Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Ulimwengu Huu Utakavyofikia Mwisho Wake

Jinsi Ulimwengu Huu Utakavyofikia Mwisho Wake

“Hamko gizani, hivi kwamba siku hiyo iwafikie ninyi kama vile ambavyo ingewafikia wezi.”​—⁠1 THE. 5:4.

1. Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kukesha na kuvumilia majaribu?

MATUKIO yenye kushtua yataitikisa dunia hivi karibuni. Kutimizwa kwa unabii mbalimbali wa Biblia kunathibitisha jambo hilo hakika, kwa hiyo tunahitaji kuendelea kukesha. Ni nini kitakachotusaidia kufanya hivyo? Mtume Paulo anatuhimiza ‘tuendelee kukaza macho yetu juu ya vitu visivyoonekana.’ Naam, tunahitaji kufikiria thawabu yetu ya uzima wa milele, iwe ni mbinguni au duniani. Kama muktadha unavyoonyesha, Paulo aliandika maneno hayo ili kuwatia moyo waamini wenzake wakazie fikira furaha watakayopata kwa sababu ya maisha yao ya uaminifu. Kufanya hivyo kungewasaidia pia kuvumilia majaribu na mateso.​—2 Kor. 4:​8, 9, 16-18; 5:7.

2. (a) Ni lazima tufanye nini ili tuendelee kuwa na tumaini thabiti? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii na ile inayofuata?

2 Himizo la Paulo lina kanuni hii muhimu: Ili tuendelee kuwa na tumaini thabiti, ni lazima tukazie fikira mambo yatakayotukia hivi karibuni. Tunahitaji kukazia fikira matukio muhimu ambayo hayaonekani sasa. (Ebr. 11:1; 12:​1, 2) Kwa hiyo, acheni tuchunguze matukio kumi ya wakati ujao ambayo yanahusiana sana na tumaini letu la uzima wa milele. *

NI MAMBO GANI YATAKAYOTUKIA KABLA TU YA ULE MWISHO?

3. (a) Ni jambo gani litakalotukia wakati ujao ambalo linatajwa katika 1 Wathesalonike 5:​2, 3? (b) Viongozi wa kisiasa watafanya nini, na ni nani watakaojiunga nao?

3 Paulo aliandika kuhusu moja kati ya matukio hayo ya wakati ujao katika barua yake kwa Wathesalonike. (Soma 1 Wathesalonike 5:​2, 3.) Anavuta uangalifu juu ya “siku ya Yehova.” Katika andiko hilo, maneno “siku ya Yehova” yanarejelea kipindi kitakachoanza wakati dini ya uwongo itakapoharibiwa na kufikia kilele chake katika vita vya Har–​Magedoni. Hata hivyo, kabla tu ya siku ya Yehova kuanza, viongozi wa ulimwengu watakuwa wakisema “Amani na usalama!” Huenda hilo likarejelea tukio moja au mfuatano wa matukio. Huenda mataifa yakafikiri kwamba yako karibu kusuluhisha baadhi ya matatizo yao makubwa. Namna gani kuhusu viongozi wa kidini? Wao ni sehemu ya ulimwengu, kwa hiyo inawezekana kwamba watajiunga na viongozi wa kisiasa. (Ufu. 17:​1, 2) Kwa kufanya hivyo, viongozi hao wa kidini watakuwa wanawaiga manabii waongo wa kale wa Yuda. Yehova alisema hivi kuhusu manabii hao: ‘Wanasema, “Kuna amani! Kuna amani!” wakati hakuna amani.’​—Yer. 6:14; 23:​16, 17.

4. Tofauti na watu wengi, sisi tunatambua nini?

4 Haidhuru ni nani watakaoshiriki kusema “Amani na usalama!” tukio hilo litaonyesha kwamba siku ya Yehova iko karibu kuanza. Ndiyo sababu Paulo alisema hivi: “Akina ndugu, hamko gizani, hivi kwamba siku hiyo iwafikie ninyi kama vile ambavyo ingewafikia wezi, kwa maana ninyi nyote ni wana wa nuru.” (1 The. 5:​4, 5) Tofauti na watu wengi, sisi tunatambua maana ya Kimaandiko ya matukio ya sasa. Unabii huu kuhusu tangazo la “Amani na usalama!” utatimia jinsi gani hasa? Ni lazima tungoje ili tuone jinsi itakavyokuwa. Kwa hiyo, acheni tuazimie ‘kukaa macho na kutunza akili zetu.’​—1 The. 5:6; Sef. 3:8.

“MALKIA” AMBAYE HAJUI KWAMBA ATAHARIBIWA

5. (a) “Dhiki kuu” itaanzaje? (b) Ni “malkia” yupi ambaye hajui kwamba ataharibiwa?

