Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Wakati Wowote Munaposali, Semeni, Baba’

‘Wakati Wowote Munaposali, Semeni, Baba’

‘Wakati Wowote Munaposali, Semeni, Baba’

Unaposikia neno “baba,” unawazia mutu wa namna gani? Mutu mwenye upendo anayewahangaikia sana watu wa familia yake? Ao mutu asiyehangaikia mutu yeyote, ambaye labda anawatendea wengine vibaya? Jibu la ulizo hilo linategemea namna baba yako alikuwa.

NENO “baba” ndilo neno ambalo Yesu alitumia mara nyingi alipokuwa akizungumuza na Mungu na alipokuwa akizungumuzia wengine juu yake. * Alipowafundisha wafuasi wake kusali, alisema hivi: ‘Wakati wowote munaposali, semeni, Baba.’ (Luka 11:2) Lakini Yehova ni baba wa namna gani? Jibu la ulizo hilo ni la maana sana. Sababu gani? Tunapoelewa vizuri Yehova ni baba wa namna gani, tutamukaribia zaidi na kumupenda sana.

Yesu ndiye anayestahili zaidi kutufundisha juu ya Baba yetu wa mbinguni kwa sababu, mbele ya kuja duniani, alikuwa na uhusiano muzuri sana pamoja na Baba yake. Alisema hivi: ‘Hakuna yeyote anayemujua Mwana kabisa ila Baba, wala yeyote hamujue Baba kabisa ila Mwana, na yeyote ambaye Mwana anapenda kumufunulia.’ (Mathayo 11:27) Kwa hiyo, njia nzuri zaidi ya kumujua Baba ni kupitia Mwana wake.

Yesu anaweza kutufundisha nini juu ya Baba yetu wa mbinguni? Ona maneno ambayo alisema: ‘Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamutoa Mwana wake muzaliwa​-pekee, ili kila mutu anayemuamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.’ (Yohana 3:16) Maneno haya ya Yesu yanaonyesha kama upendo ndiyo sifa kubwa ya Baba yetu wa mbinguni. (1 Yohana 4:8) Yehova anatuonyesha upendo wake katika njia mbalimbali: anatukubali, anatusikilia huruma, anatulinda, anaturekebisha, na anatupatia mahitaji yetu ya kimwili.

Yesu Anatuhakikishia Kama Baba Yetu Anatukubali

Watoto wanapata nguvu na wanatiwa moyo wanapojua kama wazazi wao wanapendezwa na yale wanayofanya. Wazia namna Yesu alitiwa moyo wakati Baba yake alisema hivi: ‘Huyu ni Mwanangu, mupendwa, ambaye nimemukubali.’ (Mathayo 3:17) Yesu anatuhakikishia kama Baba anatupenda na anatukubali. Alisema hivi: Yule “anayenipenda atapendwa na Baba yangu.” (Yohana 14:21) Hayo ni maneno yenye kutia moyo sana! Lakini kuna mutu anayetaka kutuvunja moyo.

Shetani anataka tuwe na mashaka, anataka tuwaze kama Yehova hapendezwe na yale tunayofanya. Anataka kutusadikisha kama hatustahili machoni pa Yehova. Anafanya hivyo mara nyingi wakati tuko katika hali isiyokuwa nzuri kama vile, ugonjwa, uzaifu, uzee ao tunapojisikia kuwa wenye kulemewa kwa sababu ya makosa yetu na wakati tunavunjika moyo. Ona mufano wa kijana anayeitwa Lucas, aliyejisikia kuwa hastahili machoni pa Mungu. Anasema kama wazazi wake walibadilika sana alipokuwa kijana; waliacha kushikamana na kanuni nyingi nzuri za kiroho walizomufundisha. Labda, hiyo ndiyo sababu aliona kuwa vigumu kufanya uhusiano pamoja na Baba yake wa mbinguni. Tena, kwa sababu Lucas alikuwa mutu wa kutenda haraka-haraka bila kufikiri, mara nyingi hakuwa na uhusiano muzuri pamoja na watu wengine. Lakini, bibi yake aliyekuwa muvumilivu na mwenye kutia moyo alimusaidia polepole abadilishe hali yake ya kutenda haraka​-haraka bila kufikiri. Lucas anamuona bibi yake kuwa “baraka ya pekee, zawadi kutoka kwa Mungu.” Lucas alifikia kutambua kama ‘Kristo Yesu alikuja ulimwenguni ili kuwaokoa watenda-zambi.’ (1 Timotheo 1:15) Lucas anasema kama kufikiri sana juu ya upendo wa Mungu na kujua kama Mungu anamukubali kumemuletea furaha na kutosheka.

