Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Mwana Anapenda Kumfunua Baba’

‘Mwana Anapenda Kumfunua Baba’

‘Mwana Anapenda Kumfunua Baba’

“Hakuna anayemjua Baba ni nani ila Mwana, na yule ambaye Mwana anapenda kumfunulia.”—LUKA 10:22.

UNGEJIBUJE?

Kwa nini Yesu alikuwa na nafasi ya pekee ya kumfunua Baba yake?

Yesu alimfunuaje Baba yake kwa wengine?

Ni kwa njia zipi unaweza kumwiga Yesu katika kumfunua Baba?

1, 2. Ni swali gani ambalo limewahangaisha watu wengi, na kwa nini?

‘MUNGU ni nani?’ Swali hilo linawahangaisha watu wengi. Kwa mfano, ingawa watu wengi wanaodai kuwa Wakristo wanaamini kwamba Mungu ni Utatu, wengi wanakiri kwamba fundisho hilo haliwezi kueleweka. Mwandikaji mmoja ambaye ni kasisi alikiri hivi: “Fundisho hilo linapita uwezo wa akili ya mwanadamu yenye mipaka. Linazidi uwezo wa kawaida wa kuelewa wa mwanadamu.” Kwa upande mwingine, watu wengi wanaokubali fundisho la mageuzi wanaamini kwamba hakuna Mungu. Wanadai kwamba maajabu yote ya uumbaji yalijitokeza yenyewe. Hata hivyo, badala ya kukana kwamba Mungu yupo, Charles Darwin alisema hivi: “Kwa maoni yangu mwanadamu hawezi kuelewa kwa ukamili suala la kuwapo kwa Mungu.”

2 Watu wengi, bila kujali imani zao, wametafakari maswali yanayohusiana na kuwapo kwa Mungu. Hata hivyo, wanaposhindwa kupata majibu yanayoridhisha, mwishowe wengi wao huacha kumtafuta Mungu. Kwa kweli, Shetani “amezipofusha akili za wasioamini.” (2 Kor. 4:4) Haishangazi kwamba wanadamu wengi wamechanganyikiwa na hawajui ukweli kumhusu Baba, yule Muumba wa ulimwengu mzima!—Isa. 45:18.

3. (a) Ni nani ambaye ametufunulia kumhusu Muumba? (b) Tutachunguza maswali gani?

3 Hata hivyo, ni muhimu watu wajifunze ukweli kumhusu Mungu. Kwa nini? Kwa sababu ni wale tu wanaoliitia “jina la Yehova” ndio watakaookolewa. (Rom. 10:13) Kuliitia jina la Mungu kunatia ndani kumjua vizuri Yehova na kumwona kuwa halisi. Yesu Kristo aliwafunulia wanafunzi wake ujuzi huo muhimu. Aliwafunulia kumhusu Baba. (Soma Luka 10:22.) Kwa nini Yesu aliweza kumfunua Baba kwa njia ambayo mtu mwingine yeyote hangeweza kumfunua? Yesu alifanyaje hivyo? Na tunawezaje kumwiga Yesu katika kuwafunulia wengine kumhusu Baba? Acheni tuchunguze maswali hayo.

YESU KRISTO ALISTAHILI KWA NJIA YA PEKEE

4, 5. Kwa nini Yesu alikuwa na nafasi ya pekee ya kumfunua Baba yake?

4 Yesu alistahili kwa njia ya pekee kumfunua Baba yake. Kwa nini? Kwa sababu kabla ya kuumbwa kwa kitu kingine chochote, tayari Yesu alikuwa mbinguni akiwa kiumbe wa roho, “Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu.” Baadaye, Yesu alikuja kuwa mwanadamu. (Yoh. 1:14; 3:18) Ni pendeleo la pekee kama nini! Wakati ambapo hakukuwa na kiumbe kingine chochote, Mwana huyo alikuwa pamoja na Baba yake ambaye alimkazia uangalifu kikamili na kumfundisha kuhusu utu na sifa Zake. Bila shaka, Baba na Mwana waliwasiliana sana na kusitawisha upendo wenye kina kati yao kwa maelfu ya miaka. (Yoh. 5:20; 14:31) Ni wazi kwamba Mwana huyo alipata kumjua vizuri sana Baba yake!—Soma Wakolosai 1:15-17.