5 Ni tukio gani lisiloonekana litakalofuata baadaye? Paulo alisema hivi: “Wakati watakapokuwa wakisema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao mara moja.” Sehemu ya kwanza ya ‘uharibifu huo wa ghafula’ ni shambulio dhidi ya “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, inayojulikana pia kuwa “yule kahaba.” (Ufu. 17:​5, 6, 15) Shambulio hilo dhidi ya aina zote za dini ya uwongo, kutia ndani dini zinazodai kuwa za Kikristo, litakuwa mwanzo wa “dhiki kuu.” (Mt. 24:21; 2 The. 2:8) Tukio hilo litawashtua watu wengi. Kwa nini? Kwa sababu kufikia wakati huo, kahaba huyo atajiona kwa uhakika kuwa “malkia” ambaye ‘hataona maombolezo kamwe.’ Lakini atagundua kwa ghafla kwamba hakujua kuwa ataharibiwa. Hata hivyo, ataharibiwa haraka sana kana kwamba ni “katika siku moja.”​—⁠Ufu. 18:​7, 8.

6. Ni nani atakayeiharibu dini ya uwongo?

6 Neno la Mungu linamtambulisha mshambuliaji wa kahaba huyo kuwa “mnyama-mwitu” mwenye “pembe kumi.” Uchunguzi wa kitabu cha Ufunuo unaonyesha kwamba huyo mnyama-mwitu anafananisha Umoja wa Mataifa (UM). “Zile pembe kumi” zinafananisha serikali zote za kisiasa zilizopo sasa zinazomuunga mkono ‘mnyama-mwitu huyo mwenye rangi nyekundu.’ * (Ufu. 17:​3, 5, 11, 12) Shambulio hilo litakuwa kubwa kadiri gani? Mataifa ya UM yatapora utajiri wa kahaba huyo, yatafunua jinsi alivyo mwovu kikweli, yatamrarua, na “kumteketeza kabisa kwa moto.” Uharibifu wake utakuwa wa milele.​—Soma Ufunuo 17:16.

7. Ni nini kitakachosababisha shambulio la “mnyama-mwitu”?

7 Unabii wa Biblia unaonyesha pia kile kitakachosababisha shambulio hilo. Kwa njia fulani, Yehova atatia wazo hilo ndani ya mioyo ya watawala wa kisiasa “ili kutekeleza wazo lake,” yaani, kumharibu kahaba huyo. (Ufu. 17:17) Dini inachochea vita na kuendelea kusababisha mvurugo ulimwenguni; kwa hiyo, huenda mataifa yakahisi kwamba yatanufaika yakimharibu kahaba huyo. Kwa kweli, watawala watakaposhambulia, watafikiri kwamba wanatimiza “wazo lao moja.” Hata hivyo, ukweli ni kwamba Mungu atawatumia kama vyombo vya kuharibu kabisa dini yote ya uwongo. Hivyo, katika hali isiyotarajiwa, sehemu moja ya mfumo wa Shetani itaishambulia ile sehemu nyingine, na Shetani hatakuwa na uwezo wa kuzuia jambo hilo.​—Mt. 12:​25, 26.

SHAMBULIO DHIDI YA WATU WA MUNGU

8. Shambulio la “Gogu wa nchi ya Magogu” ni nini?

8 Baada ya dini ya uwongo kuharibiwa, bado watumishi wa Mungu wataonekana kuwa ‘wanakaa kwa usalama’ na “bila ukuta.” (Eze. 38:​11, 14) Ni nini kitakachotukia kwa kikundi hicho cha watu wanaoonekana kuwa bila ulinzi na wanaoendelea kumwabudu Yehova? Inaelekea kwamba watakuwa shabaha ya shambulio la “vikundi vingi vya watu.” Neno la Mungu linasema kwamba tukio hilo litakuwa shambulio la “Gogu wa nchi ya Magogu.” (Soma Ezekieli 38:​2, 15, 16.) Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu shambulio hilo?

9. (a) Hangaiko kuu la Mkristo ni nini? (b) Ni hatua zipi tunazopaswa kuchukua sasa ili kuimarisha imani yetu?

9 Kujua kimbele kuhusu shambulio hilo dhidi ya watu wa Mungu hakutufanyi tuwe na wasiwasi kupita kiasi. Badala yake, hangaiko letu kuu si wokovu wetu, bali ni kutakaswa kwa jina la Yehova na kutetewa kwa enzi yake kuu. Kwa kweli, Yehova alitangaza hivi zaidi ya mara 60: “Mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Eze. 6:7) Hivyo, tunatazamia kwa hamu sana kutimizwa kwa sehemu hiyo muhimu ya unabii wa Ezekieli, huku tukiwa na uhakika wa kwamba “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.” (2 Pet. 2:9) Kwa sasa, tunahitaji kutumia kila fursa kuimarisha imani yetu ili tuendelee kushika utimilifu wetu kwa Yehova licha ya matatizo tutakayokabili. Tunapaswa kufanya nini? Tunapaswa kusali, kujifunza na kutafakari Neno la Mungu, na kuwahubiria wengine ujumbe wa Ufalme. Kwa kufanya hivyo, tunaendelea kuwa na tumaini la uzima wa milele ambalo ni thabiti kama “nanga.”​—⁠Ebr. 6:19; Zab. 25:21.