Ikiwa, wakati fulani una mashaka kama Yehova hawezi kukupenda na kukukubali, unaweza kutiwa moyo kwa kusoma na kufikiri sana juu ya andiko la Waroma 8:31-39. Katika andiko hilo, mutume Paulo anatuhakikishia kwa upendo kama hakuna kitu chochote kinachoweza “kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” *

Baba Anayetusikilia Huruma

Baba yetu wa mbinguni anatusikilia huruma tunapoteseka. Yeye ni Mungu wa “huruma.” (Luka 1:78) Kama Baba yake, Yesu aliwasikilia huruma wanadamu wasio wakamilifu. (Marko 1:40-42; 6:30-34) Wakristo wa kweli wanajikaza pia kuiga huruma ya Baba yao wa mbinguni. Wanafuata shauri hili la Biblia, linalosema: ‘Iweni wenye fazili ninyi kwa ninyi, wenye huruma.’​—Waefeso 4:32.

Ona mufano wa mwanaume anayeitwa Felipe. Siku moja, alipokuwa akienda kwenye kazi, mara moja alisikia maumivu makali; alijisikia kama vile mutu anayechomwa kisu kwenye mugongo. Alipelekwa haraka kwenye hopitali. Kisha uchunguzi uliofanywa kwa muda wa saa munane, waganga walisema kama mushipa mukubwa unaopitisha damu inayotoka katika moyo umekatika. Walisema kama atakufa katika dakika 25, na kwa hiyo haikuwa lazima kumupasua.

Wakristo fulani wenzake walikuwa hapo, na huruma waliyomusikilia iliwachochea kutenda. Walifanya mipango haraka ili apelekwe kwenye hopitali nyingine, ambako alipasuliwa bila kukawia, na walibaki pamoja naye mupaka upasuaji ulipokwisha. Jambo lenye kufurahisha ni hili: Felipe aliokoka hali hiyo ngumu. Felipe anapokumbuka hali hiyo iliyomupata, yeye ni mwenye shukurani kwa huruma ambayo Wakristo wenzake walimusikilia. Lakini Felipe ana uhakika kama Baba yake wa mbinguni ndiye aliyewachochea wamusikilie huruma hiyo na kutenda. Anasema hivi: “Kama vile baba mwenye upendo, Mungu alikuwa pembeni yangu ili kunitia nguvu.” Kwa kweli, mara nyingi Yehova anaonyesha huruma yake kwa kuwachochea watumishi wake duniani waonyeshe sifa hiyo.

Baba Yetu Anatulinda

Mutoto anapoona hatari, anaweza kukimbilia mahali baba yake alipo ili kutafuta ulinzi. Mutoto akiwa katika mikono ya baba yake anajisikia kuwa mwenye kulindwa. Yesu alitegemea kabisa ulinzi wa Yehova. (Mathayo 26:53; Yohana 17:15) Sisi pia tunaweza kulindwa na Baba yetu wa mbinguni. Leo, ulinzi ambao Yehova anatutolea ni zaidi sana ulinzi wa kiroho. Ni kusema kama anatulinda na hatari za kiroho kwa kututolea mambo tunayohitaji ili kutusaidia tuepuke hatari hizo na kuendelea kuwa na urafiki pamoja naye. Njia moja ambayo anatumia ili kutulinda ni mashauri yanayotoka katika Biblia. Tunapotolewa mashauri kama hayo, ni sawa vile Yehova anatufuata nyuma akituambia: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.”​—Isaya 30:21.

