Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni “Mfunuaji wa Siri”

Yehova Ni “Mfunuaji wa Siri”

Yehova Ni “Mfunuaji wa Siri”

“Kwa kweli Mungu wenu ni Mungu wa miungu na Bwana wa wafalme na Mfunuaji wa siri.”—DAN. 2:47.

UNGEJIBUJE?

Yehova ametufunulia mambo gani kuhusu wakati ujao?

Vichwa sita vya kwanza vya yule mnyama-mwitu vinafananisha nini?

Kuna uhusiano gani kati ya mnyama-mwitu na ile sanamu ambayo Nebukadneza aliona?

1, 2. Yehova ametufunulia nini, na kwa nini amefanya hivyo?

NI SERIKALI gani zitakazokuwa zikiitawala dunia wakati Ufalme wa Mungu utakapoukomesha utawala wa wanadamu? Tunajua jibu la swali hilo kwa sababu tumefunuliwa na Yehova Mungu ambaye ni “Mfunuaji wa siri.” Anatuwezesha kutambua serikali hizo kupitia mambo yaliyoandikwa na nabii Danieli na mtume Yohana.

2 Yehova aliwafunulia wanaume hao mfululizo wa maono kuhusu wanyama-mwitu wanaofuatana mmoja baada ya mwingine. Pia alimwambia Danieli maana ya ndoto ya kinabii kuhusu sanamu kubwa sana yenye madini mbalimbali. Yehova alihakikisha kwamba masimulizi hayo yameandikwa na kuhifadhiwa katika Biblia kwa faida yetu. (Rom. 15:4) Alifanya hivyo ili kuimarisha tumaini letu la kwamba hivi karibuni Ufalme wake utazivunja serikali zote za wanadamu.—Dan. 2:44.

3. Ili kuelewa unabii kwa usahihi, tunahitaji kuelewa nini kwanza, na kwa nini?

3 Kwa ujumla, masimulizi ya Danieli na Yohana hayafunui tu kuhusu wafalme wanane, au serikali za wanadamu, bali pia yanaonyesha jinsi ambavyo serikali hizo zingefuatana. Hata hivyo, tunaweza kuelewa kwa usahihi unabii huo mbalimbali ikiwa tu tunaelewa maana ya unabii wa kwanza kabisa ulioandikwa katika Biblia. Kwa nini? Kwa sababu kutimizwa kwa unabii huo ndilo jambo kuu linalokaziwa katika Biblia yote. Katika njia fulani, unabii mwingine wote unategemea unabii huo wa kwanza.

UZAO WA NYOKA NA MNYAMA-MWITU

4. Uzao wa mwanamke unatia ndani nani, na uzao huo utafanya nini?

4 Mara tu baada ya uasi katika Edeni, Yehova alitoa ahadi ya kwamba “mwanamke” angetokeza “uzao.” * (Soma Mwanzo 3:15.) Mwishowe, uzao huo ungemponda nyoka kichwa, yaani, Shetani. Baadaye, Yehova alifunua kwamba uzao huo ungetokana na Abrahamu, ungetoka katika taifa la Israeli, katika kabila la Yuda, na katika ukoo wa Mfalme Daudi. (Mwa. 22:15-18; 49:10; Zab. 89:3, 4; Luka 1:30-33) Kristo Yesu ndiye aliyekuwa sehemu ya msingi ya uzao huo. (Gal. 3:16) Washiriki wa kutaniko la Kikristo waliotiwa mafuta kwa roho ndio sehemu ya pili ya uzao huo. (Gal. 3:26-29) Yesu na hao watiwa-mafuta wanaungana kufanyiza Ufalme wa Mungu ambao utatumiwa na Mungu kumponda Shetani.—Luka 12:32; Rom. 16:20.

5, 6. (a) Danieli na Yohana wanataja serikali ngapi kuu? (b) Vichwa vya yule mnyama-mwitu wa kitabu cha Ufunuo vinafananisha nini?

