Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Mwanamuke Bora Sana’

‘Mwanamuke Bora Sana’

Uige Imani Yao

‘Mwanamuke Bora Sana’

RUTHU alipiga magoti karibu na marundo ya shayiri ambayo alikuwa ameokota muchana muzima. Huko Bethlehemu, kulianza kuwa giza katika mashamba na wafanyakazi wengi walikuwa njiani kuelekea mulango wa jiji lililokuwa juu ya kilima karibu na mashamba. Tunaweza kuwazia kama Ruthu alikuwa mwenye kuchoka sana kwa sababu ya kazi ngumu aliyofanya tangu asubuhi mupaka mangaribi. Ijapokuwa muchoko aliendelea kutumika, alitumia muti kupiga​-piga marundo yake ya shayiri ili mbegu zitoke. Hata hivyo, hiyo ilikuwa siku nzuri kwake kuliko alivyowazia.

Je, mambo yalianza kuwa mazuri mwishowe kwa mujane huyo kijana? Alikuwa ameamua kuenda na Naomi, mama mukwe wake, na aliahidi kubaki naye na kumufanya Yehova, Mungu wa Naomi, kuwa Mungu wake. Wajane hao wawili waliofiwa walitoka Moabu na kuja huko Bethlehemu. Bila kukawia, Ruthu mwanamuke Mumoabu, akajifunza kama Sheria ya Yehova ilikuwa na mipango yenye kufaa iliyowafanya masikini na wageni katika Israeli waheshimiwe. * Na sasa alipata kuona kama watu fulani wa Yehova walioishi chini ya Sheria na kuongozwa nayo walikuwa na mwenendo muzuri na walionyesha wema, jambo hilo lilituliza sana moyo wake.

Mumoja kati ya watu hao aliitwa Boazi, mwanaume mwenye kuzeeka aliyekuwa tajiri sana ambaye Ruthu alikuwa anaokota masalio katika mashamba yake. Boazi alimuhangaikia Ruthu kama baba. Ruthu alifurahi sana moyoni mwake alipowaza juu ya maneno mazuri ambayo Boazi alimuambia ili kumusifu, kwa sababu alimushugulikia Naomi aliyezeeka na kwa sababu aliamua kutafuta kimbilio kwa Yehova, Mungu wa kweli.​—Ruthu 2:11-13.

Lakini, labda Ruthu alijiuliza maulizo mengi juu ya maisha yake wakati ujao. Kwa sababu alikuwa mugeni masikini ambaye hakuwa na bwana wala mutoto, namna gani angepata feza za kushugulikia mahitaji yake na ya Naomi katika miaka ijayo? Je, kuokota masalio kungetimiza mahitaji yao yote? Na tena, atakapozeeka, ni nani angemushugulikia? Ikiwa mahangaiko hayo yangeulemea moyo wake, hilo lingekuwa jambo lenye kueleweka. Kwa sababu leo ni vigumu kupata feza, watu wengi wana mahangaiko kama hayo. Tutapata mambo mengi ya kuiga juu ya Ruthu kwa kujifunza namna imani yake ilivyomusaidia kushinda mahangaiko hayo.

Ni Nani Wanaofanyiza Familia?

Ruthu alipomaliza kupiga-piga mbegu zake na kuzikusanya zote, alitambua kama alikuwa ameokota karibu efa moja ya shayiri, inawezekana muzigo wake ulikuwa na kilo 14. Kisha jua kutua, labda aliufunga muzigo huo ndani ya vazi, akaunyanyua na kuubeba juu ya kichwa chake na kurudi Bethlehemu.​—Ruthu 2:17.

Naomi alifurahi sana alipomuona binti wake mukwe, na inawezekana alishituka sana kumuona na muzigo muzito wa shayiri. Ruthu alileta pia chakula chake kilichobaki wakati Boazi aliwapatia wafanyakazi chakula cha muchana, na wote wawili wakachangia chakula hicho. Naomi akamuuliza: “Uliokota masalio wapi leo, nawe ulifanya kazi wapi? Yule aliyekuona na abarikiwe.” (Ruthu 2:19) Naomi alikuwa na utambuzi; alipoona Ruthu analeta muzigo muzito, alitambua mara moja kama kunapaswa kuwa mutu fulani aliyependezwa na mujane huyo kijana na akamuonyesha wema.

Wote wawili wakaanza kuzungumuza, na Ruthu akamuambia Naomi juu ya wema wa Boazi. Hilo lilimugusa Naomi moyo, kwa hiyo akasema hivi: ‘Abarikiwe huyo na Yehova, ambaye hakuacha kuonyesha fazili zake zenye upendo kwa walio hai na wafu.’ (Ruthu 2:19, 20) Aliona kama wema wa Boazi ulitoka kwa Yehova, kwa sababu Yehova ndiye anawachochea watumishi wake wawe wakarimu na anawaahidi kama atawabiriki kwa wema wanaoonyesha. *​—Methali 19:17.

