Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Mwana anapenda kumufunua baba’

‘Mwana anapenda kumufunua baba’

‘Mwana anapenda kumufunua baba’

‘Hakuna anayemujua Baba ni nani ila Mwana, na yule ambaye Mwana anapenda kumufunulia.’​—LUKA 10:22.

UTAJIBU NAMNA GANI?

Sababu gani ni Yesu tu ndiye anayestahili kumufunua Baba kuliko mutu mwingine yeyote?

Namna gani Yesu alimufunua Baba kwa wengine?

Ni katika njia gani unaweza kumuiga Yesu ili kumufunua Baba kwa wengine?

1, 2. Watu wengi wameshindwa kupata jibu la ulizo gani, na kwa sababu gani?

 ‘MUNGU ni nani?’ Watu wengi wameshindwa kupata jibu la ulizo hilo. Kwa mufano, watu wengi wanaojiita kuwa Wakristo wanaamini Mungu ni Utatu, lakini wengi wao wanasema hakuna mutu anayeweza kuelewa fundisho hilo. Padri mumoja aliandika hivi: “Hilo ni fundisho linalopita akili ndogo ya mwanadamu, linapita uwezo wake wa kufikiri na wa kuelewa.” Kwa upande mwingine, kuna pia wale wanaokubali fundisho la mageuzi. Wao wanasema Mungu hayuko na wanasema kama vitu vyote vya ajabu ambavyo tunaona havikuumbwa lakini vilitokea kwa bahati tu. Mwanasayansi anayeitwa Charles Darwin hakukataa kuwako kwa Mungu, lakini alisema kama mwanadamu hana uwezo wa kuelewa kabisa Mungu.

2 Watu wanaamini mambo tofauti, hata hivyo wengi wanajiuliza sana ikiwa Mungu yuko. Lakini wengine kwa kuwa wanakosa majibu yenye kuwatosheleza, wanaacha kumutafuta Mungu. Kwa kweli, Shetani “amezipofusha akili za wasioamini.” (2 Kor. 4:4) Basi si jambo la kushangaza ikiwa wanadamu wengi ni wenye kuvurugika na wanakosa kujua ukweli juu ya Mungu, ambaye ni Baba na Muumbaji wa ulimwengu wote!​—Isa. 45:18.

3. (a) Ni nani ambaye amemufunua Muumbaji kwetu? (b) Tutatafuta majibu ya maulizo gani?

3 Ni lazima watu wajifunze ukweli juu ya Mungu. Sababu gani? Kwa sababu ni wale tu ‘wanaoliitia jina la Yehova’ ndio wataookolewa. (Rom. 10:13) Kuliitia jina la Mungu kunamaanisha pia kujua yeye ni nani na ni Mutu wa namna gani. Yesu Kristo aliwafundisha wanafunzi wake ukweli huo wa maana juu ya Mungu. Aliwafunulia Baba yake. (Soma Luka 10:22.) Sababu gani hakuna mutu mwingine ambaye angeweza kumufunua Baba kuliko Yesu? Yesu alimufunua Baba namna gani? Ni katika njia gani tunaweza kumuiga Yesu ili kumufunua Baba kwa wengine? Acheni tutafute majibu ya maulizo hayo.

YESU KRISTO TU NDIYE ANAYESTAHILI KUMUFUNUA BABA

4, 5. Sababu gani cheo cha pekee cha Yesu kilimufanya awe mutu anayestahili peke yake kumufunua Baba yake?

