Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Kwa nini Wayahudi walipendezwa sana na nasaba zao?

Kumbukumbu za nasaba zilikuwa muhimu katika kutambua ukoo na uhusiano wa kifamilia. Pia, kumbukumbu hizo zilihitajiwa ili kuamua mipaka ya maeneo na urithi. Nasaba ya Masihi aliyeahidiwa ilikuwa muhimu sana. Wayahudi walijua vizuri kwamba Masihi angetokea katika ukoo wa Daudi wa kabila la Yuda.​—Yohana 7:42.

Kwa kuongezea, msomi Joachim Jeremias anasema hivi: “Kwa kuwa cheo cha makuhani na Walawi kilipatikana kupitia urithi . . . lilikuwa jambo muhimu zaidi kwamba usafi wa nasaba hizo ulindwe.” Wanawake Waisraeli walioolewa katika familia za makuhani walipaswa kuthibitisha nasaba zao ili ukuhani “usichafuliwe.” Katika siku za Nehemia, familia nzima za Walawi zilinyimwa pendeleo baada ya ‘kutafuta kitabu chao cha kuandikisha, ili kuthibitisha ukoo wao waziwazi, nacho hakikupatikana.’​—Nehemia 7:61-65.

Zaidi ya hayo, Sheria ya Musa ilisema kwamba ‘mwana-haramu, Mwamoni, au Mmoabu yeyote asiingie katika kutaniko la Yehova.’ (Kumbukumbu la Torati 23:2, 3) Kwa sababu hiyo, Jeremias anaongezea kwamba “nasaba kamili ilipaswa kuthibitishwa ili mtu apate haki za kisheria na jambo hilo linathibitisha mkataa wa kwamba . . . hata Mwisraeli wa kawaida alijua watu wa ukoo wake wa karibu na angeweza kutambua alikuwa wa kabila gani kati ya yale makabila kumi na mawili.”

Wayahudi walikusanyaje na kuhifadhi nasaba zao?

Waandikaji wa Injili, Mathayo na Luka, waliandika nasaba ya Yesu iliyokuwa na habari nyingi. (Mathayo 1:1-16; Luka 3:23-38) Rekodi nyingine za nasaba zimehifadhiwa pia. Kwa mfano, kitabu cha ufafanuzi kuhusu Wayahudi, kinachoitwa midrash, kinasema hivi kumhusu Hillel, rabi aliyeishi nyakati za Yesu: “Kitabu fulani cha kukunjwa chenye rekodi za nasaba kilipatikana huko Yerusalemu, na kilikuwa kimeandikwa kwamba Hillel alikuwa wa ukoo wa Daudi.” Katika kitabu chake kinachoitwa The Life, mwanahistoria Myahudi wa karne ya kwanza Flavio Yosefo alidai kwamba mababu zake walikuwa makuhani na ukoo wa mama yake ulikuwa “wa familia ya kifalme.” Alisema kuwa alipata mambo hayo yakiwa yameandikwa katika “vitabu vya rekodi vya umma.”

Katika kitabu chake Against Apion, Yosefo aliandika kuhusu daraka la kutunza rekodi za familia za makuhani akisema kwamba taifa la Israeli liliwapa daraka hilo “wanaume wenye kuheshimika.” Kitabu The Jewish Encyclopedia kinasema: “Inaonekana kwamba afisa wa pekee alipewa daraka la kutunza rekodi hizo, na huko Yerusalemu kulikuwa na mahakama iliyoshughulikia mambo ya nasaba.” Wayahudi ambao hawakuwa makuhani walijiandikisha katika majiji ya baba zao. (Luka 2:1-5) Inaelekea kwamba waandikaji wa vitabu vya Injili walitumia maandishi hayo yaliyohifadhiwa na ambayo yalisomwa na watu wote. Pia, yaelekea kwamba kila familia ilihifadhi rekodi za kibinafsi.