Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nguvu za Neno la Mungu Zasaidia Familia ya Kihindu

Nguvu za Neno la Mungu Zasaidia Familia ya Kihindu

SITASAHAU kamwe siku ya Jumatatu asubuhi Agosti 22, 2005, wakati washiriki wa karibu wa familia yetu walipokusanyika kwa ajili ya kiamsha-kinywa. Maisha yangu yalikuwa hatarini sana, kwa sababu nilikuwa na uvimbe mkubwa kwenye ubongo. Mume wangu, Krishna, alitoa sala, kisha nikazungumza na familia.

Niliwaeleza hivi: “Ninaenda hospitali ili kufanyiwa upasuaji tata, hivyo, nyote lazima mjitayarishe kwa jambo lolote litakalotokea. Ikiwa nitakufa, tayari nimefanya mipango kwa ajili ya mazishi yangu. Ninyi ambao mnamwabudu Yehova, tafadhali msikate tamaa. Na wale ambao bado, nawasihi mkubali kujifunza Biblia na mhudhurie mikutano yetu ya Kikristo. Kwa kufanya hivyo, mnaweza kuwa na imani kama yangu kwamba kutakuwa na ulimwengu mpya ambao waabudu wa kweli wa Mungu wataishi milele wakiwa na afya kamilifu katika dunia paradiso.”

Kabla ya kueleza matokeo ya upasuaji wangu, acheni niwasimulie kuhusu malezi yangu na jinsi nilivyoweza kumjua Mungu wa kweli.

Malezi Yangu Katika Familia ya Kihindu

Familia yetu iliishi kwenye nyumba kubwa iliyojengwa kwa mbao na vyuma kwenye eneo lililoinuka katika jiji la Durban, pwani ya Afrika Kusini. Ili kufika kwenye mlango wa mbele wa nyumba yetu, kwanza tulipanda ngazi 125 kutoka kwenye barabara kuu iliyo chini katika bonde. Ngazi hizo zilielekea moja kwa moja kwenye njia iliyokuwa na miti mingi kila upande ambayo ilitupeleka mpaka kwenye lango la chuma. Upande mmoja wa lango kulikuwa na hekalu la nyanya yangu, ambalo lilikuwa limejazwa picha na sanamu za miungu ya Kihindu. Nyanya aliniambia kwamba mimi nilikuwa “mtoto wa hekaluni” (mandir kī baccā, katika Kihindi) na miungu hiyo tuliyokuwa tukiabudu ndiyo iliyofanya nizaliwe. Mbele ya hekalu hilo kulikuwa na ngazi zilizokuwa zimepakwa rangi nyekundu, ambazo zilifika mpaka kwenye mlango wa mbele. Nyumba hiyo ilikuwa kubwa, yenye kijia kirefu kilichokuwa katikati ya nyumba, sehemu kubwa ya kupikia yenye jiko la makaa ya mawe, vyumba saba vya kulala, na chumba kimoja cha ziada kilichokuwa kando ya jengo hilo. Katika nyumba hiyo tuliishi watu  27, kutia ndani nyanya na babu yangu, baba yangu, ndugu zake wadogo watatu, dada yake mdogo, na familia zao.

Haikuwa rahisi kutunza familia kubwa kama hiyo. Hata hivyo, kuishi pamoja kulituunganisha na kutufanya tuwe na kumbukumbu nyingi zenye furaha. Binti-wakwe wanne, kutia ndani mama yangu anayeitwa Gargee Devi, walifanya kazi za nyumbani pamoja. Walikuwa na zamu ya kupika na kufanya usafi. Babu yangu ndiye aliyekuwa kichwa cha familia, na alinunua chakula kwa ajili ya familia yote. Kila Jumatano babu na nyanya wangeenda sokoni kununua nyama, matunda, na mboga za majani ambazo tungetumia juma zima. Tungekaa chini ya kivuli cha mti wa msonobari uliokuwa kwenye ukingo wa bonde na kuwasubiri warudi kutoka sokoni. Mara tu tulipowaona wakishuka kutoka kwenye basi wakiwa wamebeba vikapu vikubwa, tulishuka mbio ngazi 125 na kuwasaidia kupeleka nyumbani vitu walivyonunua.

