Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kuna Thawabu kwa Ajili ya Kazi Yenu”

“Kuna Thawabu kwa Ajili ya Kazi Yenu”

“Kuna Thawabu kwa Ajili ya Kazi Yenu”

AKIONGOZA jeshi lake, Mfalme Asa anaenda kwa kasi ndani ya bonde lililo chini sana kutoka kwenye eneo lenye milima la Yudea hadi kwenye eneo tambarare la pwani. Asa anasimama akihemahema mahali ambapo bonde linakuwa pana. Chini yake kuna kambi kubwa sana ya maadui! Inaonekana kwamba idadi halisi ya wanajeshi hao Waethiopia ni milioni moja. Jeshi la Asa lina jumla ya wanaume ambao ni nusu ya idadi ya wanajeshi Waethiopia.

Anapokabili pigano hilo, ni jambo gani linalomhangaisha zaidi Asa? Je, ni kutoa amri kwa majenerali wake? Je, ni kuwatia moyo askari-jeshi wake? Je, ni kuiandikia barua familia yake? Sivyo, hata kidogo! Licha ya kwamba anakabili hali ngumu, Asa anasali.

Kabla hatujaizungumzia sala hiyo na kuchunguza kilichotukia, kwanza fikiria Asa alikuwa mtu wa aina gani. Ni nini kilichomfanya atende kwa njia hiyo? Je, alikuwa na sababu ya kumwomba Mungu msaada? Simulizi kumhusu Asa linatuonyesha nini kuhusu jinsi Yehova anavyobariki utendaji mbalimbali wa watumishi Wake?

REKODI YA ASA

Kwa miaka 20 iliyofuata baada ya Israeli kugawanyika na kuwa falme mbili, ufalme wa Yuda ulikuwa umechafuliwa kabisa na mazoea ya kipagani. Asa alipoanza kutawala akiwa mfalme mwaka wa 977 K.W.K., hata makao ya mfalme yalikuwa yamechafuliwa na ibada ya miungu ya uzazi ya Wakanaani. Lakini masimulizi yaliyoongozwa na roho ya Mungu kuhusu utawala wa Asa yanasema kwamba “akafanya yaliyokuwa mema na sawa machoni pa Yehova Mungu wake.” Asa “akaondoa madhabahu za kigeni na mahali pa juu, akazivunja nguzo takatifu na kuikata miti mitakatifu.” (2 Nya. 14:2, 3) Asa pia aliwafukuza kutoka katika ufalme wa Yuda “wanaume makahaba wa hekaluni,” ambao walifanya ulawiti kwa jina la dini. Asa alifanya mengi zaidi ya kuondoa uovu huo wote. Aliwahimiza pia watu “wamtafute Yehova Mungu wa mababu zao” na kuishika “sheria na amri” ya Mungu.​—1 Fal. 15:12, 13; 2 Nya. 14:4.

Yehova alipendezwa na bidii ya Asa kwa ajili ya ibada ya kweli, naye akamthawabisha kwa miaka mingi ya amani. Ndiyo sababu mfalme huyo alisema hivi: “Tumemtafuta Yehova Mungu wetu. Tumemtafuta, naye anatupa pumziko kuzunguka pande zote.” Watu waliitumia hali hiyo ili kuimarisha majiji ya ufalme wa Yuda. Simulizi hilo la Biblia linasema hivi: “Nao wakajenga na kufanikiwa.”​—2 Nya. 14:1, 6, 7.

KATIKA UWANJA WA VITA

Kwa sababu ya rekodi ya Asa, haishangazi kwamba alisali alipokabili jeshi kubwa zaidi la kibinadamu linalotajwa katika Maandiko. Asa alijua kwamba Mungu anathawabisha matendo ya imani. Katika sala yake, mfalme huyo alimsihi Yehova amsaidie. Asa alitambua kwamba ikiwa angemtegemea Mungu na kupata msaada wake, angeshinda vita haidhuru maadui walikuwa wengi au wenye nguvu kadiri gani. Jina la Yehova lilihusika katika vita hivyo, na hivyo Asa alimsihi Mungu amsaidie kwa msingi huo. Mfalme huyo alisali hivi: “Utusaidie, Ee Yehova Mungu wetu, kwa maana sisi tunakuegemea wewe, nasi kwa jina lako tumekuja kupigana na umati huu. Ee Yehova, wewe ni Mungu wetu. Usiache mwanadamu anayeweza kufa apate nguvu juu yako.” (2 Nya. 14:11) Ni kana kwamba alikuwa akisema: ‘Uvamizi wa Waethiopia ni shambulizi dhidi yako, Yehova. Usiache jina lako lidharauliwe kwa kuruhusu wanadamu walio dhaifu wawashinde wale wanaoitwa kwa jina lako.’ Ndipo “Yehova akawashinda Waethiopia mbele ya Asa na mbele ya Yuda, na Waethiopia wakakimbia.”​—2 Nya. 14:12.

