Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Amani Kwa Muda Wa Miaka Elfu Moja Na Kuendelea!

Amani Kwa Muda Wa Miaka Elfu Moja Na Kuendelea!

“Ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.”​—⁠1 KOR. 15:28.

1. Ni tarajio gani lenye kusisimua ambalo “umati mkubwa” unangojea?

JE, UNAWEZA kuwazia mambo yote mazuri ambayo serikali yenye nguvu chini ya uongozi wa mtawala mwenye haki na huruma inaweza kuwafanyia raia wake kwa muda wa miaka elfu moja? “Umati mkubwa” usio na hesabu, yaani, waokokaji wa “ile dhiki kuu,” wanangojea matukio mazuri yatakayokomesha kabisa mfumo huu mwovu wa mambo wa sasa.​—Ufu. 7:​9, 14.

2. Wanadamu wamepatwa na nini kwa muda wa miaka 6,000 iliyopita?

2 Kwa muda wa miaka 6,000 iliyopita, wanadamu wamejaribu kujitegemea na kujitawala wenyewe, na jambo hilo limewaletea maumivu na mateso makali. Biblia ilisema hivi zamani: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Mhu. 8:9) Tunaona nini leo? Mbali na vita na machafuko ya kijamii, kuna matatizo makubwa ya umaskini, magonjwa, uharibifu wa mazingira, mabadiliko ya hali ya hewa, na kadhalika. Maofisa wa serikali wameonya kwamba tusipobadili mtazamo wetu wa kutojali, matokeo yatakuwa mabaya sana.

3. Utawala wa ile Miaka Elfu Moja utaleta nini?

Chini ya uongozi wa Mfalme wa Kimasihi Yesu Kristo na wale 144,000 ambao watatawala pamoja naye, Ufalme wa Mungu utaondoa hatua kwa hatua madhara yote ambayo wanadamu wamepata na kurekebisha makao yao, Dunia. Wakati wa Utawala wa ile Miaka Elfu Moja, ahadi hii ya Yehova Mungu yenye kuchangamsha moyo itatimia: “Mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya; na mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.” (Isa. 65:17) Hata hivyo, ni matukio gani mazuri ajabu yasiyoonekana tunayongojea? Kwa msaada wa Neno la Mungu la kinabii, acheni tupate picha ya mambo hayo mazuri ajabu ambayo ‘hayajaonekana.’​—⁠2 Kor. 4:18.

‘WATAJENGA NYUMBA NA KUPANDA MASHAMBA YA MIZABIBU’

4. Watu wengi leo wanaishi katika nyumba za aina gani?

4 Ni nani hangependa kuwa na nyumba yake mwenyewe, ambamo yeye na familia yake wangehisi wakiwa salama salimini? Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo, ni vigumu sana kupata makao mazuri. Watu wanasongamana katika majiji yaliyojaa watu. Wengi wanaishi katika makao ya muda ya watu maskini na mitaa ya mabanda. Ni ndoto tu kwa watu hao kuwa na nyumba yao wenyewe.

5, 6. (a) Maandiko ya Isaya 65:21 na Mika 4:4 yatatimiaje? (b) Tunawezaje kupata baraka hizo?

Chini ya utawala wa Ufalme, tamaa ya kila mkaaji ya kuwa na nyumba yake mwenyewe itatoshelezwa, kwa kuwa ilitabiriwa hivi kupitia Isaya: “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.” (Isa. 65:21) Hata hivyo, mbali na mtu kuwa na nyumba yake mwenyewe kuna matarajio mengine. Baadhi ya watu leo wanaishi katika nyumba zao wenyewe, wachache hata wana nyumba za kifahari. Lakini sikuzote wana wasiwasi kwamba wataipoteza nyumba yao kwa sababu ya kuporomoka kwa thamani ya pesa au wanaogopa kwamba wataibiwa. Kila kitu kitakuwa tofauti kama nini chini ya utawala wa Ufalme! Nabii Mika aliandika hivi: “Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha.”​—⁠Mika 4:4.

