Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Unathamini Zawadi ya Mungu ya Ndoa?

Je, Kweli Unathamini Zawadi ya Mungu ya Ndoa?

Je, Kweli Unathamini Zawadi ya Mungu ya Ndoa?

“Yehova na awape zawadi, na mpate mahali pa kupumzika kila mmoja katika nyumba ya mume wake.” —RUT. 1:9.

TAFUTA MAJIBU:

Kwa nini tunaweza kusema kwamba watumishi wa zamani wa Mungu walithamini zawadi yake ya ndoa?

Tunajuaje kwamba uamuzi wetu wa kuchagua mwenzi wa ndoa ni muhimu machoni pa Yehova?

Ni shauri gani la Biblia kuhusu ndoa unalopanga kutumia katika maisha yako?

1. Eleza jinsi Adamu alivyoitikia alipopata mke.

“MWISHOWE huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu. Huyu ataitwa Mwanamke, kwa sababu huyu alitolewa katika mwanamume.” (Mwa. 2:23) Mwanamume wa kwanza, Adamu, alifurahi kama nini kupata mke! Haishangazi kwamba Adamu alitunga shairi! Baada ya Yehova kumletea Adamu usingizi mzito, Alimuumba mwanamke huyo mrembo kutokana na ubavu mmoja wa mwanamume. Baadaye Adamu alimwita mwanamke huyo Hawa. Mungu aliwaunganisha wenzi hao wawili katika ndoa yenye furaha. Kwa kuwa Yehova aliutumia ubavu wa Adamu kumuumba Hawa, wawili hao walikuwa na uhusiano wa karibu zaidi kuliko mume na mke yeyote leo.

2. Kwa nini wanaume na wanawake wanavutiana?

2 Kwa sababu ya hekima yake isiyo na kifani, Yehova aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kufurahia upendo wa kimahaba ambao unawafanya wanaume na wanawake wavutiane. Kitabu kimoja (The World Book Encyclopedia) kinasema hivi: “Mwanamume na mwanamke wanaofunga ndoa wanatumaini kwamba watakuwa na uhusiano wa kingono na kwamba upendo wao wa kimahaba utadumu.” Imekuwa hivyo kwa watumishi wengi sana wa Yehova.

WALITHAMINI ZAWADI YA NDOA

3. Isaka alipataje mke?

3 Abrahamu aliyekuwa mwaminifu alithamini sana ndoa. Hivyo, alimtuma mtumishi wake mwenye umri mkubwa zaidi huko Mesopotamia ili amtafutie Isaka mke. Sala ambayo mtumishi huyo alitoa ilikuwa na matokeo mazuri. Rebeka ambaye alimwogopa Mungu alikuja kuwa mke mpendwa wa Isaka na alitimiza sehemu fulani katika mpango wa Yehova wa kuhifadhi uzao wa Abrahamu. (Mwa. 22:18; 24:12-14, 67) Hatupaswi kutumia kisa hicho kukata kauli kwamba mtu anapaswa kujichukulia daraka la kuwatafutia wengine wenzi wa ndoa, hata ikiwa ana nia nzuri. Katika jamii ya leo, watu wengi wanajichagulia wenyewe mwenzi wa ndoa. Bila shaka, Mungu hawachagulii watu wenzi wa ndoa, lakini atawaongoza Wakristo katika jambo hilo na katika mambo mengine maishani ikiwa watamwomba mwongozo kupitia sala na kukubali kuongozwa na roho yake.—Gal. 5:18, 25.

4, 5. Ni nini kinachokusadikisha kwamba msichana Mshulami na kijana mchungaji walikuwa na hisia za pekee kuelekeana?

4 Msichana mmoja mrembo Mshulami wa taifa la kale la Israeli hakutaka marafiki wake wamshinikize kuwa mmoja wa wake wengi wa Mfalme Sulemani. Msichana huyo alisema hivi: “Nimewaapisha ninyi, enyi binti za Yerusalemu kwamba msijaribu kuamsha au kuwasha upendo ndani yangu mpaka wenyewe utake.” (Wim. 8:4) Mshulami huyo na mchungaji fulani walikuwa na hisia za pekee kuelekeana. Msichana huyo alisema hivi kwa unyenyekevu: “Mimi ni zafarani tu ya nchi tambarare ya pwani, yungiyungi la nchi tambarare za chini.” Lakini mchungaji huyo akajibu: “Kama yungiyungi katikati ya magugu yenye miiba, ndivyo alivyo msichana mwenzi wangu katikati ya mabinti”! (Wim. 2:1, 2) Walipendana kwelikweli.

