Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anawakutanisha Watu Wake Wenye Shangwe

Yehova Anawakutanisha Watu Wake Wenye Shangwe

“Wakutanishe watu, wanaume na wanawake na watoto wadogo na mkaaji mgeni.”​—KUM. 31:12.

1, 2. Tunapaswa kukazia uangalifu mambo gani kuhusu makusanyiko ya kitheokrasi?

KWA muda mrefu sana, makusanyiko ya kimataifa na ya wilaya yamekuwa sehemu ya kawaida ya historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova. Wengi wetu tumehudhuria makusanyiko hayo yenye shangwe, labda tumefanya hivyo kwa miaka mingi.

2 Kwa maelfu ya miaka iliyopita, watu wa Mungu walifanya pia makusanyiko matakatifu. Tutachunguza makusanyiko fulani yanayotajwa katika Maandiko ambayo ni kielelezo kwa makusanyiko ya leo. Angalia ulinganifu uliopo kati ya makusanyiko hayo na makusanyiko ya leo, na ukazie fikira faida tunazopata tunapohudhuria makusanyiko hayo.​—Zab. 44:1; Rom. 15:4.

MAKUSANYIKO MUHIMU YA ZAMANI NA YA LEO

3. (a) Ni nini kilichotukia katika kusanyiko la kwanza la watu wa Yehova linalotajwa katika Biblia? (b) Ni nini kilichotumiwa kuwaita Waisraeli wakusanyike pamoja?

3 Kusanyiko lililofanywa chini ya Mlima Sinai ndilo kusanyiko la kwanza kubwa zaidi la watu wa Mungu. Walikusanyika ili kupata maagizo ya kiroho. Kwa kweli lilikuwa kusanyiko muhimu katika historia ya ibada safi. Katika pindi hiyo yenye kusisimua, ambayo bila shaka wahudhuriaji hawangeweza kamwe kuisahau, Yehova aliwaonyesha Waisraeli nguvu zake alipowapa Sheria yake. (Kut. 19:​2-9, 16-19; soma Kutoka 20:18; Kumbukumbu la Torati 4:​9, 10.) Tukio hilo lilikuwa msingi wa jinsi Mungu alivyoshughulika na taifa la Israeli baadaye. Muda mfupi baadaye, Yehova alianzisha njia mpya ya kuwakusanya watu wake. Alimwagiza Musa atengeneze tarumbeta mbili za fedha ambazo zingetumiwa kuliita “kusanyiko lote” ili likutane “kwenye mwingilio wa hema la mkutano.” (Hes. 10:​1-4) Wazia msisimuko uliokuwapo katika pindi hizo!

4, 5. Kwa nini makusanyiko yaliyofanywa na Musa na Yoshua yalikuwa muhimu sana?

Walipokuwa wakikaribia mwisho wa safari yao ya miaka 40 nyikani, Musa aliwakusanya Waisraeli wenzake. Huo ulikuwa wakati muhimu zaidi katika historia ya taifa hilo jipya. Walikuwa karibu kuingia katika Nchi ya Ahadi. Huo ulikuwa wakati unaofaa kabisa wa Musa kuwakumbusha ndugu zake mambo yote ambayo Yehova alikuwa amewafanyia na yale ambayo angewafanyia.​—Kum. 29:​1-15; 30:​15-20; 31:30.

