Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kufaulu Kuishi Mapato Yanapopungua

Jinsi ya Kufaulu Kuishi Mapato Yanapopungua

Jinsi ya Kufaulu Kuishi Mapato Yanapopungua

OBED ni baba ya watoto wawili. Kwa miaka kumi alifanya kazi kwenye hoteli ya kifahari katika mojawapo ya majiji makubwa barani Afrika, na haikuwa vigumu kuandalia familia yake. Mara kwa mara, angeipeleka familia yake likizo katika mbuga za wanyama zilizo nchini kwao. Mambo hayo yote yalifikia mwisho wakati alipofutwa kazi kwa sababu ya kupungua kwa wateja.

Baada ya kufanya kazi kwa zaidi ya miaka 22, Stephen alipandishwa cheo na kuwa kati ya wasimamizi wakuu katika mojawapo ya benki kubwa. Alipata faida nyingi kutokana na kazi hiyo kutia ndani kupewa nyumba kubwa, gari, wafanyakazi wa nyumbani, na watoto wake walisomea katika shule za kifahari. Benki hiyo ilipobadili mpangilio wa wafanyakazi, Stephen alifutwa kazi. “Mimi na familia yangu tulishtuka sana,” anasema Stephen. “Nilikata tamaa, nikawa mwenye uchungu, na kujawa na wasiwasi mwingi.”

Hayo ni mambo ya kawaida. Kuzorota kwa mfumo wa kiuchumi ulimwenguni kumefanya watu wengi waliokuwa na mapato mazuri wafutwe kazi. Watu wengi kati yao ambao wamefaulu kupata kazi nyingine wamelazimika kufanya kazi zenye mshahara mdogo huku wakipambana na kupanda kwa gharama za maisha. Mataifa yote, yaliyoendelea na maskini, yanapatwa na hali mbaya ya uchumi.

Hekima Inayotumika Inahitajiwa

Mapato ya mtu yanapopungua au anapofutwa kazi, ni rahisi kulemewa na hisia zisizofaa. Ni kweli kwamba, mtu hawezi kuepuka kabisa kuwa na wasiwasi. Hata hivyo, mtu fulani mwenye hekima alisema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” (Methali 24:10) Hali ya uchumi inapokuwa mbaya, badala ya kujawa na wasiwasi tunahitaji kufanya kama tunavyohimizwa na Neno la Mungu: ‘Kujiwekea hazina ya hekima inayotumika.’​—Methali 2:7.

Ingawa Biblia si kitabu cha mwongozo wa mambo ya kiuchumi, mashauri yake yenye kutumika kuhusu jinsi ya kushughulikia mambo kama hayo yamewasaidia mamilioni ya watu ulimwenguni. Acheni tuchunguze kanuni za msingi zilizo katika Biblia.

Hesabu gharama. Fikiria maneno ya Yesu yanayopatikana katika andiko la Luka 14:28: “Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?” Kanuni iliyo katika andiko hilo ni kwamba mtu anapaswa kuandika bajeti na kutotumia zaidi ya kiasi alichopangia. Lakini kama Obed alivyojionea, si rahisi kufanya hivyo. Anasema: “Kabla sijafutwa kazi tulizoea kununua vitu vingi kuliko tulivyohitaji. Hatukuwa na bajeti kwa sababu tulikuwa na pesa za kutosha kununua chochote tulichotaka.” Kupangia matumizi ya pesa kunatusaidia kuhakikisha kwamba kiasi kidogo cha pesa tulizo nazo kinatumiwa kwa ajili ya mahitaji ya lazima ya familia.

Badili mtindo wa maisha yako. Bila shaka, ni vigumu kuanza kuishi maisha rahisi, lakini ni jambo muhimu. Methali moja ya Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) “Ili tusitumie pesa nyingi, mimi na familia yangu tulihamia kwenye nyumba yetu wenyewe iliyokuwa ndogo na isiyo na vitu vingi vya kifahari,” anasema Stephen. “Nilihitaji kuwahamisha watoto wangu na kuwapeleka kwenye shule ambazo hazikuwa ghali lakini zilitoa elimu nzuri.”

