Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usaliti Ni Ishara Yenye Kuogopesha ya Siku za Mwisho!

Usaliti Ni Ishara Yenye Kuogopesha ya Siku za Mwisho!

Usaliti Ni Ishara Yenye Kuogopesha ya Siku za Mwisho!

‘Jinsi tulivyokuwa washikamanifu na waadilifu na wasiolaumika.’—1 THE. 2:10.

TAFUTA MAMBO HAYA MAKUU:

Ni mambo gani yenye kuonya tunayoweza kujifunza kutokana na usaliti wa Delila, Absalomu, na Yuda Iskariote?

Tunaweza kuiga jinsi gani ushikamanifu ulioonyeshwa na Yonathani na Petro?

Tunawezaje kuendelea kuwa washikamanifu kwa mwenzi wetu wa ndoa na kwa Yehova?

1-3. (a) Ni ishara gani yenye kuogopesha inayoonekana katika siku za mwisho, na inahusisha nini? (b) Ni maswali gani matatu tutakayojibu?

KUNA ulinganifu gani kati ya Delila, Absalomu, na Yuda Iskariote? Wote hao hawakuwa washikamanifu. Delila hakuwa mshikamanifu kwa mwanamume ambaye alimpenda, Mwamuzi Samsoni; Absalomu hakuwa mshikamanifu kwa baba yake, Mfalme Daudi; Yuda hakuwa mshikamanifu kwa Bwana wake, Kristo Yesu. Katika visa vyote hivyo, matendo yao ya kuhuzunisha yalisababisha hasara kubwa kwa wengine! Lakini mifano yao inatuhusu namna gani?

2 Mwandishi mmoja wa kisasa anasema kwamba usaliti ni miongoni mwa mambo mabaya zaidi yaliyoenea leo. Jambo hilo halishangazi. Yesu alipozungumzia ishara ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” alisema hivi: ‘Watu wengi watasalitiana.’ (Mt. 24:3, 10) “Kusaliti” kunamaanisha “kumwacha au kumweka mtu mikononi mwa adui kwa hila au kwa ukosefu wa ushikamanifu.” Ukosefu wa ushikamanifu unathibitisha kuwa tunaishi katika “siku za mwisho” na Paulo alitabiri kwamba wakati huo watu watakuwa “wasio washikamanifu, . . . wasaliti.” (2 Tim. 3:1, 2, 4) Hata ingawa mara nyingi waandishi wa vitabu na watayarishaji wa sinema wanawatukuza watu wanafanya matendo kama hayo ya hila, ukosefu wa ushikamanifu na usaliti husababisha maumivu na mateso katika maisha halisi. Bila shaka, matendo kama hayo ni ishara yenye kuogopesha ya siku za mwisho!

3 Tunajifunza nini kutoka katika Biblia kuhusu wale ambao hawakuwa washikamanifu? Tunaweza kuiga mifano gani ya watu waliokuwa washikamanifu? Ni lazima tuazimie kuwa washikamanifu kwa nani? Acheni tuchunguze mambo hayo.

MIFANO YENYE KUONYA YA WATU WA KALE

4. Delila alimsalitije Samsoni, na kwa nini jambo alilofanya lilikuwa baya sana?

4 Kwanza, chunguza mfano wa Delila mwenye hila, ambaye Mwamuzi Samsoni alimpenda. Samsoni alikusudia kuwaongoza watu wa Mungu kupigana na Wafilisti. Huenda baada ya kujua kwamba Delila hakuwa na upendo mshikamanifu kwa Samsoni, viongozi watano Wafilisti waliahidi kumhonga Delila kwa kumpa kiasi kikubwa cha pesa ili wajue siri ya nguvu nyingi za Samsoni, kusudi wamwangamize. Delila aliyekodiwa alikubali pesa hizo, lakini alishindwa mara tatu katika jaribio lake la kugundua chanzo cha nguvu za Samsoni. Aliendelea kumshawishi kwa bidii “kwa maneno yake wakati wote na kuendelea kumsihi.” Hatimaye, ‘nafsi ya Samsoni ikakosa subira kufikia hatua ya kutaka kufa.’ Kwa hiyo, akamwambia kwamba nywele zake zilikuwa hazijawahi kamwe kunyolewa na kama angenyolewa angepoteza nguvu zake. * Baada ya kujua hivyo, Delila akafanya Samsoni anyolewe nywele zake wakati alipokuwa amelala juu ya mapaja yake na baadaye akamkabidhi kwa adui zake ili wamtendee walivyopenda. (Amu. 16:4, 5, 15-21) Alitenda jambo baya sana! Kwa sababu ya pupa, Delila alimsaliti mtu aliyekuwa akimpenda.

