Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Kuna Sawabu kwa Ajili ya Kazi Yenu’

‘Kuna Sawabu kwa Ajili ya Kazi Yenu’

‘Kuna Sawabu kwa Ajili ya Kazi Yenu’

MUFALME ASA na jeshi lake wanashuka mbio katika bonde ndefu. Wanatokea sehemu za milimani za Yuda na wanaelekea kwenye inchi isiyo na milima iliyo karibu na bahari. Wanapofika mahali ambapo bonde linapanuka zaidi, Asa anatua kidogo na kuvuta pumuzi. Kwenye upande mwengine kuna kambi kubwa ya maadui! Maadui hao ni Waethiopia ambao wanahesabika kuwa milioni moja. Lakini, hesabu ya wanajeshi wa Asa ni nusu zaidi kidogo ikilinganishwa na ile ya Waethiopia.

Kwa kuwa vita inakaribia, ni nini kinachomuhangaisha Asa sana? Je, ni maagizo ya vita anayopaswa kutolea majenerali wake? Je, ni kuwatia moyo maaskari wake? Ao je, ni kuandikia familia yake barua? Hapana! Katika hali hii ngumu, Asa anasali.

Kwanza tuone Asa alikuwa mutu wa aina gani, kisha tutachunguza sala yake na kuona mambo yaliyotokea wakati huo wa vita. Kwa nini alitenda hivyo? Je, alikuwa na sababu za kuamini kama Mungu atamusaidia? Historia ya Asa inatufundisha nini kuhusu namna Yehova anavyobariki utendaji wa watumishi Wake?

MAMBO ALIYOFANYA

Katika miaka 20 iliyofuata kugawanywa kwa Israeli kuwa falme mbili, Yuda ilikuwa imeharibika sana kwa sababu ya matendo ya kipagani. Asa alipokuwa mufalme katika mwaka wa 977 mbele ya Kristo, watu waliabudu miungu ya uzazi hata kwenye makao ya mufalme. Lakini, habari iliyoongozwa na roho ya Mungu kuhusu utawala wa Asa inasema kama ‘alifanya yaliyokuwa mema na sawa machoni pa Yehova Mungu wake.’ Asa ‘aliondoa mazabahu za kigeni na mahali pa juu, akazivunja nguzo takatifu.’ (2 Nya. 14:2, 3) Asa aliondoa pia katika ufalme wa Yuda “wanaume makahaba wa hekaluni,” waliokuwa wakifanya ngono chafu na kuamini kama matendo yao yanakubaliwa na dini. Asa hakuishia pale. Pia, aliwatia watu moyo ‘wamutafute Yehova Mungu wa mababu zao’ na kushika “sheria na amri” ya Mungu.​—1 Fal. 15:12, 13; 2 Nya. 14:4.

Bidii ya Asa kwa ajili ya ibada ya kweli ilikuwa na matokeo mazuri, Yehova alifanya amani iwe katika ufalme wake kwa miaka mingi. Kwa hiyo, mufalme huyo angeweza kusema hivi: ‘Tumemutafuta Yehova Mungu wetu. Tumemutafuta, naye anatupa pumuziko kuzunguka pande zote.’ Watu walitumia nafasi hii ili kujenga kuta zenye nguvu za ufalme wa Yuda. Biblia inasema hivi: “Nao wakajenga na kufanikiwa.”​—2 Nya. 14:1, 6, 7.

KWENYE UWANJA WA VITA

Habari inayoonyesha kama Asa alisali alipopambana na jeshi kubwa sana haiwezi kutushangaza. Asa alijua kama Mungu anabariki matendo ya imani. Katika sala yake, mufalme alimuomba Yehova amusaidie. Asa alijua kama ikiwa angemutegemea Mungu na kupata musaada wake, hesabu ao nguvu ya maadui haiwezi kuogopesha. Jina la Yehova lingelaumiwa ikiwa Asa angeshindwa, kwa hiyo Asa alisali kwa ajili ya jina hilo. Mufalme alisali hivi: “Utusaidie, Ee Yehova Mungu wetu, kwa maana sisi tunakuegemea wewe, nasi kwa jina lako tumekuja kupigana na umati huu. Ee Yehova, wewe ni Mungu wetu. Usiache mwanadamu anayeweza kufa apate nguvu juu yako.” (2 Nya. 14:11) Kwa maneno mengine, mufalme huyo alikuwa akisema hivi: ‘Waethiopia wanapigana na wewe, Yehova. Usiruhusu jina lako lizarauliwe kwa kuwaacha wanadamu wazaifu washinde wale wanaoitwa kwa jina lako.’ Kwa hiyo, “Yehova akawashinda Waethiopia mbele ya Asa na mbele ya Yuda, na Waethiopia wakakimbia.”​—2 Nya. 14:12.