5 Unabii huo wa kwanza uliotolewa katika Edeni ulisema pia kwamba Shetani angetokeza “uzao.” Uzao wake ungeonyesha uadui, au chuki, kuelekea uzao wa mwanamke. Uzao wa nyoka ni nani? Ni wote wanaomwiga Shetani kwa kumchukia Mungu na kuwapinga watu wa Mungu. Katika historia yote, Shetani amepanga uzao wake katika makundi mbalimbali ya kisiasa, au falme. (Luka 4:5, 6) Hata hivyo, ni falme chache sana za wanadamu ambazo zimejitahidi sana kuwapinga watu wa Mungu, iwe ni taifa la Israeli au kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta. Kwa nini jambo hilo ni muhimu? Kwa sababu linaeleza kwa nini maono ya Danieli na Yohana yanafafanua jumla ya falme nane kuu peke yake.

6 Mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., Yesu aliyefufuliwa alimpa mtume Yohana mfululizo wa maono yenye kustaajabisha. (Ufu. 1:1) Katika moja ya maono hayo, Yohana alimwona Ibilisi, anayefananishwa na joka mkubwa, akiwa amesimama kwenye ufuo wa bahari kubwa. (Soma Ufunuo 13:1, 2.) Yohana aliona pia mnyama-mwitu wa ajabu akipanda kutoka katika bahari hiyo, naye akapokea mamlaka kubwa kutoka kwa Ibilisi. Baadaye malaika anamwambia Yohana kwamba vichwa saba vya mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu, ambaye ni mfano wa mnyama-mwitu anayetajwa kwenye Ufunuo 13:1, vinafananisha “wafalme saba,” au serikali. (Ufu. 13:14, 15; 17:3, 9, 10) Yohana alipoandika maneno hayo, wafalme watano kati yao walikuwa tayari wameanguka, mmoja alikuwa akitawala wakati huo, na mmoja alikuwa “bado hajafika.” Falme au serikali hizo kuu za ulimwengu ni zipi? Acheni tuchunguze kila kichwa cha mnyama-mwitu huyo anayezungumziwa katika kitabu cha Ufunuo. Tutaona pia jinsi maandishi ya Danieli yalivyotaja mambo mengine ya ziada ambayo ni muhimu kuhusu nyingi kati ya falme hizo, na alitabiri baadhi ya mambo hayo karne nyingi kabla falme hizo hazijatokea.

VICHWA VIWILI VYA KWANZA —MISRI NA ASHURU

7. Kichwa cha kwanza kinafananisha nini, na kwa nini?

7 Kichwa cha kwanza cha huyo mnyama-mwitu kinafananisha Misri. Kwa nini? Kwa sababu Misri ilikuwa serikali ya kwanza kuu kuonyesha uadui dhidi ya watu wa Mungu. Wazao wa Abrahamu, ambao kupitia kwao uzao ulioahidiwa wa mwanamke ungetokea, waliongezeka na kuwa wengi huko Misri. Kisha, Misri ikaanza kuwakandamiza Waisraeli. Shetani alijaribu kuwafagilia mbali watu wa Mungu kabla ya uzao huo kutokea. Jinsi gani? Kwa kumchochea Farao awaangamize watoto wote wa kiume Waisraeli. Yehova alizuia jaribio hilo naye akawaweka huru watu wake kutoka utumwani huko Misri. (Kut. 1:15-20; 14:13) Baadaye akawawezesha Waisraeli waimiliki Nchi ya Ahadi.

8. Kichwa cha pili kinafananisha nini, na kilijaribu kufanya nini?

8 Kichwa cha pili cha yule mnyama-mwitu kinafananisha Ashuru. Ufalme huo wenye nguvu ulijaribu pia kuwafagilia mbali watu wa Mungu. Ni kweli kwamba Yehova aliutumia ufalme wa Ashuru ili kuuadhibu ufalme wa makabila kumi ya Israeli kwa sababu ya ibada ya sanamu na uasi wao. Hata hivyo, ufalme wa Ashuru ulilishambulia jiji la Yerusalemu. Huenda Shetani alikuwa na lengo la kuuangamiza kabisa ukoo wa kifalme ambao mwishowe ungetokeza Yesu. Shambulizi hilo halikuwa sehemu ya kusudi la Yehova, na kwa sababu hiyo aliwakomboa kimuujiza watu wake waaminifu kwa kuwaharibu wavamizi.—2 Fal. 19:32-35; Isa. 10:5, 6, 12-15.

KICHWA CHA TATU—BABILONI

9, 10. (a) Yehova aliwaruhusu Wababiloni wafanye nini? (b) Ili unabii utimie, ilikuwa lazima mambo gani yatukie?

