Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Wanahubiri Nyumba kwa Nyumba?

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Wanahubiri Nyumba kwa Nyumba?

▪ Katika Biblia tunasoma amri hii ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha.” (Mathayo 28:19, 20) Je, amri hiyo inawahusu Wakristo wote? Wanafunzi wa mapema wa Yesu walielewa kwamba iliwahusu Wakristo wote. Kwa mfano, mtume Petro alisema: “[Yesu] alituagiza sisi tuwahubirie watu na kutoa ushahidi kamili.” (Matendo 10:42) Naye mtume Paulo akaandika: “Nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sitangazi habari njema!”—1 Wakorintho 9:16.

Si Paulo na Petro tu bali pia Wakristo wa karne ya kwanza kwa ujumla walitii amri ya Yesu. Kazi ya kuhubiri ilikuwa muhimu zaidi kwao. (Matendo 5:28-32, 41, 42) Leo, Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kufanya hivyo pia. Wanahubiri ujumbe uleule ambao Yesu alihubiri, yaani, “ufalme wa mbinguni.”—Mathayo 10:7.

Ni nani wanaopaswa kuhubiriwa ujumbe wa Ufalme? Yesu alisema kwamba ujumbe huo unapaswa kuhubiriwa watu wote kila mahali. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Hata alitabiri kwamba kabla ya mwisho wa mfumo huu kufika, “hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi.” (Mathayo 24:14) Kwa sababu hiyo, Wakristo wa karne ya kwanza walijitahidi kuzungumza na watu wote, hawakuwahubiria tu watu waliowajua au watu wasio na dini. (Wakolosai 1:23; 1 Timotheo 2:3, 4) Vivyo hivyo leo, Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kuzungumza na kila mtu. *

Ni njia gani yenye matokeo zaidi ya kueneza ujumbe wa Ufalme? Yesu, ambaye alijua jinsi ya kuwafikia watu wengi iwezekanavyo, aliwatuma wanafunzi wake kwenye majiji, vijiji, na nyumba za watu. (Mathayo 10:7, 11, 12) Baada ya Yesu kufa na kufufuliwa, wanafunzi wake waliendelea kuhubiri “nyumba kwa nyumba.” (Matendo 5:42) Kama alivyofanya Yesu, walihubiri pia popote ambapo waliwapata watu na katika maeneo ya umma. (Yohana 4:7-26; 18:20; Matendo 17:17) Leo, Mashahidi wa Yehova wanatumia njia hizohizo kuwahubiria watu wote.

Yesu alisema kwamba si kila mtu angesikiliza. (Mathayo 10:14; 24:37-39) Je, hilo linapaswa kuwazuia Wakristo kuhubiri? Fikiria ulinganisho huu: Ikiwa ulikuwa katika kikundi cha waokoaji baada ya tetemeko kubwa la ardhi, je, ungeacha kutafuta watu walioathiriwa kwa sababu tu baada ya muda ni watu wachache wanaookolewa? Hapana, ungeendelea mradi tu kuna matumaini ya kumwokoa mtu fulani. Yesu aliwaagiza wanafunzi wake waendelee na kazi mradi tu kuna matumaini kwamba mtu fulani atakubali habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu. (Mathayo 10:23; 1 Timotheo 4:16) Kwa kuwatafuta watu kama hao nyumba kwa nyumba, Mashahidi wa Yehova wanaonyesha upendo wao kwa Mungu na kwa jirani zao, ambao wataokolewa ikiwa watasikiliza na kutii ujumbe wa Ufalme.—Mathayo 22:37-39; 2 Wathesalonike 1:8.

Gazeti hili lina ujumbe huo wa Biblia. Ili upate habari zaidi, tafadhali zungumza na Mashahidi wa Yehova watakapokutembelea, au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kufikia sasa, Mashahidi wa Yehova wanahubiri katika nchi 236. Mwaka jana, walitumia saa bilioni 1.7 katika kazi ya kuhubiri na wakaongoza mafunzo ya Biblia milioni 8.5 ulimwenguni pote.