Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupambana Sana kwa Ajili ya Habari Njema Huko Thesalonike

Kupambana Sana kwa Ajili ya Habari Njema Huko Thesalonike

Kupambana Sana kwa Ajili ya Habari Njema Huko Thesalonike

Jiji la Thesalonike, ambalo leo linaitwa Thessaloníki au Salonika, ni jiji lenye bandari linalositawi sana. Jiji hilo liko kaskazini-mashariki mwa Ugiriki. Jiji la Thesalonike lilitimiza sehemu muhimu katika historia ya Wakristo wa karne ya kwanza, hasa kuhusiana na huduma ya Paulo, mtume Mkristo kwa mataifa.​—MATENDO 9:15; WAROMA 11:13.

KARIBU mwaka wa 50 W.K., Paulo na mwandamani wake Sila walifika Thesalonike. Walikuwa katika safari ya pili ya Paulo ya umishonari. Hiyo iliwapa fursa ya kupeleka habari njema kumhusu Kristo katika eneo ambalo leo ni bara Ulaya.

Bila shaka, walipofika Thesalonike, bado walikuwa wakikumbuka jinsi walivyopigwa na kufungwa huko Filipi, jiji kuu la Makedonia. Hata baadaye Paulo aliwaambia Wathesalonike kwamba alipowatembelea alikuwa akiwahubiria “habari njema ya Mungu kwa kupambana sana.” (1 Wathesalonike 2:1, 2) Je, hali katika jiji la Thesalonike ingekuwa nzuri kwao? Huduma yao ingekuwaje katika jiji hilo? Je, ingekuwa na matokeo mazuri? Kwanza, acheni tuchunguze jiji hilo la kale.

Jiji Lenye Historia ya Machafuko

Jina lenyewe Thesalonike, ambalo linatokana na maneno mawili ya Kigiriki yanayomaanisha “wakaaji wa Thessaly” na “ushindi,” linarejelea mapambano na vita. Watu wengi wanaamini kwamba katika mwaka wa 352 K.W.K., Filipo wa Pili, Mfalme wa Makedonia ambaye pia ni baba ya Aleksanda Mkuu, alishinda kabila fulani kutoka Ugiriki ya kati katika eneo la Thessaly. Inasemekana kwamba katika kumbukumbu ya ushindi huo, aliamua kumpa mmoja wa binti zake jina Thessalonice. Binti huyo alikuja kuolewa na Kasanda, ambaye alitawala baada ya Aleksanda, kaka ya binti huyo. Karibu mwaka wa 315 K.W.K., Kasanda alijenga jiji katika upande wa magharibi ya Rasi ya Chalcidice na kulipa jiji hilo jina la mke wake. Kulingana na historia ya Thesalonike, jiji hilo lilikabiliwa na mapigano mara kwa mara.

Pia, jiji la Thesalonike lilikuwa na mafanikio mengi. Jiji hilo lilikuwa na mojawapo ya bandari nzuri za kiasili katika Bahari ya Aegea. Vilevile, katika nyakati za Waroma, barabara maarufu inayoitwa Via Egnatia ilipitia katika jiji hilo. Kwa sababu Thesalonike lilikuwa katika eneo lenye bahari na barabara kuu, jiji hilo lilikuwa mojawapo ya maeneo muhimu ya kufanyia biashara na mataifa mengine katika Milki ya Roma. Kwa muda mrefu, jiji hilo lenye mafanikio lilikuwa likitamaniwa sana na Wagothi, Waslavi, Wafranki, wenyeji wa Venice, na Waturuki. Wengine wao waliteka eneo hilo kwa nguvu na kukawa na umwagaji damu. Lakini sasa acheni tukazie fikira ziara ya Paulo, hasa wakati mapambano kwa ajili ya habari njema yalipoanza.

Paulo Awasili Thesalonike

Kwa kawaida Paulo alipofika katika jiji, alikuwa akianza kuzungumza na Wayahudi kwa sababu walifahamu Maandiko na hivyo angeweza kuyatumia katika mazungumzo yake na kuwasaidia kuelewa habari njema. Msomi fulani anadokeza kwamba huenda Paulo alifanya hivyo kwa kuwa aliwajali sana watu wa nchi yake au alitaka kuwatumia Wayahudi na watu waliomwogopa Mungu ili kuanza kazi yake ya kuwafikia Watu wa Mataifa.​—Matendo 17:2-4.