Katika bustani yetu, kulikuwa na mti mrefu wa mtende ambao ndege wa jamii ya kwezi walikuwa wamejenga viota vyao. Tungewaona wakipaa huku na huku na kuwasikia wakiimba. Nyanya yangu angeketi kwenye ngazi zilizokuwa katika mlango wa mbele na kutusimulia hadithi, kana kwamba alikuwa akifasiri sauti za ndege hao. Bado nakumbuka mambo mengi mazuri kuhusiana na maisha yetu! Tulicheka, tulilia, tulicheza, tulitabasamu, na tukashirikiana, kwa kweli tulifurahia kuishi pamoja kama familia moja kubwa. Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba, hapo ndipo mahali tulipoanza kujifunza kumhusu Muumba wetu, Yehova, na Mwana wake, Yesu Kristo.

Kabla ya kujifunza kumhusu Yehova, ibada yetu ya Kihindu ilitia ndani desturi nyingi za kila siku. Pia, tulikuwa na sherehe kubwa za mara kwa mara. Katika sherehe hizo tungealika watu ili kuabudu miungu tofauti-tofauti ya kike na ya kiume. Katika baadhi ya sherehe hizo, nyanya yangu angepata njozi na kuanza kuwasiliana na pepo, na ilipofika saa sita kamili usiku, dhabihu za wanyama zingetolewa ili kuwatuliza pepo hao. Pia, babu yangu alijulikana sana katika jamii kwa sababu ya michango yake ya hiari ya kusaidia ujenzi na kuendesha shule za umma na mahekalu ya Kihindu.

Jinsi Tulivyopata Ukweli Kumhusu Yehova

Katika mwaka wa 1972, babu yangu aliugua na kufa. Miezi michache baadaye, shangazi yangu mmoja aliyeitwa Indervathey, ambaye pia alijulikana kama Jane, alikubali magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kutoka kwa Mashahidi wawili wa Yehova. Alijiona kuwa mwenye hatia kwa sababu hakuwakaribisha Mashahidi hao ndani ya nyumba yetu kwa ajili ya mazungumzo. Sikuzote tuliwafukuza Mashahidi. Lakini wakati mwingine Mashahidi walipobisha mlango, shangazi yangu aliwakaribisha ndani na akazungumza nao juu ya tatizo la ndoa lililomhusu mjomba wangu ambaye alikuwa mlevi. Majirani zetu na watu wa ukoo walimtia moyo shangazi yangu amtaliki mjomba. Mashahidi walimweleza maoni ya Mungu kuhusu ndoa. (Mathayo 19:6) Shangazi yangu aliguswa moyo na ushauri wa Biblia pamoja na ahadi ya kuwa na maisha bora wakati ujao hapa duniani. * Alibadili maoni yake kuhusu kuachana na mjomba wangu, na akaanza kujifunza Biblia kwa ukawaida pamoja na Mashahidi. Alipokuwa sebuleni akijifunza Biblia, binti wakwe wengine walisikiliza mazungumzo hayo kutoka vyumbani mwao.

Hatimaye, binti-wakwe wote walijiunga katika funzo la Biblia. Shangazi Jane alitueleza mambo aliyokuwa akijifunza na mara kwa mara alitusomea na kutuelezea hadithi kutoka katika kitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu. * Wajomba zangu walipojua kwamba shangazi zangu walikuwa wakijifunza Biblia, walianza kutupinga. Mjombangu mmoja alichukua machapisho yetu yote, kutia ndani Biblia, na kuyachoma moto. Walitutukana na kututendea vibaya kwa sababu ya kuhudhuria mikutano. Ni babangu tu ambaye hakuonyesha mtazamo kama huo; kamwe hakutuzuia tusijifunze kumhusu Yehova. Binti-wakwe wote wanne waliendelea kuhudhuria mikutano na kukuza upendo wao kwa Yehova Mungu.

