Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Igeni Imani Yao

Aliilinda Familia Yake, Akawaandalia, na Akavumilia

Aliilinda Familia Yake, Akawaandalia, na Akavumilia

YOSEFU aliweka mzigo mwingine kwenye mgongo wa punda. Wazia akitazama huku na huku kwenye kijiji cha Bethlehemu wakati wa usiku na kumpigapiga ubavuni mwana-punda huyo mwenye nguvu. Bila shaka, alikuwa akifikiria safari ndefu iliyokuwa mbele yao. Misri! Watu wa nchi nyingine, lugha tofauti, tamaduni za kigeni—familia yake ndogo ingekabilianaje na mabadiliko hayo yote?

Haikuwa rahisi kwa Yosefu kumwambia Maria, mke wake mpendwa, habari hizo mbaya. Hata hivyo, alijikaza na kumwambia. Alimwambia kuhusu ndoto aliyoota ambapo malaika alimpa ujumbe huu kutoka kwa Mungu: Mfalme, Herode, alitaka kumuua mwana wao mchanga! Walipaswa kuondoka mara moja. (Mathayo 2:13, 14) Jambo hilo lilimhangaisha sana Maria. Kwa nini mtu fulani alitaka kumuua mtoto wake asiye na hatia? Maria na Yosefu hawakuelewa jambo hilo. Lakini waliamini jambo ambalo Yehova alisema, hivyo wakajitayarisha.

Huku watu katika kijiji cha Bethlehemu wakiwa wamelala, bila kujua kilichokuwa kikiendelea, Yosefu, Maria, na Yesu wakaondoka kimyakimya usiku. Yosefu alipoiongoza familia yake upande wa kusini huku mwangaza ukianza kuonekana upande wa mashariki, inaelekea alijiuliza jinsi ambavyo hali ingekuwa baadaye. Seremala wa hali ya chini angewezaje kuilinda familia yake kutokana na watu wenye nguvu nyingi? Je, angefaulu kuiandalia familia yake sikuzote? Je, angefanikiwa kutimiza kwa uvumilivu mgawo mzito ambao Yehova Mungu alikuwa amempa, mgawo wa kumlinda na kumlea mtoto huyo wa pekee? Yosefu alikabili hali nyingi ngumu. Tunapochunguza jinsi alivyokabiliana na kila hali, tutaona ni kwa nini akina baba leo, na sisi sote, tunahitaji kuiga imani ya Yosefu.

Yosefu Aliilinda Familia Yake

Miezi kadhaa mapema, akiwa katika mji wa kwao nyumbani, huko Nazareti, maisha ya Yosefu yalibadilika kabisa baada ya kumchumbia binti ya Heli. Yosefu alijua kwamba Maria alikuwa mwanamke mchanga, mwaminifu, na asiye na hatia. Lakini, akatambua kwamba Maria alikuwa mjamzito! Alikusudia kumtaliki kisiri ili amlinde asipatwe na aibu. * Hata hivyo, malaika alizungumza naye kupitia ndoto, na kumweleza kwamba Maria alikuwa amepata mimba kupitia kwa roho takatifu ya Yehova. Malaika aliongezea kwamba mwana ambaye angezaliwa angewaokoa “watu wake kutoka katika dhambi zao.” Pia, alimhakikishia Yosefu hivi: “Usiogope kumchukua Maria mke wako na kwenda naye nyumbani.”—Mathayo 1:18-21.