9 Kichwa cha tatu cha mnyama-mwitu ambaye Yohana aliona kinafananisha ufalme wenye mji mkuu ulioitwa Babiloni. Yehova aliwaruhusu Wababiloni walishinde jiji la Yerusalemu na kuwapeleka watu wake utekwani. Hata hivyo, kabla ya kuruhusu Waisraeli waaibishwe kwa njia hiyo, Yehova aliwaonya watu hao walioasi kwamba msiba huo ungewapata. (2 Fal. 20:16-18) Alitabiri kwamba ukoo wa wafalme wa kibinadamu ambao ilisemekana kwamba wanaketi juu ya “kiti cha ufalme cha Yehova” huko Yerusalemu ungeondolewa. (1 Nya. 29:23) Hata hivyo, Yehova pia aliahidi kwamba mzao wa Mfalme Daudi, mzao ambaye alikuwa na “haki ya kisheria,” angekuja na kuchukua mamlaka hayo.—Eze. 21:25-27.

10 Unabii mwingine ulionyesha kwamba bado Wayahudi wangekuwa wakiabudu kwenye hekalu la Yerusalemu wakati wa kuja kwa Masihi au Mtiwa-Mafuta aliyeahidiwa. (Dan. 9:24-27) Unabii fulani ulioandikwa mapema kabla ya Waisraeli kupelekwa utekwani Babiloni, ulisema kwamba huyo Masihi angezaliwa Bethlehemu. (Mika 5:2) Ili unabii huo mbalimbali utimie, Wayahudi wangehitaji kuwekwa huru kutoka utekwani, warudi katika nchi yao, na kujenga upya hekalu. Lakini sheria za Wababiloni hazikuruhusu mateka waachiliwe huru. Tatizo hilo lingetatuliwaje? Yehova aliwafunulia manabii wake jibu la swali hilo.—Amo. 3:7.

11. Ni mifano gani mbalimbali inayotumiwa kufananisha Milki ya Babiloni? (Tazama maelezo ya chini.)

11 Nabii Danieli alikuwa miongoni mwa mateka waliopelekwa Babiloni. (Dan. 1:1-6) Yehova alimtumia kufunua jinsi ambavyo falme zingefuatana baada ya serikali hiyo kuu ya ulimwengu kuanguka. Yehova alifunua siri hizo akitumia mifano mbalimbali. Kwa mfano, alimletea Mfalme Nebukadneza wa Babiloni ndoto kuhusu sanamu kubwa sana ambayo ilitengenezwa kwa madini ya aina mbalimbali. (Soma Danieli 2:1, 19, 31-38.) Kupitia Danieli, Yehova alifunua kwamba kichwa cha dhahabu cha sanamu hiyo kilifananisha Milki ya Babiloni. * Serikali kuu ya ulimwengu iliyotawala baada ya Babiloni ilifananishwa na kifua na mikono ya fedha. Ingekuwa serikali gani hiyo, na ingewatendeaje watu wa Mungu?

KICHWA CHA NNE—UMEDI NA UAJEMI

12, 13. (a) Yehova alifunua nini kuhusu kushindwa kwa Babiloni? (b) Kwa nini serikali ya Umedi na Uajemi inafananishwa kwa kufaa na kichwa cha nne cha yule mnyama-mwitu?

12 Kwa zaidi ya karne moja kabla ya siku za Danieli, Yehova alifunua kupitia nabii Isaya maelezo mengi kuhusu serikali kuu ya ulimwengu ambayo ingeshinda Babiloni. Yehova hakufunua tu jinsi ambavyo jiji la Babiloni lingeshindwa bali pia alifunua jina la yule ambaye angelishinda jiji hilo. Kiongozi huyo aliitwa Koreshi Mwajemi. (Isa. 44:28–45:2) Danieli alipata maono mengine mawili kuhusu Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Umedi na Uajemi. Katika moja ya maono hayo, ufalme huo ulifananishwa na dubu ambaye ameinuliwa upande mmoja. Dubu huyo aliambiwa ‘ale nyama nyingi.’ (Dan. 7:5) Katika maono tofauti, Danieli aliona serikali hiyo pacha ya ulimwengu yenye wafalme wawili ikifananishwa na kondoo-dume mwenye pembe mbili.—Dan. 8:3, 20.

