Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Yesu alimaanisha nini aliposema twende kilomita mbili?

Katika Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu alipendekeza hivi: “Mtu fulani aliye na mamlaka akikulazimisha uingie katika utumishi wa kilometa moja, nenda pamoja naye kilometa mbili.” (Mathayo 5:41) Inaelekea wasikilizaji wa Yesu walitambua kwamba alikuwa akirejelea kazi ya kulazimishwa ambayo wenye mamlaka waliwaamuru wananchi wafanye.

Katika karne ya kwanza W.K., nchi ya Israeli ilitawaliwa na Waroma. Hawakusita kuwalazimisha wanadamu na wanyama wafanye kazi au kuchukua hatua yoyote ambayo ingewasaidia kufanya kazi yao haraka. Kwa mfano, askari-jeshi Waroma walimlazimisha Simoni wa Kirene aubebe mti wa mateso wa Yesu hadi mahali ambapo angetundikwa. (Mathayo 27:32) Kazi kama hiyo ya kulazimishwa ilikuwa yenye kuumiza, haikupendwa na watu, na ilipingwa vikali na Wayahudi.

Hatujui wananchi walilazimishwa wabebe mzigo umbali gani. Hata hivyo, inawezekana kwamba walikubali kubeba mpaka tu mahali walipoamriwa. Kwa hiyo, Yesu alipowahimiza wasikilizaji wake kitamathali waende kilomita mbili alikuwa akiwaambia wafanye, bila kuhisi uchungu moyoni, kazi hizo ambazo wenye mamlaka walidai kisheria.—Marko 12:17.

Anasi anayetajwa katika masimulizi ya Injili alikuwa nani?

Wakati wa kushtakiwa kwa Yesu, Anasi (Ananu) anatajwa kuwa “mkuu wa makuhani.” (Luka 3:2; Yohana 18:13; Matendo 4:6) Alikuwa baba-mkwe wa kuhani mkuu wa Israeli, Kayafa, na yeye mwenyewe alikuwa ametumikia akiwa kuhani mkuu kuanzia mwaka wa 6 au wa 7 W.K. hivi hadi karibu mwaka wa 15 W.K., alipoondolewa katika cheo hicho na gavana Mroma, Valerio Grato. Lakini, hata baada ya Anasi kuondolewa katika cheo cha kuhani mkuu, bado aliendelea kutenda kwa mamlaka kubwa katika Israeli. Baadaye, watano kati ya wanawe na mwana-mkwe wake walitumika katika cheo cha kuhani mkuu.

Kwa muda ambao taifa la Israeli lilikuwa huru, kuhani mkuu aliendelea kutumika katika cheo hicho hadi alipokufa. (Hesabu 35:25) Hata hivyo, chini ya utawala wa Waroma, kuhani mkuu alichaguliwa na magavana Waroma na wafalme waliochaguliwa na serikali ya Roma, na wangemwondoa walipotaka. Mwanahistoria Flavio Yosefo anasema kwamba Kirenio, gavana Mroma aliyekuwa akisimamia Siria, alimwondoa mtu fulani aliyeitwa Joazar kutoka katika cheo cha kuhani mkuu yapata mwaka wa 6 au wa 7 W.K. na akamchagua Anasi kwenye cheo hicho. Hata hivyo, inaonekana kwamba watawala hao wapagani walihakikisha walimchagua kuhani mkuu kutoka kati ya makuhani.

Familia ya Anasi ilikuwa na pupa sana na walikuwa matajiri kwelikweli. Inaonekana walikuwa matajiri kwa sababu walisimamia uuzaji wa bidhaa zilizohitajiwa ili kutoa dhabihu hekaluni, kama vile njiwa, kondoo, mafuta, na divai. Yosefo anasema kwamba Ananu (Anania), mwana wa Anasi, alikuwa na “watumishi wasio wanyoofu hata kidogo ambao walichukua kwa nguvu sehemu ya kumi ya makuhani; na kumpiga yeyote aliyekataa kutoa.”