Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Simulizi la Maisha

“Siri” Tuliyojifunza Kutokana na Utumishi Wetu Mtakatifu

“Siri” Tuliyojifunza Kutokana na Utumishi Wetu Mtakatifu

Limesimuliwa na Olivier Randriamora

“Kwa kweli najua jinsi ya kupungukiwa na vyakula, kwa kweli najua jinsi ya kuwa na wingi. Katika mambo yote na katika hali zote nimejifunza siri ya jinsi ya kushiba na pia jinsi ya kuwa na njaa . . . Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”—Flp. 4:12, 13.

KWA muda mrefu, maneno hayo ya mtume Paulo yamekuwa yakinitia moyo sana mimi na mke wangu, Oly. Kama Paulo, tumejifunza “siri” hiyo kwa kumtegemea Yehova kikamili tunapomtumikia hapa Madagaska.

Mashahidi wa Yehova walipoanza kujifunza Biblia pamoja na mama ya Oly mwaka wa 1982, mimi na Oly tulikuwa tayari tumeamua kufunga ndoa. Mimi pia nilikubali kujifunza Biblia, naye Oly akajiunga nami baadaye. Tulifunga ndoa mwaka wa 1983, tukabatizwa mwaka wa 1985, na mara moja tukaanza upainia msaidizi. Mnamo Julai 1986, tukawa mapainia wa kawaida.

Mnamo Septemba 1987, tulianza kutumikia tukiwa mapainia wa pekee. Mgawo wetu wa kwanza ulikuwa katika mji mdogo ulio kaskazini-magharibi mwa Madagaska ambako hakukuwa na kutaniko lolote. Nchini Madagaska kuna makabila 18 makubwa na vikundi vingi sana vya ukoo, mapokeo na desturi zinatofautiana sana. Lugha rasmi ni Kimalagasi, lakini kuna lugha nyingine za kienyeji pia. Kwa hiyo, tulianza kujifunza lugha iliyozungumzwa katika mgawo wetu mpya, na hilo lilitusaidia kukubaliwa na watu.

Mwanzoni, nilitoa hotuba ya watu wote kila Jumapili, na baada ya hotuba Oly alipiga makofi kwa bidii sana, yeye peke yake akiwa msikilizaji. Pia, tulifanya sehemu zote za Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na Oly alitoa hotuba peke yake kana kwamba anazungumza na mwenye nyumba. Tulifurahi sana wakati mwangalizi wa mzunguko alipotutembelea na kwa fadhili akapendekeza kwamba tufanye mikutano kwa njia tofauti.

Hatukupokea kwa ukawaida posho ya kila mwezi kwa sababu barua hazikuwa zikija kwa ukawaida. Kwa hiyo, tulijifunza kuishi katika hali ya kupungukiwa. Pindi moja, hatukuwa na pesa za kutosha kulipia nauli ya basi ili kuhudhuria kusanyiko la mzunguko, umbali wa kilomita 130 hivi. Tulikumbuka shauri fulani zuri tulilopewa na Shahidi mwenzetu aliyesema: “Mwambieni Yehova kuhusu matatizo yenu kwa sababu mnafanya kazi yake.” Kwa hiyo, tulisali na kuamua kutembea kwa miguu. Hata hivyo, kabla tu ya kuondoka, ndugu mmoja alitutembelea kwa ghafla na kutupatia zawadi ya pesa ambazo zilitosha tu nauli ya basi!

KAZI YA MZUNGUKO

Mnamo Februari 1991, niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko. Wakati huo, kikundi chetu kidogo kilikuwa kimeongezeka na kuwa na wahubiri 9, na wahubiri 3 kati yao walikuwa wamebatizwa, na kwa wastani watu 50 walikuwa wakihudhuria mikutano. Baada ya kuzoezwa, tulitumikia mzunguko mmoja katika mji mkuu, Antananarivo. Mwaka wa 1993, tulipewa mgawo wa kutumikia mzunguko mmoja ulio mashariki mwa nchi. Hali za maisha katika sehemu hiyo zilikuwa tofauti sana na hali za mjini.

Ili kuyafikia makutaniko na vikundi vya mashambani, tulitembea kwa miguu, nyakati nyingine umbali wa kilomita 145 kuvuka milima yenye misitu mikubwa. Kwa kawaida, tulibeba mizigo michache iwezekanavyo. Bila shaka, wakati wowote ambapo hotuba ya mwangalizi wa mzunguko ilitia ndani maonyesho ya slaidi, kama ilivyokuwa nyakati nyingine siku hizo, tulibeba mizigo mizito zaidi. Oly alibeba projekta ya slaidi, nami nilibeba betri ya gari.

