Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

NI NINI kilichomchochea mwanamume fulani aanze tena kufuata kanuni za Biblia alizokuwa amefunzwa tangu utotoni? Kijana fulani alipataje kuwa na baba, jambo ambalo alitamani sana katika maisha yake yote? Soma yale wanayosema.

“Nilihitaji Kumrudia Yehova.”​—ELIE KHALIL

MWAKA WA KUZALIWA: 1976

NCHI: SAIPRASI

HISTORIA: MWANA MPOTEVU

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa nchini Saiprasi lakini nikalelewa Australia. Wazazi wangu ni Mashahidi wa Yehova, na walijitahidi sana kunisaidia nimpende Yehova na Neno lake, Biblia. Hata hivyo, nilipokuwa tineja, nilianza kuasi. Ningetoroka nyumbani usiku na kujiunga na vijana wengine. Tuliiba magari na kujiingiza katika matatizo mengine mengi.

Mwanzoni nilifanya mambo hayo kwa siri nikiogopa kuwakasirisha wazazi wangu. Lakini polepole woga huo ulikwisha. Nilianzisha urafiki na watu wenye umri mkubwa kuliko wangu ambao hawakumpenda Yehova, na walinifanya nianze kuwaiga. Mwishowe, niliwaambia wazazi wangu kwamba sikutaka tena kushirikiana na dini yao. Kwa subira walijaribu kunisaidia, lakini nilipinga jitihada zao zote. Wazazi wangu walivunjika moyo.

Nilipohama kutoka nyumbani, nilianza kutumia dawa za kulevya, nilikuza na hata kuuza bangi kwa wingi. Niliishi maisha mapotovu kiadili na nilitumia wakati wangu mwingi katika vilabu vya usiku. Pia, nilianza kukasirika upesi. Ikiwa mtu angesema au kufanya jambo ambalo halikunipendeza, ningekasirika kwelikweli, na mara nyingi ningemkemea kwa sauti au hata kumpiga. Kwa ujumla, nilifanya kila kitu ambacho nilifundishwa nisifanye nilipokuwa Mkristo.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilianzisha urafiki wa karibu pamoja na mwanamume fulani ambaye pia alikuwa akitumia dawa za kulevya na ambaye baba yake alikufa akiwa angali mvulana mdogo. Mara nyingi tulizungumza kwa muda mrefu usiku. Pindi fulani usiku, alianza kunieleza kuhusu hisia zake na akanieleza jinsi alivyomkosa sana baba yake. Kwa kuwa nililelewa nikijua kuhusu tumaini la ufufuo, nilianza kumweleza kumhusu Yesu—kwamba aliwafufua wafu na ameahidi kufanya hivyo tena wakati ujao. (Yohana 5:28, 29) “Hebu wazia ukimwona baba yako tena,” nikamwambia. “Sisi sote tunaweza kuishi milele katika paradiso duniani.” Mambo hayo yalimgusa moyo sana rafiki yangu.

Pindi nyingine, tulizungumzia mambo mbalimbali kama vile siku za mwisho na fundisho la Utatu. Nilitumia Biblia yake kumwonyesha maandiko tofauti-tofauti ambayo yalifunua ukweli kuhusu Yehova Mungu, Yesu, na siku za mwisho. (Yohana 14:28; 2 Timotheo 3:1-5) Kadiri nilivyoendelea kumweleza rafiki yangu kumhusu Yehova, ndivyo nilivyozidi kumfikiria Yehova hata zaidi.

Polepole, mbegu za kweli ya Biblia ambazo zilikuwa zimelala moyoni mwangu, yaani, kweli za Biblia ambazo wazazi wangu walinifundisha, zilianza kumea tena. Kwa mfano, nyakati fulani nilipokuwa katika karamu na rafiki zangu tukitumia dawa za kulevya, kwa ghafla nilianza kumfikiria Yehova. Rafiki zangu wengi walidai kuwa wanampenda Mungu, lakini matendo yao yalionyesha kwamba hawakumpenda kamwe. Kwa sababu sikutaka kuwa kama wao, nilitambua jambo nililopaswa kufanya. Nilihitaji kumrudia Yehova.

Bila shaka, ni rahisi kujua jambo la kufanya, lakini huenda ikawa vigumu kulifanya. Ilikuwa rahisi kufanya mabadiliko fulani; niliacha kutumia dawa za kulevya kwa urahisi. Pia, nilikatiza urafiki na watu nilioshirikiana nao zamani, na nikaanza kujifunza Biblia na mzee Mkristo.

