Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yehova Amenifungua Macho

Yehova Amenifungua Macho

Yehova Amenifungua Macho

Patrice Oyeka anaeleza maisha yake

Siku moja mangaribi, niliamua kujiua. Siku hiyo nilikuwa katika hali ya kuvunjika moyo sana. Nilijisikia kuwa peke yangu na jambo ambalo ningeweza kufanya tu ni kusikiliza radio; kwa sababu nilikuwa kipofu. Basi, nikatia sumu katika kopo ya maji na nikatia kopo hiyo kwenye meza iliyokuwa mbele yangu. Mbele ya kunywa sumu na kufa, niliona vizuri nioge maji kwa mara ya mwisho na kuvaa vizuri. Sababu gani nilitaka kujiua? Ni nini iliyonisaidia ili nibaki muzima mupaka leo na kueleza habari hii?

NILIZALIWA tarehe 2 mwezi wa 2, 1958, katika jimbo la Kasaï Oriental, Congo Kinshasa. Baba yangu alikufa nilipokuwa na miaka 9, na kwa hiyo, ndugu yangu mukubwa akanikomalisha.

Nilipomaliza masomo, nilipata kazi kwenye shamba kubwa la miti inayotoa caoutchouc. Asubuhi moja katika mwaka wa 1989, nilipokuwa nikiandika ripoti katika biro yangu, mara moja nikajikuta katika giza kubwa. Kwanza, niliwaza kama umeme (courant) ulikatwa, lakini niliendelea kusikia mungurumo wa groupe électrogène na tena ilikuwa asubuhi! Niliogopa sana kwa sababu singeweza kuona tena kitu chochote, hata karatasi zilizokuwa mbele yangu!

Mara moja, nikaita mufanyakazi mumoja kati ya wale niliokuwa nikiongoza ili anipeleke kwa muganga aliyekuwa akitunza wafanyakazi wote. Muganga huyo akanituma kwa muganga mwingine mwenye uzoefu katika muji. Muganga huyo alipoona kama macho yangu yalikuwa yamekufa kabisa, na kama hangeweza kufanya lolote, naye pia akanituma katika muji wa Kinshasa ili nionane na waganga wenye uzoefu zaidi.

Maisha Yangu Kinshasa

Huko Kinshasa, nilionana na waganga wengi wa macho, lakini hakuna hata mumoja aliyeweza kuniponyesha. Kisha siku 43 katika hospitali, waganga wa macho wakaniambia kama nitabakia kipofu muda wa maisha yangu yote! Kwa hiyo, watu wa familia yangu wakanipeleka kwenye makanisa mbalimbali ili kuona ikiwa ningeweza kuponyeshwa kwa njia ya muujiza, lakini haikuwezekana.

Mwishowe, sikuwa tena na tumaini lolote, na nikavunjika moyo sana. Sasa nilikuwa kipofu, na nilipoteza kazi yangu. Na bibi yangu alinikimbia na akabeba vitu vyote tulivyokuwa navyo nyumbani. Nilianza kusikia haya ya kutoka nyumbani na sikutaka tena kukutana na watu. Basi nikajitenga na watu na nikaanza kubaki tu nyumbani. Nilijisikia kuwa peke yangu na nilijiona kuwa mutu asiyefaa kitu.

Nilijaribu kujiua mara mbili. Mara ya pili ndiyo inayozungumuziwa mwanzoni mwa habari hii. Ni mutoto mudogo wa jamaa yangu ndiye aliyeniokoa. Namna gani? Nilipokuwa nikioga, mutoto huyo alikamata kopo iliyokuwa na sumu na kuimwanga sumu hiyo bila yeye kujua kama ni sumu. Jambo la kufurahisha ni hili: Mutoto huyo hakukunywa sumu hiyo. Lakini nilihuzunika sana kwa sababu sikuweza tena kupata kopo hiyo. Nilipoikosa, nikajulisha watu wa familia yangu sababu gani nilikuwa nikiitafuta na jambo ambalo nilitaka kufanya.

Ninamushukuru Mungu sana na watu wa jamaa yangu kwa sababu walinihangaikia; na kwa hiyo sikuweza tena kujiua.

