa mfano, Mkristo mmoja wa karne ya kwanza aliyeitwa Dema alikuwa wakati fulani ‘mfanyakazi mwenzi’ wa Paulo, lakini Dema alikengeushwa na mfumo wa mambo usiomwogopa Mungu. Badala ya kuendelea kumwimarisha kwanza ndugu yake wakati wa shida, Dema alimwacha Paulo.—Flm. 23, 24; 2 Tim. 4:10.

12. Tuna fursa gani leo, na tutakuwa na fursa gani milele?

12 Ikiwa tunataka kudumisha hisi yetu ya uharaka, tunahitaji kupambana na tamaa ya kufurahia vitu zaidi vya kimwili maishani. Tunapaswa kujitahidi ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Tim. 6:18, 19) Inaelekea huna shaka kwamba uzima wa milele duniani chini ya Ufalme wa Mungu utatupatia fursa nyingi sana za kufurahia utendaji wenye kupendeza. Lakini kwa sasa, tuna fursa ya pekee ya kuwasaidia wengine kuokoka Har–Magedoni.

13. Tukiwa Wakristo, tunawezaje kudumisha hisi yetu ya uharaka?

13 Kwa kuwa watu wengi ulimwenguni wanatenda kwa njia isiyo ya hekima kwa kulala usingizi wa kiroho, ni nini kinachoweza kutusaidia kutopoteza hisi yetu ya uharaka? Tunaweza kufikiria uhakika wa kwamba wakati mmoja tulikuwa tukilala katika giza la kiroho. Lakini tuliamshwa, na Kristo ametuangazia nuru yake, kama Paulo alivyosema. Sasa tuna pendeleo la kuwa wamulikaji wa nuru hiyo. (Soma Waefeso 5:14.) Baada ya kutaja hayo, Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa, kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.” (Efe. 5:15, 16) Katikati ya uovu huo, acheni ‘tununue wakati’ kwa ajili ya utendaji ambao unaweza kutusaidia kuendelea kubaki macho kiroho.

TUNAISHI NYAKATI MUHIMU SANA

14-16. Ni nini kinachofanya kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme iwe ya haraka zaidi sasa kuliko wakati mwingine wowote?

14 Huduma ya Kikristo imekuwa sikuzote yenye uharaka, lakini sasa ni ya haraka kuliko wakati mwingine wowote ule. Tangu mwaka wa 1914, ishara yenye matukio mbalimbali inayoelezwa katika Neno la Mungu imeonekana wazi. (Mt. 24:3-51) Wanadamu wanakabili sasa hatari ya kuangamia kuliko wakati mwingine wowote ule. Ingawa makubaliano yalifanywa hivi karibuni, bado mataifa makubwa yana makombora 2,000 hivi ya nyuklia ambayo yako tayari kurushwa. Wenye mamlaka wanaripoti mamia ya visa vya “kupotea” kwa vifaa vya nyuklia. Je, magaidi wana baadhi ya vifaa hivyo? Wachunguzi wanasema kwamba wanadamu wanaweza kuangamizwa kwa urahisi na vita vinavyoanzishwa na gaidi mmoja tu. Hata hivyo, si vita peke yake vinavyotisha kuwaangamiza wanadamu.

15 Ripoti moja ya mwaka wa 2009 ya The Lancet na University College London, inadai kwamba “mabadiliko ya hali ya hewa ndilo tishio kubwa zaidi kwa afya ulimwenguni katika karne ya 21.” Ripoti hiyo ilisema hivi: “Matokeo ya mabadiliko ya hali ya hewa juu ya afya yataathiri watu wengi zaidi kwa makumi ya miaka ijayo na kuhatarisha zaidi uhai na hali njema ya mabilioni ya watu.” Huenda maeneo mengi yakaharibiwa kwa sababu ya kuongezeka kwa kiwango cha maji ya bahari, ukame, mafuriko, magonjwa ya kuambukiza, vimbunga, na vita kwa sababu ya upungufu wa mali za asili. Naam, vita na misiba ya asili inatishia uhai wa wanadamu.

16 Huenda baadhi ya watu wakafikiri kwamba tishio la vita vya nyuklia linaweza kuongoza kwenye matukio ambayo yanatimiza ile “ishara.” Hata hivyo, wengi hawaelewi maana halisi ya ishara hiyo. Ishara hiyo imekuwa ikionekana wazi kwa makumi ya miaka sasa, jambo ambalo linaonyesha kwamba kuwapo kwa Kristo ni jambo halisi na kwamba mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo unakaribia haraka. (Mt. 24:3) Matukio mengi sana ya ile ishara yamekuwa wazi zaidi kuliko wakati mwingine wowote ule. Huu ndio wakati ambao watu wanapaswa kuamka kutoka katika usingizi wa kiroho. Huduma yetu inaweza kuwasaidia waamke.

