Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Coverdale na Biblia ya Kwanza Nzima Kuwahi Kuchapishwa Katika Kiingereza

Coverdale na Biblia ya Kwanza Nzima Kuwahi Kuchapishwa Katika Kiingereza

Coverdale na Biblia ya Kwanza Nzima Kuwahi Kuchapishwa Katika Kiingereza

BIBLIA nzima ya kwanza kuwahi kuchapishwa katika Kiingereza haikuwa na jina la mtu aliyeitafsiri. Mtafsiri huyo alikuwa Miles Coverdale, na tafsiri yake ilichapishwa mwaka wa 1535. Wakati huo, rafiki yake William Tyndale alikuwa amefungwa gerezani kwa sababu ya maandishi yake yaliyohusiana na kutafsiri Biblia. Tyndale aliuawa mwaka uliofuata.

Sehemu fulani ya tafsiri ya Coverdale ilitegemea maandishi ya Tyndale. Coverdale alifauluje kuchapisha tafsiri yake bila kuuawa, ilhali watafsiri wengine wa Biblia walikuwa wakiuawa kwa sababu ya kazi hiyo? Coverdale alitimiza nini?

Mbegu Zapandwa

Miles Coverdale alizaliwa huko Yorkshire, Uingereza. Inawezekana alizaliwa katika mwaka wa 1488. Alisomea katika Chuo Kikuu cha Cambridge na akatawazwa kuwa kasisi wa Kanisa Katoliki katika mwaka wa 1514. Tamaa yake ya kuleta marekebisho ilichochewa na mwalimu wake aliyeitwa Robert Barnes. Barnes alitoroka na kwenda barani Ulaya mwaka wa 1528. Miaka kumi na miwili baadaye viongozi wa kanisa walimfunga mtini na kumchoma mtu huyo aliyeunga mkono Marekebisho Makubwa ya Kidini.

Kufikia mwaka wa 1528, Coverdale alikuwa ameanza kuhubiri kanisani akipinga mazoea ya kikatoliki ambayo hayakupatana na maandiko kama vile kuabudu mifano, kutubu, na Misa. Kwa kuwa wakati huo uhai wake ulikuwa hatarini, alihama Uingereza na kwenda barani Ulaya, ambako aliishi kwa miaka saba hivi.

Akiwa Hamburg, Ujerumani, Coverdale aliishi na William Tyndale. Walishirikiana kwa sababu wote wawili walitamani kutokeza Biblia ambayo ingesomwa na watu. Katika kipindi hicho, Coverdale alijifunza mengi kutoka kwa Tyndale kuhusu mbinu ya kutafsiri Biblia.

Wakati wa Mabadiliko

Wakati huohuo, mambo yalikuwa yakibadilika huko Uingereza. Mwaka wa 1534, Mfalme Henry wa Nane aliasi mamlaka ya papa wa Kanisa Katoliki aliyekuwa Roma. Pia, alikubaliana na wazo la kuchapisha Biblia katika Kiingereza. Baada ya muda, Coverdale alianza kazi hiyo. Coverdale alijua Kiingereza vizuri sana lakini alikosa ustadi wa lugha ambao rafiki na mwalimu wake Tyndale, ambaye alijua vizuri Kiebrania na Kigiriki, alikuwa nao. Coverdale alifanyia marekebisho tafsiri ya Tyndale, akitumia tafsiri ya Kilatini na Kijerumani.

Biblia ya Coverdale ilichapishwa Barani Ulaya mwaka wa 1535, mwaka mmoja kabla ya Tyndale kuuawa. Ilitia ndani maneno ya heshima na ya kumfurahisha Mfalme Henry. Coverdale alimhakikishia Henry kwamba Biblia hiyo haikuwa na maelezo ya chini ya Tyndale, ambayo yangesababisha mabishano kwa kuwa, yalikazia mafundisho yasiyopatana na maandiko ya Kanisa Katoliki, na mambo mengine mengi. Hivyo, Henry alikubali Biblia hiyo ichapishwe. Mambo yalikuwa yameanza kubadilika.

Mnamo 1537, matoleo mawili ya Biblia ya Coverdale yalichapishwa, na wakati huu yalichapishwa huko Uingereza. Mwaka huohuo, tafsiri iliyoitwa Matthew’s Bible, ambayo ilikubaliwa na Mfalme Henry ilichapishwa huko Antwerp, na iliunganisha tafsiri za Tyndale na Coverdale.