Hata hivyo, haikuwa rahisi kufanya mabadiliko fulani. Ilikuwa vigumu sana kudhibiti hasira yangu. Wakati fulani ningejidhibiti kwa muda kisha ningerudia hali yangu ya kawaida. Baadaye nilihisi vibaya, na kufikiri kwamba singefaulu. Nikiwa nimevunjika moyo, nilizungumza na yule mzee aliyekuwa akinifundisha Biblia. Wakati wote mzee huyo alikuwa mwenye subira, mwenye fadhili, na alinitia moyo sana. Siku moja, aliniomba nisome makala fulani katika gazeti la Mnara wa Mlinzi iliyoelezea umuhimu wa kutokata tamaa. * Tulizungumzia hatua ambazo ningechukua nilipokasirika. Pole kwa pole, nikikumbuka makala hiyo na kusali kwa Yehova, nilifaulu kudhibiti hasira yangu. Mwishowe, mnamo Aprili 2000, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Wazazi wangu walifurahi kwelikweli.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Sasa nina amani ya akili na dhamiri safi, nikijua kwamba sichafui tena mwili wangu na dawa za kulevya au ukosefu wa maadili. Kila kitu ninachofanya, iwe ni kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kazi, au kufurahia aina fulani ya vitumbuizo, ninapata shangwe zaidi. Nina mtazamo unaofaa maishani.

Ninamshukuru Yehova kwa kunipa wazazi ambao hawakuacha kunisaidia. Pia, ninafikiria maneno ya Yesu yaliyo katika andiko la Yohana 6:44: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.” Ninaguswa moyo sana kujua kwamba nimefaulu kumrudia Yehova kwa sababu alinivuta kwake.

“Nilitamani Sana Kuwa na Baba.”​—MARCO ANTONIO ALVAREZ SOTO

MWAKA WA KUZALIWA: 1977

NCHI: CHILE

HISTORIA: MSHIRIKI WA BENDI YA MUZIKI WENYE MDUNDO MZITO

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa na mama yangu katika jiji lenye kupendeza la Punta Arenas lililo katika Mkondo wa Magellan karibu na pembe ya kusini ya bara la Amerika Kusini. Wazazi wangu walitengana nilipokuwa na umri wa miaka mitano, na jambo hilo lilifanya nihisi kana kwamba nimeachwa. Nilitamani sana kuwa na baba.

Mama yangu alijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, na nilihudhuria mikutano ya Kikristo pamoja naye katika Jumba la Ufalme. Hata hivyo, sikufurahia kuhudhuria mikutano na mara kwa mara ningelalamika kwa hasira tukiwa njiani. Nilipokuwa na umri wa miaka 13, niliacha kuhudhuria mikutano.

Kufikia wakati huo, nilikuwa nimeanza kupenda muziki sana, na nikagundua kwamba nilikuwa na kipawa cha muziki. Nilipokuwa na umri wa miaka 15, tayari nilikuwa nikicheza muziki wenye mdundo mzito katika karamu mbalimbali, kwenye mabaa, hata katika tafrija za faragha. Nilishirikiana na wanamuziki stadi na jambo hilo lilinichochea nipende muziki wa kale. Nilijiunga na shule moja ya kujifunza muziki iliyokuwa katika eneo letu. Nilipokuwa na umri wa miaka 20, nilihamia kwenye mji mkuu, Santiago, kwa ajili ya masomo zaidi. Pia, niliendelea kucheza muziki na bendi ya muziki wenye mdundo mzito.

Wakati huo wote nilikuwa nikijihisi sifai kitu. Ili kupunguza hisia hizo, nilikunywa pombe kupita kiasi na kutumia dawa za kulevya pamoja na wanamuziki wenzangu, ambao niliwaona kuwa familia yangu. Nilikuwa na mtazamo wa kuasi, ulioonekana wazi kupitia sura na mavazi yangu. Nilivalia mavazi meusi, sikunyoa ndevu, na nywele zangu zilikuwa ndefu karibu kufika kiunoni.

Mara kwa mara, mtazamo wangu ulifanya nipigane na watu na hata nilikamatwa na polisi. Siku moja, baada ya kunywa pombe kupita kiasi, nilivamia kikundi fulani cha wauzaji wa dawa za kulevya kwa sababu walikuwa wakitusumbua mimi na rafiki zangu. Watu hao walinipiga vibaya hivi kwamba wakanivunja utaya wa meno.

Hata hivyo, watu walioniumiza hisia zaidi ni rafiki zangu wa karibu sana. Siku moja, niligundua kwamba rafiki yangu wa kike, alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na rafiki yangu wa karibu, na rafiki zangu wote walijua jambo hilo lakini walinificha. Nilivunjika moyo sana.