6 Tukiwa na tarajio hilo zuri ajabu akilini, tunapaswa kufanya nini? Bila shaka, sisi sote tunahitaji nyumba nzuri. Hata hivyo, badala ya kujitahidi kupata nyumba tunayotamani sasa, labda kwa kuchukua mikopo mikubwa, je, halingekuwa jambo la hekima kwetu kukazia fikira ahadi ya Yehova? Kumbuka yale ambayo Yesu alisema kujihusu: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Luka 9:58) Yesu alikuwa na uwezo na nguvu za kujenga au kupata nyumba nzuri sana kuliko mtu mwingine yeyote. Kwa nini hakufanya hivyo? Ni wazi kwamba Yesu alitaka kuepuka jambo lolote ambalo lingemkengeusha fikira na kumsonga na hivyo kumzuia asitangulize Ufalme. Je, tunaweza kufuata mfano wake na kuendelea kuwa na jicho rahisi, yaani, kutojiruhusu tusongwe na upendo wa vitu vya kimwili na mahangaiko?​—⁠Mt. 6:​33, 34.

“MBWA-MWITU NA MWANA-KONDOO WATALISHA KAMA KITU KIMOJA”

7. Mwanzoni Yehova alikusudia kuwe na uhusiano gani kati ya wanadamu na wanyama?

7 Alipokuwa akiumba, Yehova aliwaumba wanadamu mwisho na walikuwa ndio uumbaji bora zaidi kati ya kazi zake za kidunia. Yehova alimwambia Stadi wake wa Kazi, Mwanawe mzaliwa wa kwanza, kusudi lake hususa: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu, nao watawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na wanyama wa kufugwa na dunia yote na kila mnyama anayetembea juu ya dunia.” (Mwa. 1:26) Kwa hiyo, Adamu na Hawa, na hatimaye wanadamu wote, waliamriwa watawale wanyama.

8. Kwa kawaida wanyama wanaonyesha tabia gani leo?

8 Je, kweli wanadamu wanaweza kuwatiisha wanyama wote na kuishi nao kwa amani? Watu wengi wana uhusiano wa karibu sana na wanyama wanaowapenda, kama vile mbwa na paka. Hata hivyo, namna gani kuhusu wanyama-mwitu? Ripoti moja inasema hivi: “Wanasayansi ambao wameishi kwa ukaribu pamoja na wanyama-mwitu na ambao wamejifunza kuwahusu, wamegundua kwamba wanyama wote wana hisia.” Bila shaka, tunaona wanyama wakiogopa au kukasirika wanapotishwa, lakini je, wanaweza kuonyesha hisia nyororo? Ripoti hiyo inaendelea kusema hivi: “Wanyama hufunua sifa yao kuu zaidi, yaani, uwezo wao mkubwa wa kuonyesha upendo mchangamfu hasa wanapowalea watoto wao.”

9. Tunaweza kutazamia mabadiliko gani kuhusiana na wanyama?

9 Kwa hiyo, hatupaswi kushangaa tunaposoma katika Biblia kwamba kutakuwa na amani kati ya wanadamu na wanyama. (Soma Isaya 11:​6-9; 65:25.) Kwa nini? Kumbuka kwamba Noa na familia yake walipotoka ndani ya safina baada ya Gharika, Yehova aliwaambia hivi: “Kila kiumbe hai cha dunia na kila kiumbe kinachoruka cha mbinguni kitawahofu.” Kwa hiyo, wanyama walipaswa kuwahofu wanadamu ili kujilinda. (Mwa. 9:​2, 3) Je, Yehova hataweza kuondoa kwa kiasi fulani hofu na woga huo ili uhusiano kati ya wanadamu na wanyama uwe kama alivyokusudia mwanzoni? (Hos. 2:18) Wote watakaookoka na kuishi duniani watafurahia maisha kama nini!

“ATAFUTA KILA CHOZI”

10. Kwa nini mara nyingi wanadamu hutokwa na machozi?

10 Sulemani alipoona “matendo yote ya uonevu yanayofanywa chini ya jua,” aliomboleza hivi: “Tazama! machozi ya wale wanaokandamizwa, lakini hawakuwa na mtu wa kuwafariji.” (Mhu. 4:1) Leo mambo yako vivyo hivyo, au ni mabaya hata zaidi. Ni nani kati yetu hajawahi kutokwa na machozi kwa sababu fulani? Ni kweli kwamba nyakati nyingine machozi hayo yanaweza kuwa ya shangwe. Hata hivyo, kwa ujumla, tunatokwa na machozi kwa sababu mioyo yetu imejaa huzuni.

