Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ufisadi Utakwisha!

Ufisadi Utakwisha!

“Mtumaini Yehova na kuishika njia yake . . . Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.”​—ZABURI 37:34.

JE, WEWE pia, kama watu wengine, unahisi kwamba ufisadi hauwezi kuepukika na kwamba hautawahi kuondolewa kabisa? Inaeleweka ikiwa unahisi hivyo. Katika historia yote, wanadamu wamejaribu mifumo mbalimbali ya serikali. Lakini hawajafaulu kamwe kuondoa ufisadi kabisa. Je, tunaweza kutumaini kwamba kuna wakati ambapo watu wote watashirikiana kwa unyoofu?

Jambo la kufurahisha ni kwamba Biblia inajibu ndiyo! Inasema kuwa hivi karibuni Mungu atachukua hatua na kuondoa ufisadi wote katika dunia yetu. Atafanyaje hivyo? Kupitia Ufalme wake ambao ni serikali ya mbinguni ataibadilisha dunia yetu kabisa. Huo ndio Ufalme ambao Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali uje. Katika ile sala ambayo inajulikana kama Sala ya Bwana au Baba Yetu, Yesu alisema hivi: “Ufalme wako uje. Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani.”​—Mathayo 6:10, Union Version.

Kuhusu Mtawala wa Ufalme huo, Yesu Kristo, Biblia ilitabiri hivi: “Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri.” (Zaburi 72:12-14) Ona kwamba Yesu anaelewa hali ya watu wanaoathiriwa na ufisadi, na atachukua hatua ya kuondoa ukandamizaji! Jambo hilo ni lenye kufariji kwelikweli!

Chini ya utawala wa Mfalme huyo mwenye huruma na nguvu, Ufalme wa Mungu utaondoa kabisa ufisadi duniani. Jinsi gani? Kwa kuondoa mambo matatu yanayosababisha ufisadi.

Uvutano wa Dhambi

Wakati huu, sote tunalazimika kushindana na mwelekeo wetu wa kutenda dhambi, ambao unatuchochea tutende kwa ubinafsi. (Waroma 7:21-23) Hata hivyo, bado kuna watu wazuri wanaotaka kutenda mema. Wanaonyesha imani katika thamani ya damu ya fidia ya Yesu iliyomwagwa, na hivyo wanasamehewa dhambi zao. * (1 Yohana 1:7, 9) Watu kama hao watapata fursa ya kufaidika kutokana na tendo kubwa zaidi la upendo wa Mungu, kama tunavyosoma katika Yohana 3:16: “Kwa maana Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”

Mungu atawafanyia watu waaminifu jambo fulani lenye kustaajabisha. Katika ulimwengu mpya unaokuja, mwishowe ataondoa dhambi zote, hatua kwa hatua atawarudishia wanadamu waaminifu ukamilifu na msimamo wa uadilifu. (Isaya 26:9; 2 Petro 3:13) Kamwe uvutano wa dhambi hautamchochea tena mtu yeyote atende kwa ufisadi. Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, wanadamu waaminifu ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu au ufisadi.’—Waroma 8:20-22.

Uvutano wa Ulimwengu Mwovu Tunamoishi

Inasikitisha kwamba leo watu wengi wanawanyanyasa wenzao kimakusudi. Wanawatendea isivyo haki watu wa hali ya chini na maskini, na wanawachochea wengine watende kwa ufisadi. Biblia inawahimiza hivi watu kama hao: “Mtu mwovu aiache njia yake, na mtu mwenye madhara ayaache mawazo yake.” Watu hao wafisadi wakitubu, Biblia inaahidi kwamba Mungu “atasamehe kwa njia kubwa.”​—Isaya 55:7.

Hata hivyo, Mungu atalazimika kuwaondoa watu wanaokataa kishupavu kubadili mwenendo wao. Kupitia Ufalme wa Mungu, ahadi hii ya Biblia itatimia: “Mtumaini Yehova na kuishika njia yake . . . Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.” * (Zaburi 37:34) Watu waovu wasiotaka kubadilika watakapoondolewa, waabudu waaminifu wa Mungu hawataathiriwa tena na ufisadi.

Uvutano wa Shetani Ibilisi

Shetani ndiye mtenda dhambi sugu zaidi kati ya watenda dhambi wasiotaka kubadilika. Jambo la kupendeza ni kwamba hivi karibuni Yehova atamzuia Shetani asiwachochee wanadamu. Mwishowe, Yehova atamharibu Shetani kabisa. Jitu hilo katili halitaweza tena kuwachochea watu watende kwa ufisadi.

Huenda wazo la kwamba Mungu ataondoa kabisa ufisadi likaonekana kuwa ndoto. Huenda ukajiuliza, ‘Je, kweli Mungu ana uwezo wa kuleta mabadiliko kama hayo? Ikiwa ndivyo, mbona hajachukua hatua?’ Hayo ni maswali mazuri, na Biblia inatoa majibu yenye kuridhisha. * Tunakutia moyo uchunguze mambo ambayo Biblia inasema kuhusu wakati ujao ulio karibu, wakati ambapo ufisadi wote utakuwa umeondolewa.

^ fu. 8 Ili kupata habari zaidi kuhusu jinsi kifo cha Yesu kinavyoweza kutukomboa, ona sura ya 5 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 12 Yehova ni jina la Mungu kama inavyoonyeshwa katika Biblia.