Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mkaribie Mungu

“Tafadhali Turuhusu Turudi Nyumbani”

“Tafadhali Turuhusu Turudi Nyumbani”

Je, kuna wakati ambao ulikuwa ukimtumikia Yehova? Je, umewahi kufikiria kuanza kumtumikia tena lakini ukajiuliza ikiwa atakukaribisha? Tafadhali soma makala hii na ile inayofuata kwa makini. Makala hizi zimetayarishwa kwa ajili yako.

“NILISALI kwa Yehova nikimwomba aniruhusu nirudi nyumbani na anisamehe kwa kumhuzunisha.” Ndivyo alivyosema mwanamke fulani aliyekuwa ameacha kufuata viwango vya Kikristo alivyofundishwa tangu utotoni. Je, unamhurumia? Huenda unajiuliza, ‘Mungu anahisije kuhusu watu ambao wakati fulani walikuwa wakimtumikia? Je, anawakumbuka? Je, anataka warudi “nyumbani”?’ Ili kupata majibu ya maswali hayo acheni tuchunguze maneno yaliyoandikwa na Yeremia. Bila shaka, majibu ya maswali hayo yatakuchangamsha moyo.—Soma Yeremia 31:18-20.

Fikiria hali zilizokuwapo Yeremia alipoandika maneno hayo. Katika mwaka wa 740 K.W.K., miaka mingi kabla ya siku za Yeremia, Yehova aliruhusu ufalme wa makabila kumi wa Israeli upelekwe utekwani huko Ashuru. * Mungu aliruhusu msiba huo ili kuwatia nidhamu watu wake kwa sababu walikuwa wamejiingiza katika dhambi nzito, wakipuuza maonyo yaliyotolewa tena na tena na manabii wake. (2 Wafalme 17:5-18) Je, watu hao walibadili mtazamo wao kwa sababu ya hali ngumu walizokabili utekwani, walipokuwa wametengwa kutoka kwa Mungu wao na wakiwa mbali na nchi yao? Je, Yehova alikuwa amewasahau kabisa? Je, angewakaribisha tena nyumbani?

“Nilihisi Kujuta”

Watu hao walirudiwa na fahamu wakiwa utekwani na wakachochewa kutubu. Yehova alitambua toba yao ya kweli. Sikiliza jinsi Yehova anavyoeleza mtazamo na hisia za Waisraeli hao waliokuwa utekwani, akiwarejelea wote kuwa Efraimu.

“Hakika nimemsikia Efraimu akijiombolezea,” asema Yehova. (Mstari wa 18) Yehova aliwasikia Waisraeli wakiomboleza kwa sababu ya matokeo ya dhambi zao. Msomi mmoja anasema kwamba neno lililotafsiriwa “akijiombolezea” linaweza kumaanisha “kutikisa.” Walikuwa kama mwana ambaye anatikisa kichwa chake akifikiria hali ngumu anazokabili kwa sababu ya dhambi aliyotenda huku akitamani maisha aliyokuwa akiishi nyumbani. (Luka 15:11-17) Watu hao walikuwa wakisema nini?

“Umenirekebisha . . . kama ndama ambaye hajazoezwa.” (Mstari wa 18) Watu hao walitambua kwamba walistahili nidhamu hiyo. Walikuwa kama ndama ambaye hajazoezwa. Mfano huu unaweza kumaanisha kwamba walikuwa kama ndama ambaye “alidungwa kwa michokoo kwa sababu ya kukataa kufungwa nira,” kinasema kitabu kimoja cha marejeo.

“Unigeuze mimi, nami nitageuka bila kusita, kwa maana wewe ni Yehova Mungu wangu.” (Mstari wa 18) Watu hao walinyenyekea, nao wakaanza kumlilia Mungu. Walikuwa na zoea la kutenda dhambi, lakini sasa walikuwa wakiomba msaada ili wapate kibali cha Yehova. Tafsiri moja ya Biblia inasema hivi: “Wewe ni Mungu wetu—tafadhali turuhusu turudi nyumbani.”—Contemporary English Version.

“Nilihisi kujuta. . . . Niliona aibu, na pia nikafedheheka.” (Mstari wa 19) Watu hao walijuta kwa sababu walikuwa wamefanya dhambi. Walikubali makosa yao na wakajihisi wakiwa na hatia. Ni kana kwamba walikuwa wakijipiga-piga kifua na kuhisi wameaibika na kuvunjika moyo.—Luka 15:18, 19, 21.

