Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Simama Imara na Epuka Mitego ya Shetani!

Simama Imara na Epuka Mitego ya Shetani!

Simama Imara na Epuka Mitego ya Shetani!

‘Musimame imara ili kupinga hila za Ibilisi.’​—EFE. 6:11.

UNGEJIBU NAMNA GANI?

Namna gani mutumishi wa Yehova anaweza kuepuka asinaswe na mutego wa kufuatia vitu vya kimwili?

Ni nini kinachoweza kumusaidia Mukristo aliye katika ndoa asiangukie katika mutego wa uzinifu?

Sababu gani unaamini kama kuna faida ya kusimama imara na kushindana na tamaa ya kufuatia vitu vya kimwili na mambo ya uasherati?

1, 2. (a) Sababu gani Shetani hawasikilie huruma Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine”? (b) Habari hii itazungumuzia mitego gani miwili ya Shetani?

 SHETANI IBILISI hawasikilie wanadamu huruma, zaidi sana watumishi wa Yehova. Kwa hiyo, Shetani anafanya vita na Wakristo watiwa-mafuta ambao wangali bado duniani. (Ufu. 12:17) Wakristo hao hodari wameongoza kazi ya kuhubiri Ufalme katika siku zetu na wamefunua waziwazi kama Shetani ndiye mutawala wa ulimwengu huu. Shetani anawachukia pia “kondoo wengine,” wanaotegemeza Wakristo watiwa​-mafuta katika kazi ya kuhubiri na walio na tumaini la kuishi milele, tumaini ambalo Shetani alipoteza. (Yoh. 10:16) Basi si jambo la kushangaza ikiwa Shetani ni mwenye kukasirika sana! Iwe tunatumaini kuishi mbinguni ao duniani, hayo hayamuambie Shetani kitu. Kusudi ao muradi wake ni kutunasa tu.​—1 Pet. 5:8.

2 Ili kufikia kusudi lake, Shetani ametega mitego mbalimbali. Shetani “amezipofusha akili” za wasioamini, kwa sababu hiyo, hawakubali habari njema na hawawezi kuona mitego hiyo. Hata hivyo, huyo Ibilisi anaweza pia kuwanasa wale ambao wamekubali ujumbe wa Ufalme. (2 Kor. 4:3, 4) Habari iliyotangulia ilituonyesha mitego mitatu ya Shetani na namna tunaweza kuiepuka. Mitego hiyo ni: (1) kushindwa kuzuia ulimi, (2) kuogopa watu na mikazo ya wengine, na (3) mutu kujisikia kama Mungu hawezi kumusamehe anapofanya zambi. Sasa tuzungumuzie namna tunaweza kuepuka mitego mingine miwili ya Shetani. Mitego hiyo ni kufuatia vitu vya kimwili na kushawishiwa kufanya uzinifu.

MUTEGO UNAOSONGA: KUFUATIA VITU VYA KIMWILI

3, 4. Namna gani mahangaiko ya dunia hii yanaweza kumufanya mutu afuatie vitu vya kimwili?

3 Katika mufano mumoja, Yesu alizungumuzia mbegu iliyopandwa katikati ya miiba. Alionyesha kama mutu anaweza kusikia neno, ‘lakini mahangaiko ya mufumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa utajiri hulisonga neno, naye huwa asiyezaa matunda.’ (Mt. 13:22) Kwa kweli, kufuatia vitu vya kimwili ni moja ya mitego ambayo adui yetu Shetani anatumia.

4 Kuna mambo mawili yanayosonga neno. Jambo la kwanza ni ‘mahangaiko ya mufumo huu wa mambo.’ Katika hizi ‘nyakati za hatari zilizo ngumu kushugulika nazo,’ kuna mambo mengi yanayoweza kuhangaisha mutu. (2 Tim. 3:1) Bei ya vitu inazidi kupanda na inakuwa vigumu kupata kazi; kwa hiyo mutu anakuwa na magumu ya kupata feza ili kununua vitu ambayo anahitaji. Mutu anaweza pia kuwa na wasiwasi juu ya wakati ujao na kuanza kujiuliza hivi, ‘Je, nitapata feza za kutosha ili kutimiza mahitaji yangu nitakapoacha kazi kwa sababu ya uzee?’ Mahangaiko hayo yamesukuma watu watafute utajiri; wanafikiri kama wakiwa na feza nyingi hawatakosa kitu.