Naomi alimusihi Ruthu akubali kuendelea kuokota masalio katika mashamba ya Boazi na kubaki karibu na wanawake vijana wa nyumba ya Boazi ili wanaume waliokuwa wanavuna wasimuchokoze. Ruthu alikubali shauri hilo. Tena, ‘aliendelea kukaa na mama​-mukwe wake.’ (Ruthu 2:22, 23) Maneno hayo yanatuonyesha tena sifa kubwa ya Ruthu​—upendo mushikamanifu. Mufano wake unatuchochea tujiulize ikiwa tunashikamana na watu wa familia zetu kwa kuwategemeza kwa ushikamanifu na kuwasaidia wanapohitaji musaada. Yehova hajakosa hata siku moja kupendezwa na sifa hiyo ya upendo mushikamanifu.

Je, Naomi na Ruthu, watu wawili tu, walifanyiza familia? Mahali fulani watu wanasema kama ili familia iwe ya kweli kabisa, kunapaswa kuwa bwana, bibi, mutoto mwanaume, mutoto mwanamuke, tate (nkambo) mwanaume na tate mwanamuke, na watu wengine. Lakini mufano wa Naomi na Ruthu unatukumbusha kama familia za watumishi wa Yehova zinaweza kushikamana na kuwa na shauku, wema, na upendo hata kama hazina washiriki wote. Je, wewe unapendezwa na familia yako? Yesu aliwakumbusha wafuasi wake kama kutaniko la Kikristo linaweza kuwa familia hata kwa wale wasio na familia.​—Marko 10:29, 30.

‘Yeye Ni Mumoja wa Wakombozi Wetu’

Ruthu aliendelea kuokota masalio katika mashamba ya Boazi kuanzia mavuno ya shayiri (inawezekana yalifanywa katika Mwezi wa 4) mupaka mavuno ya ngano (inawezekana yalifanywa katika Mwezi wa 6). Siku zilipopita, Naomi aliendelea kuwaza juu ya mambo ambayo angeweza kufanya kwa ajili ya binti mukwe wake mupendwa. Kisha kutoka Moabu, Naomi alikuwa hakika kama hawezi kumusaidia Ruthu kupata bwana mwengine. (Ruthu 1:11-13) Lakini sasa Naomi alianza kupata mawazo mengine. Alimukaribia Ruthu na kusema: ‘Binti yangu, je, sipaswi kukutafutia mahali pa kupumuzikia?’ (Ruthu 3:1) Katika siku hizo wazazi walikuwa na desturi ya kuwatafutia watoto wao bwana ao bibi, na Ruthu alikuwa amekuwa kama mutoto wa Naomi. Naomi alipenda Ruthu apate ‘mahali pa kupumuzikia,’ ni kusema usalama na ulinzi ambao mwanamuke anapata katika nyumba ya bwana yake. Lakini, Naomi angefanya nini?

Ruthu alipozungumuza juu ya Boazi kwa mara ya kwanza, Naomi alisema hivi: ‘Mwanaume huyo ni wa jamaa yetu. Yeye ni mumoja wa wakombozi wetu.’ (Ruthu 2:20) Hilo lilimaanisha nini? Sheria ambayo Mungu aliwapatia Waisraeli ilikuwa na mipango yenye upendo kwa ajili ya familia ambazo zilikuwa zinapambana na nyakati ngumu kwa sababu ya umasikini ao kufiwa. Mwanamuke aliyefiwa na bwana bila kuzaa watoto alivunjika moyo sana kwa sababu jina la bwana yake na mali yake vingepotea na havingejulikana kwa vizazi ambavyo vingefuata. Lakini, Sheria ya Mungu ilimuruhusu ndugu ya bwana kuoa mujane huyo ili aweze kuzaa muriti ambaye angeendeleza jina la bwana yake na kuchunga mali ya familia. *​—Kumbukumbu la Torati 25:5-7.

Naomi alieleza namna alivyopanga kufanya ndoa hiyo ya Ruthu. Tunaweza kuwazia kama mwanamuke huyo kijana alishangaa sana mama mukwe wake alipomuelezea mipango hiyo. Sheria ya Mungu kwa Waisraeli ilikuwa mupya kabisa kwa Ruthu; na alikuwa hajajua desturi nyingi za Sheria hiyo. Hata hivyo, kwa sababu alimuheshimu Naomi sana, alisikiliza kwa uangalifu kila neno alilomuambia. Labda jambo ambalo Naomi alimushauria Ruthu afanye lilikuwa ngumu ao la haya, na hata la kumushushia heshima; hata hivyo, Ruthu alilikubali. Alisema kwa upole hivi: “Yote ambayo umeniambia nitafanya.”​—Ruthu 3:5.

