Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Mwenye Hekima Tafuta “Mwongozo Stadi”

Uwe Mwenye Hekima Tafuta “Mwongozo Stadi”

Uwe Mwenye Hekima Tafuta “Mwongozo Stadi”

Maisha yamelinganishwa na safari ya baharini. Hata hivyo, mara nyingi hekima ya wanadamu imeshindwa kuwasaidia watu kufanikiwa katika safari hiyo ya maisha. Watu wengi wamevunjikiwa na meli katika dhoruba ya maisha. (Zab. 107:23, 27) Kwa nini mfano huo unafaa?

Katika nyakati za kale, safari za baharini zilikuwa hatari na kwa hiyo uzoefu ulihitajiwa. Kwa kawaida watu walifundishwa ustadi huo na mabaharia wenye uzoefu wa muda mrefu, labda nahodha wa meli. (Mdo. 27:9-11) Michoro mingi ya zamani inakazia umuhimu wa daraka la nahodha kwa kumwonyesha akiwa na mwili mkubwa kuliko wengine. Ili waweze kuendesha meli baharini, mabaharia walijifunza kuhusu nyota, upepo, na mambo mengine yaliyotumiwa kuongoza meli. Biblia inasema kwamba mabaharia fulani walikuwa “wenye ustadi,” na maneno hayo yametafsiriwa kutokana na neno linaloweza kumaanisha “wenye hekima.”—Eze. 27:8.

Matatizo ya maisha leo yanaweza kuonekana kuwa magumu kama safari za kale za baharini. Ni nini kinachoweza kutusaidia?

TUNAWEZA KUPATAJE “MWONGOZO STADI”?

Unapokumbuka mfano unaolinganisha maisha na safari ya baharini, fikiria ukweli huu wa Biblia: “Mtu mwenye hekima atasikiliza na kupata mafundisho zaidi, naye mtu mwenye uelewaji ndiye anayepata mwongozo stadi.” (Met. 1:5, 6) Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “mwongozo stadi” linaweza kufafanua utendaji wa kapteni wa meli nyakati za kale. Linamaanisha uwezo wa kuongoza na kuelekeza kwa ustadi.

Ingawa jitihada zinahitajiwa, tunaweza kupata “mwongozo stadi” na kujifunza “kusafiri” kwa mafanikio katika bahari ya maisha. Kama kitabu cha Methali kinavyoonyesha, ni lazima tuache sifa ya “hekima,” “uelewaji,” na “ufahamu,” zifanye kazi pamoja. (Met. 1:2-6; 2:1-9) Na hatuwezi kuacha kutafuta mwongozo wa Mungu, kwa kuwa hata waovu wanaweza kujua ‘kutafuta mwongozo’ ili kupata faida isiyo ya haki.—Met. 12:5.

Basi ni muhimu tuwe wanafunzi wenye bidii wa Neno la Mungu. Kupitia funzo hilo, tunaweza kujifunza habari zenye thamani kuhusu Yehova na Yesu Kristo, ambaye anamwiga kwa njia bora kabisa. (Yoh. 14:9) Tunapokea mashauri mengi yenye hekima katika mikutano ya Kikristo. Isitoshe, tunaweza kujifunza kutokana na mifano ya wengine, kutia ndani wazazi wetu.—Met. 23:22.

ONA MAMBO KIMBELE NA UFANYE MIPANGO

“Mwongozo stadi” ni muhimu hasa tunapojikuta katika bahari ya mfano iliyochafuka. Tukiwa na shaka kuhusu hatua ya kuchukua tunapokabili hali ngumu huenda tusijue jambo la kufanya, na matokeo yanaweza kuwa mabaya sana.—Yak. 1:5, 6.

Kwa wazi, neno linalotafsiriwa “mwongozo stadi” linatumiwa pia kurejelea vita. Tunasoma hivi: “Kwa mwongozo stadi [“kwa mbinu za ustadi,” The Revised English Bible] utaendeleza vita vyako, na kwa wingi wa washauri kuna wokovu.”—Met. 20:18; 24:6.