5. Namna gani “nguvu za utajiri” zinaweza kumudanganya mutu?

5 Jambo la pili ambalo Yesu alizungumuzia ni “nguvu za udanganyifu wa utajiri.” Jambo hilo na mahangaiko ya maisha vinaweza kulisonga neno. Biblia inasema kama “pesa ni ulinzi.” (Mhu. 7:12) Hata hivyo, kufuatia utajiri si jambo la hekima. Wengi wametambua kama kadiri walivyojikaza kutafuta feza juu na chini, ndivyo wamejikuta wamenaswa katika mutego wa kufuatia vitu vya kimwili. Wengine hata wamekuwa watumwa wa utajiri.​—Mt. 6:24.

6, 7. (a) Namna gani ndugu ao dada anaweza kushawishiwa na mutego wa kufuatia vitu vya kimwili mahali pake pa kazi? (b) Mukristo anapaswa kufikiria nini anapoombwa kutumika kisha saa zake za kazi?

6 Tamaa ya kupenda kuwa tajiri inaweza kuanza katika moyo wako bila wewe kujua. Kwa mufano, fikiria hali hii. Bwana wako wa kazi anakuja na kukuambia hivi: “Nina habari njema ya kukuambia! Kompanyi yetu imepata kazi kubwa. Kwa hiyo, miezi fulani inayokuja, itakuomba uendelee kutumika kisha saa zako za kazi. Lakini uwe hakika kama nitakuongezea mushahara wako na utafurahi kabisa.” Utakubali ao utakataa? Ni kweli kwamba, ni lazima utafutie familia yako mahitaji ya kimwili, lakini hilo si daraka tu ambalo unalo. (1 Tim. 5:8) Kuna mambo mengine unayopaswa kufikiria. Ni saa ngapi utakazokuwa unatumika kisha saa zako za kazi? Je, kazi yako ya kimwili itakufanya ukose wakati kwa ajili ya mambo ya kiroho kama vile mikutano ya kutaniko na Ibada ya Familia ya mangaribi?

7 Unapochukua uamuzi, ni jambo gani litakuwa la lazima sana kwako: je, ni feza ambazo bwana wako wa kazi atakuongezea ao uhusiano wako pamoja na Yehova? Je, utaacha tamaa ya kupata feza zaidi ikufanye ukose kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza? Je, unaona namna kufuatia vitu vya kimwili kunavyoweza kukunasa ikiwa unapuuza hali yako ya kiroho na ya familia yako? Ikiwa umeanza kupatwa na hali hiyo, namna gani unaweza kusimama imara ili uepuke kusongwa na tamaa ya kufuatia vitu vya kimwili?​—Soma 1 Timotheo 6:9, 10.

8. Ni mifano gani ya Maandiko inayoweza kutusaidia kuchunguza namna tunavyoishi?

8 Ili kuepuka mutego wa kufuatia vitu vya kimwili, mara kwa mara inafaa kuchunguza namna unavyoishi. Hatutaki kuwa kama Esau, ambaye kwa matendo yake alionyesha kama alikuwa mwenye kuzarau mambo ya kiroho! (Mwa. 25:34; Ebr. 12:16) Pia, hatupaswe kuwa kama mwanaume tajiri ambaye aliombwa na Yesu kuuzisha vitu alivyokuwa navyo na kuwapa maskini, na kisha amufuate. Kuliko kufanya yale Yesu alimuambia, mwanaume huyo ‘alienda zake akiwa amehuzunika, kwa maana alikuwa na mali nyingi.’ (Mt. 19:21, 22) Kwa kuwa alinaswa katika mutego wa kupenda sana mali, mwanaume huyo alipoteza pendeleo kubwa, ni kusema, kuwa mwanafunzi wa mutu mukubwa zaidi aliyepata kuishi! Fungua macho ili usipoteze pendeleo la kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo.

9, 10. Maandiko yanatutolea mashauri gani yanayofaa juu ya vitu vya kimwili?

