Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze Kutokana Na Subira Ya Yehova Na Yesu

Jifunze Kutokana Na Subira Ya Yehova Na Yesu

“Ioneni subira ya Bwana wetu kuwa wokovu.”​—2 PET. 3:15.

1. Baadhi ya watu waaminifu wanajiuliza swali gani?

DADA mwaminifu aliyevumilia matatizo mengi kwa miaka mingi aliuliza hivi kwa unyenyekevu, “Je, nitauona mwisho kabla sijafa? ” Baadhi ya watu ambao wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi wanajiuliza swali hilohilo. Tunatamani kuiona siku ambayo Mungu atafanya vitu vyote kuwa vipya, na kuondoa matatizo yote tuliyo nayo. (Ufu. 21:5) Ingawa tuna sababu nyingi za kuamini kwamba mwisho wa mfumo wa Shetani uko karibu sana, inaweza kuwa vigumu kuingoja siku hiyo kwa subira.

2. Ni maswali gani kuhusu subira ya Mungu tutakayozungumzia?

2 Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba ni lazima tuwe na subira. Kama watumishi wa Mungu waliotutangulia, tutapata mambo ambayo Mungu ameahidi tukiwa na imani yenye nguvu na tukingojea kwa subira wakati wake wa kutimiza ahadi hizo. (Soma Waebrania 6:​11, 12.) Yehova mwenyewe amekuwa na subira. Angekuwa amekomesha uovu wakati wowote, lakini anangoja wakati unaofaa. (Rom. 9:​20-24) Kwa nini ni mwenye subira sana? Yesu amekuwaje mfano bora katika kuonyesha subira kama ya Mungu? Tutapata faida gani tukisitawisha subira kama ya Mungu? Majibu ya maswali hayo yanaweza kutusaidia kusitawisha subira na kujenga imani yenye nguvu, hata ikiwa tunaona kwamba Yehova anakawia.

KWA NINI YEHOVA ANAONYESHA SUBIRA?

3, 4. (a) Kwa nini Yehova ameonyesha subira katika kutimiza kusudi lake kuhusu dunia? (b) Yehova alitenda namna gani uasi ulipotokea Edeni?

3 Yehova ana sababu nzuri ya kuonyesha subira. Ni kweli kwamba sikuzote Yehova ndiye mwenye mamlaka kuu zaidi ulimwenguni; hata hivyo, uasi uliotokea Edeni ulizusha maswali muhimu yanayohusu ulimwengu wote mzima. Yehova amekuwa mwenye subira, akijua kwamba ingechukua muda ili kujibu kikamili maswali hayo. Kwa kuwa anajua vizuri sana matendo na mielekeo ya kila kiumbe mbinguni na duniani, bila shaka anatenda kwa faida yetu.​—Ebr. 4:13.

4 Yehova alikusudia kwamba wazao wa Adamu na Hawa waijaze dunia. Shetani alipomshawishi Hawa, na kisha Adamu akaasi, Mungu hakuacha kusudi lake. Hakushtuka, hakuamua mambo haraka-haraka, au kutenda bila kufikiri, na hivyo kuitupa familia yake ya kibinadamu. Badala yake, alifikiria njia nyingine ya kutimiza kusudi lake kwa ajili ya wanadamu na Dunia. (Isa. 55:11) Ili atimize kusudi lake na kuitetea enzi yake kuu, Yehova amejidhibiti na kuonyesha subira kubwa, hata amengoja kwa maelfu ya miaka ili mambo fulani yanayohusu kusudi lake yatimie kwa njia inayofaa kabisa.

5. Subira ya Yehova inawapa wanadamu fursa ya kufurahia baraka gani?

Sababu nyingine ambayo imemfanya Yehova angojee kwa subira ni ili watu wengi zaidi wapate uzima wa milele. Kwa sasa, anafanya mipango ili kuuokoa “umati mkubwa.” (Ufu. 7:​9, 14; 14:6) Yehova anawavuta watu kupitia kazi yetu ya kuhubiri, akiwaalika wajifunze kuhusu Ufalme wake na viwango vyake vya uadilifu. Ujumbe wa Ufalme ndio habari bora zaidi kwa wanadamu​—naam, ni “habari njema.” (Mt. 24:14) Kila mtu ambaye Yehova humvuta anakuwa sehemu ya kutaniko la ulimwenguni pote la marafiki wa kweli wanaopenda kufanya yaliyo sawa. (Yoh. 6:​44-47) Baba yetu mwenye upendo huwasaidia watu kama hao kupata kibali chake. Pia, amekuwa akichagua miongoni mwa wanadamu wale watakaokuwa washiriki wa serikali yake ya kimbingu. Watakapopata pendeleo lao la kimbingu, watu hao waliojitoa kwake watawasaidia wanadamu watiifu kuwa wakamilifu na kuishi milele. Ni wazi kwamba hata ingawa anangojea kwa subira, Yehova amekuwa akifanya kazi ili atimize ahadi zake, kwa manufaa yetu.