5 Baba alimweka rasmi Mwana awe msemaji Wake, “Neno la Mungu.” (Ufu. 19:13) Kwa hiyo, Yesu alikuwa na nafasi ya pekee ya kuwafunulia wengine kumhusu Baba. Kwa kufaa, Yohana, mwandikaji wa Injili, anasema kwamba Yesu, yule “Neno,” alikuwa “kifuani pa Baba.” (Yoh. 1:1, 18) Yohana aliposema maneno hayo alirejelea desturi iliyofuatwa katika siku zake wakati wa chakula. Mgeni angeweza kuegemea mbele ya mwingine kwenye kiti kilekile. Hivyo, wawili hao wangeweza kuzungumza kwa urahisi. Basi, Mwana akiwa “kifuani,” alikuwa na mazungumzo ya kutoka moyoni pamoja na Baba yake.

6, 7. Uhusiano kati ya Baba na Mwana uliendelea kukua jinsi gani?

6 Uhusiano kati ya Baba na Mwana uliendelea kukua. Mwana ‘akawa yule ambaye Mungu alimpenda sana kwa njia ya pekee siku baada ya siku.’ (Soma Methali 8:22, 23, 30, 31.) Basi ni wazi kwamba uhusiano kati ya wawili hao ulizidi kuimarika walipofanya kazi pamoja na Mwana alipokuwa akijifunza kuiga sifa za Baba yake. Wakati wa kuumbwa kwa viumbe wengine wenye akili, Mwana aliona jinsi Yehova alivyoshughulika na kila mmoja wao, na bila shaka hilo lilimfanya athamini zaidi sifa za Mungu.

7 Hata Shetani alipopinga haki ya enzi kuu ya Yehova, Mwana alipata nafasi ya kujifunza jinsi ambavyo Yehova angeonyesha upendo, haki, hekima, na nguvu Alipokabili hali ngumu. Bila shaka hilo lilimtayarisha Yesu kukabiliana na hali ngumu ambazo yeye mwenyewe angepatwa nazo baadaye katika huduma yake duniani.—Yoh. 5:19.

8. Masimulizi ya Injili yanatusaidiaje kujifunza mengi kuhusu sifa za Baba?

8 Kwa sababu ya uhusiano wake wa karibu pamoja na Yehova, Mwana alieleza vizuri zaidi kumhusu Baba yake kwa njia ambayo mtu mwingine hangeweza kumfunua. Hakuna njia nyingine bora zaidi ya sisi kumjua Baba isipokuwa kuchunguza yale ambayo Mwana wake mzaliwa-pekee alifundisha na kutenda. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo ingekuwa vigumu kwetu kuelewa kikamili maana ya neno “upendo” kwa kusoma tu ufafanuzi wake katika kamusi. Hata hivyo, tukitafakari kuhusu masimulizi yaliyo wazi ya waandikaji wa Injili kuhusu huduma ya Yesu na jinsi alivyowajali wengine, tunaweza kuelewa kwa undani maana ya maneno “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8, 16) Ndivyo ilivyo kuhusu sifa nyingine za Mungu ambazo Yesu aliwafunulia wanafunzi wake alipokuwa duniani.

JINSI YESU ALIVYOMFUNUA BABA YAKE

9. (a) Yesu alimfunua Baba yake katika njia gani mbili kuu? (b) Toa mfano ambao unaonyesha jinsi Yesu alivyomfunua Baba yake kupitia mafundisho yake.

