Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ripoti ya Mkutano wa Kila Mwaka

Mkutano Uliokazia Umoja na Kuzungumzia Mipango Yenye Kusisimua

Mkutano Uliokazia Umoja na Kuzungumzia Mipango Yenye Kusisimua

SIKUZOTE mikutano ya kila mwaka ya Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania hutokeza msisimuko. Ndivyo ulivyokuwa mkutano wa 127 wa kila mwaka, uliofanywa Jumamosi, Oktoba 1, 2011! Wageni walioalikwa kutoka ulimwenguni pote walikusanyika katika Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Jersey City, New Jersey, Marekani.

Gerrit Lösch wa Baraza Linaloongoza aliukaribisha umati huo wenye furaha. Aliwaambia wajumbe hao kutoka katika nchi 85 kwamba wanafurahia umoja wa pekee ulimwenguni pote. Umoja huo unatoa ushahidi mzuri na kumtukuza Yehova. Kwa kweli, umoja ulikaziwa tena na tena kwenye mkutano huo.

RIPOTI NZURI KUTOKA MEXICO

Sehemu ya kwanza ya programu ilionyesha umoja uliopo miongoni mwa watu wa Yehova. Baltasar Perla aliwahoji washiriki wenzake watatu wa familia ya Betheli ya Mexico kuhusu kuunganishwa kwa ofisi sita za tawi katika bara la Amerika ya Kati na ofisi ya tawi ya Mexico. Kwa sababu ya kuunganishwa kwa ofisi hizo, sasa familia ya Betheli ya Mexico ina washiriki wengi zaidi kutoka katika tamaduni na nchi mbalimbali. Ongezeko hilo la waamini wenzetu kutoka katika nchi mbalimbali limetokeza badilishano la kitia-moyo. Ni kana kwamba Mungu alichukua kifutio kikubwa na kufuta kabisa mipaka ya kitaifa.

Changamoto moja iliyosababishwa na kuunganishwa kwa ofisi hizo ilikuwa kuwasaidia wahubiri kutohisi kwamba wako mbali sana na tengenezo la Yehova hata ingawa ofisi za tawi zimefungwa katika nchi zao. Ili kukabiliana na changamoto hiyo, kila kutaniko linawasiliana na ofisi ya tawi kupitia barua-pepe iliyo salama na kwa njia hiyo hata makutaniko ya mashambani yanaweza kuwasiliana moja kwa moja na ofisi ya tawi.

HABARI ZA KARIBUNI KUTOKA JAPANI

James Linton kutoka katika ofisi ya tawi ya Japani alieleza jinsi ndugu zetu walivyoathiriwa na tetemeko la nchi na mawimbi ya tsunami yaliyoipiga nchi hiyo mnamo Machi 2011. Mashahidi wengi walipoteza wapendwa wao na pia mali zao. Mashahidi ambao wanaishi nje ya eneo lililoathiriwa walitoa nyumba zaidi ya 3,100 na mamia ya magari ili kuwasaidia walioathiriwa. Wajitoleaji wa Halmashauri za Ujenzi wa Kimkoa walifanya kazi mfululizo ili kurekebisha nyumba za akina ndugu. Watu zaidi ya 1,700 walijitolea kutumika popote penye uhitaji. Kikundi cha wajitoleaji kutoka Marekani kilisaidia kurekebisha Majumba ya Ufalme, na kwa ujumla wajitoleaji 575 walifanya kazi katika mradi huo.

Jitihada kubwa zimefanywa ili kushughulikia hali ya kiroho na ya kihisia ya wale walioathiriwa. Wazee zaidi ya 400 walifanya kazi ya uchungaji mahali penye uhitaji. Hangaiko la Baraza Linaloongoza lilionekana wazi wakati waangalizi wawili wa eneo la dunia kutoka katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova ya ulimwenguni pote walipotembelea eneo lililokumbwa na msiba ili kuwatia moyo akina ndugu na dada. Maneno yenye kutia moyo kutoka kwa Mashahidi ulimwenguni pote yamewafariji sana wale walioathiriwa.