5. (a) Absalomu alionyeshaje ukosefu wa ushikamanifu kwa Daudi, na hilo lilifunua nini kumhusu? (b) Daudi alihisije wakati Ahithofeli alipogeuka na kuwa msaliti?

5 Mfikirie pia Absalomu mwenye hila. Akichochewa na tamaa ya kupata mamlaka, aliazimia kunyakua kiti cha ufalme cha baba yake, Mfalme Daudi. Kwanza, Absalomu ‘aliiba mioyo ya watu wa Israeli’ alipojipendekeza kwao akitumia ahadi zenye hila na kuonyesha upendo usio wa kweli. Aliwakumbatia watu na kuwabusu kana kwamba aliwajali na kuhangaikia mahitaji yao. (2 Sam. 15:2-6) Absalomu hata alimshawishi Ahithofeli, mshauri mwenye kutegemeka wa Daudi, ambaye aligeuka na kuwa msaliti kwa kuunga mkono njama ya kuunyakua ufalme. (2 Sam. 15:31) Katika Zaburi ya 3 na ya 55, Daudi anaeleza namna ukosefu huo wa ushikamanifu ulivyomwathiri. (Zab. 3:1-8; soma Zaburi 55:12-14.) Absalomu alidhihirisha mtazamo wake wa kutoheshimu enzi kuu ya Mungu kwa mipango yake ya kujitafutia mamlaka na njama zake zilizokuwa wazi dhidi ya mfalme aliyewekwa rasmi na Yehova. (1 Nya. 28:5) Mwishowe, mapinduzi hayo hayakufaulu, na Daudi akaendelea kutawala akiwa mtiwa-mafuta wa Yehova.

6. Ni katika njia gani Yuda alimsaliti Yesu, na jina lake limekuwa likitumiwa kumaanisha nini?

6 Sasa fikiria jinsi Yuda Iskariote alivyomsaliti Kristo. Katika Pasaka ya mwisho ambayo Yesu aliadhimisha pamoja na mitume wake 12, aliwaambia hivi: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, Mmoja wenu atanisaliti.” (Mt. 26:21) Usiku huohuo, Yesu alimwambia Petro, Yakobo, na Yohana hivi katika bustani ya Gethsemane: “Tazama! Msaliti wangu amekaribia.” Punde si punde, Yuda akafika katika bustani hiyo akiwa na wapanga-njama wenzake, “naye akaenda moja kwa moja kwa Yesu akasema: ‘Siku njema, Rabi!’ na kumbusu kwa wororo sana.” (Mt. 26:46-50; Luka 22:47, 52) Yuda ‘alisaliti damu yenye uadilifu’ na akamkabidhi Kristo Yesu kwa adui Zake. Kwa nini Yuda aliyependa pesa alifanya hivyo? Kwa sababu tu ya vipande 30 vya fedha! (Mt. 27:3-5) Tangu wakati huo, jina Yuda limekuwa likitumiwa kumaanisha “msaliti,” hasa mtu anayemsaliti mwenzake akijifanya rafiki. *

7. Tumejifunza nini kutokana na (a) Absalomu na Yuda na (b) Delila?

7 Tumejifunza nini kutokana na mifano hiyo yenye kuonya? Absalomu na Yuda, wote wawili walikufa vifo vya aibu kwa sababu ya kuwasaliti watiwa-mafuta wa Yehova. (2 Sam. 18:9, 14-17; Mdo. 1:18-20) Jina “Delila” litaendelea kuhusianishwa sikuzote na hila pamoja na upendo wa kinafiki. (Zab. 119:158) Ni muhimu kama nini tukatae mwelekeo wowote wa kujitakia makuu au wa pupa ambao unaweza kutufanya tupoteze kibali cha Yehova! Hiyo ni mifano inayoweza kutusaidia kabisa kukataa mwelekeo wenye kuchukiza wa kukosa ushikamanifu.