13 Yehova aliitumia Milki ya Umedi na Uajemi kutimiza unabii kwa kuishinda Babiloni na kuwarudisha Waisraeli kwenye nchi yao. (2 Nya. 36:22, 23) Hata hivyo, baadaye serikali hiyo kuu ilikuwa karibu kuwafagilia mbali watu wa Mungu. Kitabu cha Biblia cha Esta kinaeleza kuhusu njama fulani iliyopangwa na waziri mkuu wa Uajemi, aliyeitwa Hamani. Alipanga njama ili Wayahudi wote walioishi katika Milki kubwa sana ya Uajemi waangamizwe naye akapanga tarehe hususa ya kuwaangamiza Wayahudi wote. Hata hivyo, kwa mara nyingine tena Yehova aliingilia kati na kuwalinda watu Wake kutokana na chuki ya uzao wa Shetani. (Esta 1:1-3; 3:8, 9; 8:3, 9-14) Kwa hiyo, serikali ya Umedi na Uajemi inafananishwa kwa kufaa na kichwa cha nne cha mnyama-mwitu wa kitabu cha Ufunuo.

KICHWA CHA TANO—UGIRIKI

14, 15. Yehova anafunua mambo gani kuhusu Milki ya kale ya Ugiriki?

14 Kichwa cha tano cha mnyama-mwitu wa kitabu cha Ufunuo kinafananisha Ugiriki. Kama Danieli alivyokuwa amefunua mapema alipofasiri ndoto ya Nebukadneza, serikali hiyo kuu inafananishwa pia na tumbo na mapaja ya shaba ya ile sanamu. Danieli alipata pia maono mawili ambayo yanafunua mambo mengi yenye kustaajabisha kuhusu milki hiyo na kuhusu mtawala wake aliyekuwa maarufu zaidi.

15 Katika moja ya maono hayo, Danieli aliona milki ya Ugiriki ambayo ilifananishwa na chui mwenye mabawa manne, kuonyesha kwamba milki hiyo ingeshinda kwa kasi sana. (Dan. 7:6) Katika maono mengine, Danieli alieleza jinsi mbuzi mwenye pembe moja kubwa anavyomuua haraka kondoo-dume mwenye pembe mbili, yaani, Umedi na Uajemi. Yehova alimwambia Danieli kwamba mbuzi huyo alifananisha Ugiriki na ile pembe kubwa ilifananisha mmoja wa wafalme wake. Vilevile, Danieli alisema kwamba ile pembe kubwa ingevunjwa na kisha pembe nne ndogo zaidi zingekua au kutokea mahali pake. Hata ingawa unabii huo uliandikwa miaka mingi sana kabla ya Ugiriki kuanza kutawala, kila jambo lilitimia. Aleksanda Mkuu, mfalme maarufu zaidi wa Milki ya kale ya Ugiriki, aliongoza mashambulizi dhidi ya Umedi na Uajemi. Hata hivyo, pembe hiyo ilivunjika mara moja wakati mfalme huyo mkuu alipokufa akiwa katika upeo wa mamlaka yake na akiwa na umri wa miaka 32 tu. Kisha, ufalme wake uligawanyika mwishowe na kuchukuliwa na majenerali wake wanne.—Soma Danieli 8:20-22.

16. Antioko wa Nne alifanya nini?

16 Baada ya kushinda Uajemi, serikali ya Ugiriki ilitawala nchi ya watu wa Mungu. Wakati huo, Wayahudi walimiliki tena Nchi ya Ahadi na kujenga upya hekalu huko Yerusalemu. Bado walikuwa watu waliochaguliwa na Mungu, na hekalu lililojengwa upya bado lilikuwa kitovu cha ibada ya kweli. Hata hivyo, katika karne ya pili K.W.K., kichwa cha tano cha mnyama-mwitu, yaani, serikali ya Ugiriki iliwashambulia watu wa Mungu. Antioko wa Nne, mmoja wa warithi wa milki ya Aleksanda iliyogawanyika, alijenga madhabahu ya kipagani kwenye uwanja wa hekalu huko Yerusalemu na akaagiza kwamba mtu yeyote aliyefuata dini ya Kiyahudi alikuwa na hatia iliyostahili adhabu ya kifo. Uzao wa Shetani ulitenda kwa njia ya chuki kama nini! Hata hivyo, muda si muda, Ugiriki iling’olewa kuwa serikali kuu ya ulimwengu. Ni serikali gani ingekuwa kichwa cha sita cha yule mnyama-mwitu?

