Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kuwasaliti Wengine—Alama ya Siku za Mwisho!

Kuwasaliti Wengine—Alama ya Siku za Mwisho!

Kuwasaliti Wengine​—Alama ya Siku za Mwisho!

‘Tulikuwa washikamanifu na waadilifu na wasiolaumika.’​—1 THES. 2:10.

RUDILIA MAMBO MAKUU:

Tunapata onyo gani kutokana na mifano ya Delila, Absalomu, na Yuda Iskariote?

Namna gani tunaweza kuiga ushikamanifu wa Yonathani na wa Petro?

Namna gani tunaweza kubaki washikamanifu kwa mwenzi wetu wa ndoa na kwa Yehova?

1-3. (a) Ni ishara gani inayoonyesha kama tunaishi katika siku za mwisho, na hilo linatia ndani nini? (b) Ni maulizo gani matatu yatakayojibiwa katika funzo hili?

 DELILA, Absalomu, na Yuda Iskariote hawakuwa washikamanifu​—Delila alimusaliti mwanaume aliyemupenda sana: Mwamuzi Samsoni; Absalomu hakuwa mushikamamifu kwa baba yake, Mufalme Daudi; Yuda alimusaliti Bwana yake, Kristo Yesu. Kukosa ushikaminifu kwa watu hao watatu kuliwavunja wengine moyo na kuwatia katika taabu. Lakini, sababu gani sisi pia tunapaswa kufikiria sana jambo hilo?

2 Mwandikaji mumoja anataja jambo la kusaliti wengine kati ya mambo mabaya yanayoenea sana leo. Hilo halitushangazi, kwa kuwa Yesu alipozungumuzia ishara ya ‘umalizio wa mufumo wa mambo,’ yeye alisema hivi: “Wengi . . . watasalitiana.” (Mt. 24:3, 10) “Kusaliti mwengine” kunamaanisha “kumutia mutu katika mikono ya adui, kwa kutumia udanganyifu ao kwa kukosa ushikamanifu.” Ukosefu huo wa ushikamanifu unaonyesha wazi kama tunaishi katika “siku za mwisho.” Mutume Paulo alitabiri kama katika siku za mwisho, watu watakuwa “wasio washikamanifu, . . . wasaliti.” (2 Tim. 3:1, 2, 4) Mara kwa mara waandikaji wa vitabu na watungaji wa filme wanaonyesha vitendo vya ukosefu wa ushikamanifu kuwa jambo lenye kuvutia, lakini kwa kawaida kukosa ushikamanifu na kuwasaliti wengine kunatokeza huzuni na mateso. Kwa kweli, matendo kama hayo ni alama ya siku za mwisho!

3 Katika Biblia muna habari za watu ambao hawakuwa washikamanifu, habari hizo zinatufundisha nini? Ni mifano ya watu gani walioonyesha ushikamanifu kwa wengine ambayo tunaweza kuiga? Na tunapaswa kubaki washikamanifu kabisa kwa nani? Acheni tutafute majibu ya maulizo hayo.

MIFANO HIYO NI ONYO KWETU

4. Namna gani Delila alimusaliti Samsoni, na kwa sababu gani hilo lilikuwa jambo mbaya sana?

4 Mufano wa kwanza, tufikirie Delila mwanamuke mudanganyifu, ambaye alipendwa na Mwamuzi Samsoni. Samsoni alikusudia kupigana na Wafilisti kwa faida ya watu wa Mungu. Labda Wafilisti walijua kama Delila hamupendi kabisa Samsoni, kwa hiyo wakubwa wa tano wa Wafilisti, walimutolea Delila feza nyingi kusudi wajue siri ya nguvu za Samsoni ili wamuue. Kwa sababu Delila alikuwa mwanamuke mwenye pupa ao tamaa sana alikubali feza hizo. Alijaribu mara tatu kumufanya Samsoni amujulishe siri ya nguvu zake, lakini alishindwa. Basi Delila aliendelea kumusumbua sana Samsoni ‘kwa maneno yake wakati wote na kuendelea kumusihi.’ Mwishowe, “nafsi yake [Samsoni] ikakosa subira kufikia hatua ya kutaka kufa.” Kwa hiyo, Samsoni akamufunulia Delila siri, akamuambia kwamba hajakatwa nywele hata siku moja, akikatwa nywele atapoteza nguvu zake. * Delila alipojua siri hiyo, akafanya mupango ili Samsoni akatwe nywele alipokuwa akilala kwenye mapaja yake, kisha akamuacha katika mikono ya maadui ili wamutendee wanavyotaka. (Amu. 16:4, 5, 15-21) Delila alitenda jambo mbaya sana! Kwa sababu tu ya pupa Delila alimusaliti mwanaume aliyemupenda.

