Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tutangulize Utumishi wa Yehova?

Kwa Nini Tutangulize Utumishi wa Yehova?

Kwa Nini Tutangulize Utumishi wa Yehova?

“Kinywa changu mwenyewe kitasimulia uadilifu wako, wokovu wako mchana kutwa.”​—ZAB. 71:15.

UNGEJIBUJE?

Ni mambo gani yaliyowafanya Noa, Musa, Yeremia, na Paulo watumie maisha yao kumtumikia Yehova?

Ni nini kitakachokusaidia kuamua jinsi utakavyotumia maisha yako?

Kwa nini umeazimia kutanguliza utumishi wa Yehova maishani?

1, 2. (a) Mtu anaonyesha nini anapojiweka wakfu kwa Yehova? (b) Tunaweza kufaidikaje kwa kuchunguza maamuzi yaliyofanywa na Noa, Musa, Yeremia, na Paulo?

UNAPOJIWEKA wakfu na kubatizwa ukiwa mfuasi wa Yesu, unachukua hatua nzito sana. Kujiweka kwako wakfu kwa Mungu ni uamuzi mzito zaidi ambao wewe binafsi unaweza kufanya. Ni kana kwamba unasema: ‘Yehova, ninataka uwe Bwana wangu katika kila sehemu ya maisha yangu. Mimi ni mtumishi wako. Ninataka uamue jinsi ninavyopaswa kutumia wakati wangu, mambo ninayopaswa kutanguliza maishani, na jinsi ninavyopaswa kutumia mali na vipawa vyangu.’

2 Ikiwa wewe ni Mkristo aliyejiweka wakfu, hivyo ndivyo hasa ulivyomwahidi Yehova. Unastahili pongezi kwa sababu ya uamuzi wako; ulifanya uamuzi unaofaa na wenye hekima. Hata hivyo, inamaanisha nini kumtambua Yehova kuwa Bwana wako inapohusu jinsi unavyotumia wakati wako? Mfano wa Noa, Musa, Yeremia, na mtume Paulo unaweza kutusaidia kuchunguza swali hilo. Kila mmoja wao alimtumikia Yehova kwa nafsi yake yote. Hali yao ni kama yetu. Maamuzi waliyofanya kuhusu mambo waliyotanguliza maishani yanaweza kututia moyo kuchunguza jinsi tunavyotumia wakati wetu.—Mt. 28:19, 20; 2 Tim. 3:1.

KABLA YA GHARIKA

3. Siku zetu zinalinganaje na siku za Noa?

3 Yesu alilinganisha siku za Noa na siku zetu. Alisema hivi: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” Walikuwa “wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.” (Mt. 24:37-39) Wanadamu wengi leo wanaendelea na maisha yao kama kawaida bila kufikiria uharaka wa nyakati zetu. Hawajali maonyo ambayo watumishi wa Mungu wanatangaza. Kama vile watu wa siku za Noa walivyofanya, wengi leo hata wanadhihaki wazo la kwamba Mungu atawaharibu waovu. (2 Pet. 3:3-7) Hata hivyo, katika mazingira hayo yenye uadui, Noa aliutumiaje wakati wake?

4. Noa aliutumiaje wakati wake baada ya kupewa mgawo na Yehova, na kwa nini?

4 Baada ya kujulishwa kusudi la Mungu na kupewa mgawo, Noa alijenga safina ili kuokoa wanadamu na wanyama. (Mwa. 6:13, 14, 22) Pia, Noa alitangaza hukumu ya Yehova iliyokuwa ikija. Mtume Petro anamwita “mhubiri wa uadilifu,” kuonyesha kwamba Noa alijitahidi kuwasaidia majirani wake waone hatari waliyokuwa wakikabili. (Soma 2 Petro 2:5.) Je, unafikiri kwamba lingekuwa jambo la busara kwa Noa na familia yake kujitahidi kufanya biashara, kupata mali zaidi kuliko majirani wao, au kuwa na maisha yenye starehe? Bila shaka la! Kwa kuwa walijua mambo ambayo yangetukia, waliepuka mambo kama hayo yenye kukengeusha fikira.

MAAMUZI YA MWANA-MFALME MMISRI

5, 6. (a) Inaelekea elimu ambayo Musa alipata ilikusudiwa kumtayarisha kwa ajili ya nini? (b) Kwa nini Musa alikataa fursa ya kuishi akiwa mwana-mfalme huko Misri?