IGA MIFANO YA WATU WALIOKUWA WASHIKAMANIFU

8, 9. (a) Kwa nini Yonathani aliahidi kuwa mshikamanifu kwa Daudi? (b) Tunawezaje kuiga mfano wa Yonathani?

8 Biblia pia inaeleza kuhusu watu wengi waliokuwa washikamanifu. Acheni tuchunguze mifano miwili na tuone yale tunayoweza kujifunza. Tuanze na mtu ambaye alikuwa mshikamanifu kwa Daudi. Yonathani, mwana mkubwa wa Mfalme Sauli, angekuwa mrithi wa ufalme wa Israeli isipokuwa jambo moja, Yehova alikuwa amemchagua Daudi kuwa mfalme ambaye angefuata baada ya Sauli. Yonathani aliheshimu uamuzi wa Mungu. Hakuwa na wivu na kumwona Daudi kuwa adui. Badala yake, ‘nafsi ya Yonathani ilishikamana na nafsi ya Daudi,’ naye akaahidi kubaki mshikamanifu kwake. Yonathani hata alimpa Daudi mavazi yake, upanga, upinde, na mshipi wake ili kumwonyesha Daudi heshima ya kifalme. (1 Sam. 18:1-4) Yonathani alifanya yote aliyoweza ‘ili kuutia nguvu mkono wa Daudi,’ hata alifikia hatua ya kuhatarisha uhai wake mwenyewe ili kumtetea Daudi mbele ya Sauli. Yonathani alimwambia Daudi kwa ushikamanifu hivi: “Wewe utakuwa mfalme juu ya Israeli, na mimi nitakuwa wa pili kwako.” (1 Sam. 20:30-34; 23:16, 17) Si ajabu kwamba baada ya kifo cha Yonathani, Daudi alionyesha huzuni yake na upendo wake kwa Yonathani katika wimbo wa maombolezo.—2 Sam. 1:17, 26.

9 Haikuwa vigumu kwa Yonathani kuonyesha ushikamanifu. Alijitiisha kikamili kwa Mwenye Enzi Kuu, Yehova, na alimuunga mkono kikamili Daudi, mtiwa-mafuta wa Mungu. Vivyo hivyo leo, hata kama hatujapewa mapendeleo ya pekee ya utumishi kutanikoni, tunapaswa kuwaunga mkono kwa hiari ndugu ambao wamewekwa rasmi kuongoza katikati yetu.—1 The. 5:12, 13; Ebr. 13:17, 24.

10, 11. (a) Kwa nini Petro aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Yesu? (b) Tunawezaje kumwiga Petro, na jambo hilo linapaswa kutuchochea kufanya nini?

10 Mfano mwingine mzuri tutakaochunguza ni wa mtume Petro, ambaye aliahidi kuwa mshikamanifu kwa Yesu. Wakati Kristo alipotumia mfano wenye kushtua ili kukazia umuhimu wa kudhihirisha imani katika mwili wake na damu yake ambayo alikuwa karibu kuitoa kuwa dhabihu, wanafunzi wake wengi waliona maneno yake kuwa yanashtua, wakaacha kumfuata. (Yoh. 6:53-60, 66) Yesu akawageukia mitume wake 12 na kuwauliza: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” Petro akajibu: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele; na sisi tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.” (Yoh. 6:67-69) Je, inamaanisha kwamba Petro alielewa kikamili yote ambayo Yesu alikuwa ametoka tu kusema kuhusu dhabihu Yake? Huenda sivyo. Hata hivyo, Petro aliazimia kubaki mshikamanifu kwa Mwana mtiwa-mafuta wa Mungu.

