Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Hamwijui Ile Siku Wala Saa”

“Hamwijui Ile Siku Wala Saa”

“Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamwijui ile siku wala saa.”​—MT. 25:13.

1-3. (a) Ni hali gani zinazoonyesha somo la mifano miwili ambayo Yesu alitoa? (b) Tunahitaji kujibu maswali gani?

WAZIA kwamba ofisa fulani mashuhuri anakuomba umpeleke kwa gari kwenye mkutano muhimu. Hata hivyo, dakika chache kabla ya kwenda kumchukua ili umpeleke kwenye mkutano huo, unagundua kwamba gari halina mafuta ya kutosha. Unahitaji kwenda haraka kuongeza mafuta. Unapoenda, ofisa huyo anawasili. Anakutafuta kila mahali lakini hakupati. Hawezi kungoja, kwa hiyo, anamwomba dereva mwingine ampeleke kwenye mkutano huo. Punde si punde, unafika na kugundua kwamba ofisa huyo alienda zake na kukuacha. Ungehisije?

Sasa wazia kwamba wewe ni ofisa huyo na umewachagua wanaume watatu wenye uwezo ili wafanye kazi fulani muhimu. Unawaeleza kuhusu mgawo huo, na wote watatu wanaukubali kwa utayari. Hata hivyo, unaporudi muda mfupi baadaye, unagundua kwamba ni wawili tu kati yao waliofanya kazi uliyowapa. Isitoshe, yule ambaye hakufanya kazi yake anatoa visingizio. Ukweli ni kwamba hata hakujaribu kuifanya. Ungehisije?

3 Katika mifano yake kuhusu mabikira na talanta, Yesu alitumia hali zinazofanana na hizo ili kuonyesha kwa nini katika nyakati za mwisho, baadhi ya Wakristo watiwa-mafuta wangethibitika kuwa waaminifu na wenye busara, lakini wengine hawangekuwa hivyo. * (Mt. 25:​1-30) Alikazia somo la mifano hiyo kwa kusema hivi: “Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamwijui ile siku wala saa,” yaani, wakati ambapo kwa kweli Yesu atakuja kutekeleza hukumu ya Mungu juu ya ulimwengu wa Shetani. (Mt. 25:13) Tunaweza kutumia shauri hilo leo. Tunaweza kufaidikaje kwa kuendelea kukesha kama Yesu alivyotutia moyo tufanye? Ni nani ambao wamethibitisha kwamba wako tayari kuokolewa? Na ni lazima tufanye nini sasa ili tuendelee kukesha?

FAIDIKA KWA KUENDELEA KUKESHA

4. Kwa nini ‘kuendelea kukesha’ hakumaanishi kwamba ni lazima tujue ile saa?

4 Utendaji fulani, kama vile kufanya kazi katika kiwanda, kumwona daktari, au kusafiri kwa magari ya umma, hutulazimu kufuata ratiba. Hata hivyo, katika utendaji mwingine kama vile kuzima moto au kufanya kazi ya kuwaokoa watu baada ya msiba, kuangalia saa kunaweza kukengeusha fikira, na kunaweza kuwa hatari sana. Chini ya hali kama hizo, ni muhimu zaidi kukazia fikira kazi inayohitaji kufanywa badala ya kufuata ratiba fulani. Kadiri mwisho wa mfumo huu wa mambo unavyozidi kukaribia, ndivyo kazi ya kuwafundisha wengine kuhusu maandalizi ya Yehova ya wokovu inavyozidi kuwa muhimu zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Kuendelea kukesha tukiwa Wakristo hakumaanishi kwamba ni lazima tujue ile saa. Kwa kweli, tunafaidika kwa angalau njia tano kwa sababu ya kutojua siku au saa hususa ambayo mwisho utakuja.

5. Kutojua ile siku na saa kunatusaidiaje kufunua yaliyo moyoni mwetu?

5 Kwanza, kutojua wakati ambapo mwisho utakuja kunatupatia nafasi ya kufunua mambo ambayo kwa kweli yako moyoni mwetu. Kwa hakika, Yehova anatuonyesha heshima kwa kutotujulisha wakati huo na kwa njia hiyo anatupatia nafasi ya kuutumia uhuru wetu wa kuchagua kuonyesha ushikamanifu wetu kwake. Ingawa tunatazamia kuokoka mwisho wa mfumo huu wa mambo, tunamtumikia Yehova kwa sababu tunampenda, si kwa sababu tunataka tu kupata uzima. (Soma Zaburi 37:4.) Tunafurahia kufanya mapenzi yake, na tunatambua kwamba Mungu anatufundisha ili tujifaidi wenyewe. (Isa. 48:17) Hatuoni amri zake kuwa mzigo mzito.​—⁠1 Yoh. 5:3.