Leo, watu wa Yehova wanakabili wapinzani wengi wenye nguvu. Hatutapigana nao kwa kutumia silaha halisi katika uwanja halisi wa kivita. Hata hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawathawabisha watu wake wote waaminifu kwa kuwapa ushindi wanapopigana vita vya kiroho kwa ajili ya jina lake. Mapambano yetu huenda yakatia ndani kujitahidi kuishinda roho ya upotovu wa maadili iliyoenea, udhaifu wetu, au kujitahidi kuilinda familia yetu kutokana na uvutano unaopotosha. Hata tukabili matatizo ya aina gani, tunaweza kutiwa moyo na sala ya Asa. Ushindi wake ulikuwa ushindi wa Yehova. Ushindi huo unaonyesha kile ambacho wote wanaomtegemea Yehova wanaweza kutazamia. Hakuna mwanadamu anayeweza kushindana na Yehova.

KITIA-MOYO NA ONYO

Aliporudi kutoka vitani, Asa alikutana na Azaria. Nabii huyo alimtia moyo na kumwonya pia: “Mnisikilize mimi, Ee Asa na Yuda wote na Benyamini! Yehova yuko pamoja nanyi ikiwa ninyi mko pamoja naye; nanyi mkimtafuta, atawaruhusu mumpate, lakini mkimwacha yeye atawaacha ninyi. . . . Iweni hodari na msiache mikono yenu ilegee, kwa sababu kuna thawabu kwa ajili ya kazi yenu.”​—2 Nya. 15:1, 2, 7.

Maneno hayo yanaweza kuimarisha imani yetu. Yanaonyesha kwamba Yehova atakuwa pamoja nasi maadamu tunamtumikia kwa uaminifu. Tunapomlilia ili atusaidie, tunaweza kuwa na hakika kwamba anatusikiliza. Azaria alisema hivi: “Iweni hodari.” Kwa kawaida, uhodari mkubwa unahitajiwa ili kufanya mambo yanayofaa, lakini tunajua kwamba tunaweza kufanikiwa kwa msaada wa Yehova.

Kwa kuwa Maaka, nyanya ya Asa alitengeneza “sanamu yenye kutisha kwa ajili ya mti mtakatifu,” Asa alikuwa na kazi ngumu ya kumwondoa ili asiendelee kuwa “malkia.” Alishinda jaribu hilo na kuteketeza sanamu iliyotengenezwa na nyanya yake. (1 Fal. 15:13) Asa alibarikiwa kwa sababu ya azimio na uhodari wake. Sisi pia ni lazima tushikamane kabisa na Yehova na viwango vyake vya uadilifu iwe watu wetu wa ukoo ni washikamanifu kwa Mungu au la. Tukifanya hivyo, Yehova atatuthawabisha kwa sababu ya mwenendo wetu wa uaminifu.

Asa alithawabishwa alipowaona Waisraeli wengi kutoka katika ufalme wa kaskazini wenye kuasi imani wakimiminika Yuda walipoona kwamba Yehova alikuwa pamoja naye. Walithamini sana ibada safi hivi kwamba wakaamua kuacha nyumba zao ili waishi miongoni mwa watumishi wa Yehova. Kisha, Asa na watu wote katika Yuda wakafurahi na ‘kuingia katika agano ili kumtafuta Yehova Mungu kwa moyo wao wote na kwa nafsi yao yote.’ Ikawaje? Mungu “aliwaruhusu wampate; na Yehova akaendelea kuwapa pumziko kuzunguka pande zote.” (2 Nya. 15:9-15) Tunashangilia kama nini wakati watu wanaopenda uadilifu wanapoikubali ibada safi ya Yehova!

Hata hivyo, nabii Azaria alitoa pia onyo. Alionya hivi: “Mkimwacha [Yehova] atawaacha ninyi.” Isiwe hivyo kwetu kamwe, kwa kuwa matokeo yanaweza kuwa mabaya sana! (2 Pet. 2:20-22) Maandiko hayasemi kwa nini Yehova alimpa Asa onyo hilo, lakini mfalme huyo hakulitii.

