Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Ulijua?

Je, Ulijua?

Je, Ulijua?

Sababu gani Wayahudi walikuwa na maandishi yaliyoonyesha vizazi vyao?

Maandishi hayo yalikuwa ya lazima sana ili kusaidia kila mutu ajue watu wa jamaa yake na wa kabila lake. Tena, maandishi hayo yalihitajiwa ili kujua namna ya kugawanya maeneo na uriti. Na jambo la maana zaidi, yaliwasaidia Wayahudi wajue kizazi ambamo Masiya angetokea. Wayahudi walijua vizuri kama Masiya alipaswa kutokea katika kizazi cha Daudi, katika kabila la Yuda.​—Yohana 7:42.

Mutu mumoja mwenye elimu, Joachim Jeremias, alisema hivi: “Kwa sababu kazi ya kuhani na Mulawi ilikuwa inaritiwa . . . ilikuwa lazima sana kizazi hicho kibaki safi.” Wanawake Waisraeli walioolewa na makuhani waliombwa kuonyesha vizazi vyao, na hilo lilisaidia ili ukuhani uendelee kubaki “safi.” Wakati wa Nehemia, familia nzima za Walawi zilikataliwa kwa sababu ‘walitafuta kitabu chao cha kuandikisha, ili [kuonyesha] ukoo wao waziwazi, nacho hakikupatikana.’​—Nehemia 7:61-65.

Zaidi ya hilo, Sheria ya Musa ilisema kama “mwana-haramu yeyote,” ‘Muamoni ao Mumoabu yeyote asiingie katika kutaniko la Yehova.’ (Kumbukumbu la Torati 23:2, 3) Kwa sababu hiyo, Joachim Jeremias anasema tena hivi: “Ili mwanaume aweze kutumia haki yake ya uanainchi, alipaswa kuonyesha kwanza kizazi ao ukoo wake; na hilo linatusukuma tuseme kama . . . hata Muisraeli wa hali ya chini alijua vizuri mababu ao watate wake wa karibu na alijua yeye ni wa kabila gani kati ya makabila 12 ya Waisraeli.”

Namna gani Wayahudi walikusanya na kuchunga maandishi ya vizazi vyao?

Mathayo na Luka walioandika Injili walionyesha waziwazi vizazi (ao ukoo) ambamo Yesu alitokea. (Mathayo 1:1-16; Luka 3:23-38) Tena, kuna watu wengine ambao waliandika juu ya vizazi hivyo, na maandishi yao yamechungwa. Kwa mufano, kitabu fulani cha maelezo juu ya Wayahudi kinasema hivi juu ya Hillel, mwalimu wa sheria ya Wayahudi: “Kitabu fulani cha kukunjwa kinachotoa maelezo juu ya vizazi kilipatikana huko Yerusalemu. Kitabu hicho kilionyesha kama Hillel alikuwa wa kizazi cha Daudi.” Katika kitabu chake (The Life), mwanahistoria Flavius Josèphe wa wakati wa mitume, anasema kama mababu (ao watate) wake walikuwa makuhani; na kama kufuatana na kizazi cha mama yake yeye ni wa “kizazi cha wafalme.” Alisema kama habari hiyo ilikuwa “imeandikwa katika kitabu cha vizazi kilichokuwa na maandishi ambayo yalilindwa mahali ambapo watu wangeweza kuyasoma.”

Katika kitabu chake (Against Apion), Josèphe alisema kama taifa lake liliwapa “watu wa hali ya juu” kazi ya kuchunga vizuri maandishi yaliyoonyesha familia za makuhani. Kitabu kimoja (The Jewish Encyclopedia) kinasema hivi: “Inawezekana mutumishi wa pekee alikabiziwa maandishi hayo, na inasemekana kama baraza la kuchunguza mambo ya vizazi (ao ukoo) liliundwa huko Yerusalemu.” Wayahudi wasio makuhani walijiandikisha katika miji ya baba zao. (Luka 2:1-5) Labda Mathayo na Luka walioandika Injili walichunguza maandishi hayo ambayo yalilindwa mahali ambapo watu wangeweza kuyasoma. Pia, inaonekana kama watu wa kila familia walichunga maandishi ya vizazi vyao.