11. Ni simulizi gani la Biblia ambalo hasa linakugusa moyo?

11 Kumbuka masimulizi mengi yenye kugusa moyo na hisia tunayosoma katika Biblia. Sara alipokufa akiwa na umri wa miaka 127, ‘Abrahamu aliingia ndani kumwombolezea Sara na kumlilia.’ (Mwa. 23:​1, 2) Naomi alipowaaga mabinti-wakwe zake wawili wajane, “wakaanza kupaaza sauti zao na kulia,” na kisha “wakapaaza sauti zao na kulia tena.” (Rut. 1:​9, 14) Mfalme Hezekia alipokuwa mgonjwa na kujua kwamba hakika angekufa, alisali kwa Mungu na “akaanza kulia sana,” jambo lililomgusa moyo Yehova. (2 Fal. 20:​1-5) Na ni nani asiyeguswa moyo na simulizi kuhusu mtume Petro akimkana Yesu? Aliposikia jogoo akiwika, Petro “akaenda nje akalia kwa uchungu.”​—⁠Mt. 26:75.

12. Utawala wa Ufalme utawaleteaje wanadamu kitulizo cha kweli?

12 Kwa sababu ya matukio yenye kuhuzunisha yanayotupata, makubwa na madogo, wanadamu wanahitaji sana faraja na kitulizo. Hayo ndiyo mambo ambayo Utawala wa Miaka Elfu Moja utawaletea raia wake: “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufu. 21:4) Ni jambo zuri ajabu kujua kwamba maombolezo, kilio, na maumivu hayatakuwapo tena. Mungu anaahidi pia kuondoa kabisa adui mkuu wa wanadamu, yaani, kifo. Hilo litatukiaje?

‘WALE WOTE WALIOMO NDANI YA MAKABURI YA UKUMBUSHO WATATOKA’

13. Kifo kimewaathirije wanadamu tangu Adamu atende dhambi?

13 Tangu Adamu atende dhambi, kifo kimetawala kama mfalme juu ya wanadamu. Kifo kimekuwa adui asiyeshindwa, mwisho usioepukika wa wanadamu wenye dhambi, chanzo cha majonzi na huzuni isiyo na kifani. (Rom. 5:​12, 14) Kwa kweli, kwa sababu ya “kuogopa kifo,” mamilioni ya watu “wametiishwa chini ya utumwa katika maisha yao yote.”​—⁠Ebr. 2:15.

14. Ni nini kitakachotukia kifo kitakapoondolewa?

14 Biblia inataja kwamba wakati utakuja ambapo “adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.” (1 Kor. 15:26) Tunaweza kutaja vikundi viwili vitakavyofaidika na jambo hilo. Wale wa “umati mkubwa,” wanaoishi sasa wataweza kuokoka na kuingia katika ulimwengu mpya ulioahidiwa wakitarajia kupata uzima usio na mwisho. Na mabilioni ya watu ambao tayari wamekufa, wataweza kufufuliwa. Je, unaweza kuwazia shangwe na msisimuko utakaokuwapo wakati “umati mkubwa” utakapowakaribisha wale wanaofufuliwa? Kuchunguza kwa makini baadhi ya masimulizi ya Biblia kuhusu ufufuo kunaweza kutusaidia kuelewa jinsi hali itakavyokuwa wakati huo.​—⁠Soma Marko 5:​38-42; Luka 7:​11-17.

15. Inaelekea utatendaje ukimwona mpendwa wako akifufuliwa na kuishi tena?

15 Fikiria maneno “wakawa na shangwe kubwa” na “wakaanza kumtukuza Mungu.” Ikiwa ungekuwepo wakati huo, labda ungehisi vivyo hivyo. Kwa kweli, tutasisimuka sana kwa shangwe na furaha tutakapoona wapendwa wetu waliokufa wakifufuliwa na kuishi tena. Yesu alisema hivi: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yoh. 5:​28, 29) Hakuna yeyote kati yetu aliyewahi kuona jambo kama hilo likitendeka; bila shaka litakuwa mojawapo ya mambo makubwa zaidi kati ya “vitu visivyoonekana.”

MUNGU ATAKUWA “VITU VYOTE KWA KILA MTU”

16. (a) Kwa nini tunapaswa kuzungumzia kwa shauku baraka ambazo bado hatujaziona? (b) Paulo alisema nini ili kuwatia moyo Wakristo wa Korintho?