Mara nyingi tulisafiri umbali wa kilomita 40 kwa siku ili kufika kwenye kutaniko linalofuata. Njiani, tulipanda na kushuka milima, tukavuka mito, na kupitia njia zenye matope. Nyakati nyingine, tulilala kando ya barabara, lakini kwa kawaida tulijaribu kutafuta kijiji ambamo tungeweza kulala usiku. Na nyakati nyingine tuliwaomba watu tusiowajua kamwe watupatie mahali pa kulala usiku. Baada ya kupata mahali pa kulala, tulianza kupika chakula. Oly aliomba sufuria na kwenda kuchota maji kwenye mto au ziwa lililo karibu, na mimi niliazima shoka ili kupasua kuni za kupikia. Mambo hayo yote yalichukua wakati. Mara kwa mara, tulinunua kuku, tukamchinja na kumsafisha.

Baada ya chakula, tulichota maji ya kuoga. Nyakati nyingine tulilala jikoni. Mvua iliponyesha, tulilala tukiwa tumeuegemea ukuta, ili tusilowe maji yaliyokuwa yakivuja kutoka kwenye paa.

Sikuzote tulihakikisha kwamba tumewahubiria watu waliotukaribisha nyumbani kwao. Tulipofika mwisho wa safari yetu, tuliguswa moyo sana na fadhili na ukarimu tulioonyeshwa na ndugu na dada zetu Wakristo. Ndugu na dada hao walithamini sana ziara yetu hivi kwamba hatukufikiria matatizo yoyote tuliyokabili njiani.

Tulipokaa katika nyumba za Mashahidi wenzetu, tulifurahia kuwasaidia kufanya kazi za nyumbani. Na kwa hiyo walipata nafasi ya kujiunga nasi katika huduma ya shambani. Hatukutarajia kupata maisha ya starehe au chakula cha pekee ambacho wenyeji wetu hawangeweza kununua.

KUTEMBELEA VIKUNDI VYA MASHAMBANI

Tulifurahia kutembelea vikundi vya mashambani, ambako akina ndugu walitukaribisha kwa kutupatia ratiba yenye shughuli nyingi. Kwa kawaida hatukuwa na wakati wa ‘kupumzika kidogo.’ (Marko 6:31) Katika eneo fulani, mume na mke wake ambao ni Mashahidi walikuwa wamewaalika wanafunzi wao wote 40 wa Biblia nyumbani mwao ili tujifunze nao. Oly alijiunga na dada huyo kujifunza na wanafunzi 20 hivi, nami nikajiunga na ndugu kujifunza na wanafunzi wengine 20. Baada ya mwanafunzi mmoja kuondoka, tulianza papo hapo kujifunza na mwanafunzi anayefuata. Baadaye mchana, tulisimamisha mafunzo ili tufanye mikutano ya kutaniko, na baada ya mikutano tuliendelea kuongoza mafunzo ya Biblia. Siku hiyo ndefu ya utumishi iliendelea mpaka baada ya saa mbili usiku!

Tulipotembelea kikundi kingine, sote tulienda kwenye kijiji jirani karibu saa mbili asubuhi. Sote tulivaa mavazi ambayo si mapya. Baada ya kutembea kwa muda mrefu kupitia msituni, tulifika katika eneo karibu adhuhuri. Tulivaa mavazi safi na mara moja tukaanza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Nyumba zilikuwa chache lakini wahubiri walikuwa wengi. Kwa hiyo, tulihubiri eneo lote kwa dakika 30 hivi. Kisha tulienda kwenye kijiji kilichofuata. Baada ya kuhubiri katika kijiji hicho, tulianza safari ndefu ya kutembea kurudi nyumbani. Mwanzoni, hali hiyo ilituvunja moyo kidogo kwa sababu tulitumia wakati na nguvu nyingi kufika kwenye eneo lakini tulihubiri nyumba kwa nyumba kwa muda wa saa moja tu. Hata hivyo, Mashahidi wa huko hawakulalamika. Waliendelea kuwa na uchangamfu.

Kikundi kimoja cha mashambani huko Taviranambo kilikuwa juu ya mlima karibu na kilele chake. Katika kikundi hicho tulikuta familia moja ya Mashahidi ambayo iliishi katika nyumba yenye chumba kimoja. Walifanyia mikutano katika kibanda kilichokuwa karibu. Kwa ghafla, ndugu aliyetukaribisha alipaaza sauti, “Akina ndugu!” Kisha tukamsikia mtu akijibu hivi kwa sauti kubwa juu ya kilele cha mlima mwingine ulio karibu, “Ooh!” Yule aliyetukaribisha akapaaza tena sauti, “Mwangalizi wa mzunguko amefika!” Akajibiwa hivi: “Yaah!” Inaonekana kwamba ujumbe huo uliwafikia wengine walioishi mbali zaidi. Muda si muda, watu walianza kukusanyika, na mkutano ukaanza, watu zaidi ya 100 walihudhuria mkutano huo.