5 Labda katika kusanyiko hilohilo, Musa alizungumza kuhusu mipango ya kawaida ya makusanyiko na ya kuwaelimisha watu wa Mungu. Katika miaka ya Sabato, wakati wa Sherehe ya Vibanda, wanaume, wanawake, watoto, na wakaaji wageni katika Israeli walipaswa kukutana mahali ambapo Yehova alichagua ‘ili wasikilize na ili wajifunze kumwogopa Yehova na kuwa waangalifu kuyatimiza maneno yote ya sheria.’ (Soma Kumbukumbu la Torati 31:​1, 10-12.) Kwa hiyo, mwanzoni kabisa mwa historia ya watu wa Mungu, ilikuwa wazi kwamba walipaswa kukusanyika kwa ukawaida ili kujifunza neno la Yehova na makusudi yake. Waisraeli walipoimiliki kikamili Nchi ya Ahadi huku wakiwa wamezungukwa na mataifa ya kipagani, Yoshua aliwakusanya Waisraeli wote ili kuimarisha azimio lao la kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova. Waisraeli walikubali na kuapa kumtumikia Mungu.​—Yos. 23:​1, 2; 24:​1, 15, 21-24.

6, 7. Kwa nini tunaweza kusema kwamba makusanyiko ya kisasa ya watu wa Yehova yamekuwa matukio muhimu ya kihistoria?

6 Katika historia ya kisasa ya watu wa Yehova, kumekuwa pia na makusanyiko muhimu sana. Katika makusanyiko hayo, mabadiliko makubwa yametangazwa kuhusiana na utendaji wa kitheokrasi au uelewaji wa Kimaandiko. (Met. 4:18) Wanafunzi wa Biblia walifanya kusanyiko la kwanza kubwa huko Cedar Point, Ohio, Marekani, mnamo mwaka wa 1919 baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Katika kusanyiko hilo ambalo lilihudhuriwa na watu 7,000 hivi, kampeni ya kuhubiri duniani pote ilianzishwa. Mnamo mwaka wa 1922, katika kusanyiko la wilaya la siku tisa ambalo lilifanyiwa kwenye uwanja huohuo, Joseph F. Rutherford aliwahimiza wahudhuriaji waliomsikiliza kwa makini washiriki kwa bidii zaidi katika kazi hiyo. Aliwahimiza hivi: “Muwe mashahidi waaminifu na wa kweli wa Bwana. Songeni mbele katika vita mpaka kila sehemu ya Babiloni ibaki ukiwa. Utangazeni ujumbe kotekote. Ni lazima ulimwengu ujue kwamba Yehova ni Mungu na Yesu Kristo ni Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana. Hii ndiyo siku ya siku zote. Tazameni, Mfalme anatawala! Ninyi ndio mawakili wa kumtangaza. Kwa hiyo, mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Wale waliohudhuria kusanyiko hilo, na kwa kweli watu wa Mungu ulimwenguni pote, waliitikia kwa shangwe himizo hilo.

7 Katika mwaka wa 1931, huko Columbus, Ohio, Wanafunzi wa Biblia walikubali kwa msisimuko mkubwa sana jina Mashahidi wa Yehova. Kisha mwaka wa 1935, huko Washington, D.C., Ndugu Rutherford aliutambulisha “umati mkubwa,” ambao kitabu cha Ufunuo kinasema kwamba ‘umesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo.’ (Ufu. 7:​9-17) Mnamo mwaka wa 1942, wakati Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokuwa vikiendelea, Nathan H. Knorr alitoa hotuba yenye kusisimua yenye kichwa “Amani​—Je, Inaweza Kudumu? ” Katika hotuba hiyo, alimtambulisha yule “mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu” anayetajwa katika kitabu cha Ufunuo sura ya 17, kisha akasema kwamba baada ya vita kumalizika, bado kungekuwa na kazi kubwa sana ya kuhubiri.

8, 9. Kwa nini makusanyiko fulani yamekuwa yenye kugusa moyo sana?