5. (a) Namna gani Absalomu alikosa ushikamanifu kwa Daudi, na hilo lilionyesha nini juu ya Absalomu? (b) Daudi alijisikia namna gani wakati Ahitofeli alimugeuka na kuwa musaliti?

5 Mufano wa pili ni ule wa Absalomu, mudanganyifu. Kwa kuwa alipenda sana mambo makubwa, aliazimia kumunyanganya baba yake, Mufalme Daudi, ufalme. Kwanza Absalomu ‘aliiba mioyo ya watu wa Israeli,’ alikuwa akifanya mambo ili watu wamupende; alikuwa akiwaahidi mambo ya uongo na kujionyesha kuwa anawapenda. Alikuwa tayari kuwakumbatia na kuwabusu, ili kuonyesha kama alipendezwa kabisa nao na kuhangaikia shida zao. (2 Sam. 15:2-6) Absalomu alifikia hata kumufanya Ahitofeli, mushauri ambaye Daudi alitumainia sana, amusaliti Daudi na kuunga mukono uasi wa Absalomu. (2 Sam. 15:31) Katika Zaburi ya 3 na ya 55, Daudi anaeleza namna jambo hilo lilivyomusumbua sana. (Zab. 3:1-8; Soma Zaburi 55:12-14.) Absalomu alionyesha waziwazi kama yeye hakuwa akiheshimu mamlaka ya Mungu mwenye Enzi Kubwa ya kuwachagua na kuwaweka wafalme kwenye kiti cha ufalme. (1 Nya. 28:5) Mwishowe, alishindwa, na Daudi, mutiwa​-mafuta wa Yehova, akaendelea kutawala.

6. Namna gani Yuda alimusaliti Yesu, na kuanzia wakati huo watu wanatumia jina Yuda ili kumaanisha nini?

6 Tufikirie sasa mufano wa Yuda Iskariote aliyemusaliti Kristo. Kwenye Pasaka ya mwisho ambayo Yesu alifanya pamoja na mitume wake 12, aliwaambia hivi: ‘Kwa kweli ninawaambia ninyi, Mumoja wenu atanisaliti.’ (Mt. 26:21) Kisha katika bustani ya Gethsemane usiku huo, Yesu akawaambia Petro, Yakobo, na Yohana hivi: ‘Tazameni, musaliti wangu amekaribia.’ Mara moja, Yuda akatokea katika bustani akiwa pamoja na watu waliopatana naye, “akaenda moja kwa moja kwa Yesu na kusema: ‘Siku njema, Rabi!’ na kumubusu kwa wororo sana.” (Mt. 26:46-50; Luka 22:47, 52) Yuda ‘alisaliti damu yenye uadilifu’ na akamuacha Yesu katika mikono ya maadui. Basi, Yuda mupenda​-feza alimusaliti ao kumutoa Yesu kwa kiasi gani cha feza? Kwa vipande 30 tu vya feza! (Mt. 27:3-5) Kuanzia wakati huo, watu wanatumia jina Yuda ili kumaanisha ‘mutu anayemusaliti mwengine’ zaidi sana mutu anayemusaliti rafiki yake. *

7. Maisha ya Absalomu, ya Yuda na Delila yanatufundisha nini?

7 Mifano hiyo inatufundisha nini? Absalomu na Yuda walikufa vifo vya haya kwa kuwa waliwasaliti ao walikosa kuwa washikamanifu kwa watiwa​-mafuta wa Yehova. (2 Sam. 18:9, 14-17; Mdo. 1:18-20) Kila siku jina Delila linapotajwa watu wanafikiria tu udanganyifu na upendo wa kinafiki. (Zab. 119:158) Ni lazima tutupilie mbali mwelekeo wowote wa kutaka mambo makubwa, kuwa na pupa ao tamaa, kwa kuwa mambo hayo yanaweza kutufanya tusikubaliwe tena na Yehova! Mifano hiyo ni fundisho kabisa ili tuchukie na kutupilia mbali matendo hayo!