Hivyo alipofika Thesalonike, Paulo aliingia katika sinagogi, na “akajadiliana nao [Wayahudi] kwa kutumia Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na kufufuliwa kutoka kwa wafu, akisema: ‘Huyu ndiye Kristo, Yesu huyu ninayewatangazia ninyi.’”​—Matendo 17:2, 3, 10.

Jambo ambalo Paulo alizungumzia, yaani, daraka la Masihi na utambulisho wake, lilikuwa jambo lililokuwa likibishaniwa. Wayahudi walitazamia Masihi ambaye angewakomboa kutoka kwa utawala wa Waroma, hivyo kuteseka kwa Masihi kulikuwa kinyume cha matarajio yao. Ili afaulu kuwashawishi Wayahudi, Paulo ‘alijadiliana,’ ‘akaeleza,’ na ‘kuthibitisha kwa kurejelea’ Maandiko—mbinu inayotumiwa na mwalimu mwenye ustadi. * Lakini wasikilizaji wa Paulo waliitikiaje alipokuwa akiwafundisha mambo hayo mazuri?

Walipitia Hali Ngumu Lakini Wakapata Matokeo Mazuri

Wayahudi fulani na wageuzwa-imani wengi Wagiriki na pia “si wachache kati ya wanawake wenye vyeo,” walikubali ujumbe wa Paulo. Usemi “wanawake wenye vyeo” ulifaa sana, kwa sababu wanawake huko Makedonia walikuwa na vyeo katika jamii. Walikuwa na vyeo katika ofisi za serikali, walimiliki mali, na kufurahia haki fulani za kijamii, na wakajihusisha na biashara. Hata walijengewa minara ya ukumbusho ili kuwaonyesha heshima. Kama vile tu mwanamke aliyeitwa Lidia, mfanyabiashara Mfilipi alivyokubali habari njema, pia kulikuwa na itikio zuri kutoka kwa wanawake Wathesalonike wenye vyeo vya juu, huenda walikuwa wanawake kutoka kwa familia za kitajiri au wake wa watu waliokuwa maarufu.​—Matendo 16:14, 15; 17:4.

Hata hivyo, Wayahudi walijawa na wivu. Wakawakusanya “wanaume fulani waovu kati ya wazururaji wa sokoni na kufanyiza kikundi chenye ghasia ili kuzusha fujo jijini.” (Matendo 17:5) Hao walikuwa watu wa aina gani? Msomi mmoja wa Biblia anaeleza kwamba “walikuwa watu waovu na wasiofaa kitu.” Anaongeza hivi: “Inaonekana kwamba hawakupendezwa kwa njia yoyote ile na ujumbe wa Paulo; lakini kama vile tu kikundi chenye ghasia, watu hao walisisimuka haraka, na kuchochewa kujihusisha na matendo ya fujo.”

Kikundi hicho chenye fujo ‘kikaishambulia nyumba ya Yasoni [aliyekuwa amemkaribisha Paulo] na kuanza kujaribu kuwaleta mbele ya watu wenye kufanya ghasia.’ Kwa sababu hawakumpata Paulo, walianza kutafuta usaidizi kutoka kwa watawala wa kuu zaidi wa jiji. Hivyo “wakamkokota Yasoni na akina ndugu fulani na kuwapeleka kwa watawala wa jiji, wakipaaza sauti hivi: ‘Watu hawa ambao wameipindua dunia inayokaliwa wapo hapa pia.’”​—Matendo 17:5, 6.

