Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Coverdale Alitafsiri Biblia Nzima ya Kwanza Katika Kiingereza

Coverdale Alitafsiri Biblia Nzima ya Kwanza Katika Kiingereza

Coverdale Alitafsiri Biblia Nzima ya Kwanza Katika Kiingereza

BIBLIA nzima ya kwanza iliyochapishwa katika Kiingereza haikuonyesha jina la mutu aliyeitafsiri. Lakini mutu huyo alikuwa Miles Coverdale, na tafsiri yake ilitokea katika mwaka wa 1535. Wakati huo, rafiki yake William Tyndale alikuwa mwenye kufungwa kwa sababu ya kazi yake ya kutafsiri Biblia. Mwaka wa 1536, Tyndale aliuawa.

Biblia ya Tyndale ilimusaidia Coverdale kutafsiri sehemu fulani za Biblia yake. Namna gani Coverdale aliweza kumaliza tafsiri yake mupaka kuichapisha bila kuuawa, ijapokuwa watafsiri wengine wa Biblia wa wakati wake walikuwa wakiuawa? Ni kazi gani zingine ambazo Coverdale alitimiza mwishowe?

Kazi Inaanzishwa

Miles Coverdale alizaliwa Yorkshire, huko Angleterre, inawezekana katika mwaka wa 1488. Alisomea kwenye Université ya Cambridge na alifanywa kuwa padiri wa kanisa Katoliki la Roma mwaka wa 1514. Robert Barnes, mwalimu wake, ndiye aliyemuchochea kuleta mabadiliko katika kanisa Katoliki. Katika mwaka wa 1528, Barnes alitoka Angleterre na kukimbilia katika inchi nyingine ya Ulaya. Miaka 12 kisha hapo, viongozi wa kanisa wakamuua Barnes kwa kumuunguza kwenye muti.

Katika mwaka wa 1528 hivi, Coverdale alikuwa ameanza kuhubiri katika kanisa ili kupinga mazoea ya kanisa Katoliki yasiyopatana na Maandiko, kwa mufano, kuabudu sanamu, kuungama zambi, na Misa. Kwa sababu maisha yake yalikuwa katika hatari, Coverdale naye akatoka Angleterre na kukimbilia katika inchi nyingine ya Ulaya, ambamo aliishi miaka karibu 7.

Coverdale aliishi pamoja na William Tyndale huko Hamburg, katika Allemagne. Wote wawili wakatumika pamoja kwa sababu walitaka kutafsiri Biblia ambayo ingesomwa na watu wote. Wakati huo, Tyndale alimufundisha Coverdale mambo mengi juu ya ufundi wa kutafsiri Biblia.

Hali Inaanza Kubadilika

Wakati huo hali ilianza kubadilika huko Angleterre. Katika mwaka wa 1534, Mufalme Henry VIII alipinga waziwazi mamlaka ya papa wa kanisa Katoliki la Roma. Yeye pia aliunga mukono wazo la kusaidia watu wapate kusoma Biblia katika Kiingereza. Mwaka huo, Coverdale alianza tena kazi. Coverdale alielewa vizuri maneno ya Kiingereza lakini hakuwa kama mwalimu na rafiki yake Tyndale ambaye alielewa sana Kiebrania na Kigiriki. Kwa kutumia tafsiri ya Kilatini na Kijeremani, Coverdale alisahihisha tafsiri ya Tyndale.

Biblia ya Coverdale ilichapishwa katika Ulaya mwaka wa 1535, mwaka mumoja mbele Tyndale auawe. Katika Biblia ya Coverdale, mulikuwa maneno ya heshima, ya kumusifusifu Mufalme Henry. Coverdale alimuhakikishia Mufalme Henry kama, katika Biblia yake, yeye aliondoa maelezo ya chini yaliyokuwa katika Biblia ya Tyndale. Maelezo hayo yalikuwa yakileta mabishano kwa sababu nyingi. Kwa mufano, yalikazia mafundisho ya Kanisa Katoliki yasiyopatana na Maandiko. Kwa hiyo, Mufalme Henry akakubali Biblia hiyo ichapishwe na kugawanyiwa watu. Hali ilikuwa imeanza kubadilika.

Katika mwaka wa 1537, Biblia ya Coverdale ilichapishwa katika matoleo mawili mapya huko Angleterre. Katika mwaka huohuo, tafsiri inayoitwa Biblia ya Matthew iliyochapishwa huko Anvers ilikubaliwa na Mufalme Henry. Biblia hiyo ilitafsiriwa kutokana na tafsiri ya Tyndale na ya Coverdale.