MIFANO TUNAYOPASWA KUIGA

8, 9. (a) Sababu gani Yonathani alimuahidi Daudi kwamba atakuwa mushikamanifu kwake? (b) Namna gani tunaweza kumuiga Yonathani?

8 Biblia inazungumuzia pia watu wengi waliokuwa washikamanifu. Acheni tuzungumuzie watu wawili na tuone mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwao. Mufano wa kwanza ni ule wa Yonathani aliyekuwa mushikamanifu kwa Daudi. Yonathani alikuwa mwana muzaliwa wa kwanza wa Mufalme Sauli, na kwa hiyo, labda ni yeye ndiye angeriti kiti cha ufalme cha Israeli. Lakini Yehova alimuchagua Daudi awe mufalme mahali pa Sauli. Yonathani aliheshimu uamuzi wa Mungu. Hakumusikilia Daudi wivu. Lakini, “nafsi ya Yonathani ikashikamana na nafsi ya Daudi” na akamuahidi Daudi kama atakuwa mushikamanifu kwake. Ili kumuonyesha Daudi heshima ya kifalme, Yonathani alimupatia hata mavazi yake, mupanga, upinde, na mushipi wake. (1 Sam. 18:1-4) Yonathani alifanya yote awezayo ili ‘autie nguvu mukono wa Daudi,’ na alitia hata maisha yake katika hatari ili kumutetea Daudi mbele ya Sauli. Ili kumuonyesha Daudi kama kweli alikuwa mushikamanifu kwake, Yonathani alimuambia hivi: ‘Wewe utakuwa mufalme juu ya Israeli, na mimi nitakuwa wa pili kwako.’ (1 Sam. 20:30-34; 23:16, 17) Si jambo la kushangaza kwamba kisha kifo cha Yonathani, Daudi alitunga wimbo wa maombolezo ili kuonyesha huzuni yake na namna alivyomupenda Yonathani.​—2 Sam. 1:17, 26.

9 Yonathani alijua vizuri kama alipaswa kuwa mushikamanifu kwa Yehova, mukubwa wa ulimwengu wote, na alimutegemeza kabisa Daudi aliyekuwa mutiwa​-mafuta wa Mungu. Leo pia tunaweza kumuiga Yonathani, hata ikiwa hatukupewa pendeleo fulani la pekee katika kutaniko, tunapaswa kutegemeza ndugu ambao wamechaguliwa ili kutuongoza.​—1 Thes. 5:12, 13; Ebr. 13:17, 24.

10, 11. (a) Sababu gani Petro alishikamana na Yesu? (b) Namna gani tunaweza kumuiga Petro, na hilo linapaswa kutuchochea kufanya nini?

10 Mufano mwingine muzuri ambao tunaweza kuiga na ambao tutazungumuzia sasa ni ule wa mutume Petro. Yeye alisema waziwazi kuwa atabaki mushikamanifu kwa Yesu. Wakati Kristo alitumia usemi wa mufano ili kuonyesha kama ni lazima kuwa na imani katika mwili na damu yake, yaani, zabihu ya ukombozi iliyopaswa kutolewa karibuni, wanafunzi wengi waliumizwa na maneno hayo, na wakamuacha Yesu. (Yoh. 6:53-60, 66) Kwa hiyo, Yesu akawatazama wale mitume wake 12 na kuwauliza: ‘Je, ninyi pia munataka kwenda?’ Petro akajibu: ‘Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele; na sisi tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mutakatifu wa Mungu.’ (Yoh. 6:67-69) Je, hilo linamaanisha kama Petro alielewa kila jambo ambalo Yesu alisema juu ya zabihu ya ukombozi? Labda hapana. Hata hivyo, Petro aliazimia kubaki mushikamanifu kwa Mwana mutiwa​-mafuta wa Mungu.

11 Petro hakufikiri kama Yesu alikosea na kama wakati atatambua hilo atabadilisha mambo aliyosema. Petro alikuwa munyenyekevu na kwa hiyo alitambua kama Yesu ana “maneno ya uzima wa milele.” Kwa hiyo, tunaweza kujiuliza, tutafanya nini ikiwa tunasoma jambo fulani katika vitabu vya ‘musimamizi​-nyumba mwaminifu’ ambalo ni vigumu kuelewa ao ambalo halipatani na mawazo yetu? Tunapaswa kujikaza kuelewa jambo hilo kuliko kuwaza kama litabadilishwa ili liambatane na mawazo yetu.​—Soma Luka 12:42.

