Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Utumishi Mutakatifu Ulitufundisha ile “Siri”

Utumishi Mutakatifu Ulitufundisha ile “Siri”

Masimulizi Kuhusu Maisha ya Watu

Utumishi Mutakatifu Ulitufundisha ile “Siri”

Olivier Randriamora anaeleza maisha yake

“Kwa kweli najua jinsi ya kupungukiwa na vyakula, kwa kweli najua jinsi ya kuwa na wingi. Katika mambo yote na katika hali zote nimejifunza siri ya jinsi ya kushiba na pia jinsi ya kuwa na njaa . . . Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”​—Flp. 4:12, 13.

MANENO hayo ya mutume Paulo yametutia moyo sana mimi na bibi yangu Oly kwa muda murefu. Kama Paulo, tumejifunza ile “siri” kwa kumutegemea kabisa Yehova katika utumishi wetu hapa Madagascar.

Mashahidi wa Yehova walipoanza kujifunza Biblia pamoja na mama yake na Oly katika mwaka wa 1982, Oly nami tulikuwa tumekwisha kuchumbiana. Mimi pia nilikubali funzo la Biblia; kisha, Oly pia akakubali kujifunza. Tulioana mwaka wa 1983, tukabatizwa mwaka wa 1985, na mara moja tukaanza upainia musaidizi. Katika mwezi wa 7, 1986, tulianza upainia wa kawaida.

Katika mwezi wa 9, 1987, tulikuwa mapainia wa pekee. Mugawo wetu wa kwanza ulikuwa muji mudogo uliokuwa kaskazini-mangaribi mwa Madagascar. Katika muji huo hakukuwa kutaniko. Katika Madagascar kuna makabila makubwa 18 na vikundi vingine vingi vya makabila; watu wa huko wana asili na desturi zinazotofautiana sana. Luga kubwa inayozungumuziwa katika Madagascar ni Kimalagasi, lakini watu wanazungumuza pia luga za kienyeji. Basi, tulianza kujifunza luga ya kienyeji inayozungumuziwa katika mugawo wetu mupya, na kufanya hivyo kulitusaidia sana tukubaliwe na watu wa eneo hilo.

Mwanzoni, nilikuwa nikitoa hotuba ya watu wote kila Siku ya Yenga. Kisha hotuba, Oly alikuwa na desturi ya kupiga mikono. Ni sisi wawili tu tuliohuzuria. Tulikuwa tukifanya pia vipindi vyote vya Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi. Oly alikuwa akifanya kipindi chake na mwenye​-nyumba wa kuwazia tu. Tulifarijiwa kabisa wakati mwangalizi mwenye kusafiri alipendekeza kwamba tubadili namna yetu ya kufanya mikutano!

Kwa kuwa posta haikutumainiwa, hatukupokea posho yetu kwa ukawaida. Kwa hiyo, tulijifunza kubembeleza chakula chetu na kutosheleza tu mahitaji mengine ya lazima. Wakati fulani hatukuwa na feza za kutosha za kulipia motokari ili kuhuzuria mukusanyiko wa muzunguko uliofanyika umbali wa kilometre 130. Tunakumbuka shauri moja nzuri ambalo ndugu mumoja alitutolea, yeye alituambia hivi: “Mumuelezee Yehova shida zenu. Kazi munayofanya ni yake.” Kwa hiyo, tulisali na kuamua kufanya safari kwa miguu. Lakini mbele tu tuanze safari, ndugu mumoja alikuja kutuona bila kutuarifu na akatutolea feza—ndizo feza tulizohitaji kabisa ili kulipia safari yetu!

KAZI YA MUZUNGUKO

Katika mwezi wa 2, 1991, nilitiwa kuwa mwangalizi wa muzunguko. Wakati huo, kikundi chetu kidogo kilikuwa kimefikia wahubiri 9, wahubiri watatu kati yao walikuwa wenye kubatizwa, na tulikuwa tukihuzuria watu 50 kwenye mikutano. Kisha kuzoezwa, tulitumika katika muzunguko uliokuwa katika muji mukubwa, Antananarivo. Katika mwaka wa 1993, tulitumwa katika muzunguko upande wa mashariki mwa Madagascar. Hali ya maisha huko ilikuwa tofauti sana na maisha ya Antananarivo.

Ili kufika katika makutaniko na vikundi vya mbali, tulisafiri kwa miguu, wakati fulani tulifanya kilometre 145 tukipita katika milima yenye pori kubwa. Tulichukua tu vitu vya lazima. Hata hivyo, muzigo wetu ulikuwa muzito kwa sababu katika siku hizo kulikuwa na wakati ambapo hotuba ya watu wote ya mwangalizi wa muzunguko ilitia ndani filme ambayo wahuzuriaji walipaswa kutazama, kwa hiyo tulipaswa kubeba mashine ya kuonyesha filme. Oly ndiye aliyekuwa akibeba chombo hicho. Mimi, nilibeba bateri ya volte 12.