Katika mwaka wa 1974, shangazi yangu Jane alibatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na muda mfupi baadaye mama yangu na shangazi zangu wengine walibatizwa. Baada ya muda, nyanya yangu aliacha kufuata desturi za dini ya Kihindu. Kwa miaka mingi niliwafuata, na kuhudhuria mikutano yote ya Kikristo. Kisha, kwenye kusanyiko kubwa la Mashahidi wa Yehova, Shahidi anayeitwa Shameela Rampersad, aliniuliza, “Utabatizwa lini?” Nilimjibu, “Siwezi kwa sababu hakuna mtu yeyote ambaye amewahi kunifundisha Biblia.” Alijitolea kunifundisha. Kwenye kusanyiko lililofuata, Desemba 16, 1977, nilibatizwa. Hatimaye, 18 kati ya washiriki 27 wa familia yetu tulioishi pamoja, walibatizwa. Lakini kufikia wakati nilipokuwa nikifanyiwa upasuaji, bado baba yangu, Sonny Deva, alikuwa mfuasi wa dini ya Kihindu.

“Msihangaike Juu ya Kitu Chochote”

Maneno yaliyoandikwa katika Wafilipi 4:6, 7 yamekuwa msaada mkubwa kwangu, hasa baada ya kugunduliwa kwamba nilikuwa na uvimbe mkubwa kwenye ubongo. Mistari hiyo inasema: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” Ni vigumu kutokuwa na ‘mahangaiko juu ya kitu chochote,’ hasa ikiwa umeambiwa kwamba utakufa wakati wowote. Mwanzoni nililia tu, kisha nikaanza kusali kwa Yehova. Tangu wakati huo na kuendelea, nimejionea “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”

Yehova Mungu aliushika mkono wangu wa kuume kwa njia ya mfano, na kwa kweli nilihisi kuwa aliniongoza kipindi hicho chote. (Isaya 41:13) Alinisaidia niwaeleze madaktari kwa ujasiri azimio langu la kutii amri ya Biblia ya kujiepusha na damu. (Matendo 15:28, 29) Matokeo ni kwamba, madaktari na wauguzi walikubali kunifanyia upasuaji bila kutiwa damu mishipani. Baadaye, daktari aliyenifanyia upasuaji alieleza kwamba upasuaji huo ulifanikiwa na uvimbe wote ulikuwa umeondolewa. Pia, alisema kwamba hajawahi kuona mgonjwa akipona haraka hivyo baada ya kufanyiwa upasuaji mkubwa kama huo wa ubongo.

Majuma matatu baadaye, niliongoza funzo la Biblia nikiwa kwenye kitanda changu. Mwishoni mwa juma la saba, nilianza tena kuendesha gari, nilienda kuhubiri, na nikaanza tena kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Nilithamini sana msaada kutoka kwa ndugu na dada zangu Wakristo waliofanya kazi nami bega kwa bega ya kueneza injili. Walihakikisha sikuwa peke yangu na kwamba ningerudi nyumbani nikiwa salama. Ninaamini kwamba kusikiliza rekodi za Biblia na kukazia fikira mambo ya kiroho katika maisha yangu kulinisaidia nipone haraka.

Pia, baada ya kufanyiwa upasuaji nilifurahi kujua kwamba, baba yangu alikubali kujifunza Biblia na Mashahidi. Alibatizwa akiwa na umri wa miaka 73, na sasa anamtumikia Yehova kwa bidii. Zaidi ya washiriki 40 wa familia yetu sasa wamejiunga nasi katika kumwabudu Yehova. Ingawa jicho langu la kushoto lina kasoro na fuvu la kichwa changu limeunganishwa kwa chuma, ninatazamia wakati ujao Yehova atakapofanya “vitu vyote kuwa vipya” katika dunia Paradiso itakayokuja.—Ufunuo 21:3-5.

Nimebarikiwa kuwa na mume mwenye upendo, anayetumika kama mwangalizi Mkristo, na binti mrembo, Clerista, anayenisaidia ninapoendelea kutumika nikiwa mhubiri wa wakati wote. Yehova Mungu amebariki sana huduma yangu. Kufikia sasa, nimewasaidia wanafunzi wangu wa Biblia kujionea nguvu za Neno la Mungu katika maisha yao. Zaidi ya 30 kati yao sasa wamejiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa.

Nikiwa na moyo uliojaa tumaini, ninatazamia wakati ujao ambapo Yehova Mungu atatukomboa kutoka katika mfumo huu wa mambo wenye maumivu na kutuingiza katika paradiso duniani.

^ fu. 12 Kwa habari zaidi kuhusu kusudi la Mungu kwa dunia, Ona sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 13 Kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.