USHINDI MBALIMBALI WA KISHERIA

Wahudhuriaji walisikiliza kwa makini wakati Stephen Hardy kutoka ofisi ya tawi ya Uingereza alipoongoza mazungumzo kuhusu ushindi mbalimbali wa kisheria uliopatikana hivi karibuni. Kwa mfano, serikali ya Ufaransa ilikuwa ikidai kwamba shirika letu nchini Ufaransa lilipe dola milioni 82 (za Marekani) za kodi. Suala hilo lilitatuliwa wakati Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR) ilipofanya uamuzi uliotuunga mkono. Mahakama hiyo ilisema kwamba serikali ya Ufaransa ilikiuka Kifungu Namba 9 cha Mkataba wa Ulaya ambacho kinalinda uhuru wa kidini. Maelezo ya uamuzi wa mahakama hiyo yanaonyesha kwamba kesi hiyo haikuhusu pesa tu, yalisema hivi: “Kukataa kutambua shirika la kidini, kulivunja shirika hilo, kutumia lugha ya matusi kuhusu kikundi fulani cha kidini, mambo yote hayo yanathibitisha kwamba haki inayotetewa na Kifungu Namba 9 cha Mkataba huo imekiukwa.”

Pia, mahakama ya ECHR ilifanya uamuzi uliotuunga mkono katika kesi iliyohusisha nchi ya Armenia. Tangu mwaka wa 1965, mahakama ya ECHR imekuwa ikisisitiza kwamba Mkataba wa Ulaya hauwalindi watu kutokana na utumishi wa lazima wa kijeshi. Baraza Kuu, yaani, baraza la juu zaidi katika Mahakama ya Ulaya, liliamua kwamba Mkataba wa Ulaya unapaswa kutetea watu “wanaokataa utumishi wa kijeshi, ikiwa wanachochewa na sababu nzito na isiyoweza kupuuzwa.” Uamuzi huo unailazimisha nchi ya Armenia na nchi kama vile Azerbaijan na Uturuki kutambua haki hiyo.

MIRADI YA UJENZI

Msemaji aliyefuata alikuwa Guy Pierce wa Baraza Linaloongoza na alikiri kwamba wahudhuriaji wote walikuwa na hamu ya kujua kuhusu miradi yetu ya ujenzi katika Jimbo la New York. Alitumia vidio kuonyesha ujenzi unaoendelea huko Wallkill, Patterson, na kuhusu viwanja vilivyonunuliwa hivi karibuni huko Warwick na Tuxedo, New York. Huko Wallkill, kazi ya ujenzi wa jengo jipya la makao itakwisha mwaka wa 2014, na jengo hilo litakuwa na vyumba 300 zaidi.

Kuna mipango ya kujenga kwenye kiwanja cha Warwick ambacho kina ukubwa wa ekari 248. Ndugu Pierce alisema kwamba “ingawa hatujui kwa hakika mapenzi ya Yehova ni nini kuhusu Warwick, tutaanza kazi ya ujenzi ili hatimaye makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova yahamie huko.” Mipango pia inafanywa ili kutumia kiwanja chenye ukubwa wa ekari 50 ambacho kiko umbali wa kilomita 10 upande wa kaskazini wa Warwick kwa ajili ya mashini na vifaa vya ujenzi. “Mara tu baada ya kupata kibali cha kujenga, tunatumaini kukamilisha mradi wote katika muda wa miaka minne,” akasema Ndugu Pierce. “Halafu tutauza majengo yetu ya Brooklyn.”

“Je, Baraza Linaloongoza limebadili maoni yake kuhusu kukaribia kwa ile dhiki kuu?” akauliza Ndugu Pierce. Kisha akajibu, “La hasha! Ikiwa dhiki kuu itakatisha mipango yetu, hilo litakuwa jambo zuri sana, jambo zuri ajabu!”

