Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitabu Chenye Upatano

Kitabu Chenye Upatano

“Unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.”​—2 PETRO 1:21.

BIBLIA INATOFAUTIANAJE NA VITABU VINGINE? Mara nyingi, hati za kale hazipatani hata iwe ziliandikwa wakati uleule.Vitabu ambavyo vimeandikwa na watu mbalimbali, wakiwa mahali tofauti, na wakati tofauti-tofauti huwa havipatani katika sehemu zote. Hata hivyo, Biblia inadai kwamba vitabu vyake vyote 66 vilitungwa na Mtu mmoja, hivyo vina ujumbe unaopatana.​—2 Timotheo 3:16.

MFANO: Musa, mchungaji aliyeishi katika karne ya 16 K.W.K., aliandika katika kitabu cha kwanza cha Biblia kwamba kuna “uzao” ambao ungekuja kuokoa wanadamu. Baadaye, kitabu hicho kilitabiri kwamba uzao huo ungetokana na ukoo wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo. (Mwanzo 3:15; 22:17, 18; 26:24; 28:14) Miaka 500 hivi baadaye, nabii Nathani alifunua kuwa uzao huo ungetokea katika ukoo wa kifalme wa Daudi. (2 Samweli 7:12) Miaka elfu moja baadaye, mtume Paulo alieleza kwamba uzao huo ungetia ndani Yesu na kikundi cha wafuasi wake waliochaguliwa. (Waroma 1:1-4; Wagalatia 3:16, 29) Hatimaye, kufikia mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., kitabu cha mwisho katika orodha ya Biblia kilitabiri kwamba washiriki wa ule uzao wangetoa ushahidi kumhusu Yesu duniani, wainuliwe hadi mbinguni, na kutawala pamoja naye kwa miaka 1,000. Uzao huo utamharibu Ibilisi na kuokoa wanadamu.​—Ufunuo 12:17; 20:6-10.

MAONI YA WACHAMBUZI WA BIBLIA: Baada ya kuchunguza kwa kina vitabu vyote 66 vya Biblia, Louis Gaussen aliandika kwamba alishangazwa na “upatano wa ajabu wa vitabu hivyo, ambavyo viliandikwa katika kipindi cha miaka 1,500 na waandikaji wengi, . . . ambao walijaribu kutimiza lengo moja, na wakaendelea kufunua mambo kwa utaratibu fulani, ingawa wao wenyewe hawakuelewa kwa ukamili, yaani, historia ya ukombozi wa ulimwengu kupitia Mwana wa Mungu.”​—Theopneusty—​The Plenary Inspiration of the Holy Scriptures.

UNA MAONI GANI? Je, Ungetazamia kitabu kilichoandikwa kwa kipindi cha zaidi ya miaka 1,500 na waandikaji tofauti-tofauti wapatao 40 kiwe na upatano kamili? Au je, Biblia ni kitabu cha kipekee?

“Maandishi haya yanapounganishwa, yanafanyiza kitabu kimoja . . . Hakuna kitabu kingine chochote ulimwenguni kinachoweza kulinganishwa nacho.”​—KITABU THE PROBLEM OF THE OLD TESTAMENT, CHA JAMES ORR