“UMETENDA KWA UPUMBAVU”

Katika mwaka wa 36 wa utawala wa Asa, Mfalme Baasha wa Israeli alivamia Yuda. Labda ili kuwazuia raia wake wasionyeshe ushikamanifu kwa Asa na ibada safi, Baasha alianza kuimarisha jiji la mpakani la Rama, kilomita nane upande wa kaskazini wa Yerusalemu. Badala ya kumwomba Mungu amsaidie kama alivyofanya alipovamiwa na Waethiopia, Asa aliwaomba wanadamu wamsaidie. Akamtumia zawadi mfalme wa Siria, akimwomba aushambulie ufalme wa kaskazini wa Israeli. Wasiria waliposhambulia, Baasha aliondoka Rama.—2 Nya. 16:1-5.

Yehova hakupendezwa na Asa, basi akamtuma nabii Hanani amwambie hivyo. Kwa kuwa alijua jinsi Yehova alivyowatendea Waethiopia, Asa alipaswa kuwa amejifunza kwamba ‘macho ya Yehova yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.’ Labda Asa alipokea mashauri mabaya au alifikiri kwamba Baasha na wanajeshi wake hawakuwa tishio kubwa sana na hivyo angeweza kupigana nao peke yake. Kwa vyovyote vile, Asa alikuwa na maoni ya kibinadamu na hakumtegemea Yehova. “Umetenda kwa upumbavu kwa habari hii,” akasema Hanani, “kwa maana tangu sasa na kuendelea kutakuwa na vita juu yako.”​—2 Nya. 16:7-9.

Asa aliitikia vibaya. Kwa hasira, alimtupa nabii Hanani katika nyumba ya mikatale. (2 Nya. 16:10) Inawezekana kwamba Asa aliwaza hivi: ‘Je, kweli ninastahili kukaripiwa baada ya kuwa mwaminifu kwa miaka mingi?’ Kwa kuwa sasa alikuwa amezeeka, inawezekana kwamba alipoteza kwa kadiri fulani uwezo wake wa kufikiri? Biblia haisemi chochote.

Katika mwaka wa 39 wa utawala wake, Asa akapata ugonjwa mbaya sana wa miguu. Simulizi hilo linasema hivi: “Hata katika ugonjwa wake hakumtafuta Yehova bali waponyaji.” Wakati huo, inaonekana kwamba Asa alipuuza afya yake ya kiroho. Ni wazi kwamba alikufa katika mwaka wa 41 wa utawala wake akiwa katika hali mbaya kimwili na kiakili.​—2 Nya. 16:12-14.

Hata hivyo, inaonekana kwamba sifa nzuri za Asa na bidii yake kwa ajili ya ibada safi ilizidi makosa yake. Hakuacha kamwe kumtumikia Yehova. (1 Fal. 15:14) Basi, kwa msingi huo, simulizi lake la maisha linatufundisha nini? Linatusaidia kutambua kwamba tunapaswa kutafakari kuhusu jinsi Yehova alivyotusaidia wakati uliopita, kwa sababu kukumbuka mambo hayo mazuri kunaweza kutuchochea kumwomba Yehova msaada tunapokabili majaribu wakati ujao. Hata hivyo, hatupaswi kufikiri kwamba hatuhitaji mashauri ya Kimaandiko eti kwa sababu tumemtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka mingi. Hata tuwe tumemtumikia Yehova kwa miaka mingi kadiri gani, Yehova atatutia nidhamu tukikosea. Tunahitaji kukubali nidhamu kwa upole ili itufaidi. Jambo muhimu kuliko yote ni kwamba Baba yetu wa mbinguni atakuwa pamoja nasi maadamu tunathibitisha wazi kwamba tuko pamoja naye. Macho ya Yehova yanazunguka duniani pote yakiwatafuta wale wanaotenda kwa uaminifu kumwelekea. Anawathawabisha watu hao kwa kutumia nguvu zake kuwasaidia. Yehova alitumia nguvu zake kumsaidia Asa, naye anaweza kufanya hivyo kwa ajili yetu.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Yehova anawathawabisha watu waaminifu wanaopigana vita vya kiroho

[Blabu katika ukurasa wa 10]

Tunahitaji uhodari ili kufanya mambo yaliyo sawa machoni pa Yehova