Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Waliongozwa na Roho Takatifu’

‘Waliongozwa na Roho Takatifu’

‘Waliongozwa na Roho Takatifu’

“Unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.”—2 PET. 1:21.

MAMBO YA KUTAFAKARI

Roho takatifu iliwasilishaje ujumbe wa Mungu kwa waandikaji wa Biblia?

Ni mambo gani yanayothibitisha kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Mungu?

Unaweza kufanya nini kila siku ili udumishe uthamini wako kwa ajili ya Neno la Mungu?

1. Kwa nini tunahitaji Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake?

WATU wengi ulimwenguni pote wanajiuliza maswali yafuatayo: Tunatoka wapi? Kwa nini tuko hapa duniani? Tunaenda wapi? Kwa nini ulimwengu uko hivi? Inakuwaje tunapokufa? Tungejuaje majibu ya maswali hayo na mengine muhimu ikiwa hatungekuwa na Neno la Mungu lililoongozwa na roho? Bila Maandiko Matakatifu, tungejifunza kupitia mambo ambayo yangetupata maishani. Ikiwa tungejifunza mambo kwa njia hiyo, je, tungekuwa na maoni kama ya mtunga-zaburi kuhusu “sheria ya Yehova”?—Soma Zaburi 19:7.

2. Ni nini kitakachotusaidia kudumisha uthamini wetu kuelekea Biblia ambayo ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu?

2 Hata hivyo, inasikitisha kwamba wengine wameacha upendo wao wa kwanza kuelekea kweli ya Biblia upoe. (Linganisha na Ufunuo 2:4.) Wameacha kutembea katika njia inayompendeza Yehova. (Isa. 30:21) Tusiruhusu hilo litupate. Tunaweza na tunapaswa kujitahidi kudumisha uthamini wetu kuelekea Biblia na mafundisho yake. Biblia ni zawadi muhimu kutoka kwa Muumba wetu mwenye upendo. (Yak. 1:17) Ni nini kitakachotusaidia kuongeza zaidi uthamini wetu kuelekea “neno la Mungu”? Jambo kuu ni kutafakari kuhusu jinsi waandikaji wa Biblia walivyoongozwa kuandika Maandiko. Hilo linatia ndani kuchunguza baadhi ya uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Mungu. Kufanya hivyo kunapaswa kutuchochea kulisoma Neno la Mungu kila siku na kufuata mashauri yake.—Ebr. 4:12.

‘WALIONGOZWAJE NA ROHO TAKATIFU’?

3. Manabii na waandikaji wa Biblia ‘waliongozwaje na roho takatifu’?

3 Kwa kipindi cha miaka 1,610, kuanzia mwaka wa 1513 K.W.K. hadi mwaka wa 98 W.K., wanaume 40 hivi tofauti-tofauti waliandika Biblia. Baadhi yao walikuwa manabii ‘walioongozwa na roho takatifu.’ (Soma 2 Petro 1:20, 21.) Maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa ‘kuongozwa na’ yanamaanisha “kuchukua au kubeba kutoka mahali pamoja hadi mahali pengine,” na “yanaweza kutafsiriwa kwa njia mbalimbali kama vile: kuchochewa, kuongozwa, mtu kujiacha achukuliwe.” * Andiko la Matendo 27:15 linatumia maneno hayohayo linapoeleza kuhusu mashua fulani iliyoshikwa na kuchukuliwa au kusukumwa upande fulani na upepo. Manabii na waandikaji wa Biblia ‘waliongozwa na roho takatifu’ katika maana ya kwamba Mungu aliwasiliana nao, aliwachochea, na kuwaongoza kupitia nguvu yake ya utendaji. Kwa hiyo, waliandika mawazo ya Mungu, bali si mawazo yao wenyewe. Nyakati nyingine, manabii na waandikaji walioongozwa na roho ya Mungu hata hawakujua maana ya mambo waliyotabiri au kuandika. (Dan. 12:8, 9) Naam, “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu” nalo halitokani na maoni ya wanadamu.—2 Tim. 3:16.