6. Tunapomtumikia Mungu kwa sababu tunampenda, anahisije, na kwa nini?

6 Faida ya pili ya sisi kutojua ile siku na saa ni kwamba hilo linatupatia fursa ya kuufurahisha moyo wa Yehova. Tunapomtumikia kwa sababu tunampenda, bali si kwa sababu ya tarehe au kwa sababu tu ya thawabu, tunachangia jibu la Yehova kwa dhihaka zisizo na msingi za adui yake, Shetani. (Ayu. 2:​4, 5; soma Methali 27:11.) Tunapofikiria uchungu wote na huzuni ambayo Ibilisi amesababisha, tunafurahi kuitetea enzi kuu ya Yehova na kuukataa utawala mwovu wa Shetani.

7. Kwa nini unafikiri kwamba kufuatia maisha ya kujidhabihu kunapendeza?

7 Tatu, kutumika bila kuwa na tarehe hususa akilini kunatuchochea kufuatia maisha ya kujidhabihu. Watu fulani leo ambao hawamjui Mungu wanaamini pia kwamba ulimwengu huu hauwezi kuendelea kuwapo kwa muda mrefu. Kwa kuwa wanaogopa kwamba msiba fulani utatokea hivi karibuni, wana mtazamo huu, “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Kor. 15:32) Lakini, sisi hatuogopi. Tunakataa kujitenga na wengine kwa kusudi la kutosheleza tamaa zetu za kichoyo. (Met. 18:1) Badala yake, tunajikana wenyewe na kutumia kwa hiari wakati wetu, nguvu, na mali nyingine ili kuwahubiria wengine habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Soma Mathayo 16:24.) Tunafurahia kumtumikia Mungu, hasa kwa kuwasaidia wengine wamjue.

8. Ni mfano gani katika Biblia unaoonyesha kwa nini tunahitaji kumtegemea Yehova na Neno lake kwa ukamili zaidi?

8 Faida ya nne ya kutojua ile siku au saa ni kwamba kunatusaidia kumtegemea Yehova kikamili zaidi na kufuata kwa bidii Neno lake maishani mwetu. Tuna mwelekeo mkubwa wa kujitegemea kwa sababu ya hali yetu ya dhambi tukiwa wanadamu. Paulo aliwashauri Wakristo wote hivi: “Yeye anayefikiri kuwa amesimama na ajihadhari kwamba asianguke.” Watu ishirini na tatu elfu walipoteza kibali cha Yehova muda mfupi kabla ya Yoshua kuwaongoza watu wa Mungu kuingia katika Nchi ya Ahadi. “Mambo hayo,” Paulo anasema, “yaliandikwa ili kuwa onyo kwetu sisi ambao tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.”​—⁠1 Kor. 10:​8, 11, 12.

9. Matatizo yanawezaje kutusafisha na kutuwezesha kumkaribia Mungu zaidi?

9 Faida ya tano tunayopata kwa sababu ya kutojua wakati ambapo mwisho utakuja ni kwamba hilo linaruhusu matatizo tunayokabili yatusafishe ili tuwe Wakristo bora zaidi. (Soma Zaburi 119:71.) Kwa kweli, siku za mwisho za mfumo huu ni “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:​1-5) Watu wengi katika ulimwengu wa Shetani wanatuchukia, hivyo, huenda tukateswa kwa sababu ya imani yetu. (Yoh. 15:19; 16:2) Tukijinyenyekeza na kutafuta mwongozo wa Mungu wakati wa majaribu, imani yetu itasafishwa, au kutakaswa, kana kwamba kupitia moto. Hatuvunjiki moyo. Badala yake, tutamkaribia zaidi Yehova kwa njia ambayo hatukuwazia kamwe.​—⁠Yak. 1:​2-4; 4:8.

10. Ni nini kinachofanya wakati uonekane unasonga haraka?

10 Huenda wakati ukaonekana unasonga haraka au polepole. Tunapokuwa na shughuli nyingi hatuangalii-angalii saa, na wakati huonekana ukisonga haraka sana. Vivyo hivyo, tukijishughulisha sana na kazi yenye kusisimua ambayo Yehova ametupatia tufanye, huenda ile siku na saa ya mwisho ikafika haraka kuliko tunavyowazia. Watiwa-mafuta wengi wameweka mfano mzuri sana katika jambo hilo. Acheni tupitie kwa ufupi mambo yaliyotukia baada ya Yesu kutawazwa kuwa Mfalme mwaka wa 1914 ili tuone jinsi baadhi yao walivyothibitisha kwamba walikuwa tayari, tofauti na watu wengine.