Yosefu, mwanamume aliyekuwa mwadilifu, alitii na kufanya vivyo hivyo. Alikubali mgawo mgumu zaidi: kumlea na kumtunza mwana ambaye hakuwa wake lakini aliyekuwa na thamani sana kwa Mungu. Baadaye, kwa kutii agizo la serikali, Yosefu alimchukua mke wake aliyekuwa mjamzito na kwenda Bethlehemu ili kujiandikisha. Yule mtoto akazaliwa huko. *

Yosefu hakurudisha familia yake Nazareti. Badala yake, waliishi Bethlehemu, mji uliokuwa kilomita chache kutoka Yerusalemu. Walikuwa maskini, lakini Yosefu alifanya yote aliyoweza ili kumlinda Maria na Yesu wasikose mahitaji yao au kuteseka. Baada ya muda mfupi, walianza kuishi katika nyumba ndogo. Baada ya muda kupita, Yesu hakuwa mtoto mchanga bali alikuwa anaendelea kukua, labda alikuwa na umri uliozidi mwaka mmoja, wakati maisha yao yalipobadilika tena kwa ghafula.

Kikundi fulani cha wanajimu wa Mashariki kiliwasili. Huenda wanaume hao walitoka mbali, huko Babiloni. Walikuwa wamefuata nyota iliyowaelekeza nyumbani kwa Yosefu na Maria na walikuwa wakimtafuta mtoto ambaye angekuja kuwa mfalme wa Wayahudi. Wanaume hao walikuwa na heshima sana.

Iwe walijua au la, wanajimu hao walikuwa wamehatarisha uhai wa mtoto Yesu. Nyota waliyoona iliwaelekeza kwanza Yerusalemu, bali si Bethlehemu. Wakiwa huko walimwambia Mfalme Herode aliyekuwa mwovu kwamba walikuwa wakimtafuta mtoto ambaye angekuwa mfalme wa Wayahudi. Jambo hilo lilimfanya mfalme huyo awake hasira.—Ona makala “Wasomaji Wetu Wanauliza . . . Ni Nani Aliyeituma Ile ‘Nyota’?” kwenye ukurasa wa 29.

Hata hivyo, inapendeza kujua kwamba kuna nguvu zilizopita za Herode ambazo zilikuwa zinaongoza mambo. Jinsi gani? Wageni hao walitoa zawadi, na hawakuomba chochote. Yosefu na Maria walishangaa kama nini kupata kwa ghafula “dhahabu na ubani na manemane”—vitu vyenye thamani! Wanajimu hao walikusudia kumwambia Mfalme Herode mahali walipompata mtoto waliyekuwa wakimtafuta. Hata hivyo, Yehova aliingilia kati. Kupitia ndoto, aliwaagiza wanajimu hao warudi nyumbani wakitumia njia tofauti.—Mathayo 2:1-12.

Muda mfupi baada ya wanajimu hao kuondoka, Yosefu alipewa onyo hili na malaika wa Yehova: “Simama, mchukue huyo mtoto mchanga na mama yake mkimbie kuingia Misri, mkae huko mpaka nikupe agizo; kwa maana Herode yuko karibu kumtafuta huyo mtoto amwangamize.” (Mathayo 2:13) Kwa hiyo, kama tulivyoona mwanzoni, Yosefu alitii bila kusita. Alitanguliza kabisa usalama wa mtoto wake na akaondoka na familia yake kwenda Misri. Kwa kuwa wale wanajimu wapagani waliipa familia hiyo vitu vyenye thamani, sasa walikuwa na vitu ambavyo vingewasaidia katika safari iliyokuwa mbele yao.

Baadaye, mafumbo ya apokrifa na hekaya nyingine zilitia chumvi safari hiyo ya kwenda Misri, na kudai kwamba mtoto Yesu alifupisha safari hiyo kimuujiza, akawashinda nguvu majambazi, na hata akafanya mitende iiname ili mama yake achume matunda yake. * Ukweli ni kwamba walitembea mwendo mrefu wenye kuchosha bila kujua waendako.

Wazazi wanaweza kujifunza mengi kutoka kwa Yosefu. Alikuwa tayari kukatiza kazi yake na akajinyima starehe ili kuilinda familia yake kutokana na hatari. Ni wazi kwamba aliona familia yake kuwa kitu kitakatifu chenye thamani kutoka kwa Yehova. Leo, wazazi wanalea watoto wao katika ulimwengu wenye misukosuko, uliojaa uvutano unaohatarisha, kupotosha, au hata kuangamiza vijana. Inapendeza kama nini kuona akina mama na baba ambao wanachukua hatua mara moja kama Yosefu alivyofanya, na kujitahidi kuwalinda watoto wao kutokana na uvutano kama huo!