4-6. Yehova alitumia njia gani kuwasilisha ujumbe wake kwa waandikaji wa Biblia? Toa mfano.

4 Hata hivyo, ujumbe wa Mungu uliwasilishwaje kwa waandikaji wa Biblia kupitia roho takatifu? Je, walipokea maneno hususa au walipewa tu mawazo ambayo wangeweza kueleza kwa maneno yao wenyewe? Fikiria jinsi mfanyabiashara anavyoandika barua. Ikiwa ni muhimu kutumia maneno hususa, anaweza kuiandika barua hiyo yeye mwenyewe au kumwambia karani wake maneno ya kuandika. Karani anaandika barua hiyo lakini mfanyabiashara huyo ndiye anayeitia sahihi barua hiyo. Nyakati nyingine, mfanyabiashara huyo anatoa mawazo tu na karani anaiandika barua akitumia maneno au mtindo wake mwenyewe. Mfanyabiashara huyo anaweza kuipitia tena barua hiyo na kumwomba karani afanye marekebisho yoyote yanayohitajiwa. Hatimaye, tunaweza kusema kwamba barua hiyo imetoka kwa mfanyabiashara huyo kwa sababu ina sahihi yake.

5 Vivyo hivyo, sehemu fulani za Biblia ziliandikwa “kwa kidole cha Mungu.” (Kut. 31:18) Pia, Yehova aliwaambia waandikaji moja kwa moja maneno ya kuandika alipotaka maneno fulani hususa yaandikwe. Kwa mfano, katika andiko la Kutoka 34:27, tunasoma hivi: “Yehova akaendelea kumwambia Musa: ‘Jiandikie maneno haya, kwa sababu ninafanya agano pamoja nawe na Israeli kupatana na maneno haya.’” Vivyo hivyo, Yehova alimwambia hivi nabii Yeremia: “Andika katika kitabu maneno yote nitakayokuambia.”—Yer. 30:2.

6 Hata hivyo, katika visa vingi, Mungu aliweka kimuujiza ndani ya mioyo na akili za waandikaji wa Biblia mawazo badala ya maneno hususa, na hivyo akawaruhusu kuchagua maneno yao wenyewe. Andiko la Mhubiri 12:10 linasema hivi: “Mkutanishaji alijitahidi kutafuta maneno yenye kupendeza na kuandika maneno sahihi ya kweli.” Luka, mwandikaji wa Injili, ‘alifuata kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi, akaandika hayo kwa utaratibu wenye kufuatana.’ (Luka 1:3) Roho ya Mungu ilihakikisha kwamba kutokamilika kwa wanadamu hakubadili ujumbe wake.

7. Mungu anaonyeshaje hekima yake kwa kuwatumia wanadamu kuiandika Biblia?

7 Mungu alionyesha hekima yake kuu kwa kuwatumia wanadamu kuiandika Biblia. Maneno yanatusaidia kuelewa si habari tu bali pia hisia. Namna gani ikiwa Yehova angetumia malaika kuiandika Biblia? Je, malaika wangeweza kuandika mambo yanayoonyesha hisia za kawaida za wanadamu kama vile woga, huzuni, na kuvunjika moyo? Kwa kuwaruhusu watu wasio wakamilifu wachague maneno yao wenyewe ili kueleza mawazo waliyopokea kupitia roho takatifu, Mungu alihakikisha kwamba ujumbe wake umeandikwa kwa uchangamfu, kwa njia tofauti-tofauti, na kwa njia inayogusa hisia za wanadamu.

MAMBO YANAYOTHIBITISHA KWAMBA BIBLIA INATOKA KWA MUNGU

8. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Biblia ni tofauti na kitabu kingine chochote cha kidini?