Leo, watu wa Yehova wanazungukwa na maadui wenye nguvu. Hatutapigana nao kwa kutumia silaha halisi kwenye uwanja wa vita. Hata hivyo, tunaweza kuwa hakika kama Yehova atawapatia ushindi watumishi wake wote waaminifu wanaopigana vita ya kiroho katika jina lake. Vita yetu inaweza kutia ndani kujikaza kupinga roho ambayo imeenea sana ya kupuuza kanuni za Mungu, kupambana na uzaifu wetu wenyewe ao kulinda familia yetu na mambo yanayoweza kuharibu hali yake ya kiroho. Hata ikiwa tuko katika magumu ya aina gani, sala ya Asa inaweza kututia moyo. Ushindi wake ulitoka kwa Yehova. Hilo lilionyesha kama wote wanaomutegemea Mungu wanaweza kupata musaada wake. Hakuna mwanadamu anayeweza kumushinda Yehova.

ANATIWA MOYO NA KUONYWA

Aliporudi kutoka kwenye vita, Asa alikutana na nabii Azaria. Nabii huyo alimutia moyo na kumuonya hivi: ‘Munisikilize mimi, Ee Asa na Yuda wote na Benyamini! Yehova yuko pamoja nanyi ikiwa ninyi muko pamoja naye; nanyi mukimutafuta, atawaruhusu mumupate, lakini mukimuacha yeye atawaacha ninyi. Iweni hodari na musiache mikono yenu ilegee, kwa sababu kuna sawabu kwa ajili ya kazi yenu.’​—2 Nya. 15:1, 2, 7.

Maneno hayo yanaweza kutia nguvu imani yetu. Yanaonyesha kama Yehova ataendelea kuwa pamoja nasi ikiwa tunamutumikia kwa uaminifu. Tunapomuomba musaada, tunaweza kuwa hakika kama anatusikiliza. Azaria aliwaambia hivi: “Iweni hodari.” Ili kufanya yaliyo sawa, tunapaswa kuwa hodari ao hatupaswe kuwaogopa watu kwa sababu tunajua kama Yehova atatusaidia.

Kambo mwanamuke wa Asa, aliyeitwa Maaka, alikuwa ametengeneza ‘sanamu yenye kutisha kwa ajili ya muti mutakatifu,’ ndiyo maana haikuwa rahisi kwa Asa kumuondoa katika cheo chake cha “malkia” wa kifalme. Lakini, alishinda jaribu hilo na alichoma sanamu ya kambo yake. (1 Fal. 15:13) Asa alibarikiwa kwa sababu ya uhodari wake. Sisi pia tunapaswa kushikamana na Yehova na sheria zake za uadilifu hata kama watu wa familia yetu ni waaminifu kwa Mungu ao hapana. Tukifanya hivyo, Yehova atatubariki kwa sababu ya mwenendo wetu mwaminifu.

Asa alibarikiwa sana. Kwa mufano, alikuwa na pendeleo la kuona Waisraeli wengi waliokuwa wakitoka ufalme uliojaa uasi-imani wa kaskazini na kuja Yuda ili kumuabudu Yehova kwa sababu waliona kama Mungu iko pamoja na Asa. Kwa sababu walifurahia ibada safi, hawakusita kuacha nyumba zao ili kuja kuishi kati ya watumishi wa Yehova. Kisha Asa na wakaaji wote wa Yuda walifanya kwa furaha ‘agano ili kumutafuta Yehova kwa moyo wao wote na kwa nafsi yao yote.’ Matokeo yalikuwa nini? Mungu ‘aliwaruhusu wamupate; na Yehova akaendelea kuwapa pumuziko kuzunguka pande zote.’ (2 Nya. 15:9-15) Tunafurahi sana kuona wale wanaopenda haki wanapokubali ibada safi!