Yosefu Aliandalia Familia Yake

Inaonekana familia hiyo haikuishi sana huko Misri, kwa kuwa baada ya muda mfupi malaika alimwambia Yosefu kwamba Herode alikuwa amekufa. Yosefu aliirudisha familia yake katika nchi ya kwao. Unabii uliokuwa umetolewa zamani ulitabiri kwamba Yehova angemwita mwana wake “kutoka Misri.” (Mathayo 2:15) Yosefu alishiriki katika kutimiza unabii huo, lakini sasa angepeleka familia yake wapi?

Yosefu alikuwa mwenye tahadhari. Alitenda kwa hekima kwa kumwogopa mfalme aliyetawala baada ya Herode, Arkelao, ambaye pia alikuwa mkatili na muuaji. Mungu alimwongoza Yosefu kuipeleka familia yake upande wa kaskazini, katika eneo la nyumbani kwao huko Nazareti ya Galilaya, mbali na Yerusalemu na hila zake. Akiwa huko yeye na Maria waliitunza familia yao.—Mathayo 2:19-23.

Waliishi maisha rahisi, lakini bado walikabili hali ngumu. Biblia inasema kwamba Yosefu alikuwa seremala, na inatumia neno ambalo linahusisha kazi mbalimbali za mbao, kama vile kupasua mbao, kuzikokota, na kuzikausha ili zitumiwe kujenga nyumba, kutengeneza mashua, madaraja madogo, mikokoteni, magurudumu, nira, na aina mbalimbali ya vifaa vya shambani. (Mathayo 13:55) Ilikuwa kazi ngumu iliyohitaji nguvu nyingi. Mara nyingi seremala katika nyakati za Biblia alifanya kazi karibu na mlango wa nyumba yake ndogo au katika kibanda kilichokuwa kando ya nyumba yake.

Yosefu alitumia vifaa mbalimbali na huenda alirithi vingine kutoka kwa baba yake. Huenda alitumia filifili, timazi, uzi wenye chokaa, shoka, nyundo ya chuma, nyundo ya mbao, patasi, kekee ambayo aliitumia kutoboa mashimo, gundi za aina mbalimbali, na labda misumari fulani, ingawa ilikuwa ya bei ghali.

Wazia Yesu akiwa mvulana mdogo akimtazama baba yake mlezi akifanya kazi. Akiwa amemkodolea macho Yosefu akitazama kila jambo alilokuwa akifanya, bila shaka alifurahia kuona mabega na mikono yenye nguvu iliyofanya kazi kwa ustadi, na jinsi alivyotumia macho yake kwa busara. Inawezekana Yosefu alianza kumzoeza mwanawe mchanga jinsi ya kufanya kazi rahisi kama vile kusugua sehemu zenye mikwaruzo kwenye mbao akitumia ngozi ya samaki iliyokaushwa. Inaelekea alimfundisha Yesu tofauti kati ya aina mbalimbali za miti aliyotumia kama vile, mkuyu, mtini, mwaloni, au mzeituni.

Yesu alijua pia kwamba mikono hiyo yenye nguvu ambayo ilikata miti, kutengeneza maboriti, na kuunganisha mbao ndiyo mikono iliyomgusa kwa wororo na kumfariji yeye, mama yake, na ndugu na dada zake wadogo. Ndiyo, Yosefu na Maria walikuwa na familia iliyoendelea kuongezeka ambayo mwishowe ilikuwa na angalau watoto saba kutia ndani Yesu. (Mathayo 13:55, 56) Yosefu alilazimika kufanya kazi kwa bidii hata zaidi ili kuwatunza na kuwalisha wote.