Nilirudi Punta Arenas, na nikaanza kufundisha muziki na pia nilifanya kazi ya kucheza ala ya muziki inayoitwa fidla. Pia, niliendelea kucheza na kurekodi muziki pamoja na bendi za muziki wenye mdundo mzito. Nilikutana na msichana mrembo anayeitwa Sussan, na tukaanza kuishi pamoja. Baada ya muda, Sussan aligundua kwamba mama yake aliamini fundisho la Utatu na mimi sikuliamini. Basi aliniuliza, “Ukweli ni upi?” Nilimwambia nilijua kwamba fundisho la Utatu ni la uwongo lakini singeweza kumthibitishia nikitumia Biblia. Hata hivyo, nilijua mtu ambaye angemjibu. Nilimwambia kwamba Mashahidi wa Yehova wanaweza kumwonyesha ukweli kupitia Biblia. Kisha, nikafanya jambo ambalo sikuwa nimefanya kwa miaka mingi—nilisali kwa Mungu na kumwomba msaada.

Siku chache baadaye, nilikutana na mwanamume fulani niliyeona ni kana kwamba namjua, na nikamuuliza ikiwa yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ingawa alionekana kushtushwa na jinsi nilivyoonekana, kwa fadhili alijibu maswali yangu kuhusu mikutano katika Jumba la Ufalme. Nilikuwa na hakika kwamba hilo lilikuwa jibu la sala yangu. Nilienda katika Jumba la Ufalme na kukaa nyuma kabisa, mahali ambapo watu hawangeniona. Hata hivyo, watu wengi walinitambua kwa sababu walikuwa wameniona nilipohudhuria mikutano nikiwa mtoto. Walinikaribisha na kunikumbatia kwa uchangamfu hivi kwamba nikahisi amani kwelikweli. Nilihisi ni kana kwamba nimerudi nyumbani. Nilipomwona mwanamume aliyenifundisha Biblia nikiwa mtoto, nilimwomba anifundishe tena.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Siku moja, nilisoma andiko la Methali 27:11, ambalo linasema: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie.” Nilifurahi kujua kwamba mtu wa hali ya chini anaweza kumfanya Muumba wa ulimwengu ashangilie. Nilitambua kwamba Yehova ndiye Baba niliyekuwa nikimtafuta katika maisha yangu yote!

Nilitaka kumpendeza Baba yangu wa mbinguni na kufanya mapenzi yake, lakini nilikuwa mtumwa wa dawa za kulevya na pombe kwa miaka mingi. Nilikuja kuelewa fundisho la Yesu lililo katika andiko la Mathayo 6:24, linalosema kwamba “hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili.” Kadiri nilivyojitahidi kufanya mabadiliko, ndivyo andiko la 1 Wakorintho 15:33 lilivyokuwa na maana kwangu: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” Nilitambua kwamba singeacha tabia zangu mbaya ikiwa ningeendelea kwenda kwenye maeneo yasiyofaa na kushirikiana na watu walewale. Shauri la Biblia lilikuwa wazi: Nilihitaji kuchukua hatua haraka ili kuacha mambo yaliyonizuia kufanya mabadiliko.—Mathayo 5:30.

Kwa sababu nilipenda muziki, ilikuwa vigumu sana kuacha muziki wenye mdundo mzito. Lakini kupitia msaada wa rafiki zangu kutanikoni, mwishowe nilifaulu kuacha muziki huo. Niliacha kunywa pombe kupita kiasi na kutumia dawa za kulevya. Pia, nilinyoa ndevu na nywele zangu, na nikaacha kuvalia mavazi meusi tu. Nilipomweleza Sussan kwamba nilitaka kunyoa nywele zangu, alitaka sana kujua nilichokuwa nikifanya katika Jumba la Ufalme. Alisema, “Nitaenda pamoja nawe hadi katika Jumba la ufalme ili nijionee kinachoendelea huko!” Alipendezwa sana na mambo aliyojionea huko, na muda mfupi baadaye akaanza kujifunza Biblia. Mwishowe, mimi na Sussan tulifunga ndoa kisheria. Kisha, tukabatizwa mwaka wa 2008, na kuwa Mashahidi wa Yehova. Ninafurahia kwamba ninamtumikia Yehova pamoja na mama yangu.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nimeepuka ulimwengu wenye shangwe bandia na marafiki wasio waaminifu. Bado ninapenda muziki, lakini sasa ninachagua muziki ninaosikiliza. Ninatumia mambo niliyojionea ili kusaidia familia yangu na watu wengine, hasa vijana. Ninataka kuwasaidia waone kwamba mambo mengi yaliyo katika ulimwengu yanavutia, lakini mwishowe ni “takataka nyingi.”—Wafilipi 3:8.

Nimepata marafiki washikamanifu katika kutaniko la Kikristo, ambapo kuna upendo na amani ya kweli. Zaidi ya yote, kwa kumkaribia Yehova, nimefaulu kumpata Baba yangu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Makala yenye kichwa “Kufanikiwa Kupitia Udumifu,” ilichapishwa katika gazeti la Februari 1, 2000, kwenye ukurasa wa 4-6.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

“Nimefaulu kumrudia Yehova kwa sababu alinivuta kwake”