Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Inawezekana Kuwa Mnyoofu Katika Ulimwengu Wenye Ufisadi?

Je, Inawezekana Kuwa Mnyoofu Katika Ulimwengu Wenye Ufisadi?

“Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”​—WAEBRANIA 13:18.

INGAWA tunasukumwa na mwelekeo wetu wa kutenda dhambi, ulimwengu tunamoishi, na Ibilisi, bado tunaweza kushinda uvutano huo wote! Jinsi gani? Kwa kumkaribia Mungu na kufuata kanuni za Neno lake, Biblia, ambazo kwa muda mrefu zimethibitika kuwa zenye faida. Fikiria mifano miwili.

KANUNI YA BIBLIA: “Msiige tabia ya ulimwengu huu.”​—Waroma 12:2, New Jerusalem Bible.

Jambo lililoonwa: Guilherme ni mfanyabiashara mwenye mafanikio nchini Brazili. Anakubali kwamba si rahisi kuwa mnyoofu. Anasema hivi: “Ni rahisi kwa mfanyabiashara kuanza kukosa unyoofu, labda kwa sababu ya mkazo wa kutaka kutimiza malengo ya kampuni au ili afaulu katika ulimwengu wenye ushindani mkali. Watu wengi wanaona kuwa jambo la kawaida kutoa na kupokea hongo. Ni vigumu kuwa mnyoofu ukiwa mwekezaji aliye na majukumu mengi ya kifedha.”

Hata hivyo, Guilherme amefaulu kuendelea kuwa mnyoofu ingawa anakabili mkazo wa kukosa unyoofu. Anasema: “Hata unapofanya biashara ambayo watu huona ni sawa kuvunja sheria, inawezekana kuwa mnyoofu. Lazima uwe na viwango thabiti vya maadili. Biblia imenisaidia kutambua faida za kuwa mnyoofu. Mtu mnyoofu ana dhamiri safi, ana utulivu wa moyoni, na anajiheshimu. Anaweza kuwachochea watu wengine wamwige.”

KANUNI YA BIBLIA: “Watu wanaotamani kuwa na mali kwa haraka haraka huanguka kwenye majaribu na wamenaswa na tamaa nyingi za kipumbavu, zenye kudhuru zinazowazamisha watu katika uharibifu na maangamizi. Kwa maana kupenda fedha ndiyo shina moja la maovu ya kila namna.”—1 Timotheo 6:9, 10, Neno Biblia Takatifu.

Jambo lililoonwa: André ana kampuni ya kuweka mifumo ya usalama. Kati ya watu anaowahudumia ni klabu fulani kubwa ya mpira wa miguu. Wakati fulani, baada ya shindano kubwa, André alienda kwenye ofisi ya usimamizi na kupeleka karatasi ya kudai malipo ya kazi aliyokuwa amefanya. Wafanyakazi katika idara ya fedha bado walikuwa na kazi nyingi ya kuhesabu pesa walizopokea kutokana na tiketi zilizouzwa. Kwa sababu usiku ulikuwa unaingia, msimamizi wa idara hiyo aliwalipa haraka haraka watu waliotoa huduma mbalimbali, kutia ndani André.

“Nilipokuwa njiani nikienda nyumbani, niligundua kwamba yule msimamizi alikuwa amenilipa pesa nyingi zaidi,” anaeleza André. “Nilijua kwamba huenda hangejua ni nani aliyepokea pesa hizo. Lakini nilijua pia mtu huyo angelazimika kulipa pesa hizo zilizopotea! Hivyo niliamua kurudi. Nilifaulu kupita katikati ya mashabiki wengi na nikarudisha pesa hizo. Yule msimamizi alishangazwa sana na tendo hilo. Hakuna mtu aliyewahi kumrudishia pesa.”

“Tendo hilo la unyoofu lilifanya msimamizi huyo aniheshimu,” André anaendelea kusema. “Miaka mingi imepita, na kati ya watu wengi waliokuwa wakitoa huduma mbalimbali katika klabu hiyo, mimi tu ndiye niliyebaki. Ninafurahi kwamba kwa kutumia kanuni za juu za Biblia nimejulikana kuwa na sifa nzuri.”

Inatia moyo kujua kwamba kupitia msaada wa Mungu tunaweza kushinda mkazo wa kujihusisha na ufisadi. Hata hivyo, tukiwa mtu mmoja-mmoja hatuwezi kumaliza ufisadi kabisa. Mambo yanayosababisha ufisadi ni magumu sana hivi kwamba wanadamu hawawezi kuyaondoa wenyewe. Je, hilo linamaanisha kwamba ufisadi hautakwisha kamwe? Makala ya mwisho katika mfululizo huu inaonyesha jibu la Biblia lenye kutia moyo.