8 Kuna mambo mengi yanayothibitisha kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Biblia ndiyo inayotusaidia kumjua Mungu kuliko kitabu kingine chochote cha kidini. Kwa mfano, vitabu vya dini ya Kihindu vinatueleza kuhusu sherehe za ibada za dini hiyo, falsafa, hadithi, na sheria kuhusu maadili. Vitabu vya dini ya Kibudha vinaeleza kuhusu sheria na maagizo ambayo watawa wao wa kiume na wa kike wanapaswa kufuata. Pia, vinaeleza imani za Wabudha na mafundisho ya Budha. Budha mwenyewe hakusema kwamba alikuwa mungu, na alisema mambo machache sana kumhusu Mungu. Vitabu vya dini ya Confucius vinazungumzia mambo ambayo yalitukia wakati uliopita, sheria kuhusu maadili, uchawi, na nyimbo. Pia, kuna kitabu kitakatifu cha Kiislamu ambacho kinafundisha kwamba kuna Mungu mmoja ambaye anajua wakati ujao na anaudhibiti, lakini hakifunui jina la Mungu, Yehova, ambalo linapatikana maelfu kwa maelfu katika Biblia.

9, 10. Biblia inaweza kutufundisha nini kumhusu Mungu?

9 Ingawa vitabu vingi vya msingi vya kidini vinasema mambo machache sana, au hata havisemi chochote, kumhusu Mungu, Biblia inatueleza kumhusu Yehova Mungu na kazi zake. Inatusaidia kuona sifa nyingi za utu wake. Biblia inafunua kwamba Mungu ni mwenye-nguvu zote, mwenye hekima, haki, na pia ni Mungu anayetupenda. (Soma Yohana 3:16; 1 Yohana 4:19.) Zaidi ya hayo, Biblia inatueleza hivi: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Mdo. 10:34, 35) Kwa njia fulani, kutafsiriwa kwa Biblia katika lugha nyingi kunathibitisha kwamba Mungu hana ubaguzi. Wataalamu wa lugha wanasema kwamba lugha 6,700 hivi zinazungumzwa leo ulimwenguni, na karibu 100 kati ya lugha hizo zinazungumzwa na asilimia 90 hivi ya watu ulimwenguni. Hata hivyo, Biblia imetafsiriwa katika lugha zaidi ya 2,400 ikiwa nzima au sehemu. Karibu kila mtu ulimwenguni anaweza kupata angalau sehemu fulani za Biblia katika lugha yake.

10 Yesu alisema: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa, na mimi ninaendelea kufanya kazi.” (Yoh. 5:17) ‘Tangu wakati usio na kipimo mpaka wakati usio na kipimo Yehova ni Mungu.’ Kwa hiyo, fikiria mambo yote ambayo ametimiza. (Zab. 90:2) Ni Biblia tu inayotueleza kuhusu kazi za Mungu za wakati uliopita na za sasa na inafunua yale ambayo atafanya wakati ujao. Pia, Maandiko yanatufundisha kuhusu mambo yanayompendeza na yale ambayo hayampendezi, na yanaonyesha jinsi tunavyoweza kumkaribia. (Yak. 4:8) Basi tusiruhusu mahangaiko au mambo ya kibinafsi yatutenge mbali na Mungu.