5 Sasa, acheni tuone mfano wa Musa. Alikulia katika nyumba ya mfalme wa Misri na binti ya Farao akamlea kama mwanaye. Akiwa mwana-mfalme, alifundishwa “hekima yote ya Wamisri.” (Mdo. 7:22; Kut. 2:9, 10) Inaelekea elimu hiyo ilikusudiwa kumtayarisha ili afanye kazi katika nyumba ya Farao. Angekuja kuwa mtu maarufu katika serikali yenye nguvu zaidi wakati huo. Cheo hicho kingempa nafasi ya kuwa na maisha yenye starehe na kupata vitu vingi vizuri. Lakini je, lengo la Musa lilikuwa kufurahia vitu hivyo?

6 Kwa sababu ya mazoezi aliyopokea mapema maishani kutoka kwa wazazi wake halisi, inaelekea kwamba Musa alijua mambo ambayo Yehova aliwaahidi mababu zake Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Musa aliamini ahadi hizo. Bila shaka, alifikiria kwa makini wakati wake ujao na ushikamanifu wake kwa Yehova. Kwa hiyo, wakati ulipofika wa kuchagua ama kuwa mwana-mfalme wa Misri au mtumwa Mwisraeli, alichagua nini? Musa alichagua “kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu badala ya kufurahia dhambi kwa muda.” (Soma Waebrania 11:24-26.) Baadaye, alifuata mwongozo wa Yehova kuhusu jinsi alivyopaswa kutumia maisha yake. (Kut. 3:2, 6-10) Kwa nini Musa alifanya hivyo? Kwa sababu aliamini ahadi za Mungu. Alikata kauli kwamba hakukuwa na wakati ujao kwa ajili yake huko Misri. Kwa kweli, muda mfupi baadaye taifa hilo lilipondwa kwa mapigo kumi kutoka kwa Mungu. Je, kuna somo lolote leo kwa wale waliojiweka wakfu kwa Yehova? Badala ya kukazia fikira kazi au kufuatilia mambo ya starehe katika mfumo huu wa mambo, tunapaswa kumkazia fikira Yehova na utumishi wake.

YEREMIA ALIJUA MAMBO AMBAYO YANGETUKIA

7. Hali ya Yeremia inalinganaje na hali yetu?

7 Mtu mwingine aliyetanguliza utumishi wa Yehova alikuwa nabii Yeremia. Yehova alimtuma Yeremia akiwa nabii wake kuhubiri ujumbe wa hukumu juu ya majiji ya Yerusalemu na Yuda yaliyoasi imani. Kwa njia fulani, Yeremia aliishi “katika siku za mwisho.” (Yer. 23:19, 20) Alijua vizuri sana kwamba mfumo aliokuwa akiishi ndani yake haungedumu.

8, 9. (a) Kwa nini kufikiri kwa Baruku kulihitaji kurekebishwa? (b) Tunapaswa kufikiria nini tunapofanya mipango yetu?

8 Yeremia hakufanya nini kwa sababu ya mambo aliyoamini? Hakujaribu kujijengea wakati ujao katika mfumo huo ambao ungeharibiwa. Lingekuwa jambo la upumbavu kufanya hivyo. Hata hivyo, kwa wakati fulani, mwandishi wa Yeremia, Baruku, alikuwa na mtazamo tofauti. Hivyo, kupitia roho yake, Mungu alimwongoza Yeremia kumwambia mwandishi wake hivi: “Tazama! Kile ambacho nimekijenga ninakibomoa, na kile ambacho nimekipanda ninaking’oa, ndiyo, nchi yote. Na wewe unaendelea kujitafutia makuu. Usiendelee kuyatafuta. Kwa maana, tazama, ninaleta msiba juu ya wote wenye mwili, . . . nami nitakupa wewe nafsi yako kuwa nyara katika mahali pote utakapoenda.”—Yer. 45:4, 5.

9 Hatujui kwa uhakika ni mambo gani “makuu” ambayo Baruku alikuwa akijitafutia. * Hata hivyo, tunajua kwamba yalikuwa mambo ambayo hayangedumu, mambo hayo yalikoma wakati Wababiloni waliposhinda Yerusalemu katika mwaka wa 607 K.W.K. Je, tunapata somo lolote? Ili kupata mahitaji ya lazima ya maisha tunahitaji kufanya mipango fulani kwa ajili ya wakati ujao. (Met. 6:6-11) Lakini je, lingekuwa jambo la hekima kwetu kutumia wakati na nguvu nyingi kufuatilia vitu ambavyo havina thamani yenye kudumu? Ni kweli kwamba tengenezo la Yehova linaendelea kufanya mipango ya ujenzi wa Majumba mapya ya Ufalme, ofisi za tawi, na miradi mingine ya kitheokrasi. Hata hivyo, mipango hiyo itadumu kwa sababu imekusudiwa kuendeleza masilahi ya Ufalme. Lingekuwa jambo linalofaa kwa watu wote wa Yehova waliojiweka wakfu kutanguliza mambo kama hayo wanapofanya mipango yao ya wakati ujao. Je, unasadiki moyoni mwako kwamba ‘unaendelea kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wa Yehova’?—Mt. 6:33.