9 Ni katika njia gani Yesu alimfunua Baba yake kwa wanafunzi wake na pia wale ambao walikuja kuwa wafuasi wake baadaye? Alifanya hivyo kwa njia mbili kuu: kupitia mafundisho yake na kupitia mwenendo wake. Acheni kwanza tuchunguze mafundisho ya Yesu. Mambo ambayo Yesu aliwafundisha wafuasi wake yalionyesha kwamba alielewa kwa undani mawazo, hisia, na njia za Baba yake. Kwa mfano, Yesu alimfananisha Baba yake na mtu mwenye kondoo. Mtu huyo anayejali anaenda kumtafuta kondoo mmoja aliyepotea. Yesu alisema kwamba mtu huyo anapompata kondoo aliyepotea, “yeye humshangilia huyo zaidi kuliko wale 99 ambao hawakupotea.” Mfano huo ulimaanisha nini? Yesu alieleza hivi: “Vivyo hivyo Baba yangu aliye mbinguni hatamani kwamba mmoja wa wadogo hawa aangamie.” (Mt. 18:12-14) Unaweza kujifunza nini kumhusu Yehova kutokana na mfano huo? Hata ikiwa nyakati nyingine unahisi kwamba huna thamani na umesahauliwa, Baba yako wa mbinguni anapendezwa nawe naye anakujali. Machoni pake, wewe ni “mmoja wa wadogo hawa.”

10. Yesu alimfunuaje Baba yake kupitia mwenendo wake?

10 Njia ya pili ambayo Yesu aliwafunulia wanafunzi wake kumhusu Baba ni kupitia mwenendo wake. Kwa hiyo, mtume Filipo alipomwambia Yesu hivi: “Tuonyeshe Baba,” Yesu alisema hivi kwa kufaa: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yoh. 14:8, 9) Fikiria mifano kadhaa inayoonyesha jinsi Yesu alivyodhihirisha sifa za Baba yake. Mwanamume fulani mwenye ukoma alipomsihi Yesu amponye, Yesu alimgusa mwanamume huyo “mwenye kujaa ukoma” na kumwambia hivi: “Ninataka. Takasika.” Baada ya kuponywa, bila shaka mtu huyo aliyekuwa na ukoma alijua kwamba Yehova ndiye aliyempa Yesu nguvu za kumponya. (Luka 5:12, 13) Pia, Lazaro alipokufa, bila shaka, wanafunzi walitambua kwamba Baba ni mwenye huruma walipomwona Yesu ‘akiugua rohoni na kutaabika’ na pia ‘akitokwa na machozi.’ Ingawa Yesu alijua kwamba angemfufua Lazaro, alihisi uchungu uleule ambao familia na marafiki wa Lazaro walihisi. (Yoh. 11:32-35, 40-43) Bila shaka, kuna masimulizi ya Biblia unayopenda ambayo yanakusaidia kuona jinsi Yesu alivyoonyesha rehema ya Baba yake kwa matendo.

11. (a) Yesu alipolisafisha hekalu, alifunua nini kumhusu Baba yake? (b) Kwa nini simulizi la Yesu akisafisha hekalu linatufariji?

11 Hata hivyo, unajifunza nini unaposoma simulizi la Yesu akisafisha hekalu? Hebu wazia jambo lililotukia: Yesu alitengeneza mjeledi wa kamba, kisha akawafukuza wale waliokuwa wakiuza ng’ombe na kondoo. Alimwaga sarafu za watu waliokuwa wakibadili pesa na kupindua meza zao. (Yoh. 2:13-17) Wanafunzi walipoona Yesu akichukua hatua hiyo thabiti walikumbuka maneno ya kinabii ya Mfalme Daudi: “Bidii nyingi kwa ajili ya nyumba yako imenila.” (Zab. 69:9) Yesu alipochukua hatua thabiti, alionyesha tamaa yenye nguvu ya kuitetea ibada ya kweli. Je, unaona sifa au utu wa Baba katika simulizi hilo? Simulizi hilo linatukumbusha kwamba zaidi ya Mungu kuwa na nguvu zisizo na mipaka, yeye pia anatamani sana kuondoa kabisa uovu duniani pote. Simulizi hilo linaloonyesha Yesu akichukua hatua thabiti ya kuondoa uovu linafunua jinsi Baba anavyohisi anapoona uovu ambao umeenea duniani leo. Kujua jambo hilo kunatufariji tunapotendewa isivyo haki!