11. Ni hekima gani nyingi na yenye kutegemeka inayopatikana katika Biblia?

11 Hekima nyingi na yenye kutegemeka inayopatikana katika Biblia inaonyesha pia kwamba kitabu hicho kinatokana na Chanzo kilicho juu zaidi ya mwanadamu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Ni nani ameijua akili ya Yehova, ndipo amfundishe?” (1 Kor. 2:16) Mstari huo unategemea swali ambalo nabii Isaya aliwauliza watu wa siku zake: “Ni nani ambaye ameipima roho ya Yehova, na ni nani kama mtu wake wa mashauri anayeweza kumjulisha jambo lolote?” (Isa. 40:13) Bila shaka, jibu ni hakuna. Haishangazi kwamba kufuata mashauri ya Maandiko kuhusu ndoa, watoto, vitumbuizo, marafiki, bidii, unyoofu, na maadili kunaleta matokeo bora zaidi! Biblia haitoi kamwe mashauri mabaya. Kwa upande mwingine, wanadamu hawana hekima ya kutosha ili kutoa mashauri yanayofaa sikuzote. (Yer. 10:23) Mashauri yao hubadilika-badilika na wanayasahihisha wanapotambua kwamba mashauri waliyotoa awali yalikuwa yenye makosa. Biblia inasema hivi: ‘Fikira za wanadamu ni kama pumzi.’—Zab. 94:11.

12. Kwa karne nyingi watu wamejaribu jinsi gani kuiharibu Biblia?

12 Jambo lingine linalothibitisha kwamba Mungu wa kweli ndiye Mtungaji wa Biblia ni mambo ambayo historia inafunua kuhusu jitihada zilizofanywa ili kuuharibu ujumbe wa Biblia. Katika mwaka wa 168 K.W.K., Mfalme Antioko wa Nne wa Siria, alijaribu kutafuta vitabu vyote vya Sheria vilivyoongozwa na roho ya Mungu ili aviteketeze kwa moto. Katika mwaka wa 303 W.K., Diokletiani, Maliki wa Roma, alitoa amri ya kuharibu mahali pa mikutano ya Wakristo na kuteketeza Maandiko yao. Uharibifu huo uliendelea kwa miaka kumi. Baada ya karne ya 11, mapapa waliongoza jitihada za kukomesha kusambaa kwa ujuzi wa Biblia, wakipinga kutafsiriwa kwa Maandiko katika lugha za watu wa kawaida. Licha ya jitihada hizo za Shetani na watu wake, bado tuna Biblia leo. Yehova hajamruhusu mtu yeyote aiharibu zawadi hiyo ambayo amewapa wanadamu.

UTHIBITISHO AMBAO UMEWASADIKISHA WENGI

13. Ni mambo gani yanayotuthibitishia kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Mungu?

13 Kuna mambo mengine yanayothibitisha kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Mungu: upatano wa vitabu vyake, usahihi wa kisayansi, utimizo wa unabii mbalimbali, unyoofu usio wa kawaida wa waandikaji wake, uwezo wa kubadili maisha ya watu, usahihi wa kihistoria, na inajibu kwa njia yenye kuridhisha maswali yaliyo katika fungu la 1. Chunguza mambo yaliyowasaidia watu fulani kuona kwamba Biblia inatoka kwa Mungu.

14-16. (a) Ni nini kilichomsadikisha Mwislamu, mtu aliyeamini kwamba mambo ya Mungu hayajulikani, na Mhindu kwamba Biblia inatoka kwa Mungu? (b) Unapenda kutumia jambo gani katika huduma linalothibitisha kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Mungu?

14 Anwar * alilelewa akiwa Mwislamu katika nchi moja ya Mashariki ya Kati. Alipokuwa akiishi kwa muda huko Amerika ya Kaskazini, Mashahidi wa Yehova walimtembelea nyumbani kwake. Anwar anasema hivi: “Wakati huo, nilikuwa na maoni yasiyofaa kuhusu dini za Kikristo kwa sababu ya vita vya kuwalazimisha watu kuwa Wakristo na mahakama za kuwahukumu wale walioasi Ukatoliki. Hata hivyo, kwa kuwa kiasili mimi ni mdadisi, nilikubali kujifunza Biblia.” Muda mfupi baadaye, Anwar alirudi katika nchi yao na hakuweza kuwasiliana tena na Mashahidi. Miaka mingi baadaye, alihamia Ulaya, ambako alianza tena kujifunza Biblia na akafikia mkataa huu: “Kutimia kwa unabii mbalimbali wa Biblia, upatano wa Maandiko Matakatifu, kutopingana kwa vitabu vya Biblia, na upendo miongoni mwa waabudu wa Yehova, yote hayo yalinisadikisha kwamba Biblia ni Neno la Mungu.” Anwar alibatizwa mwaka wa 1998.

