Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Matatizo Si Mwisho wa Ndoa

Matatizo Si Mwisho wa Ndoa

Matatizo Si Mwisho wa Ndoa

‘Kwa watu waliofunga ndoa natoa maagizo, lakini si mimi bali ni Bwana.’​—1 KOR. 7:10.

UTAJIBU NAMNA GANI?

Ni katika maana gani wenzi wa ndoa wanaunganishwa na Mungu?

Wazee wanaweza kuwasaidia namna gani Wakristo walio na matatizo ya ndoa?

Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu ndoa?

1. Wakristo wanaiona ndoa namna gani, na kwa nini?

 WAKRISTO wanapofunga ndoa wanaweka naziri kwa Mungu, na hilo si jambo la muchezo. (Mhu. 5:4-6) Yehova ndiye ‘amewaunganisha’ kwa sababu ni yeye aliyeanzisha mupango wa ndoa. (Mk. 10:9) Hata ikiwa kila inchi ina sheria zake juu ya ndoa, wale wanaofunga ndoa wanapaswa kujua kama ni Mungu ndiye amewaunganisha. Watumishi wa Yehova wanapaswa kujua kama naziri ya ndoa haiwezi kubadilishwa, iwe walikuwa waabudu wa Yehova wakati walifunga ndoa ao hapana.

2. Habari hii itajibu maulizo gani?

2 Ndoa inaweza kuleta furaha nyingi. Lakini, tunaweza kufanya nini ikiwa ndoa yetu ina matatizo? Je, tunaweza kuiokoa ndoa hiyo? Ni mashauri gani yanayoweza kusaidia ndoa ambazo zinakosa amani?

JE, NDOA YAKO ITAKUWA YENYE FURAHA AO HAPANA?

3, 4. Matokeo yanaweza kuwa nini ikiwa Mukristo hafuati uongozi wa Yehova anapochagua mwenzi wa ndoa?

3 Ndoa ya Mukristo inapokuwa nzuri, hilo linafurahisha Mukristo huyo na jambo hilo linamuletea Yehova sifa. Lakini ikiwa mambo hayaendeki vizuri katika ndoa, jambo hilo linaumiza sana. Mukristo anayefikiria kufunga ndoa anapaswa kufuata uongozi wa Mungu ili ndoa yake iwe na musingi muzuri. Kwa upande mwingine, ikiwa mutu hachagui vizuri mwenzi wake wa ndoa, jambo hilo linaweza kumuvunja moyo na kumuletea taabu. Kwa mufano, vijana fulani wanaanza kuchumbiana wakati hawajakuwa tayari. Watu fulani wanapata muchumba kupitia Internet na hivyo wanaoa ao kuolewa haraka na kujikuta katika ndoa yenye matatizo mengi. Wengine wanatenda zambi nzito wakati wa uchumba lakini wanaamua tu kuoana, na hivyo wanaanza maisha yao ya ndoa bila kuheshimiana.

4 Wakristo wengine hawaolewi ao kuoa “katika Bwana tu,” na hilo linawaletea matatizo mengi kwa sababu mwenzi wao si Shahidi. (1 Kor. 7:39) Ikiwa uliangukia katika moja ya hali hizo, umuombe Mungu musamaha na musaada. Mungu habadili matokeo ya makosa ambayo mutu alifanya zamani, lakini mutu akitubu kwelikweli makosa yake, Yehova anaweza kumusaidia avumilie matatizo. (Zab. 130:1-4) Azimia kumupendeza Mungu tangu sasa na kuendelea, ukifanya hivyo ‘shangwe ya Yehova itakuwa ngome lako.’​—Neh. 8:10.

WAKATI NDOA INAKARIBIA KUVUNJIKA

5. Hata ikiwa ndoa yetu haina furaha, ni mawazo gani tunayopasa kuepuka?

5 Wale ambao mambo hayaendeki vizuri katika ndoa yao wanaweza kuanza kujiuliza: ‘Kwa nini nijisumbue kuiokoa ndoa hii isiyo na furaha? Labda nitakuwa vizuri ikiwa tu ninatafuta mwenzi mwengine na kuanza upya maisha yangu.’ Wanafikiri kama wanaweza kuachana na mwenzi wao na kuwa huru tena. Wanaweza kufikiri hivi: ‘Sababu gani nisivunje ndoa hii? Hata ikiwa hakuna sababu za Kimaandiko za kufanya hivyo, tunaweza kuachana ili nipate kufurahia tena maisha.’ Kuliko kuanza kuwaza-waza hivyo, na kufikiri kwamba hali ingekuwa vizuri zaidi ikiwa ungeishi na mutu mwengine, Wakristo wanapaswa kufanya yote wawezayo ili kutafuta uongozi wa Mungu katika hali yao.