12, 13. Unaweza kujifunza nini kumhusu Yehova kutokana na jinsi Yesu alivyowatendea wanafunzi wake?

12 Acheni tuchunguze mfano mwingine kuhusu namna Yesu alivyowatendea wanafunzi wake. Mara kwa mara walibishana kuhusu ni nani aliye mkuu zaidi kati yao. (Marko 9:33-35; 10:43; Luka 9:46) Baada ya kukaa na Baba yake kwa miaka mingi, Yesu alijua jinsi Yehova anavyohisi kuhusu mwelekeo huo wa kiburi. (2 Sam. 22:28; Zab. 138:6) Isitoshe, Yesu alimwona Shetani Ibilisi akiwa na mwelekeo huo. Kiumbe huyo mwenye ubinafsi alihangaikia sana kupata umashuhuri na cheo. Hivyo, Yesu alihuzunika kama nini alipoona wanafunzi ambao alikuwa amewafundisha wakiendelea kujitafutia makuu! Hata wale ambao aliwachagua kuwa mitume walionyesha mtazamo huo! Waliendelea kujitafutia makuu hadi siku ya mwisho ya maisha ya Yesu duniani. (Luka 22:24-27) Hata hivyo, Yesu aliendelea kuwarekebisha kwa fadhili, bila kupoteza kamwe matumaini ya kwamba mwishowe wangejifunza kuiga mtazamo wake wa akili wa unyenyekevu.—Flp. 2:5-8.

13 Je, unaona sifa au utu wa Yehova unapotazama jinsi Yesu alivyorekebisha kwa subira mielekeo mibaya ya wanafunzi wake? Kupitia matendo na maneno ya Yesu, je, unamwona Baba yake, ambaye hawaachi watu wake hata ingawa wanakosea mara nyingi? Je, kujua sifa hizo za Mungu hakutuchochei kumfikia na kutubu tunapokosea?

MWANA ALIPENDA KUMFUNUA BABA YAKE

14. Yesu alionyeshaje kwamba alipenda kumfunua Baba yake?

14 Madikteta wengi wanajaribu kuwadhibiti watu kwa kutowapa habari. Kinyume chake, Yesu alipenda kuwajulisha wengine habari alizojua kumhusu Baba yake, alimfunua kikamili mbele za wengine. (Soma Mathayo 11:27.) Zaidi ya hayo, Yesu aliwapa wanafunzi wake “uwezo wa akili ili [wapate] kumjua yule wa kweli,” Yehova Mungu. (1 Yoh. 5:20) Hilo linamaanisha nini? Yesu aliwasaidia wafuasi wake kuelewa mambo aliyofundisha kumhusu Baba yake. Hakuficha habari kuhusu Baba yake kwa kufundisha kwamba Yeye ni sehemu ya fumbo la Utatu ambalo halieleweki.