Nilipata Tena Furaha Katika Maisha

Siku ya Yenga moja katika mwaka wa 1992, nilipokuwa mwenye kukaa nyumbani nikivuta sigareti yangu, Mashahidi wa Yehova wawili waliokuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba walifika nyumbani. Walipoona kama mimi ni kipofu, walinisomea andiko la Isaya 35:5: “Wakati huo macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa.” Nilifurahi sana niliposikia maneno hayo! Tofauti na mambo waliyoniambia katika makanisa, Mashahidi hao hawakusema kama wanaweza kuniponyesha kwa njia ya muujiza. Lakini, walinifasiria kama nikijifunza kumujua Mungu, ninaweza kuona tena katika dunia mupya iliyoahidiwa na Mungu. (Yohana 17:3) Bila kukawia, nikaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, kwa kutumia kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Tena, nikaanza kuhuzuria mikutano yote ya Mashahidi wa Yehova kwenye Jumba la Ufalme na nikafanya mabadiliko katika maisha yangu. Na nikaacha kuvuta sigareti.

Lakini sikufanya maendeleo ya kiroho haraka kwa sababu ya kuwa kipofu. Kwa hiyo, nikaenda kwenye masomo ya vipofu ili kujifunza maandishi ya vipofu. Kujua maandishi ya vipofu kuliniwezesha nianze kufanya vipindi katika Jumba la Ufalme kwenye Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi. Bila kukawia, nikaanza kuhubiria majirani. Hivyo, nilianza kupata tena furaha katika maisha. Niliendelea kufanya maendeleo ya kiroho na nikajitoa kwa Yehova. Nikabatizwa tarehe 7 mwezi wa 5, 1994.

Kadiri upendo wangu kwa Yehova na kwa majirani ulivyokomaa, nikaanza kuwa na tamaa ya kuanza utumishi wa wakati wote. Kwa hiyo, nikaanza kazi ya upainia wa kawaida tarehe 1, mwezi 12, mwaka wa 1995. Tena, nimekuwa muzee wa kutaniko tangu mwezi wa 2, mwaka wa 2004. Wakati fulani, ninaalikwa ili kutoa hotuba za watu wote katika makutaniko jirani. Baraka hizo zote zinaniletea furaha kubwa na zinanisaidia kukumbuka kama hakuna ulemavu wowote unaoweza kutuzuia kumutumikia Yehova Mungu.

Yehova Amenipatia “Macho”

Katika habari hii, nimeeleza kama bibi yangu alinikimbia kwa sababu ya kuwa kipofu. Lakini Yehova amenipatia baraka nyingine; ninaweza kusema kama amenipatia macho. Macho hayo ni Anny Mavambu, aliyekubali niwe bwana yake ijapokuwa mimi ni kipofu. Kwa sababu yeye pia ni painia wa kawaida, ananisindikiza kwenye mahubiri sikuzote. Na tena ananisomea hotuba ambazo nitatoa ili niziandike katika maandishi ya vipofu. Anny ni baraka kwangu kabisa. Kupitia yeye, nimeona kama maneno ya andiko la Methali 19:14 ni ya kweli. Andiko hilo linasema hivi: ‘Uriti kutoka kwa baba ni nyumba na mali, lakini muke mwenye busara anatoka kwa Yehova.’

Tena, Yehova ametubariki kwa kutupatia watoto wawili; mumoja mwanaume na mwingine mwanamuke. Ninangojea kwa hamu kuona sura za watoto wangu katika Paradiso! Baraka nyingine ni hii: Ndugu yangu mukubwa anayeturuhusu tuishi katika nyumba yake amekubali kweli na yeye ni mwenye kubatizwa! Sisi wote tuko katika kutaniko moja.

Ninapofikiri juu ya baraka hizo zote, ninachochewa kumutumikia Yehova hata zaidi ijapokuwa mimi ni kipofu. (Malaki 3:10) Kila siku, ninasali Ufalme wake uje ili kumaliza mateso yote duniani. Tangu nilipomujua Yehova, ninaweza kusema kwa moyo wote: ‘Baraka ya Yehova​—hiyo ndiyo inatajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.’​—Methali 10:22.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Picha ya kwanza: Ninatoa hotuba; Ya pili: Mimi pamoja na familia yangu na mukubwa yangu