5 Kwa sababu msichana Mshulami na kijana mchungaji walimpenda Mungu sana, ndoa yao ingekuwa imara kabisa. Kwa kweli, Mshulami alimwambia hivi mpenzi wake mchungaji: “Nitie kama muhuri juu ya moyo wako, kama muhuri juu ya mkono wako; kwa maana upendo una nguvu kama kifo, msisitizo juu ya kujitoa kikamili ni wenye kudai kama Kaburi. Miwako yake ni miwako ya moto, mwali wa moto wa Yah [kwa kuwa unatoka kwake]. Maji mengi hayawezi kuuzima upendo, wala mito haiwezi kuufagilia mbali. Kama mtu angetoa vitu vyote vyenye thamani vya nyumba yake kwa ajili ya upendo, hakika watu wangevidharau.” (Wim. 8:6, 7) Mtumishi wa Yehova anapofikiria kufunga ndoa, je, hapaswi kutazamia mwenzi wake atimize kiwango hichohicho cha juu cha upendo?

UAMUZI MUHIMU MACHONI PA MUNGU

6, 7. Tunajuaje kwamba uamuzi wetu wa kuchagua mwenzi wa ndoa ni muhimu machoni pa Mungu?

6 Uamuzi wako wa kuchagua mwenzi wa ndoa ni muhimu machoni pa Yehova. Waisraeli waliamriwa hivi kuhusu wakaaji wa Kanaani: “Usifanye mapatano yoyote ya ndoa pamoja nao. Binti yako usimpe mwana wake, wala binti yake usimchukue kwa ajili ya mwana wako. Kwa maana atamgeuza mwana wako aache kunifuata, nao watatumikia miungu mingine; na hasira ya Yehova itawaka kwelikweli juu yenu, naye hakika atakuangamiza haraka.” (Kum. 7:3, 4) Baada ya karne nyingi kupita, kuhani Ezra alitangaza hivi: “Ninyi wenyewe mmetenda kwa kukosa uaminifu kwa vile mmewapa makao wanawake wa kigeni ili kuongezea hatia ya Israeli.” (Ezra 10:10) Naye mtume Paulo aliwaambia hivi Wakristo wenzake: “Mke amefungwa wakati wote ambao mume wake yuko hai. Lakini mume wake akilala usingizi katika kifo, yeye yuko huru kuolewa na yeyote anayemtaka, katika Bwana tu.”1 Kor. 7:39.

7 Ikiwa mtumishi wa Yehova ambaye amejiweka wakfu anaoa au kuolewa na mtu ambaye si mwamini, anaonyesha kwamba hamtii Mungu. Waisraeli walioishi katika siku za Ezra walitenda kwa njia isiyo ya uaminifu kwa ‘kuwapa makao wanawake wa kigeni.’ Na ni kosa kujaribu kupunguza uzito wa maagizo ya wazi yaliyo katika Maandiko. (Ezra 10:10; 2 Kor. 6:14, 15) Mkristo anayeoa au kuolewa na mtu ambaye si mwamini si mfano mzuri, naye anaonyesha kwamba hathamini kikweli zawadi ya Mungu ya ndoa. Mkristo aliyebatizwa anayeoa au kuolewa na mtu ambaye si mwamini anaweza kupoteza mapendeleo fulani katika kutaniko. Na halingekuwa jambo linalopatana na akili kutarajia baraka na wakati huohuo kukiri hivi katika sala: ‘Yehova, nilikosa kukutii kimakusudi, lakini tafadhali nibariki tu.’

BABA YETU WA MBINGUNI ANAJUA KILICHO BORA ZAIDI KWETU

8. Eleza kwa nini tunapaswa kufuata mwongozo wa Mungu kuhusu ndoa.

8 Mtengenezaji wa mashini anajua vizuri kabisa jinsi mashini hiyo inavyofanya kazi. Ikiwa mashini hiyo inahitaji kuunganishwa, anaweza kutoa maagizo yote yanayohitajiwa kuhusu mashini hiyo. Namna gani tukipuuza maagizo hayo na kuunganisha sehemu za mashini hiyo jinsi tunavyotaka? Inaelekea kwamba mashini hiyo haitafanya kazi na ikiwa itafanya kazi basi itasababisha msiba. Kwa hiyo, ikiwa tunataka kuona tamaa yetu ya kuwa na ndoa yenye furaha ikitimia, ni lazima tufuate maagizo yanayotolewa na Yehova, Mwanzilishi wa ndoa.

9. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova anaelewa hisia za upweke na pia furaha ambayo watu wanaweza kupata katika ndoa?