Waisraeli walitubu. Walijawa na huzuni, wakakiri dhambi zao kwa Mungu, na wakaacha njia zao mbaya. Je, Yehova angekubali toba yao? Je, angewaruhusu warudi nyumbani?

“Kwa Kuwa Nitamhurumia Kabisa”

Yehova alikuwa na uhusiano wa pekee na Waisraeli. Alisema hivi: “Mimi nimekuwa Baba kwa Israeli; naye Efraimu, yeye ni mzaliwa wangu wa kwanza.” (Yeremia 31:9) Bila shaka, baba mwenye upendo hawezi kukataa kumkaribisha mwana aliyetubu kikweli. Ona jinsi Yehova anavyowaonyesha watu wake hisia kama za Baba.

“Je, Efraimu ni mwana mwenye thamani kwangu, au mtoto anayetendewa kwa upendo? Kwa maana kwa kiasi ninachosema vibaya juu yake bila shaka nitamkumbuka zaidi.” (Mstari wa 20) Maneno hayo ni yenye huruma kama nini! Kama mzazi mwenye upendo lakini mwenye msimamo thabiti, Mungu alilazimika kusema “vibaya” kuwahusu watoto wake tena na tena akiwaonya kuhusu njia zao mbaya. Walipokataa kumsikiliza kwa kiburi, aliruhusu wapelekwe utekwani—ni kana kwamba alifanya waondoke nyumbani. Hata ingawa alilazimika kuwaadhibu, hakuwasahau kamwe. Baba mwenye upendo hawasahau watoto wake. Hata hivyo, Yehova alihisije alipoona watoto wake wametubu kikweli?

“Matumbo yangu yamekuwa na msukosuko kwa ajili yake. * Kwa kuwa nitamhurumia kabisa.” (Mstari wa 20) Yehova alitamani sana watoto wake wamrudie. Toba yao ya kweli iligusa moyo wake, na akatamani sana wamrudie. Kama baba anayetajwa katika mfano wa Yesu wa mwana mpotevu, Yehova ‘aliwasikitikia,’ na akatamani kuwakaribisha watoto wake warudi nyumbani.—Luka 15:20.

“Yehova Aliniruhusu Nirudi Nyumbani!”

Maneno yaliyo katika andiko la Yeremia 31:18-20 yanatusaidia kufahamu huruma nyororo na rehema za Yehova. Mungu hawasahau watu ambao wakati fulani walikuwa wakimtumikia. Vipi ikiwa watu hao wanataka kumrudia? Mungu yuko ‘tayari kuwasamehe.’ (Zaburi 86:5) Siku zote, anawakubali wote ambao wanakuja kwake wakiwa wametubu kikweli. (Zaburi 51:17) Pia, anafurahia kuwakaribisha nyumbani.—Luka 15:22-24.

Mwanamke aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii alichukua hatua ya kumrudia Yehova na akaanza kushirikiana tena na Mashahidi wa Yehova katika eneo la kwao. Mwanzoni, alihitaji kushinda hisia zake zisizofaa. Anasema: “Nilihisi sifai kabisa.” Lakini wazee wa kutaniko walimtia moyo na kumsaidia kurudia hali yake nzuri ya kiroho. Akiwa mwenye shukrani sana, anasema hivi: “Ni jambo lenye kupendeza kama nini kwamba Yehova aliniruhusu nirudi nyumbani!”

Ikiwa umewahi kumtumikia Yehova wakati fulani na unafikiria kumtumikia tena, tunakutia moyo uwatembelee Mashahidi wa Yehova walio katika eneo lenu. Kumbuka kwamba Yehova anawapokea kwa huruma na rehema watu wote ambao wanatubu na kumlilia wakisema: “Tafadhali turuhusu turudi nyumbani.”

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Aprili:

Yeremia 17-31

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Karne kadhaa mapema, katika mwaka wa 997 K.W.K., Waisraeli waligawanyika na kuwa falme mbili. Kulikuwa na ufalme wa kusini, yaani, ufalme wa Yuda uliokuwa na makabila mawili. Na ufalme wa kaskazini wa Israeli wenye makabila kumi, ambao pia uliitwa Efraimu, kwa sababu ndilo lililokuwa kabila kubwa zaidi.

^ fu. 16 Kitabu fulani cha mwongozo wa watafsiri wa Biblia kinaeleza hivi kuhusu hali hiyo ya mfano ya msukosuko wa matumbo: “Wayahudi waliona kwamba sehemu za ndani za mwili zilikuwa kiini cha hisia.”