6. Eleza yale ambayo Yesu alisema katika Mathayo 19:9.

6 Mukristo anaweza kuvunja ndoa yake na kuoa ao kuolewa tena ikiwa tu jambo hilo linaruhusiwa na maandiko. Yesu alisema hivi: ‘Mutu yeyote anayemutaliki muke wake na kumuoa mwingine, ila kwa sababu ya uasherati, anafanya uzinzi.’ (Mt. 19:9) Neno “uasherati” linatia ndani uzinifu na matendo mengine machafu ya ngono. Mbele ya kuamua kuvunja ndoa kwa sababu mwenzi amefanya uasherati, inafaa kwanza kusali kwa ajili ya jambo hilo na kufikiri kwa uzito.

7. Ikiwa Wakristo wanashindwa kuokoa ndoa yao, watu wengine wanaweza kuwaza nini?

7 Ikiwa ndoa yetu ina magumu, hilo linaweza kuonyesha kama hali yetu ya kiroho si nzuri. Mutume Paulo alitokeza ulizo hili la maana: ‘Kwa kweli ikiwa mutu yeyote hajui jinsi ya kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje kutaniko la Mungu?’ (1 Tim. 3:5) Kwa hiyo, ikiwa wenzi wawili wanaojidai kuwa Wakristo wanashindwa kuokoa ndoa yao, hilo linaweza kuwafanya watu wengine wawaze kama wenzi hao hawaishi kabisa kulingana na yale wanayohubiria wengine.​—Rom. 2:21-24.

8. Ikiwa wenzi wa ndoa walio Wakristo wanaamua kuachana, hilo linaweza kuonyesha nini?

8 Wakristo wanapofikiria kuachana ao kuvunja ndoa bila sababu za kimaandiko, hilo linaonyesha kama uhusiano wao na Yehova si muzuri. Tena hilo linaonyesha kama kuna kanuni fulani za Biblia ambazo mumoja wao hafuati ao wote wawili. Ikiwa wenzi hao ‘wanamutegemea kabisa Yehova kwa moyo wao wote,’ watafanya yote wawezayo ili kuiokoa ndoa yao.​—Soma Methali 3:5, 6.

9. Wakristo fulani walibarikiwa namna gani kwa sababu walifanya yote wawezayo ili kuiokoa ndoa yao?

9 Ndoa nyingi ambazo zilionekana kuwa zinakaribia kuvunjika zimebadilika na kuwa zenye furaha sana. Mara nyingi Wakristo ambao hawakuamua haraka kuachana na wenzi wao wa ndoa, ingawa matatizo yao, wamepata baraka nyingi. Fikiria yale yanayoweza kutokea katika familia iliyogawanyika kidini. Mutume Petro aliandika hivi: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.” (1 Pet. 3:1, 2) Unaona, mwenzi wa ndoa asiyeamini anaweza kuikubali kweli kwa sababu ya mwenendo muzuri wa mwenzi wake. Ndoa inayoponyoka kuvunjika inamuletea Mungu heshima na inaweza kuwa baraka kwa bwana, bibi na watoto.

10, 11. Ni matatizo gani yasiyotazamiwa yanayoweza kutokea katika ndoa, lakini Mukristo anaweza kutumainia musaada gani?

10 Ili kumupendeza Yehova, Wakristo wengi waseja wanaamua kufunga ndoa na Wakristo waliojitoa kwa Yehova na walio na imani kama yao. Hata hivyo, hali zisizotazamiwa zinaweza kutokea. Kwa mufano, mwenzi wa ndoa anaweza kupata magonjwa ya akili yenye kusumbua sana. Ao siku chache tu kisha kuoana, mwenzi wa ndoa anaweza kuregea katika kazi ya kuhubiri. Fikiria mufano wa Linda. * Dada huyo alikuwa Mukristo mwenye bidii na mama mwenye kuipenda familia yake. Alishangaa sana wakati bwana yake aliyekuwa ndugu mwenye kubatizwa, alijiingiza katika mwenendo mubaya na kwa kuwa hakutubu, alitengwa na ushirika. Mukristo ambaye anapatikana katika hali hiyo anaweza kuwaza kama ndoa yao haina tena tumaini. Basi ikiwa ni hivyo anaweza kufanya nini?

11 Labda unaweza kujiuliza: ‘Je, ni lazima niendelee kujisumbua hivi ili niiokoe ndoa yangu hata hali iwe namna gani?’ Uamuzi ni wako. Lakini, kuna sababu zinazopaswa kukufanya uendelee kubaki na mwenzi wako hata ikiwa inaonekana kuwa hali ni mbaya. Mungu anapendezwa sana na mwanaume ao mwanamuke anayevumilia matatizo katika ndoa kwa sababu zamiri yake haimuruhusu kuachana na mwenzi wake. (Soma 1 Petro 2:19, 20.) Kupitia Neno lake na roho yake, Yehova atamusaidia Mukristo anayejikaza kuiokoa ndoa yake yenye matatizo.

