Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Alionyesha Kiburi na Kisha Akatii

Alionyesha Kiburi na Kisha Akatii

Uwafundishe Watoto Wako

Alionyesha Kiburi na Kisha Akatii

JE, kuna siku ambayo kiburi kilikufanya usitii? * Labda siku fulani uliangalia programu ya televizyo ambayo mama ao baba yako alikukataza kuangalia. Kisha hapo, labda uliwaza juu ya jambo hilo na ukasikitika sana kwa sababu ulikosa kutii. Mutu aliyeonyesha kiburi na kisha akatii, ni Naamani. Tuone basi namna alivyosaidiwa kuacha kiburi chake.

Wazia tunaishi wakati wa Naamani miaka 3000 iliyopita. Naamani hakuwa mutu wa burebure, alikuwa mukubwa wa maaskari wa mufalme wa Siria. Ni yeye aliyekuwa anawatolea maaskari amri ya kufanya mambo fulani, nao walikuwa wanamutii. Lakini Naamani akapatwa na ugonjwa wa ukoma. Ugonjwa huo ulimuumiza kabisa na ulifanya mwili wake uonekane vibaya sana.

Bibi ya Naamani alikuwa na binti mudogo aliyekuwa anamufanyia kazi za nyumbani; binti huyo alikuwa ametoka katika inchi ya Israeli. Siku moja binti huyo akamuelezea bibi ya Naamani kama katika inchi ya Israeli kuna nabii anayeitwa Elisha ambaye anaweza kumuponyesha bwana yake. Naamani aliposikia hivyo, akaenda haraka ili kuonana na Elisha. Akamufungia Elisha zawadi nyingi sana na akafanya safari pamoja na maaskari wake mupaka Israeli. Akafika kwanza kwa mufalme wa Israeli ili kumujulisha sababu gani alikuja.

Elisha aliposikia jambo hilo, akatuma mutu ili kumuambia mufalme amutume Naamani kwake. Naamani alipofika kwa Elisha, Elisha hakutoka ili kumukaribisha lakini akatuma tu mutu ili kumuambia aende kujitumbukiza mara saba katika Muto Yordani. Elisha akasema ikiwa Naamani anafanya hivyo atapona. Unajua Naamani alifanya nini alipoambiwa hivyo?

Naamani anakasirika. Kwa sababu ya kiburi, anakataa kutii nabii wa Mungu. Anawaambia maaskari wake hivi: ‘Kuna mito bora nyumbani kwangu ambamo ninaweza kuoga.’ Naamani akaanza kuondoka. Lakini, unajua maaskari wake walimuambia nini?— Walimuambia hivi: ‘Kama nabii angekuomba jambo ngumu, je wewe haungelifanya? Basi, sababu gani usitii jambo hilo jepesi ambalo anakuomba?’

Naamani anasikiliza maaskari wake na anafanya yale waliyomuambia. Anajitumbukiza mara sita katika muto na kuinuka. Alipofanya hivyo kwa mara ya saba, anashangaa sana​—ugonjwa wake ulikuwa umepona! Ngozi yake inakuwa nzuri! Mara moja Naamani anarudia kwenye nyumba ya Elisha ili kumushukuru, nyumba ya Elisha ilikuwa umbali wa kilometre 48. Anataka kumutolea nabii Elisha zawadi zenye bei sana, lakini nabii anakataa kupokea kitu chochote.

Lakini, Naamani anamuomba nabii Elisha kitu fulani. Unajua ni kitu gani?— Anamuomba udongo ili aubebe nyumbani kwake, muzigo unaoweza kubebwa na nyumbu (wanyama wenye kufanana na punda) wawili. Unajua sababu gani aliomba udongo huo?— Naamani anasema kama anataka kumutolea Mungu zabihu kwenye udongo unaotoka katika inchi ya watu wake, Israeli. Kisha Naamani anamuahidi Elisha kama hataabudu tena Mungu mwengine isipokuwa tu Yehova! Naamani anabadilika, anaacha kiburi na anataka sasa kumutii Mungu wa kweli.

Unaona sasa namna gani unaweza kumuiga Naamani?— Ikiwa wewe ni mwenye kiburi kama Naamani, unaweza kubadilika. Ikiwa unakubali mashauri, unaweza kuacha kiburi na kuwa mutiifu.

Usome Katika Biblia Yako

2 Wafalme 5:1-19

Luka 4:27

[Maelezo ya chini]

^ Ikiwa unasoma sehemu hii pamoja na mutoto, unapoona alama hii (—), utue na umutie moyo aeleze mawazo yake.