Hata hivyo, Yosefu alijua kwamba jambo muhimu zaidi lilikuwa kuitunza familia yake kiroho. Hivyo alitumia muda fulani kuwafundisha watoto wake kumhusu Yehova Mungu na sheria Zake. Yeye na Maria walienda kwa ukawaida pamoja na watoto wao kwenye sinagogi, ambako Sheria ilisomwa kwa sauti na kufafanuliwa. Labda Yesu aliuliza maswali mengi baadaye na Yosefu alijitahidi kumsaidia mvulana huyo atosheleze uhitaji wake wa kiroho. Pia, Yosefu aliipeleka familia yake kwenye sherehe za kidini huko Yerusalemu. Ili kuhudhuria sherehe ya Pasaka iliyofanywa kila mwaka, huenda Yosefu alihitaji kusafiri kwa majuma mawili mwendo wa kilomita 113, ili kusherehekea pindi hiyo kisha wangerudi nyumbani.

Leo, vichwa vya familia wanaiga mfano kama huo. Wanajitolea kuwasaidia watoto wao, na kutanguliza mazoezi ya kiroho badala ya kuhangaikia mambo mengine, kutia ndani starehe za kimwili. Wanafanya yote wanayoweza ili kwenda pamoja na watoto wao kwenye mikutano na makusanyiko ya Kikristo. Kama Yosefu, wanajua kwamba hilo ndilo jambo lenye thamani zaidi wanaloweza kuwafanyia watoto wao.

Walikuwa na “Hangaiko la Akilini”

Yesu alipokuwa na umri wa miaka12, kama kawaida Yosefu aliipeleka familia yake huko Yerusalemu. Ulikuwa wakati wa sherehe ya Pasaka, na familia kubwa zilisafiri pamoja katika msafara mrefu wakipita kwenye maeneo ya mashambani yenye mimea na nyasi ndefu. Walipokaribia eneo lisilo na mimea karibu na jiji kuu la Yerusalemu, wengi walianza kuimba zaburi za sifa zilizojulikana sana. (Zaburi 120-134) Huenda jiji hilo lilikuwa limejaa mamia ya maelfu ya watu. Baadaye, familia na misafara yao walianza kurudi nyumbani. Wakiwa na mengi ya kufanya, huenda Yosefu na Maria walidhani kwamba Yesu alikuwa akisafiri pamoja na washiriki wengine wa familia yao. Baada tu ya kusafiri kwa mwendo wa siku moja kutoka Yerusalemu ndipo walipotambua jambo lenye kushtua—Yesu hakuwa pamoja nao!—Luka 2:41-44.

Walirudi kwa haraka mpaka Yerusalemu. Wazia jinsi walivyochanganyikiwa walipopita katika barabara za jiji hilo, huku wakiita jina la mwana wao. Mvulana huyo alikuwa wapi? Baada ya kutafuta kwa siku tatu, Yosefu alianza kujiuliza ikiwa alikuwa ameshindwa kabisa kutimiza mgawo mtakatifu aliopewa na Yehova? Mwishowe wakaenda hekaluni. Walipofika huko, waliingia katika chumba fulani ambamo wanaume wengi wenye elimu, waliojua Sheria walikuwa wamekusanyika huku kijana Yesu akiwa ameketi katikati yao! Wazia kitulizo ambacho Yosefu na Maria walipata!—Luka 2:45, 46.

Yesu alikuwa akiwasikiliza wanaume hao wenye elimu na kuuliza maswali mengi. Wanaume hao walishangazwa na ufahamu wa mtoto huyo na majibu yake. Hata hivyo, Maria na Yosefu waliduwaa. Kulingana na simulizi hilo, Yosefu hasemi chochote. Lakini maneno ya Maria yanaonyesha jinsi wote wawili walivyohisi: “Mtoto, kwa nini umetutendea hivi? Tazama, baba yako nami tumekuwa tukikutafuta tukiwa na hangaiko la akilini.”—Luka 2:47, 48.

