Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yehova Anafunua Mambo Ambayo “Lazima Yatendeke Upesi”

Yehova Anafunua Mambo Ambayo “Lazima Yatendeke Upesi”

Yehova Anafunua Mambo Ambayo “Lazima Yatendeke Upesi”

‘Ufunuo kupitia Yesu Kristo, ambao Mungu alimupa, kuwaonyesha watumwa wake mambo ambayo lazima yatendeke upesi.’​—UFU. 1:1.

UNAWEZA KUJIBU NAMNA GANI?

Ni sehemu gani za sanamu kubwa ya Danieli zinazofananisha Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika?

Namna gani Yohana anaonyesha kama Serikali Kubwa ya Uingereza na Amerika ndio imetokeza Umoja wa Mataifa?

Danieli na Yohana wanaeleza namna gani mwisho wa utawala wa wanadamu?

1, 2. (a) Unabii wa Danieli na wa Yohana unatusaidia kuelewa nini? (b) Vichwa sita vya kwanza vya munyama-mwitu vinafananisha nini?

 UNABII wa Danieli na wa Yohana unapatana kwa njia inayotusaidia kuelewa mambo mengi yanayotokea katika ulimwengu leo na yale yatakayotokea wakati ujao. Maono ya Yohana ya munyama​-mwitu na maelezo ya Danieli juu ya munyama mwenye kuogopesha aliyekuwa na pembe kumi, na mafasiriyo yake ya sanamu kubwa, yanatufundisha nini? Kuelewa vizuri maneno hayo ya kiunabii kutatuchochea kufanya nini?

2 Habari ya kwanza tuliyojifunza ilizungumuzia maono ya Yohana ya munyama​-mwitu. (Ufu., sura ya 13) Tulijifunza kama vichwa sita vya kwanza vinafananisha serikali za Misri, Asiria, Babiloni, Utawala wa Wamede na Waperse, Ugiriki na Roma. Serikali hizo zote zilichukia uzao wa mwanamuke. (Mwa. 3:15) Kichwa cha sita, ni kusema, Roma kiliendelea kuutawala ulimwengu kwa miaka mingi kisha Yohana kuandika maono yake. Hata hivyo, mwishowe utawala mwengine, maana yake, kichwa cha saba, ungechukua nafasi ya Roma. Ni utawala gani huo ambao ulichukua nafasi hiyo, na ungetendea namna gani uzao wa mwanamuke?

NAMNA SERIKALI YA UINGEREZA NA AMERIKA ILIVYOANZA

3. Munyama mwenye kuogopesha na aliye na pembe kumi anafananisha nini, na pembe kumi zinafananisha nini?

3 Ili kuelewa maana ya kichwa cha saba cha munyama​-mwitu anayetajwa katika Ufunuo sura ya 13, tunapaswa kulinganisha maono ya Yohana na maono ya Danieli inayozungumuzia munyama mwenye kuogopesha aliye na pembe kumi. * (Soma Danieli 7:7, 8, 23, 24.) Munyama huyo ambaye Danieli aliona anafananisha Serikali kubwa ya Ulimwengu ya Roma. (Ona kisanduku kwenye ukurasa wa 12-13.) Katika kipindi cha miaka 500 kisha Yesu, Utawala wa Roma ulianza kugawanyika. Pembe kumi za munyama huyo mwenye kuogopesha zinafananisha falme zilizotokana na utawala huo.

4, 5. (a) Pembe ndogo ilifanya nini? (b) Kichwa cha saba cha munyama-mwitu kinafananisha nini?

4 Katika maono yake ya munyama mwenye pembe kumi ao falme kumi, Danieli aliona pembe ingine, “ndogo,” ikitokea na kuchukua nafasi ya pembe tatu. Hilo lilitimia wakati Uingereza, iliyokuwa sehemu ndogo iliyotokana na Utawala wa Roma, ilifikia kuwa ufalme wenye nguvu. Espagne, Hollande, na France zilikuwa pia sehemu ya Utawala wa Roma. Kufikia miaka ya 1600, inchi hizo zilikuwa na nguvu sana kuliko Uingereza. Hata hivyo, Uingereza ikazishinda inchi hizo zote na kuwa ufalme wenye nguvu na wa maana kuliko falme hizo. Katika miaka ya 1700, Uingereza ilianza kuwa serikali kubwa na yenye nguvu sana duniani. Lakini mupaka hapo ilikuwa bado haijakuwa kichwa cha saba cha munyama​-mwitu.