4 Yesu tu ndiye anayestahili kumufunua Baba yake. Kwa nini? Kwa sababu mbele ya Mungu kuumba viumbe vingine vyote, Yesu alikuwa kiumbe cha kiroho aliyekuwa akiishi mbinguni. Ni yeye aliyekuwa “Mwana muzaliwa​-pekee wa Mungu.” (Yoh. 1:14; 3:18) Yesu alikuwa na cheo cha pekee kabisa! Mbele ya Mungu kuumba vitu vingine vyote, ni Yesu tu ndiye aliyekuwa akiishi pamoja na Baba yake, kwa hiyo Mwana huyo alikuwa akifurahia kuwa katika upendo wenye uchangamufu wa Baba yake. Wakati huo alijifunza Baba Yake na sifa Zake. Kwa miaka mingi sana, lazima Baba na Mwana Wake walikuwa wakizungumuza sana, na upendo wao ulikuwa ukiongezeka siku kwa siku. (Yoh. 5:20; 14:31) Kwa hiyo, Yesu alijifunza sana sifa za Baba yake!​—Soma Wakolosai 1:15-17.

5 Baba alimuchagua Mwana ili awe musemaji wake, yaani, kuwa “Neno la Mungu.” (Ufu. 19:13) Kwa hiyo, cheo hicho cha pekee kilimufanya Yesu kuwa mutu anayestahili peke yake kumufunua Yehova kwa wengine. Yohana aliandika katika injili yake kama Yesu ni Neno, na kama yuko “kifuani pa Baba.” (Yoh. 1:1, 18) Yohana alipoandika hivyo inawezekana alikuwa akifikiria desturi iliyokuwa kawaida katika siku zake wakati wa kula. Kwa mufano, mugeni angeweza kumuegemea mugeni mwingine kwenye kifua ili wapate nafasi ya kuzungumuza. Kwa hiyo, kwa kuwa, Yesu alikuwa ‘katika kifua cha Baba’ walikuwa na nafasi ya kuzungumuza mambo mengi kama watu wanaopendana sana wanapozungumuza mambo yao ya siri.

6, 7. Ni nini iliyosaidia ili uhusiano kati ya Baba na Mwana uendelee kuwa muzuri zaidi?

6 Baba na Mwana waliendelea kuwa na uhusiano muzuri sana. Mupaka Mwana ‘akawa yule ambaye [Mungu] alimupenda sana kwa njia ya pekee siku baada ya siku.’ (Soma Methali 8:22, 23, 30, 31.) Kwa sababu walikuwa wakifanya kazi pamoja na kwa sababu mwana aliendelea kujifunza na kuiga sifa za baba yake, kwa hiyo wakati Yehova alipokuwa akiumba viumbe vingine vyenye akili, Yesu aliona namna alikuwa akishugulikia kila kiumbe, na jambo hilo lilimufanya apendezwe zaidi na sifa za Mungu.

7 Tena, wakati Shetani alikuja kupinga haki ya Yehova ya kuwa Mutawala wa ulimwengu wote, jambo hilo lilimutolea Yesu nafasi ya kujifunza namna Yehova anavyoweza kuonyesha sifa zake, yaani, upendo, haki, hekima, na nguvu wakati hali ngumu zinatokea. Bila shaka, hilo lilimusaidia Yesu ajue namna angepambana na matatizo ambayo angekutana nayo duniani katika kazi yake ya kuhubiri.​—Yoh. 5:19.

8. Namna gani habari zinazopatikana katika Injili zinatusaidia kujifunza mengi juu ya sifa za Baba?

8 Kwa kuwa alikuwa na uhusiano wa kipekee sana na Yehova, Mwana alifasiria vizuri sana namna Baba yake alivyo kuliko mutu mwingine yeyote. Kwa hiyo tukitaka kumujua baba vizuri tunapaswa kujifunza yale Mwana​-muzaliwa wa pekee alifundisha na kufanya. Je, unafikiri kuna njia nyingine nzuri kuliko hiyo ambayo inaweza kutusaidia? Kwa mufano, kwa kusoma tu maelezo ya neno “upendo” katika kamusi, hatungeelewa maana ya neno hilo. Lakini tunaposoma habari ambayo Waandikaji wa Injili waliandika juu ya mahubiri ya Yesu na namna alivyohangaikia wengine, tunaweza kuelewa vizuri maana ya maneno “Mungu ni upendo.” (1 Yo. 4:8, 16) Kufanya hivyo, kunaweza kutusaidia tuelewe vizuri sifa zingine za Mungu ambazo Yesu alifunulia wanafunzi wake alipokuwa duniani.

