Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tushangilie Katika Tumaini Letu

Tushangilie Katika Tumaini Letu

Tushangilie Katika Tumaini Letu

‘[Kuna] tumaini la uzima wa milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uongo, aliahidi nyakati za zamani za kale.’​—TITO 1:2.

JE, UNAKUMBUKA

Tunajua namna gani kwamba kuna furaha kubwa mbinguni wakati Mukristo mumoja mutiwa​-mafuta anapokufa mwaminifu?

Kutimizwa kwa tumaini la kondoo wengine kunahusiana namna gani na kutimizwa kwa tumaini la watiwa​-mafuta?

Ili tumaini letu litimizwe, tunapaswa kuonyesha ‘matendo gani matakatifu ya mwenendo’ na ‘vitendo gani vya ujitoaji​-kimungu’?

1. Namna gani tumaini ambalo Yehova ametutolea linaweza kutusaidia tuvumilie?

 MUTUME Paulo alisema kwamba Yehova ni “Mungu anayetoa tumaini,” na akaongeza kwamba Yehova anaweza kutujaza na ‘shangwe yote na amani kwa kuamini kwetu, ili tuzidi katika tumaini kwa nguvu za roho takatifu.’ (Rom. 15:13) Ikiwa tunajaa na tumaini, tunaweza kuvumilia hali yoyote inayoweza kutokea, na mioyo yetu itajaa shangwe na amani. Wakati wa magumu, tumaini hilo litakuwa kama “nanga ya nafsi, likiwa hakika na imara” iwe kwa Wakristo watiwa​-mafuta ao kwa Wakristo wengine. (Ebr. 6:18, 19) Tunapaswa kushikamana sana na tumaini letu tunapopambana na matatizo ya maisha, hilo litatusaidia tusiwe na mashaka ao tusipungukiwe na imani.​—Soma Waebrania 2:1; 6:11.

2. Leo, Wakristo wana matumaini gani ya namna mbili mbele yao, na kwa nini “kondoo wengine” wanapendezwa na tumaini la Wakristo watiwa​-mafuta?

2 Wakristo wanaoishi wakati huu wa mwisho wanakazia akili zao kwenye moja ya matumaini mawili. Mabaki ya ‘kundi ndogo’ ya Wakristo watiwa-mafuta wana tumaini la kupata uzima usioweza kufa huko mbinguni watakuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo katika Ufalme wake. (Luka 12:32; Ufu. 5:9, 10) Wakristo wa ‘mukutano mukubwa’ wa “kondoo wengine” wana tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani, watakuwa raia wa Ufalme wa Kimasiya. (Ufu. 7:9, 10; Yoh. 10:16) Wakristo walio katika kondoo wengine hawapaswi kusahau hata kidogo kwamba ikiwa wataokolewa ni kwa sababu wanawaunga mukono “ndugu” za Kristo ambao wangali bado duniani. (Math. 25:34-40) Wakristo watiwa​-mafuta watapata zawadi yao, na tumaini la kondoo wengine litatimizwa bila shaka. (Soma Waebrania 11:39, 40.) Acheni tuzungumuzie kwanza tumaini la Wakristo watiwa-mafuta.

TUMAINI LILILO HAI” LA WAKRISTO WATIWA-MAFUTA

3, 4. Namna gani Wakristo watiwa-mafuta ‘wanazaliwa upya ili wawe na tumaini lililo hai,’ na tumaini hilo ni gani?

3 Mutume Petro aliandika barua mbili kwa Wakristo watiwa-mafuta; aliwaita “waliochaguliwa.” (1 Pet. 1:1) Petro alitoa maelezo zaidi kuhusu tumaini nzuri ajabu la kundi ndogo. Katika barua yake ya kwanza, aliandika hivi: ‘Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa maana kulingana na rehema yake kubwa alituzaa sisi upya [ili tuwe na] tumaini lililo hai kupitia ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu, [ili tuwe na] uriti usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia. Huo umewekwa akiba mbinguni kwa ajili yenu, munaolindwa kwa nguvu za Mungu kupitia imani kwa ajili ya wokovu ulio tayari kufunuliwa katika kipindi cha mwisho cha wakati. Nanyi munashangilia sana katika jambo hilo.’​—1 Pet. 1:3-6.