KICHWA CHA SITA CHENYE ‘KUOGOPESHA NA KUTISHA’—ROMA

17. Kichwa cha sita kilitimiza sehemu gani kubwa katika utimizo wa Mwanzo 3:15?

17 Roma ndiyo iliyokuwa serikali kuu ya ulimwengu wakati Yohana alipopata maono ya yule mnyama-mwitu. (Ufu. 17:10) Kichwa hicho cha sita kilitimiza sehemu kubwa katika utimizo wa unabii ulioandikwa katika Mwanzo 3:15. Shetani aliwatumia maofisa Waroma kuupiga na kuulemaza kwa muda ule uzao, kwa kuutia jeraha “kwenye kisigino.” Jinsi gani? Walimhukumu Yesu kwa mashtaka ya uwongo ya uchochezi na kuagiza auawe. (Mt. 27:26) Lakini punde si punde, jeraha hilo lilipona kwa sababu Yehova alimfufua Yesu.

18. (a) Yehova alichagua taifa gani jipya, na kwa nini? (b) Uzao wa nyoka uliendelea jinsi gani kuonyesha chuki dhidi ya uzao wa mwanamke?

18 Viongozi wa kidini katika Israeli walishirikiana na Roma kumpinga Yesu, na pia watu wengi katika taifa hilo wakamkataa. Kwa hiyo, Yehova aliwakataa Waisraeli wa asili wasiwe watu wake. (Mt. 23:38; Mdo. 2:22, 23) Kisha akachagua taifa jipya, “Israeli wa Mungu.” (Gal. 3:26-29; 6:16) Taifa hilo lilikuwa kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta ambalo lilitia ndani Wayahudi pamoja na watu wasio Wayahudi. (Efe. 2:11-18) Baada ya kifo na ufufuo wa Yesu, uzao wa nyoka uliendelea kuonyesha chuki dhidi ya uzao wa mwanamke. Mara nyingi, serikali ya Roma ilijaribu kufagilia mbali kutaniko la Kikristo, sehemu ya pili ya ule uzao. *

19. (a) Danieli anaeleza nini kuhusu serikali ya sita kuu ya ulimwengu? (b) Makala nyingine itazungumzia nini?

19 Katika ndoto ambayo Danieli alimfasiria Nebukadneza, Roma inafananishwa na miguu ya chuma. (Dan. 2:33) Danieli aliona pia maono ambayo hayafunui tu kuhusu Milki ya Roma bali pia serikali kuu ya ulimwengu inayofuata ambayo ingetokana na Roma. (Soma Danieli 7:7, 8.) Kwa karne nyingi, maadui wa serikali ya Roma waliiona serikali hiyo kuwa yenye ‘kuogopesha na kutisha na yenye nguvu isivyo kawaida.’ Hata hivyo, unabii ulitabiri kwamba zile “pembe kumi” zingekua kutokana na milki hiyo na pembe moja hasa ingepata umaarufu. Hizo pembe kumi zinafananisha nini, na ile pembe ndogo inafananisha nini? Ile pembe ndogo inalinganaje na maelezo kuhusu ile sanamu kubwa ambayo Nebukadneza aliona? Makala iliyo kwenye ukurasa wa 14 itajibu maswali hayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Mwanamke huyo anafananisha tengenezo la Yehova ambalo ni kama mke, linalofanyizwa na viumbe wa roho walio mbinguni.—Isa. 54:1; Gal. 4:26; Ufu. 12:1, 2.

^ fu. 11 Babiloni inafananishwa na kichwa cha ile sanamu katika kitabu cha Danieli na pia kichwa cha tatu cha yule mnyama-mwitu wa kitabu cha Ufunuo. Tazama chati kwenye ukurasa wa 12-13.

^ fu. 18 Ingawa Roma iliharibu Yerusalemu mwaka wa 70 W.K., shambulizi hilo halikuwa sehemu ya utimizo wa andiko la Mwanzo 3:15. Kufikia wakati huo, Waisraeli wa asili hawakuwa tena taifa lililochaguliwa na Mungu.

[Maswali ya Funzo]