“NAVIONA KUWA TAKATAKA NYINGI”

10, 11. (a) Paulo alifuatilia mambo gani kabla ya kuwa Mkristo? (b) Kwa nini Paulo alibadili kabisa miradi yake?

10 Hatimaye, acheni tuchunguze mfano wa Paulo. Kabla ya kuwa Mkristo, ilionekana kwamba Paulo alikuwa na fursa ya kufanikiwa maishani. Alifundishwa sheria ya Wayahudi na mmoja kati ya walimu maarufu sana wa wakati huo. Alipewa mamlaka na kuhani mkuu wa Wayahudi. Naye alikuwa akifanya maendeleo makubwa zaidi katika dini ya Kiyahudi kuliko watu wengi wa umri wake. (Mdo. 9:1, 2; 22:3; 26:10; Gal. 1:13, 14) Hata hivyo, mambo yote hayo yalibadilika Paulo alipotambua kwamba Yehova hakuwa tena akiwabariki Wayahudi wakiwa taifa.

11 Paulo alitambua kwamba kulingana na maoni ya Yehova, kufuatilia kazi katika mfumo wa Kiyahudi hakukuwa na thamani kwa kuwa mfumo huo haungedumu. (Mt. 24:2) Mtume huyo aliyekuwa Farisayo zamani hata alisema kwamba mambo ambayo wakati fulani alifikiri ni muhimu aliyaona sasa kuwa “takataka nyingi” alipoyalinganisha na uelewaji aliopata kuhusu makusudi ya Mungu na pendeleo la huduma ya Kikristo. Paulo aliacha miradi aliyokuwa akifuatilia katika dini ya Kiyahudi na akaamua kutumia kabisa muda wote uliobaki wa maisha yake duniani kuhubiri habari njema.—Soma Wafilipi 3:4-8, 15; Mdo. 9:15.

CHUNGUZA MAMBO UNAYOTANGULIZA

12. Yesu alikazia fikira nini baada ya kubatizwa?

12 Noa, Musa, Yeremia, Paulo, na wengine wengi kama wao walitumia sehemu kubwa ya wakati wao na nguvu zao kufuatilia mambo ya kiroho. Wao ni mifano mizuri kwetu. Bila shaka, Yesu ndiye mkuu zaidi kati ya watumishi wote wa Yehova waliojiweka wakfu. (1 Pet. 2:21) Baada ya kubatizwa, Yesu alitumia siku zilizobaki za maisha yake duniani kuhubiri habari njema na kumheshimu Yehova. Hivyo, ni wazi kwamba kila Mkristo anayemtambua Yehova kuwa Bwana wake anapaswa kutanguliza utumishi wa Yehova katika maisha yake. Je, hivyo ndivyo unavyofanya? Na tunawezaje kufuatilia miradi ya kiroho na wakati huohuo kushughulikia majukumu mengine muhimu?—Soma Zaburi 71:15; 145:2.

13, 14. (a) Wakristo wote waliojiweka wakfu wanatiwa moyo kuchunguza nini? (b) Ni uradhi gani ambao watu wa Mungu wanaweza kufurahia?

13 Kwa miaka mingi, tengenezo la Yehova limewatia Wakristo moyo tena na tena wasali na kufikiria uwezekano wa kufanya upainia. Kwa sababu mbalimbali, hali za watumishi fulani waaminifu wa Yehova haziwaruhusu kuhubiri wastani wa saa 70 kila mwezi. Jambo hilo halipaswi kuwavunja moyo. (1 Tim. 5:8) Lakini namna gani wewe? Je, kweli huwezi kufanya upainia?

14 Fikiria shangwe ambayo wengi wa watu wa Mungu walipata wakati wa majira ya Ukumbusho mwaka huu. Katika mwezi wa Machi, mpango wa pekee uliwawezesha mapainia wasaidizi kuchagua kuhubiri saa 30 au 50 katika utumishi wa shambani. (Zab. 110:3) Mamilioni walishiriki katika utumishi wa painia msaidizi, na kulikuwa na msisimko na shangwe nyingi sana katika makutaniko. Je, unaweza kupanga mambo yako ili ufanye kwa ukawaida zaidi utumishi wa painia msaidizi na kupata tena shangwe nyingi? Mwishoni mwa kila siku, Mkristo aliyejiweka wakfu anapata uradhi mkubwa na anaweza kusema, “Yehova, nilifanya yote niliyoweza katika utumishi wako.”