5 Ijapokuwa Uingereza ilipata nguvu sana, sehemu za Amerika ya kaskazini zilizokuwa zikitawaliwa na Uingereza, ziliasi na kuunda muungano wa Amerika. Hata hivyo, Uingereza haikuzuia Amerika kuwa inchi yenye nguvu, na ililinda wanajeshi wa maji wa Amerika. Kisha, siku ya Bwana kuanza katika mwaka 1914, Uingereza ilikuwa na nguvu sana na ikajulikana sana katika historia na Amerika ikawa tajiri sana duniani. * Wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, Amerika ilifanya urafiki wa pekee na Uingereza. Basi kichwa cha saba cha munyama kikawa Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika. Namna gani kichwa hiki kilitendea uzao wa mwanamuke?

6. Kichwa cha saba kimewatendea namna gani watu wa Mungu?

6 Siku chache kisha siku ya Bwana kuanza, kichwa cha saba kilianza kushambulia watu wa Mungu, ni kusema, ndugu za Kristo waliokuwa wangali duniani. (Mt. 25:40) Yesu alionyesha kama wakati wa kuwapo kwake, ndugu zake, ni kusema, mabaki ya uzao, wangekuwa wenye kufanya kazi nyingi duniani. (Mt. 24:45-47; Gal. 3:26-29) Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika ilianza kushambulia watakatifu hao. (Ufu. 13:3, 7) Wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, serikali hiyo iliwatesa watu wa Mungu, ikakataza vitabu vyao, na ikawafunga wawakilishi wa mutumwa mwaminifu. Kwa kipindi fulani ilionekana kama vile kichwa hicho cha saba kiliua kazi ya kuhubiri. Yehova alikuwa amekwisha kuona matukio hayo ya ajabu na alimufunulia Yohana mambo hayo. Tena, Mungu alimuambia Yohana kama sehemu ya pili ya uzao ingepata tena nguvu ili kumutumikia Yehova zaidi. (Ufu. 11:3, 7-11) Historia ya watumishi wa Yehova wa kisasa inaonyesha kama mambo hayo yalitendeka.

SERIKALI KUBWA YA ULIMWENGU YA UINGEREZA NA AMERIKA NA MIGUU YA CHUMA NA UDONGO

7. Ni sehemu gani ya munyama mwenye vichwa saba anayetajwa katika unabii wa Yohana inayolingana na sanamu kubwa inayotajwa katika unabii wa Danieli?

7 Ni sehemu gani ya munyama mwenye vichwa saba anayetajwa katika unabii wa Yohana inayolingana na sanamu kubwa inayotajwa katika unabii wa Danieli? Ni serikali ya Uingereza na Amerika iliyotokana na Utawala wa Roma. Basi, tuseme nini kuhusu miguu ya sanamu ya Danieli? Miguu hiyo, ilionekana kuwa muchanganyiko wa chuma na udongo. (Soma Danieli 2:41-43.) Muchanganyiko wa chuma na udongo ulitokea wakati kichwa cha saba, ni kusema, Uingereza na Amerika, kilianza kuwa Serikali Kubwa ya Ulimwengu. Kama vile tu chuma inapochangana na udongo inatoa chombo kilicho zaifu, ndivyo, Serikali Kubwa ya Uingereza na Amerika ni zaifu kuliko Roma. Hilo lilionekana namna gani?

8, 9. (a) Namna gani serikali kubwa ya saba ilionekana kuwa nguvu kama chuma? (b) Udongo wa miguu ya sanamu kubwa unafananisha nini?

8 Kisha wakati fulani, kichwa cha saba cha munyama kilitenda kama chuma. Kwa mufano, kilionyesha nguvu zake kwa kushinda Vita ya Kwanza ya Ulimwengu. Wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu, Serikali Kubwa ya Uingereza na Amerika ilikuwa nguvu kama chuma. * Kisha vita hiyo, kichwa cha saba kiliendelea kwa wakati fulani kuwa nguvu kama chuma. Lakini, kuanzia mwanzo na kuendelea, utawala huo ulio kama chuma umechanganywa na udongo.

