Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mkaribie Mungu

‘Nafsi Yako Itainama Juu Yangu’

‘Nafsi Yako Itainama Juu Yangu’

UNYENYEKEVU ni sifa yenye kuvutia. Mara nyingi sisi tunajihisi huru kuwakaribia watu wanyenyekevu. Hata hivyo, inasikitisha kwamba leo ni vigumu kupata watu wenye unyenyekevu wa kweli, hasa watu wenye nguvu na mamlaka kuliko wengine. Vipi kumhusu Yehova Mungu ambaye ana nguvu zaidi kuliko mtu yeyote yule? Je, Yeye ni mnyenyekevu? Acheni tuchunguze maneno ya nabii Yeremia yanayopatikana katika andiko la Maombolezo 3:20, 21.​—Soma.

Yeremia aliandika kitabu cha Maombolezo katika kipindi ambacho taifa la Israeli lilikuwa likikabili hali ngumu. Alikuwa tu ametoka kushuhudia jambo lililomhuzunisha sana—uharibifu wa jiji alilolipenda la Yerusalemu uliotekelezwa na Wababiloni. Nabii huyo mwenye huzuni, alijua kwamba msiba huo ulikuwa hukumu ya haki kutoka kwa Mungu kuelekea Waisraeli kwa sababu ya mwenendo wao wenye dhambi. Lakini je, Yeremia hakuwa na tumaini lolote? Je, alihisi kwamba Yehova alikuwa mbali au asiyeweza kufikika hivi kwamba asitambue watu wake waliotubu na kuwainua kutoka katika hali hiyo yenye kuhuzunisha? Sikiliza Yeremia anapoongea kwa niaba ya watu wake.

Ingawa watu wengi wana huzuni, Yeremia ana tumaini kwelikweli. Anamlilia Yehova akisema: “Hakika nafsi yako * [Yehova mwenyewe] itakumbuka na kuinama juu yangu.” (Mstari wa 20) Yeremia hana shaka kabisa. Anajua kwamba Yehova hatamsahau yeye, wala watu Wake wanaotubu. Hata hivyo Mungu mweza-yote atachukua hatua gani?—Ufunuo 15:3.

Yeremia ana hakika kwamba Yehova ‘atainama’ juu ya wale wanaotubu kikweli. Tafsiri nyingine zinasema hivi: “Ee unikumbuke, na kujishusha chini kwangu.” Maneno hayo yanatusaidia kumwona Yehova kuwa mwenye fadhili. Yehova ‘aliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote,’ atajishusha chini katika njia ya mfano, na kuwainua waabudu wake kutoka katika hali yao mbaya na kuwakubali tena. (Zaburi 83:18) Kwa sababu ya kuimarishwa na tumaini hilo, Yeremia anapata faraja ya kweli kwa moyo wake uliokuwa umehuzunika. Nabii huyo mwaminifu ameazimia kungoja kwa subira hadi wakati unaofaa wa Yehova atakapowakomboa watu Wake wanaotubu.​—Mstari wa 21.

Maneno ya Yeremia yanatufundisha mambo mawili kumhusu Yehova. Kwanza, yeye ni mnyenyekevu. (Zaburi 18:35) Ingawa “ameinuliwa katika nguvu,” Yehova yuko tayari kujishusha katika kiwango chetu, kwa njia ya mfano, ili atusaidie tunapovunjika moyo. (Ayubu 37:23; Zaburi 113:5-7) Kwa kweli, hilo ni jambo linalofariji kama nini! Pili, Yehova ni mwenye rehema; yuko “tayari kusamehe” watu wanaotubu na kuwakubali tena. (Zaburi 86:5) Sifa hizo mbili, yaani, unyenyekevu na rehema, zinahusiana sana.

Tunashukuru kama nini kwamba Yehova si kama watawala wa kibinadamu, ambao kwa sababu ya kiburi hawawezi kujishusha chini na hawajali wengine! Je, huchochewi kujifunza mengi zaidi kumhusu Mungu mwenye unyenyekevu ambaye yuko tayari “kujishusha chini” ili kuwainua waabudu wake kutoka katika hali ya huzuni na kuwapa tumaini?

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Juni:

Yeremia 51-52; Maombolezo 1-5Ezekieli 1-5

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Waandishi wa kale walibadili andiko hilo kuwa “nafsi yangu,” kana kwamba linamrejelea Yeremia. Ni wazi waliamini kwamba ni ukosefu wa heshima kumrejelea Mungu kuwa nafsi, neno ambalo Biblia inatumia kumaanisha viumbe walio duniani. Lakini mara nyingi Biblia inaeleza kumhusu Mungu katika njia ambayo wanadamu wanaweza kuelewa. Kwa sababu neno “nafsi” linaweza kumaanisha “uhai wetu,” hivyo basi maneno “nafsi yako” linamaanisha “wewe.”

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Yehova yuko tayari kujishusha katika kiwango chetu, kwa njia ya mfano, ili atusaidie tunapovunjika moyo