Muda mfupi baadaye, Thomas Cromwell, ambaye alikuwa mshauri mkuu wa mfalme, akiungwa mkono na Cranmer, aliyekuwa Askofu Mkuu wa Canterbury, waliona kwamba kulikuwa na uhitaji wa kufanyia marekebisho tafsiri ya Matthew’s Bible. Hivyo, akamwomba tena Coverdale afanyie marekebisho maandishi hayo yote. Mfalme Henry aliidhinisha toleo hilo jipya katika mwaka wa 1539 na akaagiza kwamba nakala za toleo hilo lililoitwa Great Bible, yaani, Biblia kubwa kwa sababu ya ukubwa wake, ziwekwe makanisani ili watu wote wazisome. Watu wote nchini Uingereza waliipokea Biblia hiyo kwa shauku nyingi.

Mambo Ambayo Coverdale Alitimiza

Baada ya kifo cha Henry wa Nane na kutawazwa kwa Edward wa Sita, Coverdale aliwekwa rasmi kuwa askofu wa Exeter mwaka wa 1551. Hata hivyo, wakati Malkia Mary aliyekuwa Mkatoliki alipoanza kutawala baada ya Edward mwaka wa 1553, Coverdale alilazimika kukimbilia Denmark. Baadaye alihamia Uswisi, ambako aliendelea na kazi yake. Pia alichapisha matoleo matatu ya Kiingereza ya vitabu ambavyo kwa kawaida vinaitwa Agano Jipya, na matoleo hayo yalikuwa na maandishi ya Kilatini ili kuwasaidia makasisi kufanya utafiti.

Jambo lisilotazamiwa katika Biblia ya Coverdale ni kuondolewa kwa jina la Mungu, yaani, “Yehova.” Tyndale alitumia jina la Mungu zaidi ya mara 20 alipotafsiri Maandiko ya Kiebrania. Katika kitabu Coverdale and His Bibles, J.  F.  Mozley anasema hivi: “Katika mwaka wa 1535 Coverdale aliacha kutumia neno [Yehova] kabisa.” Hata hivyo, alitumia jina la Mungu, Yehova, mara tatu katika ile tafsiri ya Great Bible.

Ingawa hivyo, Biblia ya Coverdale ndiyo Biblia ya awali zaidi ya Kiingereza kuwahi kutumia Tetragramatoni—herufi nne za Kiebrania ambazo zinafanyiza jina la Mungu—kwenye kichwa cha ukurasa wake wa kwanza. Kwa kupendeza, hii ndiyo Biblia ya kwanza iliyounganisha vitabu vya Apokrifa kwenye kurasa za mwisho badala ya kuvichanganya na vitabu vya Maandishi ya Kiebrania.

Baadaye, misemo na maneno mengi ya kipekee yaliyotumiwa na Coverdale yalitumiwa na watafsiri wengine. Mfano mmoja ni usemi “bonde lenye kivuli kizito” ulio kwenye andiko la Zaburi 23, mstari wa 4. Profesa S. L. Greenslade, anasema “fadhili zenye upendo” kwenye mstari wa 6, ni “usemi wa pekee unaotofautisha upendo ambao Mungu anawaonyesha watu wake na upendo kwa ujumla na pia rehema.” Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures​—With References inatumia usemi huohuo, na kuongezea maelezo haya ya chini: “Au, ‘upendo mshikamanifu.’”

Tafsiri ya Great Bible ya Coverdale “ilikuwa mkusanyo wa maandishi yote yaliyotumiwa kutokeza Biblia ya Kiingereza . . . kuanzia wakati ambao Tyndale alianza kutafsiri Agano Jipya,” kinasema kitabu The Bibles of England. Jambo muhimu ni kwamba tafsiri ya Coverdale ndiyo iliyowawezesha watu waliozungumza Kiingereza walioishi wakati huo wasome Biblia.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Kushoto, herufi za tetragramatoni, zilizo kwenye ukurasa wa kwanza wa toleo la 1537

[Picha katika ukurasa wa 10]

From the book Our English Bible: Its Translations and Translators

[Picha Hisani katika ukurasa wa 11]

Photo source: From The Holy Scriptures of the Olde and Newe Testamente With the Apocripha by Myles Coverdale