9 Kwa miaka mingi watumishi wa Yehova walitafuta kuelewa maana ya miguu ya sanamu kubwa inayozungumuziwa katika kitabu cha Danieli. Danieli 2:41 inaonyesha kama muchanganyiko wa chuma na udogo unafanisha “ufalme” mumoja, wala si falme nyingi. Kwa hiyo, udongo unafananisha sehemu ao mambo mengine yenye kuleta migawanyiko mahali pote ambapo Serikali Kubwa ya Uingereza na Amerika inatawala; na sehemu hizo ao mambo hayo yanafanya serikali hiyo iwe zaifu ao zinapunguza nguvu zake za kutenda kuliko serikali ya Roma ambayo inafananishwa na miguu ya chuma. Unabii wa Danieli unasema kama udongo unamaanisha “uzao wa wanadamu,” ao watu wa kawaida. (Dan. 2:43) Mahali pote Serikali Kubwa ya Uingereza na Amerika inapotawala, watu wanaregeza nguvu ya serikali hiyo kwa kuomba haki zao ziheshimiwe; wanafanya hivyo kupitia, kampanye za kutetea haki za raia, vyama vya wafanya​-kazi, na vyama vya kupigania uhuru. Watu wa kawaida wanaregeza uwezo wa Serikali Kubwa ya Ulimwengu, ni kusema, Uingereza na Amerika, na kuifanya isitende tena kama ilivyokuwa ikitenda hapo mwanzoni kama chuma. Tena, kwa sababu ni sehemu tu ya watu ndio imemuchagua kiongozi wakati wa uchaguzi na pia kwa sababu ya maoni tofauti ya kisiasa ya wenye kupinga, hata viongozi wenye kupendwa sana na wanainchi hawana uwezo wa kutimiza mipango yao ao mambo waliyoahidi. Danieli alitabiri kama ‘sehemu moja ya ufalme huo itakuwa yenye nguvu na nyingine itakuwa zaifu.’​—Dan. 2:42; 2 Tim. 3:1-3.

10, 11. (a) “Miguu” ya sanamu itapatwa na nini? (b) Je, hesabu ya vidole ina maana yoyote ya kiunabii? Fasiria.

10 Leo, Uingereza na Amerika zimeendelea kuwa marafiki, na mara nyingi zinatumika pamoja ili kushugulikia mambo ya ulimwengu. Unabii unaozungumuzia sanamu kubwa na munyama​-mwitu unaonyesha kama hakuna serikali nyingine kubwa ya ulimwengu itakayochukua nafasi ya Serikali Kubwa ya Uingereza na Amerika. Serikali ya Uingereza na Amerika inaweza kuwa zaifu kuliko Roma inayofananishwa na miguu ya chuma, lakini nafasi yake haitachukuliwa na serikali nyingine.

11 Je, hesabu ya vidole vya miguu ya sanamu hiyo kubwa, ina maana fulani ya pekee? Fikiria jambo hili: Katika maono mengine, Danieli anazungumuzia hesabu fulani​—kwa mufano, hesabu ya pembe juu ya vichwa vya wanyama mbalimbali. Hesabu hizo zina maana fulani. Lakini, anapozungumuzia sanamu hiyo, Danieli hataje hesabu ya vidole kwenye miguu. Kwa hiyo, inaonekana kama hesabu hiyo haina maana yoyote kama vile hesabu ya mikono, vidole vya mikono, na miguu ya sanamu haina maana yoyote. Danieli anaonyesha tu kama vidole hivyo vya miguu vinafanyizwa kwa chuma na udongo. Kupitia mafasiriyo hayo, tunaweza kusema kama Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika ndiyo serikali itakayokuwa ikitawala wakati lile “jiwe,” maana yake, Ufalme wa Mungu, litavunja miguu ya sanamu hiyo.​—Dan. 2:45.

UINGEREZA NA AMERIKA NA MUNYAMA​-MWITU MWENYE PEMBE MBILI

12, 13. Munyama-mwitu mwenye pembe mbili anafananisha nini, na anafanya nini?

12 Ijapokuwa Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika ni muchanganyiko wa chuma na udongo, mambo ambayo Yesu alimuonyesha Yohana katika Ufunuo yanaonyesha kama serikali hiyo ingeendelea kuonyesha nguvu yake katika mambo yanayotendeka katika siku za mwisho. Namna gani? Yohana aliona katika maono munyama​-mwitu mwenye pembe mbili anayesema kama joka kubwa. Munyama huyo asiye wa kawaida anafananisha nini? Munyama huyo ana pembe mbili, hiyo inamaanisha serikali mbili zenye nguvu zinazotumika pamoja. Yohana aliona tena Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika, lakini hapa inatimiza daraka fulani la kipekee.​—Soma Ufunuo 13:11-15.