Tulitembea karibu kilometre 40 muchana ili kufika kwenye kutaniko lingine. Njiani, tulipanda na kushuka milima, tulivuka mito, na kupita katika matope. Wakati mwingine, tulilala pembeni ya njia, lakini mara nyingi tulitafuta kijiji fulani ili kupata mahali pa kulala. Wakati fulani tuliomba watu tusiowajua watusaidie na mahali pa kulala. Walipotukubalia, tulianza kupika chakula. Oly aliomba chungu cha kupikia na kwenda kwenye muto wa karibu kushota maji. Wakati huo, mimi niliomba shoka ili kupasua kuni ya kupikia chakula. Kila kazi ilituchukua wakati. Wakati fulani tulinunua kuku na kuichinja.

Kisha kula, tulienda kushota maji ili kuoga. Siku zingine tulilala katika mafiga. Mvua iliponyesha, nyumba ilivuya, kwa hiyo tulilazimika kulala tukiegemea ukuta ili tusilowane.

Sikuzote, muradi wetu ulikuwa kuwahubiria wale waliotutolea mahali pa kulala. Tulipofika mahali tulipokuwa tukienda, tulifurahia sana ukaribishaji na wema wa ndugu na dada zetu. Namna walivyofurahia ziara yetu, ilitufanya tusahau taabu yote tuliyopata njiani.

Tulipopangishwa katika familia ya Mashahidi wa Yehova, tuliwasaidia kufanya kazi za nyumbani. Hilo liliwasaidia wapate wakati wa kwenda katika mahubiri pamoja nasi. Hatukulazimisha wale waliotukaribisha watutolee vitu vya beyi sana ao chakula cha hali ya juu.

KUTEMBELEA VIKUNDI VIDOGO VYA MBALI

Tulifurahia kutembelea vikundi vidogo vya mbali. Katika vikundi hivyo kulikuwa na mengi ya kufanya. Mara nyingi hatukuwa na wakati wa ‘kupumuzika kidogo.’ (Mk. 6:31) Mahali fulani, ndugu mumoja na bibi yake walialika kwao mafunzo yao yote, watu 40 ili sisi pia tushiriki wanapojifunza nao. Oly na dada yule waliongoza mafunzo 20 na mimi na ndugu yule tuliongoza mafunzo mengine 20. Kwa kuwa mwanafunzi mumoja alibaki, tulijifunza naye pia. Baadaye, tuliacha kwanza kuongoza mafunzo hayo ili kwenda kwenye mikutano. Kisha mikutano, tuliendelea tena kuongoza mafunzo. Utendaji wa siku hiyo uliweza kumalizika kisha saa mbili za usiku!

Tulienda sisi wote katika jiji jirani pa saa mbili ya asubuhi ili kutembelea kikundi kingine cha mbali. Sisi wote tulivaa manguo ya zamani. Kisha mwendo murefu tukipitia katika pori kubwa, tulifika katika eneo hilo karibu na midi. Mara moja tukavaa manguo yaliyo safi na kuanza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Tulikuwa wahubiri wengi kuliko nyumba tulizokuta katika eneo hilo. Kwa hiyo tulihubiri eneo lote kwa muda wa dakika karibu 30. Kisha tulienda katika kijiji kingine. Kisha kuhubiri hapo, tulianza tena safari yetu ndefu ya kurudi nyumbani. Ili kufika mahali hapo tulitumia wakati mwingi na nguvu nyingi ili kutembea, lakini tulihubiri nyumba kwa nyumba kwa saa karibu moja tu. Mwanzoni, hilo lilituvunja moyo. Hata hivyo, Mashahidi wa eneo hilo hawakunungunika. Waliendelea kuwa wenye shauku.

Kikundi kimoja cha mbali kilikuwa katika muji wa Taviranambo karibu na mulima. Tulipotembelea sehemu hiyo tulikuta familia moja ya Mashahidi ambao waliishi katika nyumba ya chumba kimoja. Kulikuwa nyumba nyingine ndogo iliyotumiwa kuwa mahali pa mikutano. Mara moja, ndugu aliyetupangisha akaanza kuita kwa sauti, “Wandugu!” Kutoka mulima mwingine mutu fulani akajibu, “Oh!” Ndugu huyo akasema tena kwa sauti, “Mwangalizi wa muzunguko amefika!” Ndugu waliokuwa upande mwingine wakajibu, “Ndiyo!” Kwa njia hiyo habari ikafikia pia wale waliokuwa mbali zaidi. Mara moja watu wakaanza kukusanyika, na wakati mukutano ulianza, kulikuwa na watu zaidi ya 100.