9 Ili kuepuka kuhangaikia sana mambo ya kimwili, tii shauri hili la Yesu: “Musihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ ao, ‘Tutakunywa nini?’ ao, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua munahitaji vitu hivi vyote.”​—Mt. 6:31, 32; Lu. 21:34, 35.

10 Ikiwa hautake kuangukia katika mutego wenye kudanganya wa nguvu za utajiri, basi ujikaze kuwa na maoni ya muandikaji wa Biblia Aguri, aliyemuambia Mungu hivi: “Usinipe umaskini wala utajiri. Acha nile chakula nilichoamriwa.” (Met. 30:8) Biblia nyingine inatafsiri andiko hilo hivi: ‘Usinifanye kuwa maskini sana wala tajiri sana. Unipatie tu kile ambacho ninahitaji.’ Ni wazi kwamba kwa maneno hayo Aguri alitambua kama kuwa na feza ni kwa lazima, lakini pia alitambua hatari ya nguvu za udanganyifu za utajiri. Ujue kama mahangaiko ya dunia hii na nguvu za udanganyifu za utajiri vinaweza kuharibu hali ya mutu ya kiroho. Kuhangaikia sana vitu vya kimwili kunaweza kukupondea wakati, kukumaliza nguvu, na kupunguza ao kuondoa tamaa yote ya kufuatia faida za Ufalme. Kwa hiyo, fungua macho sana ili usiangukie katika mutego wa Shetani wa kufuatia vitu vya kimwili!​—Soma Waebrania 13:5.

SHIMO LENYE KUFICHWA: UZINIFU

11, 12. Namna gani Mukristo anaweza kuangukia katika mutego wa uzinifu mahali pa kazi?

11 Wawindaji ambao wanataka kunasa munyama mwenye nguvu wanaweza kuchimba shimo mahali ambapo munyama huyo anazoeza kupita. Kwa kawaida ili kuficha shimo hilo, wawindaji wanatia majani na udongo juu ya mutego huo. Zambi ya uasherati ni mutego mumoja ambao Shetani anatumia ili kuwanasa watu wengi. (Met. 22:14; 23:27) Wakristo fulani wameangukia katika shimo hilo kwa sababu walijitia wenyewe katika hali zinazoongoza kwa urahisi kwenye uasherati. Wakristo fulani ambao wameoa wamefanya uzinifu kwa sababu walianza kufanya urafiki wa kimapenzi na mutu asiyekuwa bibi yao ao bwana yao.

12 Urafiki huo wa kimapenzi na mutu asiye bibi yako ao bwana yako unaweza kuanzishwa mahali pa kazi. Uchunguzi fulani ulionyesha kama zaidi ya nusu ya wanawake waliofanya uzinifu, na wanaume karibu 3 kati ya 4 waliofanya uzinifu, walifanya uzinifu huo pamoja na mufanya kazi mwenzao. Je, kazi yako inakulazimisha kutumika na wanaume ao wanawake? Ikiwa ni hivyo, urafiki wako pamoja nao ni wa namna gani? Je, umejiwekea mipaka ili uhusiano wako nao uwe tu wa kazi na usigeuke kuwa urafiki wa kimapenzi? Kwa mufano, dada Mukristo anaweza kuwa na zoea ya kuongeaongea na mwanaume fulani anayefanya kazi pamoja naye, mwanaume huyo anaweza kufikia kuwa mutu wake wa siri. Kwa hiyo dada anaweza kumutumainia na kuanza hata kumuambia matatizo yaliyo kati yake na bwana yake. Ao ni ndugu ambaye mahali pa kazi anafanya urafiki na mwanamuke fulani; ndugu huyo anaweza kuanza kufikiri hivi: “Mwanamuke huyu anafurahia maoni yangu na ananisikiliza kabisa ninapoongea naye. Na anapendezwa nami. Ikiwa bibi yangu angekuwa hivi, ningekuwa mwenye furaha!” Je, hauone kama hali hiyo inaweza kumuingiza kwa urahisi dada ao ndugu huyo katika uzinifu?