9 Yehova anajua kila jambo kuwahusu wanadamu na ndoa. Aliwaumba wanadamu wakiwa na uhitaji wa kufanya ngono ili ‘wazae na kuwa wengi.’ (Mwa. 1:28) Mungu anaelewa hisia za upweke, kwa kuwa kabla ya kumuumba mwanamke wa kwanza, alisema hivi: “Si vizuri huyo mwanamume awe peke yake; nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye.” (Mwa. 2:18, Byington) Pia, Yehova anajua vizuri kabisa shangwe ambayo wanadamu wanaweza kupata katika ndoa.—Soma Methali 5:15-18.

10. Ni mambo gani yanayopaswa kuwaongoza wenzi wa ndoa Wakristo katika mahusiano ya ngono?

10 Kwa sababu ya dhambi na kutokamilika ambako wanadamu walirithi kutoka kwa Adamu aliyetenda dhambi, hakuna ndoa kamilifu leo. Hata hivyo, watumishi wa Yehova wakifuata Neno la Mungu wanaweza kuwa na ndoa yenye furaha ya kweli. Kwa mfano, fikiria shauri la Paulo lililo wazi kuhusu mahusiano ya ngono katika ndoa. (Soma 1 Wakorintho 7:1-5.) Maandiko hayasemi kwamba wenzi wa ndoa wanapaswa kufanya ngono kwa kusudi tu la kuzaa watoto. Mahusiano hayo ya karibu yanaweza kutosheleza mahitaji ya kihisia na ya kimwili. Lakini bila shaka mazoea mapotovu hayampendezi Mungu. Hapana shaka kwamba waume na wake Wakristo wanapaswa kujitahidi kutendeana kwa upole na kuonyeshana upendo wa kweli katika sehemu hiyo muhimu ya maisha yao. Na bila shaka wanapaswa kuepuka matendo yoyote ambayo hayatampendeza Yehova.

11. Ruthu alibarikiwa jinsi gani kwa sababu ya kufanya mambo kupatana na njia ya Yehova?

11 Ndoa inapaswa kuwa yenye shangwe nyingi, haipaswi kuwa yenye kuchosha na isiyo na furaha. Nyumba ya Wakristo inapaswa hasa kuwa mahali penye amani na pa kupumzika. Fikiria jambo lililotukia miaka 3,000 hivi iliyopita wakati mjane mzee, Naomi, pamoja na binti-wakwe zake wajane, Orpa na Ruthu, walipokuwa njiani kutoka Moabu kwenda Yuda. Naomi aliwasihi wanawake hao vijana warudi kwa watu wao. Ruthu Mmoabu alishikamana na Naomi, alikuwa mwaminifu kwa Mungu wa kweli, na alihakikishiwa kwamba angepata ‘malipo kamili kutoka kwa Yehova, ambaye Ruthu alikuja kutafuta kimbilio chini ya mabawa yake.’ (Rut. 1:9; 2:12) Ruthu alithamini sana zawadi ya Mungu ya ndoa, akawa mke wa Boazi mwenye umri mkubwa, mwabudu wa kweli wa Yehova. Ruthu atakapofufuliwa duniani katika ulimwengu mpya wa Mungu, atafurahi kujua kwamba alikuja kuwa nyanya ya Yesu Kristo. (Mt. 1:1, 5, 6; Luka 3:23, 32) Alibarikiwa kama nini kwa sababu ya kufanya mambo kupatana na njia ya Yehova!

MASHAURI MAZURI YA KUFANIKISHA NDOA

12. Mtu anaweza kupata wapi mashauri mazuri kuhusu ndoa?

12 Mwanzilishi wa ndoa anatuambia mambo tunayohitaji kujua kuhusu ndoa yenye mafanikio. Hakuna mwanadamu aliye na ujuzi kama wake. Sikuzote Biblia hutoa mashauri yanayofaa, na njia pekee ambayo inaweza kumsaidia mtu yeyote kutoa mashauri mazuri kuhusu ndoa ni kushikamana na viwango vilivyo katika Maandiko. Kwa mfano, mtume Paulo aliandika hivi chini ya mwongozo wa roho takatifu: “Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Efe. 5:33) Hakuna jambo lolote katika shauri hilo la Biblia ambalo Wakristo wakomavu hawawezi kuelewa. Swali ni, Je, watafuata Neno la Yehova? Watafuata Neno lake ikiwa wanathamini kikweli zawadi yake ya ndoa. *

13. Kukosa kufuata shauri la 1 Petro 3:7 kunaweza kuwa na matokeo gani?

13 Mume Mkristo anapaswa kumtendea mke wake kwa upendo. Mtume Petro aliandika hivi: “Enyi waume, endeleeni kukaa nao vivyo hivyo kulingana na ujuzi, mkiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi, yaani, mwanamke, kwa kuwa ninyi pia ni warithi pamoja nao wa pendeleo lisilostahiliwa la uzima, kusudi sala zenu zisizuiwe.” (1 Pet. 3:7) Sala za mume zinaweza kuzuiwa ikiwa hafuati shauri la Yehova. Inaelekea kwamba hali ya kiroho ya wenzi wote wawili itaathiriwa kabisa na huenda hilo likasababisha mkazo mkubwa, ugomvi wa daima, na kuwachochea kutendeana kwa ukali.