Kwa sababu lilikuwa ndilo jiji kuu la Makedonia, jiji la Thesalonike lilikuwa likijitawala kwa kadiri fulani. Sehemu ya mamlaka yake ilikuwa ni baraza la watu au baraza la wananchi ambalo lilishughulikia matatizo ya watu. “Watawala wa jiji,” au mapolitaki, * walikuwa maofisa wakuu walio na jukumu la kudumisha utaratibu na kutatua hali ambazo zingefanya Waroma waingilie kati na hivyo kufanya jiji lipoteze mapendeleo yake. Hivyo basi, watawala hao wa jiji wangekuwa na wasiwasi kusikia kwamba amani ya watu imeharibiwa na “watu hao waliosababisha fujo.”

Kisha wakatoa shtaka zito sana wakisema: ‘Watu hawa wanapingana na maagizo ya Kaisari, wakisema kuna mfalme mwingine, Yesu.’ (Matendo 17:7) Mchambuzi mmoja anasema kwamba shtaka hilo lilikuwa “uchochezi na uasi” dhidi ya wakuu ambao “hawangeruhusu jina la mfalme [mwingine] litajwe katika mikoa waliyoteka isipokuwa wawe wamewaruhusu.” Vilevile, kwa kuwa Yesu, ambaye Paulo alikuwa akimtaja kuwa Mfalme, alikuwa ameuawa na mamlaka ya Waroma kwa shtaka hilohilo la uchochezi jambo hilo lingefanya watawala hao waamini kuwa ni kweli.​—Luka 23:2.

Watawala hao wa jiji walichukizwa na jambo hilo. Lakini kwa sababu hakukuwa na ushahidi wa kutosha na washtakiwa hawakupatikana, basi “baada ya kuchukua dhamana ya kutosha kutoka kwa Yasoni na wale wengine wakawaacha waende zao.” (Matendo 17:8, 9) Huenda utaratibu huo ulirejelea aina fulani ya malipo ambayo yalimaanisha kwamba Yasoni na Wakristo wengine walipaswa kuhakikisha kuwa Paulo angeondoka jijini na hangerudi na kusababisha fujo tena. Yaelekea Paulo alirejelea kisa hicho aliposema “Shetani aliizuia njia [yake]” na kumfanya asirudi katika jiji hilo.​—1 Wathesalonike 2:18.

Kwa sababu ya hali hiyo, Paulo na Sila walisaidiwa kuondoka usiku-usiku kuelekea Beroya. Utumishi wa Paulo ulikuwa na matokeo mazuri huko pia, lakini matokeo hayo yaliwafanya wapinzani wake Wayahudi walio Thesalonike wakasirike na kufunga safari ya kilomita 80 hadi Beroya ili kuuchochea umati na kuufanya umpinge Paulo na Sila. Muda mfupi baadaye Paulo alianza safari tena kuelekea Athene lakini mapambano kwa ajili ya habari njema bado yangeendelea.​—Matendo 17:10-14.

Mapambano kwa Ajili ya Kutaniko Jipya

Jambo linalofurahisha ni kwamba kutaniko lilianzishwa huko Thesalonike, lakini Wakristo wa eneo hilo walikabili matatizo mengine kando na upinzani. Walizungukwa na wapagani, na watu wenye maadili mapotovu na jambo hilo lilimtia Paulo wasiwasi. Hali ya ndugu zake ingekuwaje?​—1 Wathesalonike 2:17; 3:1, 2, 5.

Wakristo wa Thesalonike walijua kwamba kwa kuacha kushiriki katika shughuli za kijamii na za kidini za jiji hilo, wangekabili chuki na hasira za rafiki zao wa zamani. (Yohana 17:14) Kwa kuongezea, Thesalonike lilijaa madhabahu ya miungu ya Kigiriki kama vile Zeu, Artemi, na Apolo, vilevile na miungu fulani ya Wamisri. Ibada ya Kaisari pia ilitia mizizi, na raia wote walipaswa kushiriki desturi za ibada hiyo. Ikiwa mtu angekataa kushiriki, basi angeonekana kuwa mwasi dhidi ya Roma.