8 Katika Kusanyiko la Kitheokrasi lenye kichwa, “Mataifa Yenye Furaha,” lililofanywa huko Cleveland, Ohio, mwaka wa 1946, Ndugu Knorr alitoa hotuba nzuri sana yenye kichwa “Matatizo ya Kujenga Upya na Kupanua.” Akieleza kuhusu msisimuko uliochochewa na hotuba hiyo, mhudhuriaji mmoja aliandika hivi: “Jioni hiyo nilikuwa na pendeleo la kuwa nyuma yake jukwaani, na alipokuwa akieleza kuhusu kazi na kisha kuhusu mipango ya kupanua makao ya Betheli ya Brooklyn na kiwanda, umati huo mkubwa wa wasikilizaji ulipiga makofi mfululizo kwa msisimuko mkubwa sana. Ingawa hungeweza kuona nyuso zao waziwazi ukiwa jukwaani, bila shaka ungeweza kuhisi shangwe waliyokuwa nayo.” Katika kusanyiko la kimataifa lililofanywa huko New York City mwaka wa 1950, wasikilizaji walifurahi kupokea Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, Biblia ya kwanza ya kisasa iliyorudisha jina la Mungu mahali panapofaa katika Neno lake.​—Yer. 16:21.

9 Makusanyiko yaliyotumiwa na Yehova kuwakusanya Mashahidi wake waaminifu baada ya vipindi vya mateso au marufuku yalikuwa pia yenye kugusa moyo sana. Adolf Hitler aliapa kwamba angewaangamiza Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani, lakini mwaka wa 1955, Mashahidi 107,000 walifurika katika kusanyiko lililofanywa huko Nuremberg, kwenye uwanja ambao Hitler alitumia zamani kwa ajili ya magwaride ya kijeshi. Watu wengi waliohudhuria walitokwa na machozi ya shangwe! Kati ya wajumbe 166,518 waliohudhuria makusanyiko matatu yenye kichwa “Ujitoaji wa Kimungu” yaliyofanywa nchini Poland mwaka wa 1989, kulikuwa na idadi kubwa ya wajumbe kutoka katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti na nchi iliyoitwa Czechoslovakia, na kutoka katika nchi nyingine za Ulaya Mashariki. Ilikuwa mara ya kwanza kwa baadhi yao kuhudhuria kusanyiko la watu wa Mungu lililo na watu zaidi ya 15 au 20. Hebu wazia shangwe iliyokuwa katika Kusanyiko la Kimataifa la mwaka wa 1993 lenye kichwa “Ufundishaji wa Kimungu,” huko Kiev, Ukrainia, ambako watu 7,402 walibatizwa. Hiyo ndiyo idadi kubwa zaidi ya Mashahidi wa Yehova kuwahi kubatizwa kwa siku moja.​—Isa. 60:22; Hag. 2:7.

10. Ni makusanyiko gani ya wilaya unayokumbuka zaidi, na kwa nini?

10 Labda kuna makusanyiko ya wilaya au ya kimataifa ambayo unakumbuka zaidi. Je, unakumbuka kusanyiko la kwanza la wilaya ulilohudhuria au labda kubatizwa? Hayo yalikuwa matukio muhimu sana ya kiroho maishani mwako. Usisahau kamwe kumbukumbu hizo zenye thamani!​—Zab. 42:4.

PINDI ZA KAWAIDA ZENYE SHANGWE

11. Mungu alianzisha mpango gani wa sherehe za kawaida za majira katika taifa la kale la Israeli?

11 Kila mwaka, Yehova aliwataka Waisraeli wakusanyike huko Yerusalemu kwa ajili ya sherehe tatu za majira, yaani, Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu, Sherehe ya Majuma (baadaye iliitwa Pentekoste), na Sherehe ya Vibanda. Mungu aliamuru hivi kuhusu sherehe hizo: “Pindi tatu katika mwaka kila mwanamume wa kwako ataonekana mbele za uso wa Bwana wa kweli, Yehova.” (Kut. 23:​14-17) Kwa kuwa walitambua thamani kubwa ya kiroho ya sherehe hizo, vichwa vingi vya familia walihudhuria pamoja na washiriki wote wa familia zao.​—1 Sam. 1:​1-7; Luka 2:​41, 42.

12, 13. Waisraeli wengi walihitaji kufanya jitihada gani ili kuhudhuria sherehe za kila mwaka?