Kama mtaalamu wa kupanga mbinu za vita, ni vyema tuone kimbele mambo yanayoweza kuhatarisha hali yetu ya kiroho. (Met. 22:3) Kwa mfano, huenda ukahitaji kuamua kama utakubali kazi mpya au kupandishwa cheo kazini. Ni jambo la busara kufikiria mshahara, wakati wa kusafiri kwenda na kutoka kazini, na mambo mengine. Hata hivyo, kuna mambo mengine ambayo unapaswa kufikiria: Je, kazi hiyo itapatana na kanuni za Biblia? Saa za kazi, kama vile zamu za kazi, zitaathirije utendaji wangu wa Kikristo?—Luka 14:28-30.

Loretta, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alikuwa na kazi nzuri katika kampuni ya kutayarisha vyakula. Kampuni ilipokuwa ikihamia eneo jipya, Loretta alipewa cheo kikubwa katika eneo hilo jipya. Wakurugenzi walimwambia hivi: “Hutapata nafasi nyingine kama hii maishani. Tayari tumegundua kwamba kuna Jumba la Ufalme huko.” Lakini Loretta alitaka kuishi maisha rahisi ili amtumikie Muumba kikamili zaidi. Aliona kwamba ikiwa angekubali cheo hicho kipya hangekuwa na wakati wa kutosha kwa ajili ya utendaji wa Kikristo. Hivyo, aliomba kujiuzulu, hata ingawa mkurugenzi alimwambia faraghani kwamba yeye ndiye mfanyakazi pekee ambaye walitaka abaki kwenye kampuni hiyo. Loretta, ambaye sasa amekuwa painia wa kawaida kwa miaka 20, anasadiki kwamba matokeo mazuri ambayo amepata yanahusiana moja kwa moja na mipango aliyofanya kwa kutegemea “mwongozo stadi,” naam, kupatana na mashauri yaliyo katika Neno la Mungu. Aliimarisha uhusiano wake na Yehova na amekuwa na pendeleo la kuwasaidia wengi kukubali kweli ya Biblia.

Bila shaka, “mwongozo stadi” unahitajika katika familia. Kuwalea watoto ni kazi ya muda mrefu, na maamuzi tunayofanya kuhusiana na mambo ya kiroho au ya kimwili yanaweza kuwa na matokeo mazuri au mabaya katika maisha ya wakati ujao ya wote katika familia. (Met. 22:6) Kwa mfano, wazazi Wakristo, wanaweza kujiuliza hivi: ‘Je, mazungumzo na mfano wetu unawafundisha watoto wetu mambo ya kiroho ambayo yatawasaidia kuishi kwa hekima wakiwa watu wazima? Je, maisha yetu yanawasaidia kuelewa jinsi ya kuridhika na maisha rahisi na kukazia fikira huduma yao ya Kikristo?’—1 Tim. 6:6-10, 18, 19.

Mafanikio ya kweli hayategemei miradi ya kimwili au ya kijamii ambayo kwa kawaida watu wa ulimwengu wanafuatilia. Mfalme Sulemani alielewa jambo hilo. Aliongozwa na roho takatifu kuandika hivi: “Mambo yatawaendea vyema wale wanaomwogopa Mungu wa kweli, kwa sababu walimwogopa.” (Mhu. 8:12) Bila shaka, hilo linaonyesha hekima ya kutafuta “mwongozo stadi” unaotegemea na unaopatana na Neno la Mungu.—2 Tim. 3:16, 17.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Ili kukazia daraka lao, kwa kawaida michoro ilionyesha manahodha wakiwa na mwili mkubwa kuliko mabaharia wengine

[Hisani]

Su concessione del Ministero per i Beni e le Attività Culturali. It is forbidden to reproduce or duplicate this image in any way or by any means.