13. Urafiki wa kimapenzi usiofaa unaweza kuanza namna gani kati ya ndugu na dada katika kutaniko?

13 Urafiki wa kimapenzi unaweza pia kuanza kati ya ndugu na dada katika kutaniko. Fikiria jambo hili lililofikia ndugu Daniel na bibi yake, Sara, * waliokuwa mapainia wa kawaida. Daniel alikuwa pia muzee ambaye alikuwa anakubali kwa furaha kila mugawo aliokuwa akipewa katika kutaniko. Daniel alijifunza Biblia pamoja na wanaume vijana watano, na watatu kati yao walibatizwa. Ndugu hao wapya walihitaji kabisa kusaidiwa kiroho. Kwa sababu ya kushugulikia migawo mbalimbali ya kiteokrasi, Daniel alikosa wakati wa kufanya hivyo, na kila mara bibi yake Sara ndiye aliyekuwa akiwasaidia. Kisha urafiki wao ukakomaa sana; ndugu hao waliojifunza na Daniel walipohitaji kitia-moyo, Sara aliwatia moyo. Sara naye alipohitaji kutiwa moyo, ndugu hao walikuwa karibu sana naye ili kumutia moyo. Hali hiyo ilikuwa mutego hatari. Daniel anasema hivi: “Bibi yangu alijikaza kuwasaidia vijana hao mwezi baada ya mwezi, lakini hali yake mwenyewe ya kiroho iliregea na alikosa mutu wa kuwa karibu naye. Kwa kuwa sikumuhangaikia, hilo lilizaa matokeo mabaya. Bibi yangu alifanya uzinifu na ndugu mumoja kati ya ndugu hao niliojifunza nao Biblia na akaendelea kuwa muzaifu kiroho. Nilihangaikia sana madaraka yangu hivi kwamba sikuweza kuona kama Sara amekuwa muzaifu kiroho.” Namna gani tunaweza kuepuka hali hiyo mbaya?

14, 15. Ni mambo gani yanayoweza kuwasaidia Wakristo walio katika ndoa ili wasiangukie katika mutego wa uzinifu?

14 Ili kuepuka mutego wa uzinifu, inafaa kufikiria sana naziri uliyofanya ya ndoa. Yesu alisema hivi: ‘Kile ambacho Mungu ameunganisha mutu yeyote asikitenganishe.’ (Mt. 19:6) Usifikiri hata kidogo kama mapendeleo yako katika kutaniko ni ya lazima sana kuliko bibi ao bwana yako. Zaidi ya hayo, ujue kama kumuacha bibi yako ao bwana yako yeye mwenyewe kwa sababu ya mambo yasiyokuwa ya lazima kunaweza kuregeza ndoa yenu na hali hiyo inaweza kukutia katika jaribu na labda hata kukuongoza katika zambi nzito ya uzinifu.

15 Basi, ikiwa wewe ni muzee, utashugulikia kundi namna gani? Mutume Petro aliandika hivi: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu.” (1 Pet. 5:2) Ni kweli kwamba hamupaswe kuwasahau ndugu na dada katika kutaniko walio chini ya uangalizi wenu. Hata hivyo, hamupaswe kusahau bibi zenu kwa sababu ya kutaniko. Kutumikia sana ndugu na dada katika kutaniko ili kuwasaidia kiroho wakati bibi yako nyumbani anaendelea “kukufa na njaa kiroho,” haina maana yoyote na ni hatari kabisa. Daniel anasema hivi: “Usihangaikie mapendeleo ya kutaniko hivi kwamba yakukoseshe wakati wa kuitunza familia yako.”

16, 17. (a) Wakristo walio katika ndoa wanaweza kuchukua mipango gani ili kuonyesha wazi kwamba hawapendi kuwa na uhusiano wa kimahaba ao kimapenzi mahali pao pa kazi? (b) Toa mufano wa habari fulani zilizochapishwa katika magazeti yetu zinazoweza kuwasaidia Wakristo waepuke uzinifu.