12 Hebu fikiria jitihada ambazo familia ya Mwisraeli ilihitaji kufanya ili kufunga safari hiyo. Kwa mfano, Yosefu na Maria walisafiri umbali wa kilomita 100 hivi kutoka Nazareti kwenda Yerusalemu. Unafikiri ingekuchukua muda gani kufunga safari hiyo, huku ukitembea pamoja na watoto wadogo? Simulizi kuhusu safari ya Yesu ya kwenda Yerusalemu akiwa mvulana linaonyesha kwamba nyakati nyingine watu wa ukoo na marafiki walifunga safari kama hizo wakiwa kikundi. Bila shaka, walifurahi sana kusafiri pamoja na kupika chakula pamoja na kutafuta mahali panapofaa pa kulala katika maeneo wasiyojua. Inaonekana kwamba kulikuwa na usalama wa kutosha kwa sababu mtoto mwenye umri wa miaka 12 kama Yesu alipewa kiasi fulani cha uhuru na wazazi wake. Wazia jinsi ambavyo sherehe hizo hazingeweza kusahaulika, hasa kwa watoto!​—Luka 2:​44-46.

13 Waisraeli walipotawanywa katika sehemu mbalimbali nje ya mipaka ya nchi yao, wale waliohudhuria sherehe hizo walitoka katika mataifa mengi. Wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., Wayahudi na watu waliogeuzwa imani waliothamini sherehe hizo walisafiri kwenda Yerusalemu kutoka katika maeneo kama vile Italia, Libya, Krete, Asia Ndogo, na Mesopotamia.​—Mdo. 2:​5-11; 20:16.

14. Waisraeli walifaidikaje kwa kuhudhuria sherehe za kila mwaka?

14 Kwa Waisraeli waaminifu, jambo muhimu kuhusiana na safari hizo lilikuwa faida za kiroho, yaani, kumwabudu Yehova kwa bidii pamoja na maelfu ya waabudu wenzao waliothamini sherehe hizo. Matokeo yalikuwa nini kwa waliohudhuria? Jibu linapatikana katika maagizo ambayo Yehova aliwapa watu wake kuhusu Sherehe ya Vibanda: “Nawe utashangilia wakati wa sherehe yako, wewe na mwana wako na binti yako na mtumishi wako na kijakazi wako na Mlawi na mkaaji mgeni na mvulana asiye na baba na mjane, walio ndani ya malango yako. Siku saba utamfanyia Yehova Mungu wako sherehe katika mahali ambapo Yehova atapachagua, kwa sababu Yehova Mungu wako atakubariki katika mazao yako yote na katika kila tendo la mkono wako, nawe utakuwa na shangwe kwelikweli.”​—Kum. 16:​14, 15; soma Mathayo 5:3.

KWA NINI TUTHAMINI MAKUSANYIKO YA LEO?

15, 16. Umejidhabihu kwa njia gani ili uhudhurie makusanyiko? Umefaidikaje kwa sababu ya jitihada hizo?

15 Makusanyiko hayo ya zamani yanawawekea watu wa Mungu leo vielelezo bora kama nini! Ingawa kwa karne nyingi mambo mengi yamebadilika, mambo muhimu kuhusiana na makusanyiko hayo hayajabadilika. Katika nyakati za Biblia, wale waliohudhuria makusanyiko walihitaji kujidhabihu ili kuhudhuria. Ndivyo wengi wanavyofanya leo. Hata hivyo, wanafaidika sana wanapojitahidi kuhudhuria. Makusanyiko hayo yalikuwa​—na bado ni​—pindi muhimu za kiroho. Katika makusanyiko hayo tunapata uelewaji na mafundisho tunayohitaji sana ili kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Makusanyiko yanatuchochea kutumia mambo tunayojifunza, yanatusaidia kuepuka matatizo, na yanatutia moyo tuendelee kukazia fikira mambo na utendaji ambao unatuburudisha badala ya kutuchosha.​—Zab. 122:​1-4.

