Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Likizo Ambayo Nilifurahia Zaidi!

Likizo Ambayo Nilifurahia Zaidi!

Barua Kutoka Ireland

Likizo Ambayo Nilifurahia Zaidi!

“UNAHITAJI kufanya jambo lenye kusisimua ili uache kufikiria mtihani wako,” wazazi wangu wakaniambia. “Twende tukawatembelee binamu zako huko Ireland na tuwahubirie watu ambao hawahubiriwi habari njema za Ufalme kwa ukawaida.”

Sikufurahia wazo hilo. Mbali na kujitayarisha kwa ajili ya mtihani, nilikuwa na wasiwasi kuhusu safari hiyo kwa sababu sikuwa nimewahi kutoka nje ya Uingereza wala kusafiri kwa ndege. Msichana mwenye umri wa 17 anayeishi katika kitongoji cha jiji la London, chenye shughuli nyingi, angewezaje kukabiliana na maisha ya polepole katika mji mdogo ulio kwenye ncha ya kusini-magharibi mwa Ireland?

Sikupaswa kuwa na wasiwasi. Mara tu ndege ilipotua, nilianza kupendezwa na nchi hiyo. Hata hivyo, kwa sababu tulianza safari yetu asubuhi na mapema, nilianza kulala mara tu tulipoanza kusafiri kwa gari. Barabara tuliyotumia ilikuwa nyembamba na ilikuwa na ukingo wa mawe. Mara kwa mara, niliamka na kuona maeneo yenye kupendeza ya mashambani yenye mawe makubwa.

Usiku wa kwanza tulipowasili kwenye mji wa Skibbereen, tulifurahia jioni yenye kujenga kiroho pamoja na familia ambayo ilikuwa imehamia Ireland ili kusaidia katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Tulicheza michezo ya Biblia. Kila mmoja wetu alichagua jina la mtu anayetajwa katika Biblia kutoka kwenye mfuko fulani, na kuigiza tukio linalohusiana na mtu huyo. Kisha, wengine wangejaribu kutambua ni nani.

Siku iliyofuata, mimi, wazazi wangu, ndugu yangu mdogo, binamu zangu, na familia nyingine, tulisafiri kwa feri hadi kwenye kisiwa kidogo kinachoitwa Kisiwa cha Heir. Kisiwa hicho kina watu wasiozidi 30. Yesu alisema kwamba ni lazima habari njema ihubiriwe katika dunia yote inayokaliwa. Basi, siku hiyo tuliwahubiria habari za Kimaandiko zenye kutia moyo watu hao wenye kufanya urafiki na wakarimu huku tukifurahia mandhari nzuri ajabu ambayo haijachafuliwa.

Jua liliangaza katika anga lisilo na mawingu. Kulikuwa na harufu nzuri na tamu kama ya nazi iliyotoka kwenye miti fulani yenye maua ya rangi ya manjano. Maua yalitanda kila sehemu ya eneo hilo. Kulikuwa na fuo za bahari zenye mchanga na miamba, ambako ndege wanaoitwa mnandi na ganeti huangua mayai yao. Tulipotazama maeneo yaliyokuwa mbali tuliona visiwa vingi vidogo-vidogo, vingi kati yavyo havikuwa na wakaaji, vyote vilikuwa katika eneo linaloitwa Ghuba ya Roaringwater. Tulithamini sana kuona mambo hayo yote katika uumbaji wa Yehova!

Huko Skibbereen, nilifurahia kupata marafiki wengi wazuri katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova la eneo hilo na nikafanya mambo ambayo sikuwa nimewahi kufanya. Mchezo niliofurahia zaidi ni kuendesha mtumbwi kwenye maporomoko ya maji. Ilifurahisha sana kutazama pwani ya Ireland tukiwa kwenye mitumbwi! Tulienda kuvua samaki ili tupate chakula cha jioni, lakini wanyama wanaoitwa sili waliwala samaki kabla hatujawavua. Tulibuni michezo ya ufuoni, na hata nilijaribu kucheza dansi ya Ireland.

Pia, tulitumia muda fulani kujifunza kuhusu mji wa Skibbereen. Viazi mviringo vilipoacha kukuzwa huko Ireland katika miaka ya 1840, mji huo na maeneo yaliyo karibu yaliathiriwa sana. Maelfu ya watu walikufa njaa, na karibu 9,000 kati yao walizikwa kwenye kaburi la ujumla. Tulifarijiwa sana kujua kwamba chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, hakutakuwa tena na janga la njaa, na maelfu ya watu waliokufa kwa sababu ya janga hilo watafufuliwa katika paradiso duniani.

Tulijiunga na Mashahidi katika eneo hilo kuzungumza na watu ambao hawahubiriwi kwa ukawaida kwenye eneo kubwa la kutaniko hilo. Tuliendesha gari kwenye barabara nyembamba na yenye mteremko mkali ili kufikia nyumba zilizokuwa kwenye jabali lililo kando ya Bahari ya Ireland. Watu tuliokuta katika eneo hilo pia walikuwa wenye kufanya urafiki na wakarimu. Kama tulivyofanya katika Kisiwa cha Heir, tulianza kwa kuwaambia kwamba tulikuwa kwenye likizo na tulikuwa tukiwaeleza watu ujumbe wenye kugusa moyo unaopatikana kwenye Biblia.

Mama yangu alizungumza na mwanamke ambaye alikubali kwa utayari magazeti yetu, yaani, Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Tulipokutana tena naye siku chache baadaye, alisema kwamba alikuwa amefurahia kusoma yale magazeti.

Alitusihi hivi: “Tafadhali rudini tena siku nyingine mkiwa na magazeti mengine mengi ili tuzungumze zaidi.” Tulimtajia kwamba tulikuwa karibu kurudi nyumbani lakini tungemtuma mtu mwingine arudi kumtembelea.

Akajibu hivi: “Basi, mtakaporudi siku nyingine, msikose kunitembelea. Watu wa Ireland hawasahau sura za watu!”

Siku ya mwisho ya likizo yetu tulishinda kwenye ufuo wa bahari pamoja na ndugu na dada wa kutaniko la eneo hilo. Tulitengeneza jiko kwa kutumia mawe na kuni zilizokuwa kwenye ufuo. Pia, tulipika wanyama wa baharini wanaoitwa kome waliokuwa wamebebwa na maji safi ya bahari mpaka kwenye mawe yaliyo ufuoni. Nilifurahia sana kila pindi!

Baada ya hapo, nilikuwa na maoni gani kuhusu likizo ya juma moja huko Ireland? Ndiyo likizo ambayo nilifurahia zaidi! Hakikuwa tu kipindi chenye kufurahisha bali hasa chenye kuridhisha kwa kujua kwamba nilikuwa nimefanya jambo lenye kumpendeza Yehova na lililomletea sifa. Ninapenda kumtumikia Mungu, na ninapata furaha hata zaidi kwa kuwa nina marafiki wazuri pamoja na watu wa familia ambao wanahisi kama mimi na wanaoshirikiana nami. Nilipofika nyumbani, nilimshukuru Yehova kwa kunipa marafiki wengi wapendwa ambao wanapenda mambo ya kiroho na kwa mambo mengi niliyojionea ambayo nitayakumbuka sikuzote.

[Picha Hisani katika ukurasa wa 25]

An Post, Ireland