17, 18. (a) Kuishi katika “majira” haya ya siku za mwisho kuna uvutano gani juu yetu? (b) Ni nini kinachoweza kuwachochea watu wabadili maoni yao kuhusu ujumbe wa Ufalme?

17 Ni wakati mfupi tu unaobaki wa kuthibitisha upendo wetu kwa Yehova na kumaliza kazi ya kuhubiri tuliyopewa katika siku hizi za mwisho. Mambo ambayo Paulo aliwaambia Wakristo wa karne ya kwanza huko Roma yana maana kubwa hata zaidi leo: “Mnayajua majira, kwamba tayari ni saa ya ninyi kuamka kutoka katika usingizi, kwa maana sasa wokovu wetu uko karibu zaidi kuliko wakati tulipokuwa waamini.”—Rom. 13:11.

18 Matukio ya siku za mwisho yaliyotabiriwa yanaweza kumsaidia mtu mmoja-mmoja atambue uhitaji wake wa kiroho. Wengine wanatambua kwamba mwanadamu anahitaji msaada wanapofikiria jinsi ambavyo serikali za wanadamu zimeshindwa kutatua matatizo makubwa ya kiuchumi, tishio la nyuklia, uhalifu wenye jeuri, au uharibifu wa mazingira. Hata hivyo, wengine wanatambua uhitaji wao wa kiroho wakati familia zao zinapopatwa na mambo fulani, kama vile kuzorota kwa afya, talaka, au kifo cha mpendwa. Hivyo, tunaposhiriki katika huduma, tunakuwa na fursa ya kuwasaidia watu hao.

WANACHOCHEWA NA HISI YA UHARAKA

19, 20. Hisi ya uharaka imewachochea jinsi gani Wakristo wengi kufanya mabadiliko katika maisha yao?

19 Hisi ya uharaka imewachochea Wakristo wengi waongeze utendaji wao katika huduma. Kwa mfano, wenzi wawili wa ndoa vijana huko Ekuado waliamua kurahisisha maisha yao baada ya kusikia programu ya kusanyiko la pekee la mwaka wa 2006 lenye kichwa “Uwe na Jicho Rahisi.” Waliandika orodha ya vitu ambavyo hawakuhitaji, na baada ya miezi mitatu walitoka katika nyumba yao yenye vyumba vitatu vya kulala na kuhamia nyumba yenye chumba kimoja, wakauza baadhi ya vitu vyao, na wakalipa madeni yao yote. Punde si punde, walianza utumishi wa painia msaidizi na wakakubali pendekezo la mwangalizi wa mzunguko la kutumika katika kutaniko moja ambalo lilikuwa na uhitaji mkubwa zaidi.

20 Ndugu mmoja wa Amerika ya Kaskazini anaandika hivi: “Mimi na mke wangu tulipohudhuria kusanyiko moja katika mwaka wa 2006, tulikuwa tumebatizwa miaka 30 iliyopita. Nilipokuwa nikiendesha gari kurudi nyumbani baada ya programu, tulizungumzia jinsi ambavyo tungeweza kutumia mashauri yaliyotolewa kuhusu kurahisisha maisha yetu. (Mt. 6:19-22) Tulikuwa na nyumba tatu, shamba, magari ya kifahari, mashua moja, na nyumba inayokokotwa na gari. Kwa kuwa tulihisi kwamba tulipoteza wakati na nguvu zetu kutafuta vitu vya kimwili, tuliamua kufanya huduma ya wakati wote iwe mradi wetu. Katika mwaka wa 2008 tulijiunga na binti yetu katika utumishi wa painia wa kawaida. Imekuwa shangwe kama nini kufanya kazi kwa ukaribu zaidi pamoja na akina ndugu! Tumeweza kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa. Pia, nafasi ya kutimiza mengi zaidi kwa ajili ya Yehova imetufanya tumkaribie zaidi. Pendeleo lenye kuthawabisha zaidi ni lile la kuona macho ya watu yaking’aa wanaposikia na kuelewa kweli ya Neno la Mungu.”

21. Ni ujuzi gani unaotuchochea kutenda?

21 Tunajua kile ambacho hivi karibuni kitaupata mfumo huu mwovu wa mambo, yaani, “ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Pet. 3:7) Ujuzi wetu wa Neno la Mungu unatuchochea kutangaza kwa bidii kuhusu dhiki kuu inayokuja na ulimwengu mpya utakaofuata baadaye. Tunaendelea kuwa na hisi kubwa zaidi ya uharaka katika kuwasaidia watu kuwa na tumaini la kweli. Tunaposhiriki kikamili katika kazi hii ya haraka, tunaonyesha upendo wa kweli kwa Mungu na kwa wanadamu wenzetu.

[Maswali ya Funzo]