Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Wakristo wa Karne ya Kwanza Walijihusisha na Siasa?

Je, Wakristo wa Karne ya Kwanza Walijihusisha na Siasa?

▪ Kabla ya kupaa mbinguni, Yesu aliwapa wanafunzi wake maagizo yaliyo wazi kuhusu jinsi ambavyo wangetimiza huduma yao, lakini hakuwapa mashauri yoyote ya kisiasa. (Mathayo 28:18-20) Hivyo, wanafunzi wake waliendelea kutii kanuni ambayo Yesu alikuwa amewapa mapema: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.”—Marko 12:17.

Kanuni hiyo iliwasaidiaje wafuasi wa Yesu waishi katika ulimwengu lakini wasiwe sehemu yake? Walitenganishaje kati ya mambo ya Serikali, au ya Kaisari, na mambo ya Mungu?

Mtume Paulo aliona kwamba mtu angekosa kutii kanuni ya Yesu ikiwa angeshiriki katika siasa. Kitabu Beyond Good Intentions—A Biblical View of Politics kinasema: “Paulo alikuwa tayari kutumia haki yake akiwa raia Mroma kupata ulinzi kupitia mfumo wa kisheria, lakini hakuunga mkono mabishano yaliyohusu sera za serikali.”

Paulo aliwapa Wakristo wenzake mwongozo gani? Kitabu hichohicho kinaongezea hivi: “Barua zake kwa waamini katika majiji muhimu kama vile Korintho, Efeso, na hata Roma hazikutaja mizozano yoyote ya kisiasa.” Pia, kitabu hicho kinasema kwamba Paulo “aliwaamuru wazitii serikali, lakini hakuandika kamwe katika barua zake nyingi kuhusu sera yoyote ambayo kanisa lilipaswa kupendekeza kwa serikali.”—Waroma 12:18; 13:1, 5-7.

Wakristo walioishi miaka mingi baada ya kifo cha Paulo walidumisha mpaka huo kati ya wajibu wao kumwelekea Mungu na wajibu wao kuelekea Serikali. Waliendelea kuheshimu mamlaka za kisiasa lakini hawakujihusisha na shughuli za kisiasa. Kitabu Beyond Good Intentions kinasema hivi kuhusu waamini hao: “Ingawa waliamini kwamba walikuwa na wajibu wa kuheshimu mamlaka za kiserikali, Wakristo wa mapema hawakuamini kwamba walipaswa kushiriki katika mambo ya kisiasa.”

Hata hivyo, mambo yalibadilika miaka 300 hivi baada ya kifo cha Kristo. Mwanatheolojia Charles Villa-Vicencio anasema hivi: “Mifumo ya kisiasa ilipobadilishwa chini ya utawala wa Konstantino, inaonekana Wakristo wengi walianza kufanya kazi katika serikali na jeshi na wakakubali vyeo vya kisiasa.” (Between Christ and Caesar) Matokeo yalikuwa nini? Mwishoni mwa karne ya nne W.K., muungano huo wa dini na siasa ulibadilika na kuwa Serikali ya kidini ya Milki ya Roma.

Leo, dini nyingi zinazodai kumfuata Kristo zinaendelea kuwatia moyo wafuasi wake wajihusishe na siasa. Hata hivyo dini hizo hazifuati mfano wa Kristo, wala hazifuati mfano wa Wakristo wa karne ya kwanza.