Ili mfanikiwe kubadili mtindo wenu wa maisha ni jambo muhimu kuwasiliana waziwazi. Austin aliyefanya kazi katika benki kwa miaka tisa kabla ya kufutwa kazi, anasema: “Mimi na mke wangu tuliketi na kuandika vitu ambavyo hasa tulihitaji. Tulilazimika kupunguza vyakula vya bei ghali tulivyonunua, likizo za gharama kubwa, na tukaepuka kununua nguo mpya tusizohitaji. Ninafurahi kwamba tulishirikiana katika familia kufanya mabadiliko hayo.” Ni kweli kwamba watoto wadogo hawawezi kuelewa kabisa kwa nini mabadiliko kama hayo yanahitajiwa, lakini wazazi wanaweza kuwasaidia waelewe.

Uwe tayari kufanya kazi tofauti. Ikiwa umezoea kufanya kazi ofisini, huenda ikiwa vigumu kufanya kazi inayohitaji nguvu. “Haikuwa rahisi kukubali kazi za hali ya chini, kwa sababu nilikuwa nimezoea kufanya kazi ya usimamizi katika kampuni kubwa,” anasema Austin. Jambo hilo halishangazi kwa kuwa Biblia inasema hivi katika Methali 29:25: “Kutetemeshwa na wanadamu ndiko huleta mtego.” Kuwaza sana jinsi watu wanavyokuona hakuwezi kukusaidia kupata pesa za kutimizia mahitaji ya familia yako. Ni nini kitakachokusaidia kushinda mawazo kama hayo yasiyofaa?

Siri ni unyenyekevu. Baada ya Obed kufutwa kazi kwenye hoteli, mtu fulani aliyekuwa akifanya naye kazi zamani alimwajiri katika karakana yake ya kurekebisha magari. Kazi hiyo ilitia ndani kutembea mwendo mrefu kwenye barabara zenye vumbi ili kununua rangi na vifaa vingine vya magari. Obed anasema: “Sikupenda kazi hiyo lakini sikuwa na la kufanya. Unyenyekevu ulinisaidia kukubali kazi ambayo mshahara wake ulikuwa robo ya mshahara niliokuwa nikipata, lakini ulitosha kutimiza mahitaji ya familia yangu.” Je, unaweza kufaidika kwa kuwa na mtazamo kama huo?

Uwe mwenye kuridhika. Kamusi moja inasema kwamba mtu anayeridhika ni “mtu aliye na furaha na anayetosheka na jinsi mambo yalivyo.” Huenda ikawa vigumu kwa mtu mwenye matatizo ya kifedha kuelewa ufafanuzi huo. Hata hivyo, fikiria maneno ya mtume Paulo, mmishonari ambaye alielewa maana ya kuwa na uhitaji: “Nimejifunza kuwa mwenye kujitosheleza katika hali zozote nilizo nazo. Kwa kweli najua jinsi ya kupungukiwa na vyakula, kwa kweli najua jinsi ya kuwa na wingi.”​—Wafilipi 4:11, 12.

Huenda sasa hali yetu ni nzuri, lakini katika nyakati hizi zenye mabadiliko, hali inaweza kuwa mbaya sana. Tunaweza kufaidika kikweli ikiwa tutachukua kwa uzito shauri hili la Paulo lililoongozwa na roho ya Mungu: “Kwa hakika, huo ni njia ya kupata faida kubwa, huu ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu. Kwa hiyo, tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.” Bila kuwahimiza watu wawe wavivu, Paulo alikuwa akionyesha jinsi ya kuwa na maoni yanayofaa kuelekea mahitaji ya kimwili.​—1 Timotheo 6:6, 8.

Chanzo cha Furaha ya Kweli

Furaha ya kweli haitokani tu na kukusanya kila kitu tunachohitaji au kuishi maisha ya raha mstarehe. Yesu mwenyewe alisema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” Kwa kweli, furaha ya kweli inatokana na kutumia vitu tulivyo navyo kuwasaidia na kuwatia moyo wengine.—Matendo 20:35.

Muumba wetu, Yehova Mungu, anajua vizuri sana mahitaji yetu. Kupitia Neno lake Biblia, ametoa mashauri ambayo yamewasaidia watu wengi kuboresha maisha yao na kuwasaidia wasihangaike kupita kiasi. Bila shaka, hali ya kifedha haitabadilika tu kwa ghafla au kimuujiza. Lakini Yesu aliwahakikishia wale ‘wanaotafuta kwanza ufalme na uadilifu wa Mungu’ kwamba watatimiziwa mahitaji yao yote ya kila siku.​—Mathayo 6:33.