15. Kijana Mkristo anapaswa kuwa na malengo au miradi gani kuhusu elimu?

15 Ikiwa unakaribia kumaliza shule, huenda una afya nzuri na majukumu machache. Je, umefikiria kwa uzito kuwa painia wa kawaida? Bila shaka, washauri wa shule wanaamini kwa unyoofu kwamba ni kwa faida yako kufuatia elimu ya juu ili upate kazi nzuri ya kimwili wakati ujao. Hata hivyo, uhakika wao unategemea mfumo wa kijamii na kifedha ambao hautadumu milele. Kwa upande mwingine, ukitumia maisha yako kumtumikia Mungu, utakuwa ukifuatilia malengo au miradi inayofaa na yenye kudumu. Na utakuwa ukifuata mfano mkamilifu wa Yesu. Uamuzi huo wenye hekima utakuletea furaha. Utakulinda. Na utaonyesha kwamba umeazimia kuishi kulingana na wakfu wako kwa Yehova.—Mt. 6:19-21; 1 Tim. 6:9-12.

16, 17. Ni maswali gani tunayopaswa kujiuliza kuhusu kazi yetu ya kimwili na mambo mengine tunayofuatilia?

16 Watumishi wengi wa Mungu leo wanafanya kazi kwa saa nyingi ili kutosheleza mahitaji ya msingi ya familia zao. Hata hivyo, huenda wengine wanafanya kazi kwa saa nyingi zaidi isivyo lazima. (1 Tim. 6:8) Ulimwengu wa kibiashara unafanya yote uwezayo ili kutufanya tuamini kwamba hatuwezi kuishi bila vitu vingi vipya vinavyoendelea kutengenezwa. Lakini Wakristo wa kweli hawataki ulimwengu wa Shetani uwaamulie mambo wanayopaswa kutanguliza. (1 Yoh. 2:15-17) Na kwa wale waliostaafu, hakuna njia nyingine bora zaidi ya kutumia wakati wao kuliko kufanya utumishi wa upainia, na hivyo kutanguliza utumishi wa Yehova.

17 Watumishi wote waliojiweka wakfu kwa Yehova wanaweza kujiuliza hivi: Lengo au mradi wangu mkuu maishani ni upi? Je, ninatanguliza masilahi ya Ufalme? Je, ninaiga mtazamo wa Yesu wa kujidhabihu? Je, ninatii shauri la Yesu la kuendelea kumfuata daima? Je, ninaweza kurekebisha ratiba yangu ili nitumie wakati zaidi katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme au kufuatilia mambo mengine ya kiroho? Hata ikiwa hali zangu haziniruhusu kwa sasa kupanua utumishi wangu, je, ninaendelea kusitawisha roho ya kujidhabihu?

“MUWE NA NIA NA KUTENDA”

18, 19. Unapaswa kusali kuhusu nini, na kwa nini ombi hilo linaweza kumfurahisha Yehova?

18 Ni shangwe kama nini kuona bidii ya watu wa Mungu! Hata hivyo, huenda wengine wakahisi kwamba hawatamani kufanya kazi ya upainia au hawastahili kuifanya, hata ingawa hali zao zinawaruhusu kuifanya. (Kut. 4:10; Yer. 1:6) Wafanye nini? Je, hilo si jambo linalofaa kutajwa katika sala? Bila shaka. Paulo aliwaambia waamini wenzake kwamba Yehova, “kwa ajili ya mapenzi yake mema, anatenda ndani yenu ili ninyi muwe na nia na kutenda pia.” (Flp. 2:13) Ikiwa unahisi kwamba hutamani kupanua huduma yako, sali ili Yehova akupe nia na uwezo wa kufanya hivyo.—2 Pet. 3:9, 11.

19 Noa, Musa, Yeremia, Paulo, na Yesu, wote walikuwa wanaume waliojitoa. Walitumia wakati wao na nguvu zao kuhubiri ujumbe wa onyo kutoka kwa Yehova. Hawakukubali kukengeushwa. Mwisho wa mfumo huu wa mambo unakaribia; hivyo, sisi sote ambao tumejiweka wakfu kwa Mungu tunahitaji kuhakikisha kwamba tunaendelea kufanya yote tuwezayo kufuata mifano hiyo bora ya Kimaandiko. (Mt. 24:42; 2 Tim. 2:15) Tukifanya hivyo, tunaweza kumfurahisha Yehova na kupata baraka nyingi.—Soma Malaki 3:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Tazama kitabu Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia, ukurasa wa 104-106.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Watu hawakutii onyo la Noa

[Picha katika ukurasa wa 24]

Je, umefikiria kwa uzito kuwa painia wa kawaida?