JIHADHARI NA SIMBA ANAYENGURUMA

Msemaji aliyefuata, Stephen Lett, ambaye pia ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alizungumzia andiko la 1 Petro 5:8: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” Ndugu Lett alisema kwamba simba wana sifa kadhaa ambazo zinaufanya mfano ambao Petro alitoa kuhusu Ibilisi ufae kabisa.

Kwa kuwa simba wana nguvu zaidi na wanakimbia kwa kasi zaidi kuliko wanadamu, hatupaswi kujaribu kupigana na Shetani au kujaribu kumkimbia kwa kutegemea nguvu zetu wenyewe. Tunahitaji msaada wa Yehova. (Isa. 40:31) Simba huwinda kwa kunyemelea, kwa hiyo ni lazima tuepuke giza la kiroho ambamo Shetani anatafuta windo lake. Kama vile tu simba anavyomuua paa mnyonge au ndama wa pundamilia anayelala, vivyo hivyo, Shetani hana huruma na angependa kutuua. Na baada ya simba kushiba, mara nyingi mnyama aliyeliwa hatambuliki, vivyo hivyo “hali ya mwisho” ya wale wanaoliwa kiroho na Shetani ‘inakuwa mbaya zaidi kwao kuliko ile ya kwanza.’ (2 Pet. 2:20) Kwa hiyo, tunahitaji kuchukua msimamo wetu kumpinga Shetani na kushika imara kanuni za Biblia ambazo tumejifunza.​—1 Pet. 5:9.

THAMINI NAFASI YAKO KATIKA NYUMBA YA YEHOVA

Msemaji aliyefuata, Samuel Herd wa Baraza Linaloongoza alisema hivi: “Sisi sote tuna nafasi fulani katika nyumba ya Yehova.” Wakristo wote wana nafasi yao katika “nyumba” ya Mungu, hekalu lake la kiroho, yaani, mpango wa kumwabudu kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu. Tunapaswa kuithamini sana nafasi hiyo kwa sababu ni pendeleo lenye thamani. Kama Daudi, tunatamani “kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha [yetu].”​—Zab. 27:4.

Ndugu Herd alirejelea Zaburi 92:12-14 na kuuliza, “Yehova anatuwezesha jinsi gani kufanikiwa?” Akajibu: “Katika paradiso ya kiroho, Mungu anatupasha joto kwa njia ya mfano, anatulinda, na kutupatia maji yenye kuburudisha ya kweli. Na tumshukuru kwa sababu ya mambo hayo.” Kisha, Ndugu Herd akawahimiza hivi wasikilizaji: “Acheni tutosheke kwa kukaa katika nyumba ya Yehova, si kwa muda mfupi tu bali milele.”

WAKRISTO WANALIHESHIMU NENO LA MUNGU

David Splane, ambaye pia ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alieleza katika hotuba iliyofuata kwamba Wakristo wa kweli wameliheshimu sikuzote Neno la Mungu. Katika karne ya kwanza, walilitegemea ili kusuluhisha suala la tohara. (Mdo. 15:16, 17) Lakini wale waliodai kuwa Wakristo katika karne ya pili ambao walifundishwa falsafa za Wagiriki walianza kutanguliza tamaa yao ya kupata elimu badala ya kufuata Maandiko. Baadaye, wengine waliacha mafundisho ya Biblia na kufuata maoni ya maliki wa Roma na wale walioitwa eti Mababa wa Kanisa, na hivyo wakaanzisha mafundisho mengi ya uwongo.