16 Kwa kawaida tunapata shangwe tunapohudhuria makusanyiko. Ripoti kuhusu kusanyiko kubwa lililofanywa mwaka wa 1946 inasema hivi: “Ilisisimua sana kuona maelfu kwa maelfu ya mashahidi wakiwa wamekaa pamoja kwa starehe, na ilisisimua hata zaidi kusikiliza okestra kubwa ikipiga muziki huku umati wa watu ukiimba kwa sauti za juu nyimbo tamu za Ufalme za kumsifu Yehova.” Ripoti hiyo iliongezea hivi: “Wajumbe walijiandikisha katika Idara ya Utumishi wa Kujitolea na kufanya kazi katika idara zote, wakichochewa tu na shangwe ya kuwatumikia mashahidi wenzao.” Je, umewahi kusisimuka vivyo hivyo katika kusanyiko la wilaya au la kimataifa?​—Zab. 110:3; Isa. 42:​10-12.

17. Mipangilio ya makusanyiko imebadilikaje katika nyakati za hivi karibuni?

17 Mipangilio fulani ya makusanyiko imebadilika. Kwa mfano, baadhi ya watu wa Mungu wanakumbuka wakati ambapo makusanyiko yalifanywa kwa siku nane! Kulikuwa na vipindi vya asubuhi, alasiri, na hata vipindi vya jioni. Kwa kawaida programu ilitia ndani kushiriki katika utumishi wa shambani. Sehemu chache zilianza saa tatu asubuhi, na mara nyingi vipindi viliendelea mpaka saa tatu usiku. Wajitoleaji walifanya kazi kwa bidii na kwa saa nyingi ili kutayarisha kiamsha-kinywa, chakula cha mchana, na chakula cha jioni kwa ajili ya wahudhuriaji. Siku hizi makusanyiko yanafanywa kwa siku chache zaidi, na familia na watu mmoja-mmoja wanajibebea vyakula wanapokuja kusanyikoni na hilo linawawezesha kukazia fikira zaidi programu ya chakula cha kiroho.

18, 19. Ni sehemu gani katika programu za makusanyiko unazotazamia kwa hamu, na kwa nini?

18 Wahudhuriaji wengi hutazamia kwa hamu sehemu fulani katika programu ya makusanyiko ya wilaya ambazo zimekuwapo kwa muda mrefu. Kupitia hotuba na vilevile machapisho mapya yanayotolewa katika makusanyiko hayo, tunapata ‘chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa,’ ambacho kinatusaidia kuelewa vizuri zaidi mafundisho na unabii mbalimbali wa Biblia. (Mt. 24:45) Kwa kawaida, vifaa hivyo vipya vinawasaidia watu wanyoofu kuthamini kweli za Kimaandiko. Drama zenye kusisimua zinazotegemea Biblia zinawatia moyo vijana na wazee wachunguze nia yao na kujilinda dhidi ya misongo inayotokana na mawazo ya ulimwengu usiomwogopa Mungu. Hotuba ya ubatizo pia inatupatia sisi sote fursa ya kuchunguza upya mambo tunayotanguliza maishani na pia tunapata shangwe tunapoona wengine wakionyesha wakfu wao kwa Yehova.

19 Naam, makusanyiko yamekuwa sehemu ya ibada safi kwa muda mrefu, na yanawasaidia watu wa Yehova wenye shangwe wamtumikie kwa njia inayofaa katika nyakati ngumu. Makusanyiko hayo yanatuchochea kiroho, yanatupatia nafasi za kukutana na marafiki wapya, yanatusaidia kuthamini ushirika wa ndugu zetu ulimwenguni pote, na ni njia muhimu ambayo Yehova anatumia kuwabariki na kuwatunza watu wake. Bila shaka, kila mmoja wetu anapaswa kupanga vizuri mambo yake ili ahudhurie na kunufaika na kila kipindi katika kila kusanyiko.​—Met. 10:22.