4 Yehova alichagua hesabu ndogo ya Wakristo ili kutawala na Kristo katika Ufalme ao serikali ya mbinguni, wao ‘wanazaliwa upya’ na kuwa wana wa Mungu waliozaliwa kwa roho. Wanatiwa mafuta kwa roho takatifu ili kuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo. (Ufu. 20:6) Petro alisema kwamba ‘kuzaliwa upya’ huko kunawatolea “tumaini lililo hai,” ambalo anataja kuwa ‘uriti usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia’ unaolindwa kwa ajili yao “mbinguni.” Haishangazi kwamba watiwa​-mafuta ‘wanashangilia sana’ katika tumaini lao lililo hai! Lakini wataona utimizo wa tumaini hilo ikiwa wanaendelea kubaki waaminifu.

5, 6. Kwa nini Wakristo watiwa​-mafuta wanapaswa kujikaza ili kufanya mwito wao wa mbinguni uwe hakika?

5 Katika barua yake ya pili, Petro aliwahimiza Wakristo watiwa​-mafuta ‘wafanye hata zaidi yote wanayoweza ili kufanya mwito na kuchaguliwa kwao kuwe hakika.’ (2 Pet. 1:10) Wanapaswa kujikaza sana ili kuonyesha sifa za Kikristo kama vile imani, kushikamana na Mungu, upendo wa kindugu, na upendo. Petro alisema hivi: ‘Mambo hayo yakikaa ndani yenu na kufurika, yatawazuia kuwa ama wasiotenda ao wasiozaa matunda.’​—Soma 2 Petro 1:5-8.

6 Kristo aliyekuwa amekwisha kufufuliwa na kuwa mbinguni aliwatumia ujumbe wazee waliozaliwa kwa roho waliokuwa katika kutaniko la Filadelfia huko Asia Ndogo. Alisema hivi: “Kwa sababu ulilishika neno juu ya uvumilivu wangu, mimi pia nitakulinda kutokana na ile saa ya jaribu itakayokuja juu ya dunia nzima inayokaliwa, ili kuwatia katika jaribu wale wanaokaa duniani. Mimi ninakuja upesi. Endelea kushika sana kile ulicho nacho, ili yeyote asilichukue taji lako.” (Ufu. 3:10, 11) Ikiwa Mukristo mutiwa​-mafuta anakosa kuwa mwaminifu, hatapokea “taji la utukufu lisiloweza kufifia” ambalo limeahidiwa wachaguliwa watakaobaki waaminifu mupaka kifo.​—1 Pet. 5:4; Ufu. 2:10.

KUINGIA KATIKA UFALME

7. Ni tumaini gani nzuri ajabu ambalo Yuda alizungumuzia katika barua yake?

7 Mwaka wa 65 hivi, Yuda, ndugu ya Yesu aliwaandikia Wakristo-watiwa mafuta wenzake, ambao aliwataja kuwa “walioitwa.” (Yuda 1; linganisha na Waebrania 3:1.) Alikusudia kuwaandikia barua iliyokazia tumaini nzuri la wokovu ambalo Wakristo walioitwa ili kuwa katika Ufalme mbinguni ‘wanalo kwa pamoja.’ (Yuda 3) Ijapokuwa alikuwa na mambo mengine ya lazima ya kuwaandikia, kwenye maneno ya kumalizia ya barua yake fupi, alizungumuzia tumaini nzuri la Wakristo watiwa​-mafuta, aliandika hivi: ‘Sasa kwake yeye ambaye anaweza kuwalinda ninyi ili musijikwae na kuwaweka muwe bila dosari mbele ya utukufu wake kwa shangwe kuu, kwake Mungu pekee aliye Mwokozi wetu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu, na kuwe utukufu, ukuu, nguvu na mamlaka kwa umilele wote uliopita na sasa na mupaka umilele wote.’​—Yuda 24, 25.

8. Kulingana na Yuda 24, ni nini kinachoonyesha kwamba kuna shangwe mbinguni wakati Mukristo mutiwa​-mafuta anapokufa kwa uaminifu?

8 Bila shaka, Wakristo watiwa​-mafuta waaminifu wanataka Mungu awalinde ili wasijikwae kwenye kitu chochote kinachoweza kuwafanya wasiwe waaminifu na kuingia hivyo katika uharibifu. Tumaini lao linalotegemea Biblia ni kwamba Yesu Kristo atawafufua viumbe vya kiroho, na hilo linaweza kuwatolea nafasi ya kuonekana mbele ya Mungu kwa shangwe kubwa. Mukristo mutiwa​-mafuta anapokufa mwaminifu, ana tumaini hakika la ‘kufufuliwa akiwa na mwili wa roho, katika kutoweza kuharibika, katika utukufu.’ (1 Kor. 15:42-44) Ikiwa kuna ‘shangwe zaidi mbinguni juu ya mutenda-zambi mumoja anayetubu,’ wazia shangwe iliyo mbinguni mumoja wa ndugu za Kristo waliozaliwa kwa roho anapobaki mushikamanifu mupaka kufa. (Luka 15:7) Yehova na viumbe waaminifu wa kiroho watashangilia pamoja na Mukristo mutiwa-mafuta anapopokea zawadi yake “kwa shangwe kuu.”​—Soma 1 Yohana 3:2.