NAMNA YESU ALIVYOMUFUNUA BABA YAKE

9. (a) Ni njia gani mbili za maana ambazo Yesu alitumia ili kumufunua Baba yake? (b) Toa mufano unaoonyesha namna Yesu alivyomufunua Baba yake kupitia mafundisho yake.

9 Namna gani Yesu alimufunua Baba yake kwa wanafunzi wake na kwa wale waliopaswa kuwa wanafunzi wake wakati ujao? Alitumia njia mbili za maana ili kumufunua Baba yake: Mafundisho yake na matendo yake. Acheni tuzungumuzie kwanza mafundisho yake. Mambo ambayo Yesu aliwafundisha wafuasi wake yalionyesha kama alijua vizuri mawazo ya Baba yake, namna anavyojisikia, na njia zake. Kwa mufano, Yesu alimulinganisha Baba yake na muchungaji anayehangaikia kondoo zake, ambaye anaacha kondoo wengine na kwenda kutafuta kondoo moja aliyepotea. Yesu alisema kama alipopata kondoo aliyepotea, ‘alimushangilia huyo zaidi kuliko wale 99 ambao hawakupotea.’ Yesu alitoa mufano huo ili kutufundisha nini? Anasema hivi: ‘Vivyo hivyo Baba yangu aliye mbinguni hatamani kama mumoja wa wadogo hawa aangamie.’ (Mt. 18:12-14) Mufano huo unatufundisha nini juu ya Yehova? Hata ikiwa wakati fulani unajisikia kama wewe si mutu wa lazima na kwamba umesahauliwa, Baba yako wa mbinguni anapendezwa nawe na anakuhangaikia. Machoni pake wewe ni mumoja wa “wadogo” hao.

10. Namna gani Yesu alimufunua Baba yake kwa matendo yake?

10 Njia ya pili ambayo Yesu alitumia ili kufunulia wanafunzi wake Baba yake ni matendo yake. Kwa hiyo, Filipo alipomuuliza Yesu: “Tuonyeshe Baba,” Yesu alisema waziwazi: ‘Yule ambaye ameniona mimi amemuona Baba pia.’ (Yoh. 14:8, 9) Acheni tujifunze mifano fulani inayotusaidia kuona namna Yesu alivyoonyesha sifa za Baba yake. Mutu mwenye ukoma alipomusihi Yesu amuponye, Yesu alimugusa mwanaume “mwenye kujaa ukoma” na akamuambia: “Ninataka. Takasika.” Kwa kweli, kisha tu kuponywa, mwanaume huyo aliyekuwa na ukoma alielewa kuwa ni kwa nguvu za Yehova ndio Yesu alitimiza muujiza huo. (Luka 5:12, 13) Tena, Lazaro alipokufa, wanafunzi wa Yesu waliona huruma aliyo nayo Baba, walipoona namna Mwana wake ‘alivyougua rohoni na kutaabika’ na ‘kutokwa na machozi.’ Hata ikiwa Yesu alijua kama atamufufua Lazaro, alipatwa na huzuni ambayo familia na marafiki wa Lazaro walikuwa nayo. (Yoh. 11:32-35, 40-43) Hakika, katika Biblia kuna habari unazofurahia zinazokusaidia kuona namna Yesu alivyoonyesha rehema ya Baba yake kwa matendo yake.

11. (a) Alipofukuza watu wabaya katika hekalu, Yesu alifunua nini juu ya Baba yake? (b) Sababu gani habari hiyo inatufariji leo?