Ibada ya sanamu ilifanya watu waishi maisha mapotovu kiadili. Cabirus, mungu-mlinzi wa Wathesalonike; miungu Dionisio na Afrodito; na Isisi wa Misri ilihusiana kwa jambo moja: ibada yenye sherehe za ngono za vikundi-vikundi na ulevi kupindukia. Desturi ya kuwa na masuria na ukahaba ulienea sana. Watu hawakuona uasherati kuwa dhambi. Jamii yao iliathiriwa na utamaduni wa Kiroma, ambao kulingana na habari fulani, “kulikuwa na wanaume na wanawake wengi katika jiji ambao kazi yao ilikuwa kutimiza tamaa yoyote ya kimwili ya raia wa jiji hilo—na madaktari waliwashauri watu wasizuie tamaa hizo.” Kwa sababu hiyo, Paulo aliwashauri Wakristo wa jiji hilo ‘wajiepushe na uasherati’ na wajiepushe na “hamu yenye tamaa ya ngono” na “uchafu.”—1 Wathesalonike 4:3-8.

Walishinda Mapambano Hayo

Wakristo wa Thesalonike walihitaji kuazimia kupambana kwa ajili ya imani. Hata hivyo, ingawa walikabili upinzani, hali ngumu, na kuzungukwa na wapagani wenye maadili mapotovu, Paulo aliwapongeza kwa sababu ya ‘kazi yao ya uaminifu, kazi yao ya jasho yenye upendo, na uvumilivu,’ pia kwa sababu ya mambo waliyotimiza katika kueneza habari njema duniani kote.​—1 Wathesalonike 1:3, 8.

Mnamo mwaka wa 303 W.K., wote waliodai kuwa Wakristo katika Milki ya Roma walinyanyaswa vikali. Kiongozi mkuu wa mnyanyaso huo alikuwa Kaisari Galeriasi, ambaye makao yake makuu yalikuwa Thesalonike, ambako alijenga majengo mengi ya kifahari. Leo bado kuna majengo fulani katika jiji hilo ambayo hutembelewa na watalii.

Leo, Mashahidi wa Yehova katika jiji la Thessaloníki, wanawahubiria jirani zao na mara nyingi wanafanya hivyo karibu sana na majengo hayo yaliyojengwa na adui mkatili wa Ukristo. Ingawa kuna vipindi katika karne ya 20 ambapo Mashahidi walihubiri wakikabiliwa na upinzani mkali, sasa kuna makutaniko zaidi ya 60 yenye bidii katika jiji hilo. Bidii yao inaonyesha kwamba jitihada za kupambana kwa ajili ya habari njema ambazo zilianza karne nyingi zilizopita bado zinaendelea kwa mafanikio.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Huenda Paulo alirejelea maandiko ambayo sasa yanajulikana kama Zaburi 22:7; 69:21; Isaya 50:6; 53:2-7; na Danieli 9:26.

^ fu. 16 Neno hilo halikupatikana katika maandishi ya Kigiriki. Hata hivyo, maandishi fulani yaliyokuwa na neno hilo yalivumbuliwa katika eneo la Thesalonike. Baadhi ya maandishi hayo yalikuwa na tarehe ya karne ya kwanza K.W.K., hivyo kuthibitisha masimulizi ya kitabu cha Matendo.

[Ramani katika ukurasa wa 18]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Via Egnatia

MAKEDONIA

Filipi

Amfipoli

Thesalonike

Beroya

THESSALY

Bahari ya Aegea

ATHENE

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Juu: Jiji la Thessaloníki leo

Chini: barabara na bafu la Kiroma katika soko

[Picha Hisani katika ukurasa wa 21]

Jengo la Duara karibu na Tao la Galeriasi; mchongo wa Kaisari Galeriasi; kuhubiri karibu na Tao la Galeriasi

[Picha Hisani katika ukurasa wa 18]

Head medallion: © Bibliothèque nationale de France; stone inscription: Thessalonica Archaeological Museum, copyright Hellenic Ministry of Culture and Tourism

[Picha Hisani katika ukurasa wa 20]

Two bottom left images: 16th Ephorate of Prehistoric and Classical Antiquities, copyright Hellenic Ministry of Culture and Tourism

[Picha Hisani katika ukurasa wa 21]

Middle image: Thessalonica Archaeological Museum, copyright Hellenic Ministry of Culture and Tourism