WAZEE WANAWEZA KUSAIDIA

12. Wazee watatuona namna gani ikiwa tunawaomba musaada?

12 Ikiwa ndoa yako ina matatizo, usisite kutafuta musaada wa Wakristo ambao wamekomaa kiroho. Wachungaji wa kundi la Mungu, yaani, wazee watafurahi kukutolea mashauri yaliyoongozwa na roho ya Mungu, yanayopatikana katika Biblia. (Mdo. 20:28; Yak. 5:14, 15) Usifikiri kama wewe na mwenzi wako mutazarauliwa na wazee kwa sababu munawaomba musaada ao kwa sababu munawaelezea matatizo yenu. Tofauti na hilo, wazee watawaheshimu zaidi kwa sababu wataona kama munapenda kabisa kumupendeza Mungu.

13. Ni shauri gani linalopatikana katika 1 Wakorintho 7:10-16?

13 Wakristo wanaoishi katika familia iliyogawanyika kidini wanapoomba wazee musaada, wazee wanaweza kutumia shauri hili la Paulo, aliyeandika: ‘Kwa watu waliofunga ndoa natoa maagizo, lakini si mimi bali ni Bwana, kwamba muke hapaswi kuondoka kwa mume wake; lakini kwa kweli akiondoka, na akae museja kama sivyo apatane tena na mume wake; na mume hapaswi kumuacha muke wake. Kwa maana, wewe muke, unajuaje kama utamuokoa mume wako? Ao, wewe mume, unajuaje kama utamwokoa muke wako?’ (1 Kor. 7:10-16) Inafurahisha sana wakati mwenzi asiye Shahidi anavutwa kwenye ibada ya kweli.

14, 15. Ni hali gani zinazoweza kuwafanya wenzi wa ndoa waachane, lakini kwa nini kusali sana juu ya jambo hilo na kufikiri kwa uzito ni kwa lazima?

14 Ni hali gani zinazoweza kumufanya dada Mukristo aachane na bwana yake? Dada fulani anaweza kuamua hivyo kwa sababu mwenzi amekataa kimakusudi kumupatia mahitaji yake ya kimwili. Wengine wamefanya hivyo kwa sababu waume wao wamewatendea vibaya sana kimwili hivi kwamba maisha yao yamekuwa katika hatari ao hali ya bwana imefanya hali ya kiroho ya dada iwe katika hatari.

15 Katika hali hizo, kuachana na mwenzi wa ndoa ao kubaki naye ni uamuzi wa pekee. Hata hivyo, ndugu ao dada anapaswa kusali sana juu ya jambo hilo na kulifikiria kwa uzito mbele ya kuchukua uamuzi wowote. Kwa mufano anaweza kujiuliza: Je, ni yule asiyeamini ndiye anahatarisha kabisa hali ya kiroho ya yule aliye Mukristo ao ni yule aliye Mukristo yeye mwenyewe ndiye amehatarisha hali yake ya kiroho kwa sababu amekuwa muvivu wa kujifunza Biblia, hahuzurie tena mikutano wala kuhubiri kwa ukawaida?

16. Ni jambo gani linaloweza kumuzuia ndugu ao dada asiamue haraka-haraka kuvunja ndoa?

16 Kwa kuwa tunaona uhusiano wetu pamoja na Mungu kuwa wa maana sana, na kwa kuwa tunafurahia na kuheshimu zawadi ya ndoa ambayo Mungu ametutolea, hatupaswi kuamua haraka-haraka kuvunja ndoa. Sisi ni watumishi wa Yehova, na kwa hiyo, hatupendi jina takatifu la Yehova litukanwe kwa sababu ya mwenendo wetu. Kwa hiyo, si vizuri kufanya mipango katika moyo wetu ya kuvunja ndoa kwa sababu moyo wetu umekwisha kupendezwa na mutu mwengine ili tuoane naye.​—Yer. 17:9; Mal. 2:13-16.

17. Ni wakati gani tunaweza kusema kama Mungu amewaita Wakristo waliooana kwenye amani?

17 Ndugu ao dada aliye na mwenzi asiyeamini anapaswa kujikaza kabisa ili ndoa yake isivunjike. Ikiwa amefanya namna yake yote ili kuiokoa ndoa hiyo na mwenzi asiyeamini anakataa kabisa kuishi pamoja naye, Mukristo hapaswi kujihukumu akifikiri kama ni kosa lake. Paulo aliandika hivi: “Lakini yule asiyeamini akiondoka, acha aondoke; ndugu au dada hayumo katika utumwa chini ya hali za namna hiyo, lakini Mungu amewaita ninyi kwenye amani.”​—1 Kor. 7:15. *

MUTUMAINI YEHOVA

18. Hata ikiwa umefanya yote ili ndoa yako isivunjike, lakini inafikia tu kuvunjika, kwa nini hatuwezi kusema kama umepoteza wakati wako bure?