MATAIFA YATALAZIMIKA KUMTAMBUA YEHOVA

10, 11. Ni nini itakayokuwa ishara ya kuanza kwa ­Har–​Magedoni, na ni nini kitakachotukia wakati huo?

10 Ni tukio gani lenye kushtua litakalosababishwa na shambulio dhidi ya watumishi wa Yehova? Yehova, kupitia Yesu na majeshi ya kimbingu, ataingilia kati kwa ajili ya watu Wake. (Ufu. 19:​11-16) Hatua hiyo ya kuingilia kati ndiyo itakayokuwa “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” yaani, ­Har–​Magedoni.​—Ufu. 16:​14, 16.

11 Kuhusu vita hivyo, Yehova anatangaza hivi kupitia Ezekieli: “‘Nitaita upanga juu [ya Gogu] kotekote katika eneo langu lote lenye milima,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. ‘Upanga wa kila mmoja utakuwa juu ya ndugu yake.’ ” Wale walio upande wa Shetani wataingiwa na hofu kubwa na kuanza kuuana wenyewe kwa wenyewe, yaani, mpiganaji dhidi ya mpiganaji mwenzake. Hata hivyo, Shetani pia atashambuliwa. Yehova anasema hivi: “Nitanyesha . . . moto na kiberiti juu [ya Gogu] na juu ya vikosi vyake na juu ya vikundi vingi vya watu vitakavyokuwa pamoja naye.” (Eze. 38:​21, 22) Kutakuwa na matokeo gani Mungu atakapochukua hatua hiyo?

12. Mataifa yatalazimika kutambua nini?

12 Mataifa yatalazimika kutambua kwamba Yehova ndiye aliyetoa amri ili yapondwe na kushindwa. Kisha, kama jeshi la kale la Misri lililowafuatilia Waisraeli kwenye Bahari Nyekundu lilivyolia, huenda majeshi ya Shetani yakalia hivi kwa kukata tamaa: “Hakika Yehova anawapigania”! (Kut. 14:25) Naam, mataifa yatalazimika kumtambua Yehova. (Soma Ezekieli 38:23.) Tuko karibu kadiri gani kuona mwanzo wa mfuatano wa matukio hayo?

HAKUNA SERIKALI NYINGINE KUU YA ULIMWENGU ITAKAYOTOKEA

13. Tunajua nini kuhusu sehemu ya tano ya sanamu ambayo Danieli anafafanua?

13 Unabii mmoja katika kitabu cha Danieli unatuwezesha kujua tuko wapi katika mkondo wa wakati. Danieli anafafanua sanamu ya umbo la kibinadamu ambayo inafanyizwa kutokana na madini mbalimbali. (Dan. 2:​28, 31-33) Sanamu hiyo inafananisha mfuatano wa serikali kuu za ulimwengu ambazo zilikuwa na uvutano mkubwa juu ya watu wa Mungu, zamani na sasa. Serikali hizo ni Babiloni, Umedi na Uajemi, Ugiriki, Roma, na serikali kuu ya mwisho ambayo inatawala sasa. Uchunguzi wa unabii wa Danieli unaonyesha kwamba serikali hii kuu ya mwisho ya ulimwengu inafananishwa na miguu na vidole vya sanamu hiyo. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Uingereza na Marekani zilianzisha ushirikiano wa pekee. Naam, sehemu ya tano ya sanamu ya Danieli ni Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Miguu ndiyo sehemu ya mwisho ya sanamu hiyo, na hilo linaonyesha kwamba hakuna serikali nyingine kuu ya kibinadamu itakayotokea baada ya serikali hiyo. Miguu na vidole vimefanyizwa kwa chuma na udongo, kuonyesha kwamba Muungano wa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani umedhoofika.