Wakati fulani ni vigumu kwa vijana kusikiliza mashauri ya watu waliozeeka na wenye uzoefu mwingi. Ni vyepesi kuwaza kama watu waliozeeka hawaelewe kabisa hali ngumu na matatizo ambayo vijana wanapambana nayo. Mufano wa unyenyekevu wa Ruthu unatukumbusha kama kusikiliza hekima ya watu waliozeeka wanaotupenda na wanaotutakia mema kunaweza kutuletea baraka. Lakini, Naomi alimushauria Ruthu afanye nini, na je, kweli Ruthu alibarikiwa kwa kufanya hivyo?

Ruthu Kwenye Uwanja wa Kupigia-pigia Nafaka

Mangaribi hiyo, Ruthu alienda kwenye uwanja wa kupigia​-pigia nafaka​—mahali penye udongo mugumu ambapo wavunaji walikuwa wanapeleka nafaka zao ili kuzipiga​-piga na kuzipepeta (kuzipepula). Mara nyingi, uwanja huo ulikuwa kwenye kilima ao juu ya kilima, mahali ambapo upepo ulikuwa mukali mangaribi. Ili kuondoa uchafu katika mbegu, wafanyakazi walitumia chombo kikubwa kinachofanana na kanya ao sepetu (bêche): walitupa hewani mbegu zenye kuchangana na uchafu, upepo ulipeperusha uchafu na mbegu zilianguka kwenye udongo.

Ruthu alijificha mahali fulani ili kungojea kazi imalizike mangaribi. Boazi alisimamia kazi ya kupepeta mbegu zake, mbegu zenye kupepetwa zilifikia kuwa marundo makubwa. Alipomaliza kula kwa hamu nyingi, alilala kwenye rundo moja la mbegu. Watu walizoea kufanya hivyo katika siku hizo, labda ili kulinda mavuno yao yasiibwe. Ruthu aliona mahali ambapo Boazi alilala. Huo ndio ulikuwa wakati wa kutumikisha shauri la Naomi.

Ruthu alimukaribia Boazi, moyo wake ukiwa wenye kupiga-piga. Kisha kuhakikisha kama Boazi alikuwa amelala sana, alienda kwenye miguu yake, akaifunua na kulala pembeni, kama Naomi alivyomuambia. Kisha akangojea. Wakati ukapita, lakini Boazi akaendelea kulala. Mwishowe, akaanza kujitikisa katikati ya usiku. Kwa sababu ya baridi alianza kutetemeka, kwa hiyo akaamuka ili kufunika tena miguu yake. Ndipo akatambua kama mutu fulani alikuwa pale. Biblia inasema hivi: ‘Tazama! mwanamuke alikuwa amelala miguuni pake!’​—Ruthu 3:8.

Boazi akamuuliza hivi: “Wewe ni nani?” Kwa sauti yenye kutetemeka, Ruthu akamujibu hivi: ‘Mimi ni Ruthu kijakazi wako, basi mufunike kijakazi wako kwa upindo wa nguo yako, kwa maana wewe ni mukombozi.’ (Ruthu 3:9) Watu fulani wanaofasiria Biblia wanawaza kama mambo ambayo Ruthu alifanya na maneno aliyomuambia Boazi yalikuwa ya kumushawishi alale naye, lakini wanasahau mambo haya mawili yanayofuata. Jambo la kwanza, Ruthu alitenda kulingana na desturi za siku hizo, ambazo tunaona kuwa hazifae leo. Kwa hiyo, ni kosa kumuhukumu Ruthu kulingana na namna tunavyoona mambo leo; mwanamuke akifanya hivyo leo ataonwa kuwa kahaba. Jambo la pili, jibu la Boazi lilionyesha waziwazi kama aliona mwenendo wa Ruthu kuwa muzuri na wenye kusifika sana.

Sauti ya Boazi yenye upole na yenye kutuliza, ilimufariji Ruthu sana. Alisema hivi: ‘Yehova na akubariki, binti yangu. Umeonyesha fazili zako zenye upendo kwa njia bora zaidi mara hii ya mwisho kuliko mara ya kwanza. Haukuwafuata vijana, wawe ni wa hali ya chini ao matajiri.’ (Ruthu 3:10) Boazi alipotaja “mara ya kwanza” alipenda kuzungumuzia upendo mushikamanifu ambao Ruthu alimuonyesha Naomi kwa kurudi naye huko Israeli na kwa kumushugulikia. “Mara ya mwisho” ilimaanisha jambo alilofanya kwa kumufuata Boazi kuliko kuwafuata wanaume vijana. Boazi aliona kama mwanamuke kijana kama Ruthu angeweza kutafuta bwana aliye kijana, awe masikini ao tajiri. Kuliko kufanya hivyo, alitaka kufanya mema kwa Naomi na kwa bwana yake aliyekufa, ili kumuendelezea jina katika inchi yake. Ni wazi kama mwanamuke huyo kijana hakuwa mwenye kutafuta faida yake mwenyewe, ndiyo maana Boazi alivutiwa naye.