Ona mufano wa Tiago na ndugu zake wawili, Fernando na Rafael, ambao walikuwa katika kikundi fulani cha wanamuziki. Walifurahi sana walipochaguliwa ili kucheza katika chumba cha muziki chenye kujulikana sana huko São Paulo, Brésil. Waliona kama watapata feza nyingi. Lakini, Mukristo mwenzao aliwashauria juu ya hatari za kufanya urafiki na watu ambao maisha yao hayaheshimu kanuni za Mungu. (Methali 13:20) Ili kukazia shauri hilo la Biblia, aliwaelezea mufano wa ndugu yake mukubwa. Kwa sababu ya kuwa na marafiki wabaya, ndugu yake alijiingiza katika mwenendo mubaya. Tiago na ndugu zake waliamua kuacha kazi ya wanamuziki. Sasa wote watatu wanafanya utumishi wa wakati wote. Wanaamini kama kufuata shauri la Neno la Mungu kuliwasaidia kuepuka hatari za kiroho.

Baba Yetu wa Mbinguni Anaturekebisha

Baba mwenye upendo anawarekebisha watoto wake, kwa sababu anataka wawe watu wazuri. (Waefeso 6:4) Baba huyo habadilike-badilike anapowarekebisha watoto wake, lakini hafanye hivyo kwa ukali. Vilevile, wakati fulani Baba yetu wa mbinguni anaweza kuona kuwa ni jambo la lazima kuturekebisha. Lakini kila mara Mungu anapoturekebisha, anafanya hivyo kwa upendo na upole. Yesu alimuiga Baba yake, kwa sababu hakuwa mukali alipowarekebisha wafuasi wake hata ikiwa wakati fulani hawakutenda kwa haraka waliporekebishwa.​—Mathayo 20:20-28; Luka 22:24-30.

Ona namna mwanaume anayeitwa Ricardo alivyokubali kurekebishwa na Yehova kwa njia ya upendo. Baba yake alimuacha alipokuwa tu na miezi saba. Alipokuwa kijana, Ricardo alisumbuliwa sana kwa sababu hakuwa na baba. Kwa hiyo, alijiingiza katika mwenendo mubaya, na zamiri yake ilianza kumusumbua. Alipoona kama maisha yake hayakupatana na kanuni za Kikristo, aliamua kuzungumuzia wazee wa kutaniko lake jambo hilo. Wazee walimutolea mashauri yenye upendo, yenye kutoka katika Biblia. Ricardo alikubali mashauri hayo, lakini aliendelea kuteseka sana kwa sababu ya mambo aliyofanya. Aliendelea kukosa usingizi usiku, kulia, na kuvunjika moyo. Mwishowe, alielewa kama Yehova anaendelea kumupenda hata ikiwa alimurekebisha. Ricardo anakumbuka maneno haya ya Waebrania 12:6: ‘Yeye ambaye Yehova anamupenda, anamutia nizamu.’

Ni vizuri tukumbuke kama kurekebishwa hakumaanishe tu kutiwa adabu ao kukaripiwa kwa ajili ya matendo mabaya. Biblia inalinganisha pia kurekebishwa na kufundishwa. Kwa hiyo, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anaweza kuturekebisha wakati fulani kwa kuruhusu tupatwe na matokeo mabaya ya makosa yetu. Lakini, Biblia inaonyesha kama Yehova anaturekebisha ili kutufundisha, na hilo linatusaidia tuendelee kufuata njia nzuri. (Waebrania 12:7, 11) Ndiyo, Baba yetu anatuhangaikia sana na anaturekebisha kwa faida yetu wenyewe.