WATIWA-MAFUTA WATHIBITISHA KWAMBA WAKO TAYARI

11. Baada ya mwaka wa 1914, kwa nini watiwa-mafuta fulani walifikiri kwamba Bwana amekawia?

11 Kumbuka mifano ya Yesu kuhusu wale mabikira na talanta. Ikiwa mabikira au watumwa katika mifano hiyo wangejua wakati ambapo bwana-arusi au bwana mkubwa angekuja, hawangehitaji kuendelea kukesha. Lakini hawakujua, kwa hiyo, walihitaji kuendelea kuwa tayari. Ingawa kwa miongo mingi watiwa-mafuta waliuona mwaka wa 1914 kuwa mwaka wa pekee, hawakuelewa waziwazi ni nini ambacho kingetukia. Mambo yalipokosa kutukia kama walivyotarajia, huenda baadhi yao walidhani kwamba Bwana-arusi amekawia. Baadaye, ndugu mmoja alikumbuka hivi: “Wachache kati yetu walifikiri kwa hakika kwamba tungeenda mbinguni katika juma la kwanza la Oktoba [mwaka wa 1914].”

12. Watiwa-mafuta walionyeshaje kwamba ni waaminifu na wenye busara?

12 Hebu fikiria jinsi ilivyovunja moyo kutarajia mwisho uje lakini haukuja! Isitoshe, akina ndugu walikabiliana na upinzani wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu! Kisha kukawa na kipindi cha kutotenda, kama cha usingizi. Lakini mwaka wa 1919, kulikuwa na mwito wa kuamka! Yesu alikuja katika hekalu la kiroho la Mungu, na wakati wa ukaguzi ulikuwa umefika. Hata hivyo, baadhi ya Wakristo hawakufaulu kupita ukaguzi huo na hivyo wakapoteza pendeleo lao la kuendelea kufanya “biashara” ya Mfalme. (Mt. 25:16) Kama wale mabikira wapumbavu, ni kana kwamba hawakuwa na bidii ya kuongeza mafuta yao ya kiroho. Na kama yule mtumwa goigoi, hawakuwa tayari kujidhabihu kwa ajili ya Ufalme. Hata hivyo, idadi kubwa ya watiwa-mafuta walionyesha ushikamanifu usioyumba-yumba na tamaa kubwa ya kumtumikia Bwana wao hata katika ile miaka migumu ya vita.

13. Jamii ya mtumwa ilikuwa na mtazamo gani baada ya mwaka wa 1914, na ina mtazamo gani leo?

13 Baada ya mwaka wa 1914, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilikuwa na maneno haya mazito: “Akina ndugu, wale kati yetu ambao wana mtazamo unaofaa kumwelekea Mungu hawavunjiki moyo kwa sababu ya mipango yoyote ya Mungu. Hatukutaka mapenzi yetu wenyewe yatendeke; hivyo tulipogundua kwamba tulikuwa tukitarajia jambo lisilofaa mnamo Oktoba, 1914, tulifurahi kwamba Bwana hakubadili Mpango Wake ili utufae. Hatukutarajia Afanye hivyo. Tulitaka tu kuelewa mipango na makusudi Yake.” Bado watiwa-mafuta wa Bwana wanaonyesha mtazamo huo wa unyenyekevu na wa kujitoa. Hawadai kwamba wamepuliziwa na roho takatifu, lakini wameazimia kufanya “biashara” ya Bwana duniani. Na sasa “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” yaani, Wakristo walio na tumaini la kuishi milele duniani, wanawaiga kwa kuendelea kukesha na kuonyesha bidii.​—⁠Ufu. 7:9; Yoh. 10:16.