15 Asha mwenye umri wa miaka 16 anatoka katika familia inayoshikilia sana dini ya Kihindu. Anasema hivi: “Nilisali tu wakati nilipoenda hekaluni au nilipokabili hali ngumu, lakini sikumfikiria kamwe Mungu maisha yalipokuwa mazuri.” Anaendelea kusema hivi: “Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova walipobisha mlango wangu, maisha yangu yalibadilika kabisa.” Asha alijifunza Biblia, akamjua Mungu na kuwa Rafiki yake. Ni nini kilichomsadikisha kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Mungu? Anaeleza hivi: “Biblia ilijibu kila swali nililouliza. Ilinisaidia kuwa na imani bila hata kumwona Mungu, yaani, bila kwenda hekaluni kuinama mbele ya sanamu.”

16 Paula alilelewa katika familia ya Kikatoliki, lakini alipokuwa mtu mzima aliamini kwamba mambo ya Mungu hayajulikani. Kisha, jambo fulani likatokea. Anaeleza: “Nilikutana na rafiki fulani ambaye sikuwa nimeonana naye kwa miezi kadhaa. Kwa ujumla, watu walizoea kufuga nywele ndefu wakati huo. Nilipoona jinsi alivyobadilika, yaani, sasa alikuwa amenyoa nywele vizuri na alikuwa mwenye furaha, nilimuuliza, ‘Imekuwaje ukabadilika, na ulikuwa wapi?’ Mwanamume huyo alisema kwamba alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova naye akaanza kunihubiria.” Paula ambaye zamani aliamini kwamba mambo ya Mungu hayajulikani alipoona jinsi kweli ya Biblia ilivyobadili rafiki yake, alipendezwa na ujumbe wa Biblia naye akakubali kwamba imeongozwa na roho ya Mungu.

“NENO LAKO NI TAA YA MGUU WANGU”

17. Kusoma Neno la Mungu kila siku na kutafakari mambo unayosoma kunaweza kukusaidiaje?

17 Biblia ni zawadi nzuri ajabu ambayo Yehova ameandaa kupitia roho yake takatifu. Furahia kusoma Biblia kila siku, na upendo wako kuielekea na kuelekea Mtungaji wake utaongezeka. (Zab. 1:1, 2) Anza kila kipindi cha funzo kwa sala, ukiomba roho ya Mungu iongoze mawazo yako. (Luka 11:13) Biblia ina mawazo ya Mungu, hivyo unapotafakari mambo inayosema, unaweza kujifunza kufikiri kama Mungu anavyofikiri.

18. Kwa nini unataka kuendelea kujifunza Biblia?

18 Unapoendelea kukua katika ujuzi sahihi wa kweli, ishi kulingana na mambo unayojifunza. (Soma Zaburi 119:105.) Chunguza Maandiko kama vile ambavyo ungejiangalia kwenye kioo. Hivyo, ukiona kwamba unapaswa kufanya mabadiliko fulani, fanya mabadiliko hayo. (Yak. 1:23-25) Tumia Neno la Mungu kama upanga ili kutetea imani yako na kukatakata na kuondoa mafundisho ya uwongo ndani ya mioyo ya watu wapole. (Efe. 6:17) Unapofanya hivyo, shukuru kwamba manabii na wanaume waliotumiwa kuandika ujumbe wa Biblia kwa kweli ‘waliongozwa na roho takatifu.’

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kitabu A Greek-English Lexicon of the New Testament and Other Early Christian Literature.

^ fu. 14 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Soma Biblia kila siku, na upendo wako kuelekea Mtungaji wake utaongezeka

[Picha katika ukurasa wa 26]

Barua inaonwa kuwa imetoka kwa mtu ambaye ameitia sahihi