16 Magazeti Munara wa Mulinzi na Amkeni! yamewatolea Wakristo walio katika ndoa mashauri mengi mazuri ili kuwasaidia wasimame imara na wasiangukie katika mutego wa uzinifu. Kwa mufano, Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 mwezi wa 9, 2006 ulitoa mashauri haya: ‘Unapokuwa kazini na kwingineko, jihazari na hali zinazoweza kufanya uwe na uhusiano wa karibu pamoja na mutu wa jinsia tofauti. Kwa mufano, kufanya kazi kwa ukaribu pamoja na mutu wa jinsia tofauti baada ya saa za kazi kunaweza kutokeza kishawishi. Ikiwa wewe ni mwanamume ao mwanamuke aliyefunga ndoa, unapaswa kuonyesha waziwazi kwa maneno na matendo kwamba hautaki kuwa na uhusiano wa kimahaba isipokuwa na mwenzi wako. Kwa kuwa unafuatia ujitoaji-kimungu, bila shaka haungependa kuwavutia watu kwa kucheza-cheza nao kimapenzi ao kwa kuvalia na kujipamba kwa njia isiyofaa. Kuweka picha za mwenzi wako wa ndoa na za watoto wako mahali pa kazi kutakukumbusha na kuwakumbusha wengine kwamba unaipenda familia yako. Azimia kutochochea wala kuruhusu vishawishi vya uhusiano wa kimahaba.’

17 Habari yenye kichwa “Uaminifu Katika Ndoa Unamaanisha Nini Hasa?” iliyotolewa katika Amkeni! ya Mwezi wa 4, 2009 ilionya kuhusu hatari za kuwazia uko unafanya kitendo cha ndoa pamoja na mutu asiyekuwa bibi yako ao bwana yako. Habari hiyo ilionyesha kama kuwaziawazia uko unafanya kitendo cha ndoa kunaweza kuchochea mutu awe na tamaa ya kufanya uzinifu. (Yak. 1:14, 15) Ikiwa umefunga ndoa, basi ingekuwa vizuri kurudilia mara kwa mara habari hiyo wewe na bwana ao bibi yako. Ndoa ni mupango ulioanzishwa na Yehova na ndoa ni kitu kitakatifu. Kujiwekea wakati ili kuongea na bibi yako ao bwana yako kuhusu ndoa yenu ni njia bora ya kuonyesha kama unaheshimu mambo matakatifu.​—Mwa. 2:21-24.

18, 19. (a) Uzinifu unaleta matokeo gani mabaya? (b) Uaminifu katika ndoa unaleta faida gani?

18 Ukitambua kama umeanza kukomalisha urafiki wa kimapenzi na mutu asiye bibi yako ao bwana yako, fikiria juu ya matokeo mabaya ya uasherati na uzinifu. (Met. 7:22, 23; Gal. 6:7) Wale wanaofanya uasherati wanamuchukiza Yehova, wanajiumiza na wanaumiza bibi zao ao bwana zao. (Soma Malaki 2:13, 14.) Pia, fikiria faida wanazopata wale wanaofuatia mwenendo safi. Watu hao wanatumaini kupata uzima wa milele na kuanzia sasa wanafurahia maisha mazuri, kutia ndani zamiri safi.​—Soma Methali 3:1, 2.

19 Mutunga​-Zaburi aliimba hivi: “Wale wanaoipenda sheria yako [ya Mungu] wana amani nyingi, na hakuna kitu cha kuwakwaza.” (Zab. 119:165) Kwa hiyo, tupende kweli na ‘tuendelee kuangalia sana jinsi tunavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima’ katika nyakati hizi zenye hatari. (Efe. 5:15, 16) Leo, Shetani ametia mitego mingi katika njia ili kuwanasa waabudu wa kweli. Lakini, tuna vifaa vya kutulinda. Yehova ametupatia kila kitu tunachohitaji ili ‘kusimama imara’ na “kuizima mishale yote inayowaka ya yule mwovu”!​—Efe. 6: 11, 16.

[Maelezo ya chini]

^ Majina yamebadilishwa.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kufuatia vitu vya kimwili kunaweza kumusonga mutu na kuharibu hali yake ya kiroho. Usiruhusu jambo hilo likupate

[Picha katika ukurasa wa 29]

Ikiwa unapendezwa kimapenzi ao ukimuacha mutu asiye bibi yako ao bwana yako apendezwe na wewe kimapenzi, unaweza kuangukia katika uzinifu