USHIKAMANIFU KWA MWENZI WA NDOA

12, 13. Nini inayoweza kumufanya mutu aanze kuwa na mawazo ya kumusaliti mwenzi wa ndoa, na kwa sababu gani umri wa mutu anayetenda hivyo haupaswi kuwa kisababu cha kumusaliti mwenzi wake wa ndoa?

12 Hakuna namna ya kusaliti mutu ambayo ni nzuri na mutu anayetenda hivyo hapaswi kuruhusiwa aendelee kuvuruga amani na umoja wa familia na kutaniko. Hilo ni jambo linalofaa kukumbuka, na kwa hiyo tuzungumuzie sasa namna tunavyoweza kubaki washikamanifu kwa mwenzi wetu wa ndoa na pia kwa Mungu wetu.

13 Mutu anayefanya uzinifu anamusaliti mwenzi wake wa ndoa na jambo hilo linaumiza sana. Mutu anayefanya uzinifu anavunja ahadi aliyofanya ya kubaki mwaminifu kwa mwenzi wake wa ndoa kwa kuwa anaanza kuwaza sana na kupendezwa na mutu mwingine. Mwenzi asiye na kosa kwa gafula anaachwa peke yake na maisha yake yanavurugika sana. Namna gani kukosa ushikamanifu kunaweza kutokea kati ya watu wawili ambao wakati fulani walipendana? Mara nyingi, hatua ya kwanza inayoongoza kwenye hali hiyo ni wakati kila mumoja hapendi tena kumufurahisha mwingine ao hafurahiwi tena na mwingine. Profesa wa Sociolojia Gabriella Turnaturi anaeleza kwamba ikiwa wenzi wawili waliofunga ndoa wanaacha kabisa kufanya mambo wanayopaswa kufanya ili uhusiano wao uwe nguvu, mwenzi mumoja anaweza kuanza kuwa na mawazo ya kumusaliti mwengine. Hilo linaweza kuwafikia hata wale ambao wamekwisha kufanya miaka mingi katika ndoa. Kwa mufano, mwanaume mumoja mwenye umri wa miaka 50 alivunja ndoa na bibi yake ili kuoa mwanamuke mwingine aliyemuvutia; ndoa yao ilikuwa imekwisha fanya miaka 25. Watu fulani walisema kama hilo ni jambo la kawaida kwa wanaume wenye umri huo. Lakini mwanaume kuwa na umri huo haipaswi kuwa kisababu cha kumusaliti mwenzi wa ndoa, kufanya hivyo ni kukosa kabisa ushikamanifu. *

14. (a) Yehova anajisikia namna gani wakati mutu anamutendea mwenzi wake wa ndoa kwa udanganyifu? (b) Yesu alisema nini kuhusu uaminifu katika ndoa?

14 Yehova anajisikia namna gani wakati mutu anamuacha mwenzi wake wa ndoa bila sababu ya Kimaandiko? Mungu wetu ‘anachukia talaka,’ na anakaripia kwa ukali wale wanaoacha wenzi wao wa ndoa na kuwatendea kwa udanganyifu. (Soma Malaki 2:13-16.) Yesu pia anajisikia kama Baba yake. Kwa hiyo, Yesu alisema kama kumufukuza mwenzi wa ndoa asiye na kosa si jambo la muchezo.​—Soma Mathayo 19:3-6, 9.

15. Bibi na bwana wanaweza kufanya nini ili kila mumoja aendelee kuwa mushikamanifu kwa mwingine?

15 Namna gani wale wenye kufunga ndoa ao kuolewa wanaweza kubaki washikamanifu kwa wenzi wao? Neno la Mungu linasema: “Ushangilie pamoja na muke [ao mume] wa ujana wako” na, ‘Furahia maisha pamoja na muke [ao mume] unayemupenda.’ (Met. 5:18; Mhu. 9:9) Bwana na bibi wanapoendelea kuzeeka wanapaswa kufanya yote wawezayo ili waendelee kushikamana katika upendo wao na katika mambo mengine. Hilo linamaanisha kuhangaikia mwingine, kusaidiana, kupitisha wakati pamoja na kuzungumuza. Wanapaswa kufanya nguvu ili kulinda ndoa yao na kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova. Ili kufikia jambo hilo, bibi na bwana wanapaswa kujifunza Biblia pamoja, kuhubiri pamoja kwa ukawaida, na kusali pamoja ili kuomba baraka za Yehova.