Hivyo, kwa ufupi, Neno la Mungu linatuonyesha kihalisi hali ambazo wazazi hupitia. Wazazi wanaweza kupatwa na mkazo hata kama mtoto ni mkamilifu! Wazazi katika ulimwengu huu ulio hatari wanaweza kupatwa na “hangaiko la akilini” kwa kiwango kikubwa, lakini akina baba na mama wanaweza kufarijiwa kujua kwamba Biblia inaonyesha kuwa wazazi wanakabili hali ngumu.

Jambo la kupendeza ni kwamba Yesu alikuwa amebaki mahali pekee ambapo angejihisi akiwa karibu zaidi na Baba yake wa mbinguni, Yehova, huku akijitahidi kujifunza mambo mengi iwezekanavyo. Hivyo, aliwajibu wazazi wake kwa njia rahisi na kwa unyoofu: “Kwa nini mlilazimika kunitafuta? Je, hamkujua kwamba ni lazima niwe katika nyumba ya Baba yangu?”—Luka 2:49.

Bila shaka, Yosefu alifikiria maneno hayo tena na tena. Labda maneno hayo yalimfurahisha. Kwa kweli, alikuwa amejitahidi kumfundisha mwana wake mlezi ahisi hivyo kumwelekea Yehova Mungu. Akiwa bado mvulana, tayari Yesu alitambua maana ya neno “baba”—huenda alijua maana ya neno hilo hasa kwa kushirikiana na Yosefu.

Ikiwa wewe ni baba, je, unatambua jinsi ulivyo na pendeleo kubwa la kuwasaidia watoto wako wajue maana ya kuwa baba mwenye upendo na mwenye kulinda? Vilevile, ikiwa unawalea watoto ambao si wako, kumbuka mfano wa Yosefu na umtendee kila mmoja wao kwa njia ya pekee na kumthamini. Wasaidie wamkaribie zaidi Baba yao wa mbinguni, Yehova Mungu.

Yosefu Alivumilia Hali Ngumu kwa Uaminifu

Biblia inafunua habari nyingine chache kuhusu maisha ya Yosefu, lakini ni vizuri tuzichunguze pia. Tunasoma kwamba Yesu ‘aliendelea kujitiisha kwa’ wazazi wake. Pia, tunasoma kwamba “Yesu a[li]zidi kufanya maendeleo katika hekima na ukuzi wa kimwili, akipata kibali kwa Mungu na wanadamu.” (Luka 2: 51, 52) Maneno hayo yanafunua nini kumhusu Yosefu? Mambo kadhaa. Tunajifunza kwamba Yosefu aliendelea kuiongoza familia yake, kwa kuwa mwanawe mkamilifu aliheshimu mamlaka ya baba yake na akaendelea kujitiisha kwake.

Pia, tunajifunza kwamba Yesu aliendelea kuongeza hekima yake. Bila shaka, Yosefu alifanya mengi ili kumsaidia mwanawe apate hekima hiyo. Siku hizo, Wayahudi walikuwa na methali waliyoipenda sana. Ilisema kwamba wanaume walioishi maisha ya starehe ndio tu waliokuwa wenye hekima kwelikweli, na watu wenye ujuzi mbalimbali kama vile maseremala, wakulima, na wahunzi “hawakujua sheria na hukumu; na hawangepatikana mahali ambapo mafumbo yalitolewa.” Baadaye, Yesu alithibitisha kwamba methali hiyo ilikuwa ya uwongo. Akiwa mvulana, Yesu alimsikia mara ngapi baba yake mlezi akifundisha kwa njia inayofaa kuhusu “sheria na hukumu” za Yehova, hata ingawa alikuwa seremala maskini? Bila shaka, alimsikia mara nyingi sana.