11 Petro hakufikiri kwamba huenda Yesu alikuwa na maoni yasiyofaa na kwamba baada ya muda, angebadili maoni hayo. Badala yake, Petro alitambua kwa unyenyekevu kwamba Yesu alikuwa na “maneno ya uzima wa milele.” Vivyo hivyo leo, tunatendaje tunapoona jambo katika machapisho yetu ya Kikristo kutoka kwa “msimamizi-nyumba mwaminifu” ambalo tunaona vigumu kulielewa au halipatani na maoni yetu? Tunapaswa kujitahidi kabisa kulielewa jambo hilo badala ya kutarajia kwamba mabadiliko yatafanywa ili yapatane na maoni yetu.—Soma Luka 12:42.

ENDELEA KUWA MSHIKAMANIFU KWA MWENZI WAKO WA NDOA

12, 13. Usaliti katika ndoa unaanzaje, na kwa nini umri wa mtu haupaswi kuwa kisingizio cha usaliti?

12 Usaliti wa aina yoyote ni tendo ovu ambalo halipaswi kuruhusiwa kuvuruga amani na umoja wa familia na kutaniko la Kikristo. Tukiwa na wazo hilo akilini, acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kuendelea kuwa washikamanifu kabisa kwa mwenzi wetu wa ndoa na kwa Mungu.

13 Uzinzi ni mojawapo ya usaliti mbaya sana. Mzinzi anavunja uaminifu wake kwa mwenzi wake wa ndoa na anaanza kumkazia fikira mtu mwingine. Kwa ghafula, mwenzi aliyesalitiwa anabaki peke yake na maisha yanakuwa yamegeuka juu chini. Hali kama hiyo inatokeaje kati ya watu wawili ambao awali walikuwa wanapendana? Mara nyingi, matatizo yanaanza wakati wenzi wa ndoa wanapotengana kihisia. Profesa wa Soshiolojia Gabriella Turnaturi anasema kwamba usaliti unaweza kutokea ikiwa wenzi wa ndoa wanaacha kuonyeshana upendo kikamili. Hali kama hiyo imetokea hata kwa baadhi ya watu ambao wana umri wa makamo. Kwa mfano, mwanamume mwenye umri wa miaka 50 ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 25 anamtaliki mke wake mwaminifu ili kumchukua mwanamke mwingine ambaye amevutiwa naye. Wengine wanatoa kisingizio kwa kusema kwamba ni tatizo la kawaida kwa watu wenye umri wa makamo. Badala ya kusema kwamba tatizo hilo ni la kawaida na lisiloepukika, acheni tuseme kwamba huo ni usaliti katika umri wa makamo. *

14. (a) Yehova anahisije kuhusu udanganyifu katika ndoa? (b) Yesu alisema nini kuhusu uaminifu katika ndoa?

14 Yehova anahisije kuhusu wale ambao wanawaacha wenzi wao wa ndoa bila msingi wa Kimaandiko? Mungu wetu ‘anachukia talaka,’ na amesema maneno makali kuhusu wale ambao wanawatendea vibaya na kuwaacha wenzi wao wa ndoa. (Soma Malaki 2:13-16.) Kama Baba yake, Yesu alifundisha kwamba mtu hawezi kumfukuza au kumwacha mwenzi wake wa ndoa asiye na hatia na ajifanye kwamba hakuna tatizo.—Soma Mathayo 19:3-6, 9.

15. Wale ambao wamefunga ndoa wanawezaje kuimarisha ushikamanifu kwa mmoja na mwenzake?

15 Ni kwa njia gani wale wote ambao wamefunga ndoa wanaweza kubaki wakiwa washikamanifu kwa wenzi wao? Neno la Mungu linasema hivi: “Ushangilie pamoja na mke [au mume] wa ujana wako,” na, “Furahia maisha pamoja na mke [au mume] unayempenda.” (Met. 5:18; Mhu. 9:9) Kadiri wenzi wa ndoa wanavyozidi kuzeeka, wanapaswa kuonyeshana upendo kamili kimwili na kihisia pia. Hilo linamaanisha kwamba kila mmoja amsikilize mwenzi wake, atumie muda pamoja na mwenzi wake, na aendelee kuwa karibu na mwenzi wake. Wanapaswa kuwa na lengo la kudumisha ndoa na vilevile uhusiano wao pamoja na Yehova. Ili kufanikiwa, wenzi wa ndoa wanapaswa kusoma Biblia pamoja, kuhubiri kwa ukawaida pamoja, na kusali pamoja ili wapate baraka za Yehova.