6. (a) Ni katika njia gani Yehova alionyesha subira katika siku za Noa? (b) Yehova anaonyesha subira jinsi gani leo?

6 Yehova huonyesha subira hata anapochokozwa kupita kiasi, na tunaweza kuona hilo tunapoona jinsi alivyoshughulikia uovu uliokuwapo kabla ya Gharika. Wakati huo, dunia ilijaa upotovu wa maadili na jeuri, na Yehova “akaumia moyoni mwake” kwa sababu ya hali mbaya sana ya wanadamu. (Mwa. 6:​2-8) Hangeweza kuvumilia hali hiyo milele, kwa hiyo akaamua kuleta Gharika ili kuwaangamiza wanadamu wasiotii. Wakati “subira ya Mungu ilipokuwa ikingoja katika siku za Noa,” Yehova alifanya mipango ili amwokoe Noa na familia yake. (1 Pet. 3:20) Kwa wakati unaofaa, Yehova alimjulisha Noa kuhusu uamuzi wake na akampa kazi ya kujenga safina. (Mwa. 6:​14-22) Kwa kuongezea, Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu,” akiwaonya jirani zake kuhusu uharibifu uliokuwa ukikaribia. (2 Pet. 2:5) Yesu alisema kwamba siku zetu ni kama siku za Noa. Yehova ameamua ni lini atakapoukomesha mfumo huu mwovu wa mambo. Hakuna mwanadamu anayejua “siku ile na saa.” (Mt. 24:36) Kwa sasa, tuna kazi tuliyopewa na Mungu ya kuwaonya watu na kuwajulisha jinsi wanavyoweza kuokolewa.

7. Je, Yehova anakawia kutimiza ahadi zake? Eleza.

7 Ni wazi kwamba subira ya Yehova haimaanishi kwamba anangojea tu wakati upite. Hapana, hatupaswi kamwe kudhani kwamba subira yake inaonyesha kwamba hawajali au hapendezwi na wanadamu! Hata hivyo, ukweli ni kwamba inaweza kuwa vigumu kukumbuka jambo hilo tunapoendelea kuzeeka au kuteseka katika mfumo huu mwovu. Tunaweza kuvunjika moyo au kuhisi kwamba Mungu anakawia kutimiza ahadi zake. (Ebr. 10:36) Usisahau kamwe kwamba ana sababu nzuri za kuwa mwenye subira na anautumia vizuri wakati uliosalia kwa manufaa ya watumishi wake washikamanifu. (2 Pet. 2:3; 3:9) Pia, fikiria jinsi Yesu alivyoonyesha subira kama ya Mungu.

YESU AMEWEKAJE MFANO MZURI KATIKA KUONYESHA SUBIRA?

8. Yesu alionyesha subira chini ya hali gani?

8 Yesu anafanya mapenzi ya Mungu na amekuwa akiyafanya kwa bidii kwa maelfu ya miaka isiyojulikana. Shetani alipoasi, Yehova aliamua kwamba Mwana wake mzaliwa-pekee angekuja duniani akiwa Masihi. Fikiria kile ambacho jambo hilo lilimaanisha kwa Yesu; alihitaji kungoja kwa subira kwa maelfu ya miaka hadi wakati huo ufike. (Soma Wagalatia 4:4.) Hakukaa kitako tu akingojea muda upite; badala yake, aliendelea kufanya kazi aliyopewa na Baba yake. Hatimaye alipokuja duniani, alijua kwamba ilikuwa lazima afe mikononi mwa Shetani, kama ilivyotabiriwa. (Mwa. 3:15; Mt. 16:21) Kwa subira, alijinyenyekeza ili kufanya mapenzi ya Mungu, licha ya kwamba hilo lilimaanisha kupata maumivu makali sana. Alionyesha ushikamanifu wa pekee sana. Hakujielekezea fikira au kuhangaikia cheo chake, na tunaweza kufaidika kutokana na mfano wake.​—Ebr. 5:​8, 9.

9, 10. (a) Yesu amekuwa akifanya nini huku akingojea kwa subira Yehova achukue hatua? (b) Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu ratiba ya Yehova?

9 Baada ya kufufuliwa, Yesu alipewa mamlaka mbinguni na duniani. (Mt. 28:18) Anatumia mamlaka hayo kutimiza kusudi la Yehova kulingana na ratiba ambayo Mungu ameweka. Yesu alingojea kwa subira kwenye mkono wa kuume wa Mungu hadi mwaka wa 1914 ili adui zake wawekwe kuwa kiti cha miguu yake. (Zab. 110:​1, 2; Ebr. 10:​12, 13) Hivi karibuni, atachukua hatua ya kuukomesha mfumo wa Shetani. Kwa sasa, Yesu anawasaidia watu na kuwaongoza kwa subira kwenye “maji ya uzima.”​—Ufu. 7:17.