9. Namna gani kuingia katika Ufalme ‘kutawawezesha’ Wakristo watiwa​-mafuta wawe na utukufu mwingi, na namna gani tumaini hilo linawasaidia?

9 Petro pia aliwaandikia Wakristo watiwa-mafuta kwamba ikiwa wanafanya mwito wao kuwa hakika kwa kubaki waaminifu, ‘watawezeshwa kwa wingi kuingia katika ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.’ (2 Pet. 1:10, 11) “Watawezeshwa kwa wingi” katika maana ya kwamba wataingia mbinguni wakiwa na utukufu mwingi. Hilo linaweza kumaanisha pia baraka nyingi sana ambazo Wakristo watiwa​-mafuta watapata, Wakristo ambao wamejikaza kubaki katika mbio kwa ajili ya uzima. Watakumbuka maisha yao ya uaminifu wakiwa na moyo wenye kujaa shangwe na shukrani. Bila shaka tumaini hilo linawatia nguvu Wakristo watiwa-mafuta ambao wangali duniani ili ‘kukaza akili zao kwa ajili ya utendaji wenye kuendelea.’​—1 Pet. 1:13.

“MUSINGI WA TUMAINI” KWA AJILI YA KONDOO WENGINE

10, 11. (a) Kondoo wengine wana tumaini gani? (b) Namna gani kutimizwa kwa tumaini la kidunia kunahusiana na Kristo na kufunuliwa kwa “wana wa Mungu”?

10 Mutume Paulo aliandika kuhusu tumaini nzuri la “wana wa Mungu” waliozaliwa kwa roho ambao ni ‘wariti’ pamoja na Kristo. Kisha akazungumuzia tumaini lingine nzuri ajabu ambalo Yehova anatolea kondoo wengine: ‘Kwa maana uumbaji [wanadamu] unangojea na kutazamia kwa hamu kufunuliwa kwa wana wa Mungu [watiwa​-mafuta]. Kwa maana uumbaji ulitiishwa chini ya ubatili, si kwa mapenzi yake wenyewe bali kupitia yeye aliyeutiisha hivyo, juu ya musingi wa tumaini kwamba uumbaji wenyewe pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’​—Rom. 8:14-21.

11 Yehova alitolea wanadamu “musingi wa tumaini” alipoahidi kutokea kwa “uzao” utakaoharibu “nyoka ya zamani,” Shetani Ibilisi, na hivyo kuwakomboa wanadamu. (Ufu. 12:9; Mwa. 3:15) Yesu Kristo ndiye aliyekuwa sehemu ya kwanza ya “uzao” huo. (Gal. 3:16) Kupitia kifo na ufufuo wake, Yesu alifanya iwezekane wanadamu wawe na tumaini hakika la kuwekwa huru, na watoke katika utumwa wa zambi na kifo. Kutimizwa kwa tumaini hilo kunahusiana na “kufunuliwa kwa wana wa Mungu.” Watiwa-mafuta waliotukuzwa ni sehemu ya pili ya “uzao” huo. Wao ‘watafunuliwa’ wakati watashiriki pamoja na Kristo ili kuharibu ulimwengu muovu wa Shetani. (Ufu. 2:26, 27) Jambo hilo litaletea wokovu kondoo wengine watakaookoka ile ziki kubwa.​—Ufu. 7:9, 10, 14.

12. Kufunuliwa kwa watiwa-mafuta kutawafaidi wanadamu namna gani?

12 Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu moja utawafariji wanadamu kabisa! Wakati huo, “wana wa Mungu” waliotukuzwa ‘watafunuliwa’ katika njia nyingine. Wakiwa makuhani pamoja na Kristo, watatumika ili kusaidia wanadamu wafaidike na zabihu ya ukombozi wa Yesu. “Uumbaji,” yaani, wanadamu watakuwa raia wa Ufalme wa Mungu, wataanza kukombolewa kutoka katika matokeo ya zambi na kifo. Hatua kwa hatua wanadamu watiifu ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu.’ Ikiwa wanabaki waaminifu kwa Yehova wakati wa utawala wa Miaka Elfu moja na wakati wa jaribu la mwisho litakalotokea mwisho wa utawala huo, majina yao yatabaki yenye kuandikwa milele katika “kitabu cha uzima.” Wataingia katika “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Ufu. 20:7, 8, 11, 12) Hilo ni tumaini nzuri kabisa!