MAGUMU YA KUSAFIRI

Katika mwaka wa 1996 tulitumwa katika muzunguko karibu na Antananarivo, sehemu yenye milima. Muzunguko huu nao ulikuwa na magumu yake ya pekee. Hakukuwa motokari za kusafirisha watu kwa ukawaida ili kwenda katika maeneo ya mbali. Tulikuwa na programu ya kutembelea kikundi kimoja huko Beankàna (Besakay), umbali wa kilometre 240 kutoka Antananarivo. Kisha kusikilizana na shofere, tuliingia katika kamio kidogo iliyokuwa ikijielekeza katika eneo hilo. Tulikuwa zaidi ya watu 30 katika motokari hiyo, wamoja wakiwa juu ya motokari na wengine wakininginia nyuma.

Kamio hiyo ilikufa, nasi tukaendelea kwa miguu. Kisha kutembea kwa muda wa saa fulani, motokari moja kubwa ilikuja. Ilikuwa imekwisha kujaa watu na mizigo, lakini tuliisimamisha. Tukapanda ndani na kusafiri tukiwa wima. Kisha tukafika ku mutoni, kilalo kilikuwa kinatengenezwa. Mara nyingine tena tukashuka na kutembea kwa miguu, mwishowe tukafika katika kijiji kimoja kidogo, ambapo mapainia fulani wa pekee waliishi. Ijapokuwa hatukuwa na programu ya kutembelea kijiji hicho, tulipitisha wakati pamoja nao tukihubiri na kungojea kilalo kitengenezwe ili tupate motokari ingine na kuendelea na safari.

Motokari ilifika kisha juma moja, kwa hiyo tukaendelea na safari yetu. Barabara ilikuwa na mashimo-mashimo makubwa. Mara kwa mara tulipaswa kusaidia kusukuma motokari katika maji mengi, yaliyotufikia kwenye magoti, na mara nyingi tulianguka na tulishindwa kufanya motokari itembee. Asubuhi sana tulifika katika kijiji kimoja kidogo, mahali tuliposhuka. Tukaacha barabara kubwa, tukaendelea kwa miguu kupitia katika mashamba ya mupunga, katika njia mbaya yenye kujaa matope yenye maji yenye kutufikia kwenye viuno. Kisha tukafika mahali tulipokwenda.

Hiyo ilikuwa mara yetu ya kwanza kutembelea eneo hilo, kwa hiyo tukaamua kuhubiria watu waliokuwa wakitumika katika mashamba ya mupunga na kuwauliza mahali Mashahidi wa hapo wanaweza kupatikana. Tulifurahi sana tulipoambiwa kama wafanyakazi hao katika mashamba ya mupunga ni ndugu zetu, Mashahidi wa Yehova!

KUWATIA WENGINE MOYO ILI WAANZE UTUMISHI WA WAKATI WOTE

Kwa miaka mingi, tulipata furaha sana kuona matokeo ya kuwatia wengine moyo ili waanze utumishi wa wakati wote. Tulipotembelea kutaniko moja lililokuwa na mapainia wa kawaida 9, tulitia moyo kila painia ajitilie muradi wa kusaidia muhubiri mumoja aanze upainia. Tulipotembelea tena kijiji hicho kisha miezi sita, hesabu ya mapainia wa kawaida ilikuwa imepanda kufikia 22. Dada wawili mapainia waliwatia moyo baba zao, waliokuwa wazee wa kutaniko, ili kuwa mapainia wa kawaida. Ndugu hao pia, wakamutia moyo muzee mwenzao mwengine wa kutaniko kuwa painia wa kawaida. Kisha wakati kidogo, muzee huyo wa tatu akawa painia wa pekee. Baadaye, yeye na bibi yake wakaanza kutumika katika muzunguko. Namna gani wale wazee wengine wawili? Mumoja ni mwangalizi wa muzunguko na mwengine anatukimika katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme.

Tunamushukuru Yehova kila siku kwa musaada wake; tunatambua kabisa kama hatuwezi kutimiza lolote kwa nguvu zetu wenyewe. Ni kweli kwamba wakati fulani tunajisikia kuwa wenye kuchoka na wakati mwengine tunakuwa wangojwa, lakini tunafurahi tunapoona matokeo ya utumishi wetu. Yehova anasaidia kazi yake isonge mbele. Sisi sasa ni mapainia wa pekee na tunafurahi kutoa muchango wetu mudogo katika kazi hiyo. Ndiyo, tumejifunza ile “siri,” kwa kumutegemea Yehova, ‘anayetupatia nguvu.’

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 6]

Tumejifunza ile “siri,” kwa kumutegemea Yehova

[Karte/​Picha kwenye ukurasa wa 4]

Madagascar, inayoitwa Kisiwa Kikubwa Chekundu, ni kisiwa cha ine kikubwa duniani. Udongo wake ni mwekundu, na kuna wanyama na miti ya aina ya pekee katika kisiwa hicho

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kusafiri ndio ilikuwa shida kubwa zaidi tuliyopambana nayo

[Picha katika ukurasa wa 5]

Tunafurahia kuongoza mafunzo ya Biblia