Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Ni Muhimu Kupata Majibu?

Je, Ni Muhimu Kupata Majibu?

Je, Ni Muhimu Kupata Majibu?

“Mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.”—YOHANA 8:32.

BIBLIA ina ukweli unaoweza kutuweka huru na mafundisho yanayotatanisha au ya uwongo kumhusu Yesu. Lakini, je, mafundisho tunayoamini ni muhimu? Ndiyo. Ni muhimu kwa Yehova na kwa Yesu. Na yanapaswa kuwa muhimu kwetu.

Kwa nini ni muhimu kwa Yehova? Ni kwa sababu “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Yehova anataka tuwe na maisha yenye furaha milele. Yesu alisema: “Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu] sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini . . . awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Mungu alimtuma Mwana wake ili atukomboe na kutufungulia njia ya kuishi milele katika Paradiso duniani, kama alivyokusudia mwanzoni. (Mwanzo 1:28) Mungu anatamani kuwapa uzima wa milele watu wanaojifunza ukweli kumhusu Yesu na kutenda kupatana na ukweli huo.—Waroma 6:23.

Kwa nini ni muhimu kwa Yesu? Yesu pia anawapenda wanadamu. Alionyesha upendo wake kwa kuwa tayari kufa kwa ajili yetu. (Yohana 15:13) Alijua kwamba hiyo ndiyo njia pekee ya kuwakomboa wanadamu. (Yohana 14:6) Yesu anataka watu wengi wafaidike na dhabihu yake ya fidia. Hivyo, Yesu aliwaagiza wafuasi wake wa kweli wawafundishe watu duniani kote kuhusu mapenzi ya Mungu na kusudi lake.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

Kwa nini inapaswa kuwa muhimu kwetu? Fikiria kidogo juu ya mambo ambayo bila shaka ni muhimu kwako, kama vile afya yako na familia yako. Je, ungependa wewe na wapendwa wako mwe na afya na maisha bora? Yehova kupitia Yesu anakupa wewe na wapendwa wako tumaini la kuwa na afya kamilifu na uzima wa milele katika ulimwengu mpya ambako watu hawatateseka. (Zaburi 37:11, 29; Ufunuo 21:3, 4) Je, mambo hayo yanakuvutia? Ikiwa ndivyo, kuna jambo unalopaswa kufanya.

Soma tena andiko lililonukuliwa mwanzoni mwa makala hii: “Mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” Ukweli kumhusu Yesu na majukumu yake katika kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu utatuweka huru kutoka katika utumwa mbaya zaidi wa dhambi na kifo. Hata hivyo, ili upate uhuru huo unahitaji ‘kujua ukweli.’ Tunakutia moyo ujifunze mengi zaidi kuhusu ukweli huo na jinsi wewe na wapendwa wako mnavyoweza kufaidika na ukweli huo. Mashahidi wa Yehova wangependa kukusaidia ujifunze ukweli huo.