11 Siku fulani Yesu aliwafukuza watu wabaya katika hekalu. Jambo hilo linatufundisha nini? Wazia kidogo: Yesu anatengeneza fimbo ya kamba, na anawafukuza wale waliokuwa wakiuzisha ngombe na kondoo. Anamuanga feza za wale wabadilisha-feza na kupindua meza zao. (Yoh. 2:13-17) Tendo hilo la bidii la Yesu liliwasaidia wanafunzi wake wakumbuke maneno ya kiunabii ya Mufalme Daudi: ‘Bidii nyingi kwa ajili ya nyumba yako imenikula.’ (Zab. 69:9) Kwa kutenda hivyo, Yesu alionyesha kama anataka kabisa kutetea ibada ya kweli. Je, habari hiyo inakusaidia kuelewa sifa za Mungu? Habari hiyo inatukumbusha kama Mungu ana nguvu ya kuwafagia kabisa watu wabaya duniani, lakini pia ana nia kabisa ya kufanya hivyo. Namna Yesu alivyotenda alipoona mambo mabaya inaonyesha namna Baba anavyojisikia anapoona namna mambo mabaya yanavyoenea duniani. Hilo linatufariji kujua kama Yehova na Yesu wanajisikia vibaya tunapotendewa isivyo haki!

12, 13. Unaweza kujifunza nini juu ya Yehova kupitia namna Yesu alivyowatendea wanafunzi wake?

12 Mufano mwingine ni ule unaozungumuzia namna Yesu alivyowatendea wanafunzi wake. Wanafunzi hao walikuwa wakiendelea kubishana ili kujua ni nani aliye mukubwa kati yao. (Marko 9:33-35; 10:43; Luka 9:46) Kwa kuwa aliishi kwa muda wa miaka mingi sana na Baba, Yesu alijua maoni ya Yehova juu ya mawazo kama hayo ya kiburi. (2 Sam. 22:28; Zab. 138:6) Tena, Yesu alikuwa ameona namna Shetani Ibilisi alivyojiacha kuongozwa na kiburi. Kwa sababu ya kutafuta faida yake mwenyewe, Shetani anajifikiria tu na kutafuta mambo makubwa. Kwa hiyo, Yesu alihuzunika sana alipoona mawazo hayo ya kiburi ao ya kutafuta ukubwa kati ya wanafunzi wake! Mawazo hayo ya kiburi ao ya kutafuta ukubwa yalipatikana katika mitume wake hata siku ya mwisho ya maisha ya Yesu duniani. (Luka 22:24-27) Hata hivyo, Yesu aliendelea kuwakaripia kwa upole, na alitumaini kama siku fulani wangejifunza kuiga sifa ya unyenyekevu ambayo alikuwa nayo.​—Flp. 2:5-8.

13 Je, unaona sifa ya uvumilivu ya Baba kupitia namna Yesu alivyowakaripia kwa uvumilivu wanafunzi wake? Je, kupitia matendo na maneno ya Yesu, unamuona Baba asiyewaacha watu wake ijapokuwa wanamukosea mara nyingi? Tukijua sifa hizo za Mungu, tunachochewa kumukaribia ili kutubu tunapomukosea, sivyo?

MWANA ANAPENDA KUMUFUNUA BABA YAKE

14. Namna gani Yesu alionyesha kama alipenda kumufunua Baba Yake?

14 Watawala wengi wanatawala watu kwa kuwaficha mambo fulani wanayopaswa kujua. Lakini Yesu alikuwa tayari kuwajulisha wengine mambo aliyojua juu ya Baba yake; alimufunua kabisa kwa wengine. (Soma Mathayo 11:27.) Tena, Yesu aliwapa wanafunzi wake ‘uwezo wa akili ili wapate kumujua yule wa kweli,’ yaani, Yehova Mungu. (1 Yo. 5:20) Hilo linamaanisha nini? Yesu alifungua akili ya wafuasi wake ili waelewe mafundisho yake juu ya Baba yake, alimufunua Baba yake. Katika mafundisho yake, Yesu hakusema kama Baba yake ni sehemu ya fumbo la Utatu, fundisho lisiloeleweka.