KUTHIBITISHA KWAMBA TUKO TAYARI

14. Tutalindwa jinsi gani tukishikamana na jamii inayotumiwa na Mungu kuandaa chakula cha kiroho?

14 Kama Wakristo watiwa-mafuta, washiriki wa umati mkubwa ambao wako macho wanashikamana kabisa na jamii hiyo iliyowekwa rasmi na Mungu ili kuandaa chakula cha kiroho. Kwa njia hiyo, ni kana kwamba wao pia wanaongeza mafuta yao ya kiroho kutoka katika Neno la Mungu na roho yake. (Soma Zaburi 119:130; Yohana 16:13.) Wakiwa wameimarishwa hivyo, wao pia wanaonyesha kwamba wako tayari kwa ajili ya kurudi kwa Kristo, wakiendelea kuonyesha bidii hata chini ya majaribu makali. Kwa mfano, katika kambi moja ya Wanazi, mwanzoni akina ndugu walikuwa na Biblia moja tu. Basi, wakasali ili wapate chakula zaidi cha kiroho. Muda mfupi baadaye walipata habari kwamba ndugu aliyeletwa kambini humo alifaulu kuficha magazeti machache mapya ya Mnara wa Mlinzi ndani ya mguu wake bandia wa mbao na kuyaleta kambini. Ndugu Ernst Wauer, ndugu mtiwa-mafuta aliyekuwa miongoni mwa watu waliookoka kutoka katika kambi hiyo, alikumbuka hivi baadaye: “Yehova alitusaidia kwa njia ya ajabu kukumbuka mawazo yenye kuimarisha yaliyokuwa katika makala hizo.” Kisha akasema: “Siku hizi, ni rahisi sana kupata chakula cha kiroho, lakini je, sikuzote tunakithamini? Nina hakika kwamba Yehova atawabariki sana wale wanaomtegemea, wanaobaki washikamanifu, na kula kwenye meza yake.”

15, 16. Wenzi fulani wa ndoa walithawabishwaje kwa sababu ya bidii yao katika huduma ya Kikristo, na unaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi kama hayo?

15 Kondoo wengine pia wanajishughulisha sana na kazi ya Bwana, wakiwaunga mkono kikamili ndugu za Kristo. (Mt. 25:40) Wao si kama yule mtumwa mwovu aliye goigoi katika mfano wa Yesu, wako tayari kujidhabihu na kujikakamua kabisa ili kutanguliza masilahi ya Ufalme. Kwa mfano, Jon na Masako walipoalikwa wasaidie kuhubiri eneo la Kichina nchini Kenya, mwanzoni walisitasita. Lakini baada ya kusali na kufikiria hali zao, waliamua kuhamia nchini Kenya.

16 Walithawabishwa sana kwa sababu ya jitihada zao. Walisema hivi: “Huduma hapa inafurahisha sana.” Walianzisha mafunzo saba ya Biblia. Walipata mambo mengine mengi yenye kusisimua katika huduma. Walifikia mkataa huu, “Tunamshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya kuturuhusu kuwa hapa.” Bila shaka, kuna ndugu na dada wengine wengi ambao wameonyesha kupitia maamuzi yao kwamba wameazimia kujitoa kikamili katika utumishi wa Mungu haidhuru mwisho utakuja wakati gani. Wafikirie maelfu ambao wamehitimu katika Shule ya Gileadi na kuanza utumishi wa umishonari. Kwa nini usisome kuhusu utumishi huo wa pekee katika makala yenye kichwa “Tunafanya Yote Tuwezayo! ” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 2001? Unaposoma masimulizi hayo yenye kusisimua kuhusu maisha ya kila siku katika kazi ya umishonari, fikiria njia ambazo unaweza kuongeza utumishi wako na hivyo kumsifu Mungu. Ukifanya hivyo, utapata shangwe zaidi.

NINYI PIA ENDELEENI KUKESHA

17. Tumefaidikaje kwa sababu ya kutojua ile siku na saa?

17 Ni wazi kwamba tumefaidika kwa sababu ya kutojua siku au saa hususa ambayo mfumo huu utafikia mwisho. Badala ya kukata tamaa au kuvunjika moyo, kadiri tunavyojitoa zaidi kufanya mapenzi ya Baba yetu mwenye upendo, Yehova, ndivyo tunavyomkaribia zaidi. Kuendelea kushika jembe la ng’ombe kwa njia ya mfano, na kuepuka mambo yanayokengeusha fikira kumetuletea shangwe nyingi sana katika utumishi wa Bwana wetu.​—⁠Luka 9:62.

18. Kwa nini hatutaki imani yetu idhoofike?

18 Tunaikaribia haraka siku ya Mungu ya hukumu. Hakuna yeyote kati yetu anayetaka kumtamausha Yehova au Yesu. Wametukabidhi mapendeleo ya utumishi yenye thamani katika siku hizi za mwisho. Tunathamini kama nini kuona kwamba wanatuamini!​—⁠Soma 1 Timotheo 1:12.

19. Tunawezaje kuendelea kuwa tayari?

19 Iwe tuna tumaini la kufurahia maisha mbinguni au katika Paradiso duniani, acheni tuazimie kuendelea kutimiza kwa uaminifu mgawo tuliopewa na Mungu wa kuhubiri na kufanya wanafunzi. Bado hatujui siku au saa hususa ambayo siku ya Yehova itakuja, na kwa kweli hatuhitaji kuijua. Tunaweza na tutaendelea kuwa tayari. (Mt. 24:​36, 44) Tuna hakika kwamba maadamu tunamtegemea Yehova kikamili na kutanguliza Ufalme wake, hatutakata tamaa.​—⁠Rom. 10:11.