10 Kutokana na mfano wa Yesu, je, unaona maoni unayopaswa kuwa nayo kuhusu ratiba ya Yehova? Bila shaka, Yesu alitamani sana kufanya jambo lolote ambalo Baba yake alimwomba afanye; hata hivyo, alikuwa tayari kungojea wakati uliowekwa na Mungu ufike. Tunapongojea mwisho wa mfumo huu mwovu wa Shetani, sote tunahitaji kuiga subira ya Mungu, na hatupaswi kamwe kumtangulia Mungu au kukata tamaa kwa sababu ya kuvunjika moyo. Tunaweza kufanya nini ili tusitawishe subira kama ya Mungu?

NITASITAWISHA JINSI GANI SUBIRA KAMA YA MUNGU?

11. (a) Kuna uhusiano gani kati ya imani na subira? (b) Kwa nini tuna sababu nzuri za kuwa na imani yenye nguvu?

11 Kabla ya Yesu kuja duniani, manabii na watumishi wengine waaminifu waliweka mfano mzuri unaoonyesha jinsi ambavyo hata wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kuvumilia kwa subira. Kulikuwa na uhusiano wa moja kwa moja kati ya imani yao na subira yao. (Soma Yakobo 5:​10, 11.) Ikiwa kwa kweli hawakuamini mambo ambayo Yehova alikuwa amewaambia, yaani, ikiwa hawakuwa na imani, je, wangengojea kwa subira utimizo wa ahadi zake? Mara kwa mara, walikabili majaribu yenye kutisha au majaribu magumu ya imani wakiwa na uhakika kabisa kwamba hatimaye Mungu angetimiza ahadi zake. (Ebr. 11:​13, 35-40) Tuna sababu nyingi hata zaidi za kuwa na imani yenye nguvu, kwa kuwa Yesu anatumikia sasa akiwa “Mkamilishaji wa imani yetu.” (Ebr. 12:2) Alitimiza unabii na kufunua makusudi ya Mungu kwa njia inayotupatia sababu nzuri za kuwa na imani.

12. Tunaweza kufanya nini ili tujenge imani yetu?

12 Ni hatua gani zinazofaa tunazoweza kuchukua ili tuimarishe imani yetu na hivyo kusitawisha subira? Ni jambo muhimu sana kutii mashauri ya Mungu. Kwa mfano, fikiria sababu za kutanguliza masilahi ya Ufalme katika maisha yako. Je, unaweza kujitahidi zaidi kutumia shauri linalopatikana katika Mathayo 6:33? Huenda hilo likamaanisha kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma au kufanya mabadiliko fulani katika mtindo wako wa maisha. Usipuuze jinsi ambavyo Yehova amebariki jitihada zako kufikia sasa. Huenda amekuwezesha kuongoza funzo jipya la Biblia au labda amekusaidia kuwa na “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” (Soma Wafilipi 4:7.) Kwa hiyo, unapokazia fikira faida ambazo wewe binafsi umepata kwa sababu ya kufuata maagizo ya Yehova, utaithamini hata zaidi sifa ya subira.​—Zab. 34:8.

13. Kujenga imani na kusitawisha subira kunaweza kulinganishwa na utaratibu gani?

13 Kujenga imani na kusitawisha subira kunaweza kulinganishwa na utaratibu wa kupanda, kupalilia, na kuvuna. Kila mara mkulima anapovuna kwa wingi, anachochewa zaidi kupanda mbegu msimu unaofuata. Bila shaka, atahitaji kungojea mavuno kwa subira, lakini jambo hilo halitamzuia kupanda mbegu, labda hata atapanda mbegu katika mashamba mengi zaidi kuliko msimu uliotangulia. Anaamini kwamba atavuna. Vivyo hivyo, kadiri tunavyojifunza na kufuata mashauri ya Yehova, na kisha kupata faida, ndivyo tunavyochochewa kumtegemea zaidi Yehova. Imani yetu pia inakua, na inakuwa rahisi zaidi kungojea baraka tukiwa na uhakika kwamba zitakuja.​—Soma Yakobo 5:​7, 8.

14, 15. Tunahitaji kuwa na maoni gani kuhusu kuteseka kwa wanadamu?