15. Kwa nini Yesu hakufunua habari fulani kumhusu Baba yake?

15 Je, Yesu alifunua kila jambo ambalo alijua kumhusu Baba yake? Hapana, kwa hekima hakufunua mambo mengi aliyojua. (Soma Yohana 16:12.) Kwa nini? Kwa sababu wakati huo, wanafunzi wake ‘hawangeweza kustahimili’ ujuzi huo. Hata hivyo, Yesu alisema kwamba wangefunuliwa ujuzi mwingi zaidi wakati “msaidizi,” angefika, yaani, roho takatifu ambayo ingewaongoza “ndani ya kweli yote.” (Yoh. 16:7, 13) Kama vile wazazi wenye hekima wanavyoweza kuamua kutowaambia watoto wao mambo fulani mpaka watoto hao wanapokuwa na umri wa kutosha kuelewa, ndivyo Yesu alivyongoja mpaka wanafunzi wake walipokomaa vya kutosha kuweza kuelewa kweli fulani kumhusu Baba yake. Kwa fadhili, Yesu alitilia maanani uwezo wao wenye mipaka.

MWIGE YESU KWA KUWASAIDIA WENGINE WAMJUE YEHOVA

16, 17. Kwa nini una nafasi ya kuwafunulia wengine kumhusu Baba?

16 Unapomjua mtu fulani vizuri na kuthamini sifa au utu wake wenye kuvutia, je, huchochewi kuwaambia wengine kumhusu? Yesu alipokuwa duniani, alizungumza kumhusu Baba yake. (Yoh. 17:25, 26) Je, tunaweza kumwiga Yesu kwa kuwafunulia wengine kumhusu Yehova?

17 Kama tulivyoona, Yesu alimjua kwa undani sana Baba yake kuliko wengine walivyomjua. Hata hivyo, alikuwa tayari kuwaambia wengine mambo fulani aliyojua, hata aliwapa wafuasi wake uwezo wa akili wa kuelewa mambo ya ndani sana kuhusu utu wa Mungu. Je, si kweli kwamba Yesu ametusaidia kumjua Baba yetu kwa njia ambayo watu wengi leo hawamjui? Tunathamini kama nini kwamba Yesu alitufunulia kwa kupenda kumhusu Baba yake kupitia mafundisho na mwenendo wake! Kwa kweli, tunapaswa kujisifu ifaavyo kwa sababu tunamjua Baba. (Yer. 9:24; 1 Kor. 1:31) Kwa kuwa tumejitahidi kumkaribia Yehova, yeye pia ametukaribia sisi. (Yak. 4:8) Kwa hiyo, sasa tunaweza kuwasaidia wengine kupata ujuzi huo. Tunawezaje kufanya hivyo?

18, 19. Unaweza kuwafunulia wengine kumhusu Baba katika njia zipi? Eleza.

18 Tunahitaji kumwiga Yesu kwa kumfunua Baba kwa maneno na kwa matendo yetu. Kumbuka kwamba watu wengi tunaokutana nao katika utumishi wa shambani hawamjui Mungu. Huenda maoni yao kumhusu Mungu yamepotoshwa na mafundisho ya uwongo. Tunaweza kuwaambia watu hao mambo tunayojua kuhusu jina la Mungu, kusudi lake kwa ajili ya wanadamu, na utu wake ambao unafunuliwa katika Biblia. Zaidi ya hayo, tunaweza kuzungumza na waamini wenzetu kuhusu masimulizi ya Biblia ambayo yanafunua utu wa Mungu kwa njia ambayo hatukujua mwanzoni. Tukifanya hivyo, wao pia wanaweza kufaidika.

19 Unapaswa kujitahidi kumwiga Yesu kwa kumfunua Baba kupitia mwenendo wako. Watu wanapoona upendo wa Kristo kupitia matendo yetu, watavutiwa kumkaribia Baba na pia Yesu. (Efe. 5:1, 2) Mtume Paulo alitutia moyo ‘tuwe waigaji wake, kama vile yeye alivyokuwa mwigaji wa Kristo.’ (1 Kor. 11:1) Tuna pendeleo kubwa kama nini la kuwasaidia watu kumjua Yehova kupitia mwenendo wetu! Naam, sote na tuendelee kumwiga Yesu kwa kuwafunulia wengine kumhusu Baba.

[Maswali ya Funzo]