TUENDELEE KULINDA TUMAINI LETU HAI

13. Tumaini letu linategemea nini, na Kristo atafunuliwa wakati gani?

13 Petro aliandika barua mbili zilizoongozwa na roho takatifu ambazo zina mashauri mengi ili kuwasaidia Wakristo watiwa-mafuta na kondoo wengine waendelee kulinda tumaini lao hai. Alionyesha kwamba tumaini lao halitegemei matendo yao, lakini linategemea fazili zisizostahiliwa za Yehova. Aliandika hivi: ‘Tunzeni akili zenu kwa ukamili; kazeni tumaini lenu juu ya fazili zisizostahiliwa zitakazoletwa kwenu wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo.’ (1 Pet. 1:13) Kristo atafunuliwa wakati atakuja ili kuwakomboa wafuasi wake waaminifu na kutimiza hukumu ya Yehova juu ya wale wasiomuogopa Mungu.​—Soma 2 Wathesalonike 1:6-10.

14, 15. (a) Ili kuendelea kulinda tumaini letu hai, tunapaswa kukazia akili yetu juu ya nini? (b) Petro alitutolea shauri gani?

14 Ili kulinda tumaini letu hai, tunapaswa kukaza akili yetu juu ya “siku ya Yehova.” Siku hiyo italeta uharibifu wa “mbingu” za sasa, yaani, utawala wa wanadamu, na “dunia,” yaani, watu waovu na ‘vitu vyake vya musingi.’ Petro aliandika: ‘Ninyi munapaswa kuwa watu wa namna gani, mukingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova, ambayo kupitia hiyo mbingu zikiwa zimewaka moto zitayeyushwa na vitu vya musingi vikiwa moto sana vitayeyuka!’​—2 Pet. 3:10-12.

15 ‘Mbingu mupya [Serikali ya mbinguni] na dunia mupya [jamii mupya ya watu duniani]’ zitachukua nafasi ya “mbingu” na “dunia” za sasa. (2 Pet. 3:13) Kisha Petro alitoa shauri lililo wazi ili Wakristo wajue kile wanachopaswa kufanya ili ‘kungojea,’ ao kuendelea kulinda tumaini lao hai kwa ajili ya ulimwengu mupya huo ulioahidiwa. Alisema hivi: ‘Kwa hiyo, wapendwa, kwa kuwa munangojea mambo hayo, fanyeni yote munayoweza ili mwishowe yeye awapate ninyi mukiwa bila doa na bila dosari na mukiwa katika amani.’​—2 Pet. 3:14.

KUISHI KULINGANA NA TUMAINI LETU

16, 17. (a) Tunapaswa kuonyesha ‘matendo gani matakatifu ya mwenendo’ na ‘vitendo gani vya ujitoaji​-kimungu’? (b) Tumaini letu litatimizwa jinsi gani?

16 Zaidi ya kuendelea kulinda tumaini letu hai, tunapaswa pia kuishi kulingana na tumaini hilo. Tunapaswa kuwa waangalifu sana ili kuendelea kuwa watu wa kiroho wenye “matendo matakatifu ya mwenendo,” yaani, watu wenye ‘kudumisha mwenendo muzuri katikati ya mataifa,’ kwa kufanya mambo yaliyo sawa. (2 Pet. 3:11; 1 Pet. 2:12) Tunapaswa kuwa na ‘upendo kati yetu.’ Hilo linamaanisha kufanya yote tuwezayo ili kulinda umoja wetu na ndugu zetu ulimwenguni, tukianzia katika kutaniko letu. (Yoh. 13:35) “Vitendo vya ujitoaji​-kimungu” ni matendo yanayoonyesha kwamba tuna uhusiano muzuri kabisa pamoja na Yehova. Hayo ni matendo kama vile sala zetu, kusoma Biblia kila siku, funzo la pekee la Biblia, ibada ya familia, na kuhubiri kwa bidii “habari njema ya ufalme.”​—Math. 24:14.

17 Kila mumoja wetu anataka kuwa mutu ambaye Yehova anakubali na ambaye ataokoa wakati ulimwengu huu muovu ‘utakapoyeyushwa.’ Wakati huo tutaona utimizo wa tumaini letu, ‘tumaini la uzima wa milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uongo, aliahidi nyakati za zamani za kale.’​—Tito 1:2.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 22]

Wakristo watiwa​-mafuta ‘wanazaliwa upya [ili wawe na] tumaini lililo hai’

[Picha katika ukurasa wa 24]

Endelea kulinda tumaini hai katika familia yako