14 Njia nyingine ya kusitawisha subira ni kufikiria jinsi tunavyopaswa kuuona ulimwengu na hali zetu binafsi. Jaribu kuona mambo kama Yehova anavyoyaona. Kwa mfano, fikiria maoni yake kuhusu kuteseka kwa wanadamu. Kwa muda mrefu, Yehova ameumia kuona wanadamu wakiteseka; hata hivyo, hajalemewa sana na huzuni na kushindwa kutenda mema. Alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee “ili azivunje kazi za Ibilisi” na kuondoa madhara yote ambayo Shetani amewaletea wanadamu. (1 Yoh. 3:8) Ukweli ni kwamba mateso yataonekana kuwa ya muda mfupi yakilinganishwa na suluhisho la milele ambalo Mungu ataleta. Vivyo hivyo, badala ya kujiruhusu tuvunjike moyo kwa sababu ya utawala mwovu wa Shetani uliopo sasa au kukosa subira tukifikiri kwamba mwisho unakawia, acheni tuweke imani katika mambo yasiyoonekana yatakayodumu milele. Yehova ameamua wakati hususa wa kukomesha uovu, na atachukua hatua kwa wakati unaofaa kabisa.​—Isa. 46:13; Nah. 1:9.

15 Katika siku hizi ngumu za mwisho za mfumo huu wa mambo, huenda tutakabili majaribu ya pekee ya imani yetu. Badala ya kukasirika tunapotendewa kwa jeuri au wapendwa wetu wanapoteseka, tunahitaji kuazimia kumtegemea Yehova kabisa. Sisi si wakamilifu, kwa hiyo si rahisi kufanya hivyo. Hata hivyo, kumbuka jambo ambalo Yesu alifanya, lililoandikwa katika Mathayo 26:39.​Soma.

16. Tunahitaji kuepuka kufanya nini katika wakati huu unaobaki?

16 Mtu ambaye ana shaka kwamba mwisho uko karibu anaweza kuanza kuwa na mtazamo usiofaa. Huenda akafikiri kwamba anahitaji kufanya mipango yake endapo ahadi za Yehova hazitatimia. Kwa maneno mengine, huenda akawaza hivi: ‘Nitasubiri nione ikiwa kwa kweli Yehova hutimiza neno lake.’ Kisha, anaweza kujaribu kujitafutia umashuhuri katika ulimwengu huu, kujitafutia usalama wa kifedha badala ya kutanguliza Ufalme wa Mungu, au kuitegemea elimu ya juu ili kuwa na maisha ya starehe sasa. Lakini je, si ni kweli kwamba kufanya hivyo kunathibitisha kwamba mtu hana imani? Kumbuka kwamba Paulo alituhimiza tuwaige watu waaminifu waliorithi ahadi kutoka kwa Yehova “kupitia imani na subira.” (Ebr. 6:12) Yehova hataruhusu mfumo huu mwovu wa mambo uendelee kuwapo kwa muda mrefu isivyo lazima kulingana na kusudi lake. (Hab. 2:3) Kwa sasa, ni lazima tuepuke kumtumikia Yehova kidesturi tu. Badala yake, tunahitaji kuendelea kuwa macho na kuhubiri habari njema kwa bidii, na hilo litatuletea uradhi usio na kifani hata sasa.​—Luka 21:36.

SUBIRA HULETA BARAKA GANI?

17, 18. (a) Tuna fursa ya kufanya nini sasa kwa sababu ya subira ya Mungu? (b) Tunapata baraka gani sasa kwa sababu ya kuonyesha subira?

17 Iwe tumemtumikia Yehova kwa miezi michache au kwa miaka mingi, tunataka kuendelea kumtumikia milele. Subira hutusaidia kuvumilia hadi tupate wokovu, haidhuru ni muda gani unaobaki kabla ya mfumo huu kukoma. Sasa Yehova anatupatia fursa ya kuthibitisha ikiwa tunatumaini kabisa maamuzi yake na, ikiwa ni lazima, kuwa tayari kuteseka kwa ajili ya jina lake. (1 Pet. 4:​13, 14) Pia, Mungu anatuzoeza kwa njia ambayo inaweza kutusaidia kuwa na subira tunayohitaji ili tuokolewe.​—1 Pet. 5:10.

18 Yesu ana mamlaka yote mbinguni na duniani, na hakuna chochote kinachoweza kukuondoa chini ya ulinzi wake, isipokuwa wewe mwenyewe ujiondoe. (Yoh. 10:​28, 29) Hatuhitaji kuogopa wakati ujao au hata kifo. Wale wanaovumilia kwa subira hadi mwisho wataokolewa. Kwa hiyo, ni lazima tuhakikishe kwamba hatuuruhusu ulimwengu utushawishi na kutufanya tuache kumtegemea Yehova. Badala yake, ni lazima tuazimie kukua katika imani na kutumia kwa hekima wakati huu ambao Mungu anatuonyesha subira.​—Mt. 24:13; soma 2 Petro 3:​17, 18.