15. Sababu gani Yesu hakuwafunulia wanafunzi wake mambo fulani juu ya Baba yake?

15 Je, Yesu alifunua mambo yote aliyojua kuhusu Baba yake? Hapana, na lilikuwa jambo la hekima kutowafunulia mambo yote aliyojua juu ya Baba yake. (Soma Yohana 16:12.) Sababu gani? Kwa sababu wakati huo wanafunzi wake hawakuwa bado na uwezo wa kuchukua ujuzi wote huo. Hata hivyo, Yesu alieleza kama wangefunuliwa mambo mengi wakati wangepata “musaidizi,” roho takatifu, ambayo ingewaongoza “ndani ya kweli yote.” (Yoh. 16:7, 13) Muzazi mwenye hekima anaweza kukosa kuwafunulia watoto wake mambo fulani mupaka wakati watakapokomaa vya kutosha. Vivyo hivyo, Yesu alingojea mupaka wakati wanafunzi wake wangekomaa kiroho na kuwa na uwezo wa kuelewa mambo fulani juu ya Baba yake. Kwa sababu Yesu aliwapenda, alifikiria uwezo wao.

UMUIGE YESU KWA KUWASAIDIA WENGINE WAMUJUE YEHOVA

16, 17. Sababu gani inawezekana tuwafunulie wengine Baba?

16 Unapomujua mutu vizuri na kuelewa sifa zake nzuri, unachochewa kumujulisha kwa wengine, sivyo? Alipokuwa duniani, Yesu alielezea wengine juu ya Baba yake. (Yoh. 17:25, 26) Je, tunaweza kumuiga kwa kumufunua Yehova kwa wengine?

17 Kama tulivyojifunza hapo juu, Yesu alijua Baba yake sana kuliko mutu mwingine yeyote. Kwa hiyo, alipendezwa kuwajulisha wengine mambo fulani kati ya yale aliyojua, na hata kuwatolea wafuasi wake uwezo wa kuelewa vizuri sifa za Mungu. Kwa musaada wa Yesu, tumefikia kuelewa Baba yetu vizuri zaidi kuliko watu wengi leo, sivyo? Sisi ni wenye shukrani kabisa kwa kuwa Yesu alipenda kutufunulia Baba yake kupitia mafundisho yake na matendo yake! Kwa kweli tuna sababu ya kujisifu kwa kuwa tunamujua Baba. (Yer. 9:24; 1 Kor. 1:31) Kwa kuwa tumejikaza kumukaribia Yehova, yeye pia ametukaribia. (Yak. 4:8) Kwa hiyo, kwa kuwa tuna ujuzi unaofaa juu ya Baba tunaweza kuwafunulia wengine Baba. Namna gani tunaweza kufanya hivyo?

18, 19. Katika njia gani tunaweza kumufunua Baba kwa wengine? Eleza.

18 Ni lazima tumuige Yesu kwa kumufunua Baba kupitia maneno na matendo yetu. Kila mara, tukumbuke kwamba watu wengi tunaokutana nao katika mahubiri hawajui Mungu ni nani. Wanaweza kuwa na mawazo yasiyofaa juu ya Mungu kwa sababu ya mafundisho ya uongo waliyofundishwa. Tunaweza kuwajulisha wengine mambo tunayojua juu ya jina la Mungu, kusudi lake kwa wanadamu, na sifa zake, kama Biblia inavyofundisha. Tena, tunaweza kuzungumuza pamoja na mashahidi wenzetu habari fulani za Biblia zinazofunua sifa za Mungu katika njia ambayo hatukuelewa hapo mbele. Kwa njia hiyo wao pia wanaweza kufaidika.

19 Tuseme nini juu ya kumufunua Baba kupitia mwenendo wetu tunapojikaza kumuiga Yesu? Watu wanapoona upendo wa Kristo kupitia matendo yetu, watachochewa kumukaribia Baba na Yesu. (Efe. 5:1, 2) Mutume Paulo alitutia moyo ‘tuwe waigaji wake, kama vile alivyo muigaji wa Kristo.’ (1 Kor. 11:1) Ndiyo, tuna pendeleo kubwa la kuwasaidia wengine wamujue Yehova kupitia mwenendo wetu! Acheni basi tuendelee kumuiga Yesu kwa kumufunua Baba kwa wengine.

[Maulizo ya Funzo]