18 Unapopambana na matatizo yoyote katika ndoa, umuombe Yehova akupe ujasiri na umutumainie siku zote. (Soma Zaburi 27:14.) Fikiria hali ya dada Linda, ambaye tulizungumuzia hapo mbele. Ijapokuwa kwa miaka mingi alifanya namna yake yote ili ndoa yao isivunjike, ilivunjika. Je, alifikiri kama alipoteza wakati wake? “Hapana.” Yeye anasema: “Nguvu nilizofanya ili kuokoa ndoa yetu ulikuwa ushahidi muzuri kwa wengine. Nilikuwa na zamiri safi. Zaidi ya yote, mambo yaliyopita katika miaka yote hiyo yalimusaidia binti yetu kubaki imara katika kweli. Alibatizwa na akawa Shahidi wa Yehova mwenye bidii.”

19. Matokeo yanaweza kuwa nini ikiwa mutu anajikaza kabisa kuiokoa ndoa yake?

19 Dada anayeitwa Marilyn alipata furaha kwa sababu alimutumaini Mungu na alijikaza sana kuiokoa ndoa yao. Yeye anasema: “Nilitaka kuachana na bwana yangu kwa sababu hakuwa tena akinipatia mahitaji yangu ya kimwili na hali yangu ya kiroho ilikuwa katika hatari. Hapo mbele bwana yangu alikuwa muzee wa kutaniko, kisha alianza kufanya biashara fulani isiyofaa. Alianza kukosa mikutano, na kisha hatukuwa tena tukizungumuza. Wateroriste walishambulia muji wetu, jambo hilo liliniogopesha sana hivi kwamba sikutaka tena kuwa ninaongea na watu. Kisha nikatambua kama mimi pia nilikuwa na kosa katika matatizo yetu. Tulianza tena kuongea, tukarudilia funzo letu la familia, na tukaanza tena kukusanyika kwa ukawaida. Wazee walitutendea kwa upole na walitusaidia sana. Ndoa yetu ikawa kama ni ndoa mupya. Kisha muda fulani, bwana yangu alipewa tena mapendeleo katika kutaniko. Tulipata fundisho, hata hivyo jambo hilo lilizaa matokeo mazuri.”

20, 21. Kuhusiana na ndoa, tunapaswa kuazimia kufanya nini?

20 Iwe sisi ni waseja ao tumefunga ndoa, acheni siku zote tutende kwa ujasiri na tumutumaini Yehova. Ikiwa tunapambana na matatizo katika ndoa, tunapaswa kufanya namna yetu yote ili kuyatatua, na tusisahau kama wale ambao wamefunga ndoa ‘si wawili tena, bali mwili mumoja.’ (Mt. 19:6) Tena tusisahau jambo hili: Ikiwa tunavumilia matatizo ya ndoa kwa sababu mwenzi wetu si Shahidi, tunaweza kupata furaha ya kumuvuta kwenye ibada ya kweli.

21 Hata tuwe katika hali gani, acheni tuazimie kuwa na mwenendo unaotolea ushahidi muzuri watu wasio Mashahidi. Ikiwa ndoa yetu iko karibu kuvunjika, tunapaswa kusali kwa bidii, kuchunguza nia yetu kwa uaminifu, kutafakari juu ya Maandiko, na kutafuta musaada wa kiroho kutoka kwa wazee. Zaidi ya yote, na tuazimie kumupendeza Yehova Mungu katika mambo yote na kuonyesha kabisa kwamba tunaheshimu zawadi nzuri ya ndoa.

[Maelezo ya chini]

^ Jina limebadilishwa.

^ Soma kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” ukurasa wa 219-221; Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 mwezi wa 11, 1988, ukurasa wa 26-27; tarehe 1 mwezi wa 1, 1976, ukurasa wa 31 (Kifaransa).

[Maulizo ya Funzo]

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 10]

Mara nyingi Wakristo ambao hawaamue haraka kuvunja ndoa wanapata baraka

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 12]

Tumaini Yehova siku zote na umuombe ujasiri

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yehova anawabariki wenzi Wakristo wanaojikaza kuokoa ndoa yao

[Picha katika ukurasa wa 11]

Kutaniko la Kikristo linaweza kufariji na kutoa musaada wa kiroho