Baba Yetu Anatupatia Mahitaji Yetu ya Kimwili

Baba mwenye upendo anahangaikia sana mahitaji ya kimwili ya watu wa familia yake. Yehova pia anafanya hivyo. Yesu alisema hivi: ‘Baba yenu wa mbinguni anajua munahitaji vitu hivi vyote.’ (Mathayo 6:25-34) Yehova anaahidi hivi: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.”​—Waebrania 13:5.

Mwanamuke anayeitwa Nice alijionea kama maneno hayo ni ya kweli wakati bwana yake alipoteza kazi. Nice alikuwa ameacha kazi yake iliyokuwa na mushahara muzuri, ili kupitisha wakati mwingi pamoja na watoto wake wawili na pia kuhubiri zaidi. Sasa wangeishi namna gani? Nice alimuomba Yehova. Siku iliyofuata, bwana yake alienda mahali alipokuwa akitumika ili kuchukua vitu vyake. Bwana yake alishangaa sana kuona kama mukubwa wake wa kazi alimuambia kama kazi nyingine imepatikana na akamupa tena kazi! Ni kusema kama bwana yake na Nice alipoteza kazi yake siku moja, na kuipata siku iliyofuata. Nice na bwana yake walimushukuru Baba yao wa mbinguni kwa sababu ya matokeo mazuri waliyopata. Habari yao inatukumbusha kama Yehova atatupatia mahitaji yetu ya kimwili na hawezi hata kidogo kuwasahau watumishi wake waaminifu.

Sisi Ni Wenye Shukurani kwa Sababu ya Upendo wa Baba Yetu

Kwa kweli, tunakosa maneno ili kueleza upendo wa ajabu wa Baba yetu wa mbinguni! Tunapochunguza namna mbalimbali anavyotuonyesha upendo wake​—kwa kutukubali, kutusikilia huruma, kutulinda, kuturekebisha, na kutupatia mahitaji yetu ya kimwili​—tunaweza kusema kwa uhakika kama yeye ni Baba muzuri sana!

Namna gani tunaweza kuonyesha shukurani kwa ajili ya upendo ambao Baba yetu wa mbinguni ametuonyesha? Tunaweza kujikaza kujifunza mengi zaidi juu yake na kusudi lake. (Yohana 17:3) Tunaweza kuishi kulingana na mapenzi yake na njia zake. (1 Yohana 5:3) Tunaweza kuiga upendo wake kupitia namna tunavyowatendea wengine. (1 Yohana 4:11) Kupitia njia hizo mbalimbali, tunaweza kuonyesha kama tunamuona kabisa Yehova kuwa Baba yetu na kama ni pendeleo kuwa watoto wake.

[Maelezo ya chini]

^ Mara nyingi, Biblia inamuita Yehova kuwa baba yetu. Kwa mufano, Yesu alitumia neno “Baba” karibu mara 65 katika Injili ya Mathayo, Marko, na Luka; na zaidi ya mara 100 katika Injili ya Yohana. Mutume Paulo anamuzungumuzia pia Mungu kuwa “Baba” zaidi ya mara 40 katika barua zake. Yehova ni Baba yetu kwa sababu ni yeye aliyetupatia uzima.

^ Soma kitabu Mkaribie Yehova, sura ya 24 yenye kichwa “Hakuna Kitu Kinachoweza ‘Kututenga na Upendo wa Mungu.’” Kitabu hicho kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 19]

Tunapoelewa vizuri Yehova ni baba wa namna gani, tutamukaribia zaidi na kumu- penda sana

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 22]

Tunaweza kuonyesha kama tunamuona kabisa Yehova kuwa Baba yetu na kama ni pendeleo kuwa watoto wake

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 21]

KAMA BABA, YEHOVA ANATUONYESHA UPENDO WAKE KATIKA NJIA MBALIMBALI

ANATUKUBALI

ANATUSIKILIA HURUMA

ANATULINDA

ANATUREKEBISHA

ANATUPATIA MAHITAJI YETU YA KIMWILI