Hata hivyo, nabii Azaria alimuonya Asa hivi: “Ikiwa unamuacha [Yehova], yeye pia atakuacha.” Tusiruhusu hata kidogo hilo litufikie kwa sababu matokeo yanaweza kuwa mabaya sana! (2 Pet. 2:20-22) Maandiko hayaonyeshe kwa nini Yehova alituma nabii wake kumuonya Asa hivyo, lakini mufalme hakutii onyo hilo.

“UMETENDA KWA UPUMBAVU”

Katika mwaka wa 36 wa utawala wa Asa, Mufalme Baasha wa Israeli alishambulia Yuda. Labda alifanya hivyo ili kuwazuia watu wake wasiwe waaminifu kwa Asa na kwa ibada safi, kwa hiyo Baasha alianza kuimarisha muji wa Rama uliokuwa kwenye mupaka wa kaskazini, kilometre munane mbali na Yerusalemu. Kuliko kutafuta musaada wa Mungu kama alivyofanya aliposhambuliwa na Waethiopia, Asa alitafuta musaada wa wanadamu. Alimutumia zawadi mufalme wa Siria na kumuomba ashambulie ufalme wa kaskazini wa Israeli. Aliposhambuliwa na Waasiria, Baasha alikimbia muji wa Rama.​—2 Nya. 16:1-5.

Yehova hakupendezwa na jambo ambalo Asa alifanya na alimutumia nabii Hanani. Kukumbuka namna Yehova alivyotendea Waethiopia, kungemusaidia Asa kujua kama macho ya Yehova ‘yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mukamilifu kumuelekea yeye.’ Labda Asa alipata mashauri mabaya ao aliwaza kama Baasha na majeshi yake hawakuwa na nguvu na kama atawashinda kwa nguvu zake mwenyewe. Lakini, hata sababu iwe gani, jambo tunalojua ni kwamba Asa alitafuta musaada wa wanadamu kuliko kumutegemea Yehova. Hanani alimuambia hivi: “Umetenda kwa upumbavu kwa habari hii, kwa maana tangu sasa na kuendelea kutakuwa na vita juu yako.”​—2 Nya. 16:7-9.

Asa hakufurahia maneno ya nabii. Kwa hasira, Asa alimutupa nabii Hanani katika nyumba ya mikatale ao kifungo. (2 Nya. 16:10) Labda Asa alifikiri hivi, ‘Je, ninahitaji kukaripiwa kisha kuwa mwaminifu kwa miaka mingi?’ Je, alikuwa amepoteza kidogo uwezo wake wa kufikiri kwa sababu ya uzee? Biblia haieleze lolote.

Katika mwaka wa 39 wa utawala wake, Asa alipata ugonjwa wa miguu. Maandiko yanaonyesha kama ‘hata katika ugonjwa wake hakumutafuta Yehova bali waponyaji.’ Wakati huo, Asa alionekana kama haangaikie tena afya yake ya kiroho. Inaonekana kama Asa alikufa katika hali hiyo, katika mwaka wa 41 wa utawala wake.​—2 Nya. 16:12-14.

Ijapokuwa hivyo, sifa nzuri za Asa kutia ndani bidii yake kwa ajili ya ibada safi zilikuwa nyingi kuliko makosa yake. Hakuacha hata kidogo kumutumikia Yehova. (1 Fal. 15:14) Basi tunajifunza nini kutokana na historia ya maisha yake? Tunajifunza kama hatupaswe kusahau namna Yehova alivyotusaidia wakati uliopita, kwa maana hilo linaweza kutuchochea kusali kwa Yehova ili atusaidie tena tunapopambana na majaribu mengine. Lakini, tusifikiri kama hatuna lazima ya mashauri ya Biblia eti kwa sababu tumemutumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka mingi. Hata kama tumemutumikia Yehova kwa miaka ngapi, atatukaripia ikiwa tunakosea. Tunapaswa kukubali karipio hilo kwa upole ili tufaidike nalo. Zaidi ya yote, Baba yetu wa mbinguni ataendelea kuwa pamoja nasi ikiwa hatumuache. Macho ya Yehova yanatafuta katika dunia yote wale wanaomutumikia kwa uaminifu. Anawabariki kwa kutumia nguvu yake ili kuwasaidia. Yehova alimusaidia Asa na anaweza pia kutusaidia.

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 9]

Yehova anawabariki watumishi wake waaminifu wanaopigana vita ya kiroho

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 10]

Inafaa kuwa hodari ili kufanya yaliyo sawa machoni pa Yehova