14. Ni serikali gani kuu ya ulimwengu itakayokuwa ikitawala vita vya ­Har–​Magedoni vitakapoanza?

14 Unabii huohuo unaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu, unaofananishwa na jiwe kubwa, ulikatwa kutoka kwenye mlima wa enzi kuu ya Yehova katika mwaka wa 1914. Jiwe hilo sasa linasonga kwa kasi sana ili kugonga shabaha yake, yaani, miguu ya sanamu hiyo. Katika vita vya ­Har–​Magedoni, miguu na sehemu nyingine za sanamu hiyo zitapondwa kabisa. (Soma Danieli 2:​44, 45.) Kwa hiyo, Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani bado itakuwa serikali kuu wakati vita vya ­Har–​Magedoni vitakapoanza. Itasisimua kama nini kuona unabii huo ukitimizwa kikamili! * Hata hivyo, Yehova atamchukulia Shetani hatua gani?

HATUA AMBAYO MUNGU ATAMCHUKULIA ADUI YAKE MKUU

15. Baada ya ­Har–​Magedoni, itakuwaje kwa Shetani na roho wake waovu?

15 Kwanza, Shetani atashuhudia tangu mwanzo hadi mwisho tengenezo lake lote duniani likiangamizwa. Kisha, Shetani mwenyewe ataelekezewa fikira. Mtume Yohana anaripoti kinachofuata. (Soma Ufunuo 20:​1-3.) Yesu Kristo, ambaye ni “malaika . . . mwenye ufunguo wa abiso,” atamshika Shetani na roho wake waovu na kuwatupa ndani ya abiso, kisha atawafungia humo kwa miaka elfu moja. (Luka 8:​30, 31; 1 Yoh. 3:8) Tendo hilo ni hatua ya kwanza ya kukiponda kichwa cha yule nyoka. *​—⁠Mwa. 3:15.

16. Itamaanisha nini kwa Shetani kuwa ndani ya “abiso”?

16 “Abiso” ambamo Shetani na roho wake waovu watatupwa ni nini? Neno la Kigiriki aʹbys·sos linalotumiwa na Yohana linamaanisha “-enye kina sana au kina kisicho cha kawaida.” Linatafsiriwa pia kuwa “shimo lisilo na mwisho,” “lisilo na mipaka,” na “lisilo na kikomo.” Kwa hiyo, ni mahali ambapo hapawezi kufikiwa na mtu yeyote yule isipokuwa Yehova tu na malaika wake aliyewekwa rasmi “mwenye ufunguo wa abiso.” Humo, Shetani atakuwa katika hali ya kutotenda kama ya mfu ili “asipotoshe mataifa tena.” Kwa kweli, ‘simba huyo anayenguruma’ atanyamazishwa!​—⁠1 Pet. 5:8.

MATUKIO YANAYOONGOZA KWENYE KIPINDI CHA AMANI

17, 18. (a) Kufikia hapa, tumezungumzia matukio gani ambayo hayajaonekana? (b) Baada ya matukio hayo, tutafurahia kipindi gani cha wakati?

17 Matukio muhimu yatakayoitikisa dunia yako mbele yetu. Tunatazamia kuona jinsi tangazo la “Amani na usalama! ” litakavyotolewa. Kisha, tutashuhudia uharibifu wa Babiloni Mkubwa, shambulio la Gogu wa Magogu, vita vya ­Har–​Magedoni, na kutupwa kwa Shetani na roho wake waovu ndani ya abiso. Baada ya matukio hayo, na uovu wote utakapokuwa umetoweka, tutaingia katika kipindi kipya cha maisha, yaani, Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo, wakati tutakapofurahia “wingi wa amani.”​—⁠Zab. 37:​10, 11.

18 Zaidi ya matukio hayo matano ambayo tumechunguza kufikia hapa, bado kuna ‘vitu vingine visivyoonekana’ ambavyo tunapaswa ‘kuendelea kuvikazia macho.’ Matukio hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.

^ fu. 2 Matukio hayo kumi yanazungumziwa katika makala hii na ile inayofuata.

^ fu. 6 Tazama kitabu Ufunuo​—⁠Upeo Wao Mtukufu U Karibu! ukurasa wa 251-258.

^ fu. 14 Maneno “kuzikomesha falme hizi zote” yaliyo katika Danieli 2:44 yanarejelea falme, au serikali kuu za ulimwengu, zinazofananishwa na sehemu mbalimbali za sanamu hiyo. Hata hivyo, unabii mwingine wa Biblia kama huo unaonyesha kwamba “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” watajipanga dhidi ya Yehova katika “siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” (Ufu. 16:14; 19:​19-21) Kwa hiyo, si falme zinazofananishwa na sanamu hiyo tu zitakazoharibiwa kwenye ­Har–​Magedoni bali pia falme nyingine zote za ulimwengu huu.

^ fu. 15 Kichwa cha yule nyoka kitapondwa kwa mara ya mwisho baada ya ile miaka miaka elfu moja wakati Shetani na roho wake waovu wanapotupwa ndani ya “lile ziwa la moto na kiberiti.”​—⁠Ufu. 20:​7-10; Mt. 25:41.