Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Kwa nini Mungu aliwaagiza waabudu wake wafunge ndoa na waabudu wenzao tu?

Kwa nini Mungu aliwaagiza waabudu wake wafunge ndoa na waabudu wenzao tu?

▪ Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilitia ndani amri iliyohusu mataifa yaliyowazunguka: “Usifanye mapatano yoyote ya ndoa pamoja nao. Binti yako usimpe mwana wake, wala binti yake usimchukue kwa ajili ya mwana wako.” (Kumbukumbu la Torati 7:​3, 4) Kwa nini Mungu aliwakataza?

Kwanza kabisa, Yehova alijua kwamba Shetani alitaka kuwapotosha watu Wake kwa kuwafanya waabudu miungu ya uwongo. Hivyo, Mungu aliwaonya kwamba watu wasioamini “[wa]tamgeuza mwana wako aache kunifuata, nao watatumikia miungu mingine.” Mambo mengi yalihusika. Ikiwa Waisraeli wangeanza kuabudu miungu mingine, wangepoteza kibali na ulinzi wa Mungu, na hivyo kushindwa kwa urahisi na maadui wao. Kwa hiyo, taifa hilo halingetokeza Masihi aliyeahidiwa. Ndiyo sababu Shetani alitaka kuwashawishi Waisraeli wafunge ndoa na watu wasioamini.

Sababu nyingine ni kwamba Mungu aliwajali watu wake wakiwa mtu mmoja-mmoja. Alijua kwamba ili kila mmoja wao awe na maisha mazuri na yenye furaha alipaswa kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye akiwa Mungu wao. Je, Yehova alikuwa na sababu nzuri ya kutoruhusu Mwisraeli afunge ndoa na mtu asiyeamini? Fikiria mfano wa Mfalme Sulemani. Alijua onyo hili la Yehova kuhusu wake wasio waamini: “Watageuza moyo wenu uifuate miungu yao.” Kwa sababu alikuwa mwanamume mwenye hekima isiyo ya kawaida, labda alifikiri hakuhitaji kufuata mashauri ya Mungu, na kwamba hayakumhusu. Aliyapuuza. Matokeo yalikuwa nini? “Wake zake wakaugeuza moyo wake . . . ukaifuata miungu mingine.” Huo ulikuwa msiba mkubwa! Solomoni alipoteza kibali cha Yehova, na watu wake wakagawanyika kwa sababu ya kukosa kuwa mwaminifu.​—⁠1 Wafalme 11:​2-4, 9-13.

Watu fulani wanaweza kudai kwamba kuna wengine waliofunga ndoa na watu wasioamini. Kwa mfano, Maloni aliyekuwa Mwisraeli, alimwoa Ruthu aliyekuwa Mmoabu ambaye alikuja kuwa mwabudu mwaminifu. Lakini ilikuwa hatari kuoa wanawake Wamoabu. Maloni hakusifiwa kwa kumwoa msichana Mmoabu; alikufa akiwa kijana, huenda hata kabla Ruthu hajaanza kumwabudu Yehova. Ndugu ya Maloni aliyeitwa Kilioni, alimwoa Orpa, mwanamke Mmoabu ambaye alishikamana na “miungu yake.” Kwa upande mwingine, Boazi alimwoa Ruthu miaka mingi baada ya kuwa mwamini. Hata baadaye Wayahudi walimwona kuwa “mgeuzwa imani kabisa.” Ndoa ya Ruthu na Boazi iliwaletea wote wawili baraka.​—⁠Ruthu 1:​4, 5, 15-17; 4:​13-17.

Je, ni jambo la busara kufikiri kwamba mfano wa Maloni na Ruthu unapingana kwa kiasi fulani na shauri la Yehova kwa waabudu wake kwamba wafunge ndoa na waamini wenzao tu? Je, kwa kweli kufikiria hivyo si ni sawa na kusema kwamba kwa kuwa mcheza-kamari fulani ameshinda pesa nyingi basi kucheza kamari ni njia inayofaa ya kutafuta riziki?

Biblia inawahimiza Wakristo leo, wafunge ndoa “katika Bwana tu.” Pia, inaonya hivi: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.” Shauri hili linaelekezwa kwa Wakristo wa kweli ambao wanatafuta wenzi wa ndoa. Kwa wale ambao tayari wamefunga ndoa na mtu asiyemwamini, Biblia inatoa mashauri mazuri ambayo yanaweza kuwasaidia kukabiliana na hali ngumu. (1 Wakorintho 7:​12-16, 39; 2 Wakorintho 6:14) Mashauri hayo yote yanaonyesha kwamba Yehova Mungu, Mwanzilishi wa ndoa, anataka sote tuwe na furaha tukiwa waabudu wake​—⁠iwe tumefunga ndoa au sisi ni waseja.