13 Munyama aliye na pembe mbili anawaambia watu wafanye sanamu ya yule munyama​-mwitu aliye na vichwa saba. Yohana aliandika kama sanamu hiyo ya munyama​-mwitu itatokea, kisha itapotea, na baadaye itatokea tena. Jambo hilo lilitokea wakati serikali ya Uingereza na Amerika ilianzisha shirika fulani ili kuunganisha mataifa ya ulimwengu na kuwakilisha serikali zingine za ulimwengu. * Shirika hilo lilitokea kisha Vita ya Kwanza ya Ulimwengu na lilitwa Shirika la Mataifa. Shirika hilo lilipotea wakati Vita ya Pili ya Ulimwengu ilianza. Wakati wa vita hiyo, watu wa Mungu walitangaza kama kulingana na unabii ulio katika Ufunuo, sanamu ya munyama-mwitu ingeinuka tena. Na ndivyo ilivyokuwa, iliinuka ikiwa na jina la Umoja wa Mataifa.​—Ufu. 17:8.

14. Kwa sababu gani Yohana anasema kama sanamu ya munyama-mwitu ni ‘mufalme wa munane’?

14 Yohana alisema kama sanamu ya munyama ni ‘mufalme wa munane.’ Katika maana gani? Sanamu hiyo ya munyama si kichwa cha munane cha munyama​-mwitu. Ni sanamu tu ya munyama​-mwitu huyo. Mamlaka yoyote ya sanamu hiyo inatokana na mataifa yanayofanyiza umoja huo, zaidi sana Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika. (Ufu. 17:10, 11) Lakini, Yohana anasema kama sanamu hiyo ya munyama ni ‘mufalme’ kwa sababu sanamu hiyo inapata mamlaka ya kutenda mambo fulani yatakayobadilisha historia ya ulimwengu huu.

SANAMU YA MUNYAMA INAMURARUA KAHABA

15, 16. Kahaba anafananisha nini, na ni jambo gani limetokea juu ya wale waliokuwa wakimutegemeza?

15 Yohana alizungumuzia mwanamuke kahaba, ambaye anaketi juu ya munyama​-mwitu mwenye rangi nyekundu na kumuongoza. Munyama huyo ndiye sanamu ya munyama​-mwitu mwenye vichwa saba. Kahaba huyo anaitwa ‘Babiloni Mukubwa.’ (Ufu. 17:1-6) Kahaba huyo anafananisha dini zote za uongo, zaidi sana dini zinazojiita kuwa za Kikristo. Dini za uongo zimeendelea kutegemeza sanamu ya munyama-mwitu, yaani, Umoja wa Mataifa, na kujaribu kuongoza shirika hilo.

16 Lakini, katika siku ya Bwana, maji ya Babiloni Mukubwa yangekauka kabisa; maji hayo yanamaanisha watu wanaomutegemeza. (Ufu. 16:12; 17:15) Kwa mufano, wakati sanamu ya munyama ilitokea kwa mara ya kwanza, dini zinazojiita kuwa za Kikristo, ambazo ni sehemu kubwa ya Babiloni Mukubwa, zilikuwa na nguvu katika inchi za Ulaya. Lakini leo, watu wengi hawaheshimu tena dini na viongozi wa kidini na hawaziunge tena mukono. Kwa kweli, watu wengi leo wanasema kama dini zimekuwa chanzo cha vita mbalimbali na matatizo katika ulimwengu. Wengine hata wanasema waziwazi kama inafaa kukataza dini ulimwenguni.

17. Dini ya uongo itapatwa na nini hivi karibuni, na kwa nini?

17 Hata hivyo, dini ya uongo haitapoteza tu nguvu yake polepole na kisha imalizike. Kahaba ataendelea kuwa na nguvu, na atajaribu kuwavuta wafalme wafanye mapenzi yake mupaka wakati Mungu atatia katika mioyo ya wafalme hao wazo fulani. (Soma Ufunuo 17:16, 17.) Hivi karibuni, Yehova atachochea watawala wa dunia hii inayotawaliwa na Shetani, wanaowakilishwa na Umoja wa Mataifa, washambulie dini ya uongo. Wataharibu mali ya kahaba huyo na hataweza tena kuwatawala wafalme wa dunia. Miaka 20 ao 30 iliyopita, jambo hilo lingeweza kuonekana kama haliwezekane. Lakini, mambo yameanza kubadilika. Leo, kahaba ni kama mwenye kuyumbayumba juu ya mugongo wa munyama mwenye rangi nyekundu. Hata hivyo, kahaba huyo hataendelea kumuikalia ao kumuongoza munyama-mwitu milele. Uharibifu wake utakuwa mukubwa na utatokea kwa gafula.​—Ufu. 18:7, 8, 15-19.