14. Mke mwenye upendo anaweza kuwa na uvutano gani katika maisha ya familia?

14 Mke ambaye anaongozwa na Neno la Yehova na roho yake takatifu anaweza kuchangia sana hali ya utulivu na furaha nyumbani mwake. Ni jambo la kawaida kwa mume anayemwogopa Mungu kumpenda mke wake na kumlinda kimwili na kiroho. Mke anatamani sana kupendwa na mume wake, lakini ili apendwe anahitaji kuonyesha sifa zenye kuvutia. Andiko la Methali 14:1 linasema hivi: “Mwanamke mwenye hekima kwelikweli amejenga nyumba yake, lakini aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe.” Mke mwenye hekima na upendo anaisaidia sana familia yake kufanikiwa na kupata furaha. Anaonyesha pia kwamba anathamini kikweli zawadi ya Mungu ya ndoa.

15. Ni shauri gani linalopatikana katika Waefeso 5:22-25?

15 Waume na wake wanathamini zawadi ya Mungu ya ndoa wanapofuata mfano wa jinsi Yesu anavyolitendea kutaniko lake. (Soma Waefeso 5:22-25.) Wenzi wa ndoa wanapata baraka nyingi kama nini wanapopendana kikweli na kutoruhusu kamwe kiburi, tabia ya kitoto ya kunyamaziana, au tabia nyingine ambazo si za Kikristo ziharibu ndoa yao!

MTU YEYOTE ASIWATENGANISHE

16. Kwa nini baadhi ya Wakristo wanabaki waseja?

16 Ingawa watu wengi wanapanga kufunga ndoa wakati fulani maishani, baadhi ya watumishi wa Yehova wangali waseja kwa sababu hawajapata mwenzi wa ndoa anayewapendeza na kumpendeza Yehova. Wengine wana zawadi ya useja kutoka kwa Mungu inayowaruhusu kujitoa kabisa katika utumishi wa Yehova bila kukengeushwa fikira na mambo ya ndoa. Bila shaka, wanapaswa kufurahia useja kwa kufuata mipaka ambayo Yehova ameweka.—Mt. 19:10-12; 1 Kor. 7:1, 6, 7, 17.

17. (a) Tunapaswa kukumbuka maneno gani ya Yesu kuhusu ndoa? (b) Mkristo yeyote akianza tu kumtamani mwenzi wa ndoa wa mtu mwingine, anapaswa kufanya nini bila kukawia?

17 Iwe sisi ni waseja au tumefunga ndoa, sote tunahitaji kukumbuka maneno haya ya Yesu: “Je, hamkusoma kwamba yeye [Mungu] aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mt. 19:4-6) Kumtamani mwenzi wa ndoa wa mtu mwingine ni dhambi. (Kum. 5:21) Mkristo yeyote akianza kusitawisha tamaa hiyo, anapaswa kung’oa haraka tamaa hiyo chafu, hata ikiwa kufanya hivyo kutamletea maumivu makali ya kihisia kwa sababu ya kuruhusu tamaa hiyo ya kichoyo isitawi. (Mt. 5:27-30) Ni muhimu sana kurekebisha maoni ya aina hiyo na kudhibiti tamaa ya dhambi ya moyo wenye hila.—Yer. 17:9.

18. Unafikiri tunapaswa kuhisije kuhusu zawadi ya Mungu ya ndoa?

18 Hata watu wengi ambao hawajui mengi au hawajui lolote kumhusu Yehova Mungu na zawadi yake nzuri ajabu ya ndoa wameonyesha kwamba wanathamini kwa kadiri fulani kifungo cha ndoa. Sisi ambao tumejiweka wakfu kwa “Mungu mwenye furaha,” Yehova, je, hatupaswi kufurahia hata zaidi maandalizi yake yote na kuonyesha kwamba kwa kweli tunathamini zawadi ya Mungu ya ndoa?—1 Tim. 1:11.

[Maelezo ya Chini]

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Ndoa nzuri inamletea Yehova heshima na inaweza kumletea kila mtu katika familia furaha nyingi

[Picha katika ukurasa wa 5]

Ruthu alithamini zawadi ya Mungu ya ndoa

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, unaonyesha kwamba kwa kweli unathamini zawadi ya ndoa kutoka kwa Yehova?