ENDELEA KUWA MSHIKAMANIFU KWA YEHOVA

16, 17. (a) Ushikamanifu wetu kwa Mungu unawezaje kujaribiwa katika familia na kutanikoni? (b) Ni mfano gani unaoonyesha matokeo mazuri ya kutii amri ya Mungu ya kutoshirikiana na watu wa ukoo waliotengwa na ushirika?

16 Kuna washiriki wa kutaniko ambao walitenda dhambi nzito na walikaripiwa “kwa ukali, ili wawe na afya katika imani.” (Tito 1:13) Imekuwa lazima baadhi yao watengwe na ushirika kwa sababu ya mwenendo wao. Kwa “wale ambao wamezoezwa nayo,” nidhamu imewasaidia kuwa tena na uhusiano wa kiroho pamoja na Yehova. (Ebr. 12:11) Vipi ikiwa rafiki wa karibu au mtu wa ukoo ametengwa na ushirika? Ushikamanifu wetu unapaswa kuwa kwa Mungu wala si kwa mtu aliyetengwa na ushirika. Yehova anatutazama ili aone ikiwa tutafuata amri yake ya kutoshirikiana na mtu yeyote aliyetengwa na ushirika.—Soma 1 Wakorintho 5:11-13.

17 Fikiria faida moja ambayo familia itapata ikiwa itafuata kwa ushikamanifu amri ya Yehova ya kutoshirikiana na watu wa ukoo waliotengwa na ushirika. Mwanamume mmoja kijana alikuwa ametengwa na ushirika kwa miaka zaidi ya kumi, katika kipindi hicho baba yake, mama yake, na ndugu zake wanne ‘waliacha kuchangamana katika ushirika’ pamoja naye. Nyakati nyingine, alijaribu kushiriki katika utendaji wa familia, lakini kila mshiriki wa familia alisimama imara kwa kutoshirikiana naye. Baada ya kurudishwa kutanikoni, alisema kwamba alikosa sana ushirika wa familia, hasa usiku alipokuwa peke yake. Alikiri kwamba angetosheka ikiwa familia yao ingeshirikiana naye hata kwa kiasi kidogo tu. Hata hivyo, hakupata nafasi hata kidogo ya kuwasiliana na mtu yoyote yule wa familia yake, hali hiyo ilimchochea sana kufanya maendeleo na kurekebisha uhusiano wake pamoja na Yehova. Endelea kufikiria mfano huo ikiwa utashawishiwa kuvunja amri ya Mungu ya kutoshirikiana na watu wa ukoo waliotengwa na ushirika.

18. Baada ya kuzungumzia faida za kuwa washikamanifu na matokeo mabaya ya kutokuwa washikamanifu, umeazimia nini?

18 Tunaishi katika ulimwengu usio na ushikamanifu na wenye usaliti. Hata hivyo, katika kutaniko la Kikristo tunaweza kupata mifano mizuri ya ushikamanifu ya kuiga. Maisha yao yanathibitisha ukweli wa maneno haya: “Ninyi ni mashahidi, na Mungu pia, kuhusu tulivyokuwa washikamanifu na waadilifu na wasiolaumika kwenu ninyi waamini.” (1 The. 2:10) Acheni sisi sote tuendelee kuwa imara na washikamanifu kwa Mungu na kwa mmoja na mwenzake.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Nguvu za Samsoni hazikutokana na nywele zake, badala yake, zilitokana na uhusiano wake wa pekee pamoja na Yehova akiwa Mnadhiri. Nywele zake ziliwakilisha uhusiano huo.

^ fu. 6 Kwa hiyo, katika baadhi ya lugha, msemo “busu la Yuda” unamaanisha “kitendo cha usaliti.”

^ fu. 13 Kwa msaada zaidi kuhusu kukabiliana na usaliti wa mwenzi wa ndoa, tazama makala yenye kichwa “Kushughulika na Hali Mwenzi wa Ndoa Anapokusaliti,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 2010, ukurasa wa 29-32.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Ingawa wengine walimkataa Mwana mtiwa-mafuta wa Mungu, Petro alikuwa mshikamanifu kwake