KUHARIBIWA KWA MUNYAMA-MWITU

18. (a) Munyama-mwitu atafanya nini, na matokeo yatakuwa nini? (b) Ni serikali gani zitakazoharibiwa na Ufalme wa Mungu kulingana na Danieli 2:44? (Soma kisanduku kilicho kwenye ukurasa wa 17.)

18 Kisha kuharibiwa kwa dini ya uongo, munyama-mwitu, ni kusema, serikali za kidunia zinazoongozwa na Shetani, atachochewa ili ashambulie Ufalme wa Mungu. Kwa kuwa hawawezi kufika mbinguni, wafalme wa dunia watawashambulia vikali watumishi wa Mungu walio duniani, kwa sababu wao wanaunga mukono Ufalme wa Mungu. Hapo sasa vita ya mwisho ya Mungu itapiganwa. (Ufu. 16:13-16; 17:12-14) Danieli anazungumuzia jambo fulani juu ya vita hiyo ya mwisho. (Soma Danieli 2:44.) Munyama​-mwitu anayetajwa katika Ufunuo 13:1, sanamu yake, na munyama​-mwitu mwenye pembe mbili, zitaharibiwa.

19. Tunaweza kuwa na uhakika gani, na sasa ndio wakati wa kufanya nini?

19 Tunaishi katika siku za utawala wa kichwa cha saba. Hakuna kichwa kingine kitakachotokea kwenye munyama mwitu huyo kabla hajaharibiwa. Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika itaendelea kutawala dunia wakati dini ya uongo itaangamizwa. Kila jambo lililoelezwa katika unabii wa Danieli na wa Yohana, limetimia kwelikweli. Kwa hiyo, tunaweza kuwa hakika kama uharibifu wa dini ya uongo na pia vita ya Har-Magedoni vitatukia karibuni. Mungu ametujulisha mambo hayo mbele ya wakati. Je, tutatii maonyo hayo ya kiunabii? (2 Pet. 1:19) Sasa ndio wakati wa kujiweka upande wa Yehova na kuunga mukono Ufalme wake.​—Ufu. 14:6, 7.

[Maelezo ya chini]

^ Katika Biblia namba kumi inatumiwa ili kuonyesha kitu kilicho kamili ao chenye kuenea. Kwa hiyo, katika unabii huu namba kumi inafananisha falme zote zilizotokana na Utawala wa Roma.

^ Uingereza na Amerika zilianza katika miaka ya 1700. Lakini, maono ya Yohana yalionyesha kama serikali kubwa hiyo ingetokea mwanzoni mwa siku ya Bwana. Maono ya kitabu cha Ufunuo yalitimia katika “siku ya Bwana.” (Ufu. 1:10) Uingereza na Amerika zilianza kutumika pamoja zikiwa serikali kubwa ya dunia wakati Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ilianza.

^ Danieli aliona mbele ya wakati namna serikali hiyo ingetokeza uharibifu mukubwa wakati wa vita hiyo, kwa hiyo aliandika hivi: “Naye atasababisha uharibifu kwa njia [yenye kuogopesha].” (Dan. 8:24) Kwa mufano, Amerika ilitupia adui zao bombe mbili za atomike na hilo lilitokeza uharibifu mukubwa sana ambao ulikuwa bado haujafanyika.

^ Soma Ufunuo​—Upeo Wake Mutukufu U Karibu! ukurasa wa 240, 241, 253.

[Maulizo ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

“FALME HIZI ZOTE” NI FALME GANI?

Andiko la Danieli 2:44 linasema kama Ufalme wa Mungu “utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote.” Unabii huo unazungumuzia tu falme zote zinazofananishwa na sehemu mbalimbali za sanamu ambayo mufalme Nebukadneza alilota.

Tuseme nini kuhusu serikali zingine zote za wanadamu? Kitabu cha Ufunuo kinazungumuzia pia wafalme na kinatoa maelezo zaidi. Kitabu hicho kinaonyesha kama “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” watakusanywa ili kupigana na Yehova katika ‘siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote.’ (Ufu. 16:14; 19:19-21) Kwa hiyo, kwenye Har-Magedoni si zile serikali tu zinazofananishwa na sehemu mbalimbali za sanamu ndizo zitaharibiwa, lakini serikali zingine zote za wanadamu zitaharibiwa pia.