MATATIZO YA USAFIRI

Mwaka wa 1996, tulipewa mgawo wa kutumika katika mzunguko ulio karibu na Antananarivo, kwenye nyanda za juu katikati ya nchi. Mzunguko huo pia ulikuwa na matatizo ya pekee. Hakukuwa na magari ya abiria ya kusafirisha watu kwa ukawaida kwenye maeneo ya karibu. Tulipaswa kutembelea kikundi fulani huko Beankàna (Besakay), kilomita 240 hivi kutoka Antananarivo. Baada ya kukubaliana na dereva, tulipanda lori dogo lililokuwa likielekea upande huo. Lori hilo lilikuwa na abiria wengine 30 na baadhi yao walikuwa ndani na wengine walikuwa wamelala juu ya lori hilo, huku wengine wakining’inia upande wa nyuma.

Na kama kawaida, baada ya muda mfupi, lori hilo liliharibika, tukaendelea kusafiri kwa miguu. Baada ya kutembea kwa saa kadhaa, lori kubwa likatufikia. Tayari lilikuwa limejaa watu na mizigo, hata hivyo, dereva alisimama. Tukapanda, na kukubali kusafiri tukiwa tumesimama. Baadaye, tulifika mahali penye mto, lakini daraja lilikuwa likirekebishwa. Kwa mara nyingine tena tulianza kutembea kwa miguu na hatimaye tukafika katika kijiji kidogo, ambako mapainia fulani wa pekee walikuwa wakiishi. Hata ingawa hawakuwa wakitarajia ziara ya mwangalizi, tulihubiri pamoja nao huku tukingojea daraja lirekebishwe na gari lingine la abiria lije.

Gari la abiria lilifika baada ya juma moja, basi tukaendelea na safari yetu. Barabara ilijaa mashimo makubwa. Mara kwa mara tulilazimika kulisukuma gari hilo ili lipite kwenye maji yaliyotufikia magotini, na mara nyingi tulijikwaa na kuanguka tulipokuwa tukilisukuma gari hilo. Alfajiri na mapema, tulifika kwenye kijiji fulani kidogo na hivyo tukashuka. Kutoka kwenye barabara kuu, tuliendelea kutembea kupitia katika mashamba ya mpunga, katika maji yenye matope yaliyotufikia kiunoni ili kuelekea kwenye ziara yetu.

Hiyo ilikuwa ziara yetu ya kwanza katika eneo hilo, kwa hiyo tuliamua kuwahubiria watu fulani waliokuwa wakifanya kazi katika mashamba ya mpunga na kuwaomba watuonyeshe mahali ambapo Mashahidi waliishi. Tulifurahi kama nini tulipogundua kwamba kwa kweli wafanyakazi hao walikuwa ndugu zetu wa kiroho!

KUWATIA MOYO WENGINE WAINGIE KATIKA HUDUMA YA WAKATI WOTE

Kwa miaka mingi, tumepata shangwe kubwa kuona wengine tuliowatia moyo wakiingia katika huduma ya wakati wote. Tulipokuwa tukitembelea kutaniko moja ambalo lilikuwa na mapainia tisa wa kawaida, tulimtia moyo kila painia ajiwekee lengo au mradi wa kusaidia mhubiri mmoja kuwa painia. Tulipotembelea kutaniko hilo miezi sita baadaye, idadi ya mapainia wa kawaida ilikuwa imeongezeka sana kufikia 22. Dada wawili mapainia walikuwa wamewatia moyo baba zao ambao walikuwa wazee wa kutaniko kuwa mapainia wa kawaida. Ndugu hao pia walimchochea mzee wa tatu ajiunge nao. Muda mfupi baadaye, mzee huyo wa tatu aliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee. Baadaye, yeye na mke wake walianza kazi ya mzunguko. Vipi wale wazee wengine wawili? Mmoja anatumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko, na yule mwingine anajitolea katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme.

Tunamshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya msaada wake, kwa kuwa tunatambua kwamba hatuwezi kutimiza jambo lolote kwa uwezo wetu wenyewe. Ni kweli kwamba nyakati nyingine tunahisi tumechoka, tunakuwa wagonjwa, hata hivyo, tunafurahi tunapofikiria matokeo ya huduma yetu. Yehova anaiwezesha kazi yake iendelee. Tunafurahi kushiriki kwa kadiri fulani katika kazi hiyo na kumtumikia sasa tukiwa mapainia wa pekee. Naam, tumejifunza ile “siri” kwa kumtegemea Yehova, ‘anayetupa sisi nguvu.’

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Tumejifunza ile “siri” kwa kumtegemea Yehova

[Ramani/​Picha katika ukurasa wa 4]

Kisiwa cha Madagaska, kinachoitwa Kisiwa Kikubwa Chekundu, ndicho kisiwa cha nne kwa ukubwa duniani. Kina udongo mwekundu, na mimea na viumbe wengi wa pekee wanapatikana huko

[Picha katika ukurasa wa 5]

Tunafurahia kushiriki na wengine katika mafunzo ya Biblia

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kusafiri kulikuwa moja ya matatizo makubwa sana tuliyokabili