USHIKAMANIFU KWA YEHOVA

16, 17. (a) Namna gani ushikamanifu wetu kwa Mungu unaweza kujaribiwa katika familia na katika kutaniko? (b) Ni mufano gani unaoonyesha kama kutii amri ya Mungu ya kuacha kushirikiana na watu wa jamaa waliotengwa kunaweza kuwasaidia?

16 Kuna ndugu na dada fulani ambao waliangukia katika zambi nzito na kwa hiyo walikaripiwa “kwa ukali ili wawe na afya katika imani.” (Tito 1:13) Wengine walitengwa na ushirika kwa kuwa iliomba watengwe. Kwa wale ambao wamekubali ‘kuzoezwa’ na nizamu ao discipline hiyo, wamesaidiwa na sasa wako tena na afya njema kiroho. (Ebr. 12:11) Itakuwa namna gani ikiwa mutu wa jamaa ao rafiki yetu anatengwa? Hapo sasa ndipo ushikamanifu wetu unajaribiwa. Je, tutabaki washikamanifu kwa Mungu ao kwa mutu? Yehova anatutazama ili kuona ikiwa tutatii amri yake inayotukataza kushirikiana na mutu yeyote anayetengwa.​—Soma 1 Wakorintho 5:11-13.

17 Kuna mufano mumoja unaoweza kutusaidia ili tuone faida ya kuunga mukono kwa ushikamanifu amri ya Yehova inayotukataza kushirikiana na watu wa jamaa waliotengwa. Kijana mumoja alitengwa na ushirika kwa zaidi ya miaka 10. Muda wa miaka yote hiyo, baba yake, mama yake, kaka yake na wadogo zake watatu ‘waliacha kuchangamana pamoja’ naye. Nyakati fulani, alikuwa akijaribu kuwakaribia ili kupitisha wakati pamoja nao lakini kila mushiriki wa familia hakukubali kushirikiana naye. Aliporudishwa katika tengenezo, alisema kwamba kila siku alisumbuka sana kwa sababu watu wa familia hawakukubali kushirikiana naye, zaidi sana wakati wa usiku alipokuwa peke yake. Lakini, alisema ikiwa baba yake, mama yake na ndugu zake wangeshirikiana naye hata wakati kidogo tu, jambo hilo lingemufanya asijisikie upweke. Lakini, kwa kuwa hawakupashana habari naye hata kidogo, alikuwa na tamaa sana ya kuwa pamoja nao, na jambo hilo lilimuchochea ili arudilie tena uhusiano wake pamoja na Yehova. Kumbuka mufano huo wakati wowote unapojaribiwa ili kuvunja amri ya Mungu inayokataza kushirikiana na watu wa jamaa waliotengwa.

18. Kisha kujifunza faida za kubaki washikamanifu na matokeo mabaya ya kukosa ushikamanifu, unaazimia kufanya nini?

18 Tunaishi katika ulimwengu wa watu wadanganyifu na wasio washikamanifu. Lakini, katika kutaniko tunaweza kupata mifano ya kuiga ya ndugu na dada washikamanifu. Mwenendo wao unawatetea, ni kama vile wanatuambia: “Ninyi ni mashahidi, na Mungu pia, kuhusu tulivyokuwa washikamanifu na waadilifu na wasiolaumika kwenu ninyi waamini.” (1 Thes. 2:10) Acheni sisi wote tubaki washikamanifu kwa Mungu na kwa ndugu zetu.

[Maelezo ya chini]

^ Samsoni alikuwa na nguvu kwa sababu ya uhusiano wa pekee aliokuwa nao pamoja na Yehova kwa kuwa yeye alikuwa Munaziri; haikukuwa kwa sababu ya nywele zake, nywele hizo zilikuwa tu alama ya uhusiano huo.

^ Usemi “busu la Yuda” unamaanisha “tendo la kusaliti.”

^ Ili kupata habari zaidi za kujua namna ya kufanya wakati mwenzi wa ndoa anakosa kuwa mushikamanifu, soma habari “Kushughulika na Hali Mwenzi wa Ndoa Anapokusaliti,” katika Mnara wa Mlinzi wa tarehe 15 mwezi wa 6, 2010, ukurasa wa 29-32.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Petro alisema kama yeye atabaki mushikamanifu kwa Mwana mutiwa​-mafuta wa Mungu