Thomas Cromwell, mushauri mukubwa wa mufalme, aliyeungwa mukono na Cranmer, Askofu mukubwa wa kanisa la huko Canterbury, aliwaza mara moja kama ilikuwa lazima kusahihisha Biblia ya Matthew. Kwa hiyo, akamuomba tena Coverdale asahihishe Biblia hiyo yote nzima. Katika mwaka wa 1539, Mufalme Henry akakubali kazi hiyo ifanywe na akaomba tafsiri hiyo mupya itiwe katika makanisa ili watu wote waisome. Tafsiri hiyo iliitwa Great Bible (Biblia Kubwa) kwa sababu ilikuwa kubwa. Watu walifurahia sana Biblia hiyo mahali pote katika inchi.

Uriti wa Coverdale

Coverdale alifanywa kuwa askofu wa Exeter katika mwaka wa 1551, wakati wa utawala wa Edward VI aliyechukua nafasi ya Mufalme Henry VIII kisha kifo chake. Lakini, katika mwaka wa 1553, Mufalme Mwanamuke Mukatoliki anayeitwa Mary alianza kutawala mahali pa Edward, kwa hiyo, Coverdale alilazimika kukimbilia huko Danemark. Kisha hapo, Coverdale akahamia huko Suisse, ambako aliendelea kufanya kazi yake. Tena akachapisha tafsiri tatu za Kiingereza za ile inayoitwa na watu wengi Agano Jipya, ambazo zilikuwa pia na maandishi ya Kilatini ili kuwasaidia mapadiri Wakatoliki kujifunza maandiko.

Jambo moja lenye kushangaza lililoonekana katika Biblia ya Coverdale ni kwamba aliliondoa jina la Mungu “Yehova” katika tafsiri yake ya Biblia. Lakini Tyndale alitumia jina la Mungu zaidi ya mara 20 katika tafsiri yake ya Maandiko ya Kiebrania. Katika kitabu chake (Coverdale and His Bibles), James Frederic Mozley anasema hivi: “Katika mwaka wa 1535 Coverdale alikataa kabisa neno [Yehova].” Lakini, baadaye alitumia jina Yehova mara tatu katika tafsiri inayoitwa Great Bible (Biblia Kubwa).

Hata hivyo, kwenye ukurasa wa kwanza, Biblia ya Coverdale ilionyesha herufi ine za Kiebrania (YHWH) zinazounda jina la Mungu. Hiyo ndiyo Biblia ya kwanza ya Kiingereza iliyofanya hivyo. Jambo la maana zaidi, Biblia hiyo ndiyo ilikuwa ya kwanza kukusanya pamoja vitabu vya apokrifa (vitabu ambavyo havikuongozwa na roho) katika nyongeza kuliko kuvichanga pamoja na vitabu vya Maandiko ya Kiebrania.

Kisha watafsiri wengine walitumia maneno mengi ya pekee ya Coverdale katika tafsiri zao. Mufano mumoja wa jambo hilo ni maneno “bonde la kivuli cha mauti” yanayopatikana katika Zaburi 23, mustari wa 4. Profesere Greenslade anasema kama neno ‘fazili zenye upendo’ linalotumiwa katika mustari wa 6 ni “neno la pekee linalotofautisha upendo wa Mungu kwa watumishi wake na upendo wake kwa watu wote na rehema.” Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatumia maneno hayohayo, na kwenye maelezo ya chini (katika Kifaransa) inaongeza: “Ao, ‘upendo mushikamanifu.’”

Kitabu kimoja (The Bibles of England) kinasema kama Biblia ya Coverdale inayoitwa Great Bible “ndiyo Biblia iliyotafsiriwa vizuri kabisa kuliko tafsiri zingine zote za Biblia ya Kiingereza . . . tangu wakati Tyndale alianza kutafsiri Agano Jipya.” Kwa kweli, tafsiri ya Coverdale ndiyo iliyofanya watu wanaozungumuza Kiingereza, katika siku hizo, wasome Biblia katika luga yao.

[Maneno ili kueleza mahali picha ilitokea, ukurasa wa 10]

Picha hii ilichukuliwa katika kitabu Our English Bible: Its Translations and Translators

[Picha katika ukurasa wa 11]

Kushoto, herufi ine zinazounda jina la Mungu, zilionekana kwenye ukurasa wa kwanza wa tafsiri ya 1537

[Maneno ili kueleza mahali picha ilitokea, ukurasa wa 11]

Picha hizi zilichukuliwa katika The Holy Scriptures of the Olde and Newe Testamente With the Apocripha by Myles Coverdale