16 Naam, wakati ujao wenye utukufu unawangojea wale ambao ni waaminifu kwa Yehova katika nyakati hizi ngumu! Hata ingawa bado hatujaziona baraka hizo kubwa za wakati ujao, kuendelea kuzifikiria kutatusaidia kukazia akili mambo yaliyo muhimu kwelikweli na kuepuka kukengeushwa na mambo ya muda tu yanayovutia ya mfumo huu wa mambo. (Luka 21:34; 1 Tim. 6:​17-19) Wakati wa funzo na ibada ya familia, katika mazungumzo pamoja na waamini wenzetu, na katika mazungumzo pamoja na wanafunzi wa Biblia na wale wanaopendezwa, acheni tuzungumzie kwa shauku tumaini na tarajio letu zuri ajabu. Kufanya hivyo kutafanya mambo hayo yawe wazi katika akili na mioyo yetu. Mtume Paulo alifanya vivyo hivyo alipowatia moyo Wakristo wenzake. Maneno yake yaliwasaidia kupiga picha akilini mambo ambayo yangetukia mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo. Jaribu kuwazia maana kamili ya maneno ya Paulo katika 1 Wakorintho 15:​24, 25, 28.​—⁠Soma.

17, 18. (a) Ni katika njia gani Yehova alikuwa “vitu vyote kwa kila mtu” mwanzoni mwa historia ya wanadamu? (b) Yesu atafanya nini ili kurudisha umoja na upatano?

17 Hakuna maneno yanayoweza kueleza kwa njia bora zaidi jinsi maisha yatakavyokuwa mwishoni mwa ile miaka elfu moja kuliko haya: “Ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.” Hilo linamaanisha nini? Fikiria jinsi mambo yalivyokuwa katika Edeni wakati wanadamu wakamilifu, Adamu na Hawa, walipokuwa sehemu ya familia ya Yehova ya ulimwenguni pote yenye amani na upatano. Yehova, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, alitawala moja kwa moja juu ya uumbaji wake wote, malaika na wanadamu. Waliweza kuwasiliana naye kibinafsi na kumwabudu, naye aliwabariki. Mungu alikuwa “vitu vyote kwa kila mtu.”

18 Uhusiano huo mzuri uliharibika wakati ambapo wanadamu, wakichochewa na Shetani, waliasi enzi kuu ya Yehova. Hata hivyo, tangu mwaka wa 1914, Ufalme wa Kimasihi umekuwa ukipiga hatua ili kurudisha tena amani na upatano. (Efe. 1:​9, 10) Wakati wa ule Utawala wa Miaka Elfu Moja, mambo mazuri ajabu ambayo sasa ‘hayaonekani’ yatakuwa halisi. Kisha “ule mwisho” utakuja, yaani, mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo. Baadaye kutatokea nini? Ingawa amepewa “mamlaka yote mbinguni na duniani,” Yesu hataki makuu. Hana nia ya kunyakua cheo cha Yehova. Kwa unyenyekevu, ‘anamkabidhi ufalme Mungu wake ambaye pia ni Baba yake.’ Atatumia cheo chake cha pekee na mamlaka “kwa utukufu wa Mungu.”​—⁠Mt. 28:18; Flp. 2:​9-11.

19, 20. (a) Raia wote wa Ufalme wataonyeshaje kwamba wanaikubali enzi kuu ya Yehova? (b) Ni tarajio gani kubwa ambalo tunangojea?

19 Wakati huo, raia wa kidunia wa Ufalme watakuwa wamefanywa kuwa wakamilifu. Watafuata mfano wa Yesu na watatambua kwa unyenyekevu na kwa hiari enzi kuu ya Yehova. Watakuwa na fursa ya kuonyesha tamaa yao ya kutambua enzi kuu ya Yehova kwa kufanikiwa kupita lile jaribu la mwisho. (Ufu. 20:​7-10) Kisha, waasi wote, yaani, wanadamu na roho waovu, wataharibiwa milele. Huo utakuwa wakati wenye shangwe na furaha kama nini! Familia ya Yehova ya ulimwenguni pote itamsifu kwa furaha, kwa sababu Yehova atakuwa “vitu vyote kwa kila mtu.”​—⁠Soma Zaburi 99:​1-3.

20 Je, mambo hayo mazuri ajabu ambayo Ufalme utaleta hivi karibuni yatakuchochea kukazia fikira mapenzi ya Mungu na kujitahidi kuyafanya? Je, unaweza kuepuka kukengeushwa fikira na faraja na tumaini la uwongo ambalo ulimwengu wa Shetani unatoa? Je, utaimarisha azimio lako la kuunga mkono na kuitegemeza enzi kuu ya Yehova? Matendo yako na yathibitishe kwamba unatamani kufanya hivyo milele. Kisha, utakuwa na pendeleo la kufurahia amani na ufanisi kwa muda wa miaka elfu moja na kuendelea!