Ndugu Splane alisema kwamba Yesu alionyesha katika mfano mmoja kwamba Wakristo wa kweli waliotiwa mafuta wangeendelea kuwapo duniani ili kuitetea kweli. (Mt. 13:24-30) Hatuwezi kusema kwa hakika watiwa-mafuta hao walikuwa akina nani. Hata hivyo, kwa karne nyingi, watu wengi wameshutumu mafundisho na mazoea yasiyo ya kimaandiko. Baadhi yao ni Askofu-mkuu Agobard wa Lyons katika karne ya 9, Peter wa Bruys, Henry wa Lausanne, na Valdès (au, Waldo) katika karne ya 12, John Wycliffe katika karne ya 4, William Tyndale katika karne ya 16, na Henry Grew na George Storrs katika karne ya 19. Mashahidi wa Yehova leo wanaendelea kushikamana na viwango vya Maandiko na wanatambua kwamba Biblia ndiyo msingi wa mafundisho ya kweli. Ndiyo sababu Baraza Linaloongoza limechagua andiko la Yohana 17:17 kuwa andiko letu la mwaka wa 2012: “Neno lako ni kweli.”

MABADILIKO YENYE KUSISIMUA YANAYOHUSU MAZOEZI NA UTUMISHI

Anthony Morris wa Baraza Linaloongoza alitoa tangazo kuhusu mabadiliko yanayowahusu wamishonari na mapainia wa pekee. Kuanzia Septemba 2012, madarasa ya Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo yatafanywa katika nchi fulani zilizochaguliwa. Kusudi la Shule ya Gileadi limebadilishwa. Kuanzia Oktoba mwaka uliopita, wote wanaozoezwa katika Gileadi ni wale ambao tayari wamekuwa wakishiriki katika aina fulani ya utumishi wa pekee wa wakati wote, kwa mfano, wamishonari ambao hawajaenda Gileadi, mapainia wa pekee, waangalizi wanaosafiri, au Wanabetheli. Wahitimu watatumiwa kuwaimarisha na kuwatia nguvu watu wa Mungu ama wakiwa katika ofisi za tawi, katika kazi ya kusafiri, au katika maeneo yenye watu wengi ambako wanaweza kuyatia moyo makutaniko katika kazi ya kuhubiri.

Mapainia zaidi wa pekee watahubiri katika maeneo mpya ya mashambani. Kuanzia Januari 1, 2012, baadhi ya wahitimu wa Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja na Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo walipewa migawo ya kutumikia wakiwa mapainia wa pekee wa muda ili wahubiri katika maeneo mapya na kutumiwa kupanua kazi hiyo katika maeneo ya mashambani. Wanapewa migawo ya kuwa mapainia wa pekee kwa muda wa mwaka mmoja-mmoja mpaka miaka mitatu. Wale wanaopata matokeo mazuri wanaweza kupewa migawo ya kudumu.

Mkutano wa mwaka wa 2011 ulikuwa wenye shangwe. Tunatumaini kwamba Yehova atabariki mipango mipya ya kuongeza kazi yetu ya kuhubiri na kuimarisha zaidi umoja wa undugu wetu ili tumletee sifa na utukufu.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 18, 19]

Kuwajua Vizuri Zaidi

Pia, wakati wa programu hiyo, wajane watano kati ya wajane tisa walio hai wa washiriki wa Baraza Linaloongoza walihojiwa. Dada Marina Sydlik, Edith Suiter, Melita Jaracz, Melba Barry, na Sydney Barber walieleza jinsi walivyojifunza kweli na kuingia katika utumishi wa wakati wote. Kila mmoja wao aliwasimulia wasikilizaji mambo mazuri aliyokumbuka kuhusu mume wake, na baraka ambazo walifurahia pamoja. Baada ya mahojiano hayo, wasikilizaji waliguswa moyo walipoimba wimbo namba 86, wenye kichwa “Wanawake Waaminifu, Dada Wakristo.”

[Picha]

(Juu) Daniel na Marina Sydlik; Grant na Edith Suiter; Theodore na Melita Jaracz

(Chini) Lloyd na Melba Barry; Carey na Sydney Barber

[Ramani katika ukurasa wa 16]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Ofisi sita za tawi ziliunganishwa chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi ya Mexico

MEXICO

GUATEMALA

HONDURAS

EL SALVADOR

NIKARAGUA

KOSTA RIKA

PANAMA

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mchoro wa makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova ambayo yanakusudiwa kujengwa huko Warwick, New York