Vilevile, tunaweza kuona uthibitisho wa kwamba Yosefu alishiriki kumsaidia Yesu akomae kimwili. Kwa sababu alitunzwa vizuri alipokuwa mvulana, Yesu alikomaa na kuwa mwanamume, mwenye afya na nguvu. Zaidi ya hayo, Yosefu alimzoeza mwanawe kuwa seremala stadi. Yesu hakujulikana tu kama mwana wa seremala, bali pia kama “yule seremala.” (Marko 6:3) Hivyo, mazoezi ya Yosefu yalikuwa na matokeo mazuri. Kwa hekima, vichwa vya familia wanamwiga Yosefu, kwa kutunza hali nzuri ya watoto wao na kuhakikisha kwamba wanaweza kujitegemea.

Baada ya Biblia kutaja kuhusu kubatizwa kwa Yesu alipokuwa na umri wa miaka 30, Yosefu hatajwi tena katika hadithi hiyo. Uthibitisho unaonyesha kwamba Maria alikuwa mjane Yesu alipoanza huduma yake. (Ona sanduku “Yosefu Alikufa Wakati Gani?” kwenye ukurasa wa 27.) Hata hivyo, Yosefu aliweka mfano mzuri wa baba ambaye aliilinda familia yake, akawaandalia, na kuvumilia kwa uaminifu mpaka mwisho. Kila baba, kila kichwa cha familia, au Mkristo yeyote, anapaswa kuiga mfano wa Yosefu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Siku hizo, watu waliochumbiana walionwa ni kana kwamba walikuwa wameoana.

^ fu. 8 Ona makala “Igeni Imani Yao—Alikata ‘Kauli Moyoni Mwake’” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 2008.

^ fu. 14 Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Yesu alifanya muujiza wake wa kwanza baada ya kubatizwa. (Yohana 2:1-11) Kwa habari zaidi kuhusu masimulizi ya injili za apokrifa, ona makala “Injili za Apokrifa—Je, Zina Ukweli Uliofichwa Kumhusu Yesu?” kwenye ukurasa wa 18.

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

Yosefu Alikufa Wakati Gani?

Tunajua kwamba Yosefu alikuwa hai Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12. Wakiwa na umri huo, vijana wengi Wayahudi walianza kujifunza kazi ya baba yao na kuwa stadi wakiwa na umri wa miaka 15. Inaelekea Yosefu aliishi muda mrefu vya kutosha kumfundisha Yesu kuwa seremala. Je, Yosefu alikuwa hai Yesu alipoanza huduma yake akiwa na umri wa miaka 30? Inaonekana hakuwa hai. Mama ya Yesu, ndugu zake, na dada zake wote wanatajwa kwamba walikuwa hai wakati huo lakini Yosefu hatajwi. Hata pindi moja Yesu aliitwa “mwana wa Maria,” bali si mwana wa Yosefu. (Marko 6:3) Biblia inamtaja Maria akijifanyia maamuzi fulani, bila kushauriana na mumewe. (Yohana 2:1-5) Hilo halingekuwa jambo la kawaida katika nyakati za Biblia isipokuwa kama angekuwa mjane. Mwishowe, Yesu alipokaribia kufa, alimpa mtume Yohana daraka la kumtunza mama yake. (Yohana 19:26, 27) Yesu hangehitajika kufanya hivyo ikiwa Yosefu bado alikuwa hai. Hivyo basi, inawezekana kwamba Yosefu alikufa Yesu alipokuwa bado kijana mdogo. Akiwa mwana wa kwanza katika familia yao, bila shaka Yesu aliendeleza kazi ya useremala na akaitunza familia mpaka alipobatizwa.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Yosefu alichukua hatua mara moja na akatenda bila ubinafsi ili kumlinda mtoto wake

[Picha katika ukurasa wa 25]

Yosefu alifanya kazi kwa bidii ili kuiandalia familia yake

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yosefu aliipeleka familia yake kwa ukawaida kuabudu katika hekalu huko Yerusalemu

[Picha katika ukurasa wa 28]

Yosefu alimzoeza mwanawe kuwa seremala