Boazi aliendelea kusema: ‘Basi sasa, binti yangu, usiogope. Yote utakayosema nitakufanyia, kwa maana kila mutu aliye katika lango la watu wangu anajua kwamba wewe ni mwanamuke bora sana.’ (Ruthu 3:11) Wazo la kumuoa Ruthu lilimupendeza Boazi sana; inawezekana hakushangaa sana alipoombwa amukomboe. Hata hivyo, Boazi hakutaka kutenda tu kulingana na mapendezi yake mwenyewe kwa sababu alikuwa mwanaume mwenye haki. Boazi alimuambia Ruthu kama kulikuwa mukombozi mwengine aliyekuwa wa jamaa ya karibu zaidi ya Elimeleki, marehemu bwana ya Naomi; alisema kama atamuambia kwanza mwanaume huyo ikiwa atapenda kumuoa.

Kwa sababu ilikuwa ingali usiku sana, Boazi alimusihi Ruthu alale tena ili kuondoka asubuhi sana bila kuonwa na mutu yeyote. Hakupenda sifa yake mwenyewe na sifa ya Ruthu iharibiwe, kwa sababu watu wangewaza kama walifanya jambo fulani mbaya. Ruthu alilala tena karibu na miguu ya Boazi, inawezekana alikuwa sasa mwenye kutulia kwa sababu Boazi alikuwa amemujibu vizuri. Kwa hiyo, asubuhi ilipokaribia, Boazi alijaza vazi lake kwa shayiri nyingi, na ndipo Ruthu akaondoka kuenda Bethlehemu.

Ruthu alifurahi sana alipokuwa akiwaza juu ya jambo ambalo Boazi alimuambia—kama alijulikana kuwa ‘mwanamuke bora sana.’ Alijulikana hivyo kwa sababu ya tamaa yake ya kutaka kumujua Yehova na kumutumikia. Pia, alikuwa ameonyesha upendo mwingi kwa Naomi na kwa watu wake, kwa sababu bila kulazimishwa, alijipatanisha na desturi ambazo hakujua katika inchi yake. Ikiwa tunaiga imani ya Ruthu, tutawaheshimu wengine na kuheshimu desturi zao. Tukifanya hivyo, sisi pia tunaweza kujulikana kuwa watu wazuri.

Ruthu Anapata Mahali pa Kupumuzikia

Ruthu alipofika nyumbani, Naomi alimuuliza hivi: “Wewe ni nani, binti yangu?” Inawezekana Naomi alimuuliza hivyo kwa sababu kulikuwa giza na hakumuona vizuri, lakini Naomi alipenda pia kujua ikiwa Ruthu alibaki mujane ao ikiwa mukombozi wake alikubali kumuoa. Bila kukawia Ruthu alimuelezea mama mukwe wake mambo yote yaliyopitika kati yake na Boazi. Alimutolea pia zawadi ya shayiri ambayo Boazi alimutumia. *​—Ruthu 3:16, 17.

Kwa hekima, Naomi alimusihi Ruthu abaki nyumbani siku hiyo kuliko kuenda kuokota masalio katika mashamba. Alimuhakikishia Ruthu hivi: ‘Mwanaume huyo hatapumuzika mupaka amalize jambo hilo leo.’​—Ruthu 3:18.

Naomi alielewa mawazo ya Boazi. Ileile siku Boazi alienda kwenye mulango wa muji, ambapo wazee wa muji walizoea kukutana, na akangojea mupaka yule mutu wa jamaa ya karibu alipopita. Mbele ya mashahidi, Boazi alimuuliza mutu huyo ikiwa atapenda kukomboa lile shamba la ndugu yao Elimeleki aliyekufa na kumuoa Ruthu. Lakini, mutu huyo akakataa, akaonyesha kama akifanya hivyo atapoteza uriti wake mwenyewe. Kisha, mbele ya mashahidi hao waliokusanyika kwenye mulango wa muji, Boazi alionyesha kama yeye atakuwa mukombozi, kwa kununua shamba la marehemu Elimeleki, bwana ya Naomi, na kumuoa Ruthu, bibi ya marehemu Maloni, mutoto wa Elimeleki. Boazi alionyesha tumaini alilokuwa nalo, kwa kusema kama akifanya hivyo ‘atamuinulia jina mwanaume huyo katika uriti wake.’ (Ruthu 4:1-10) Kwa kweli, Boazi alikuwa mutu mwenye haki na asiyetafuta faida zake mwenyewe.

Boazi akamuoa Ruthu. Kisha hapo, Biblia inasema kama ‘Yehova akamuwezesha kupata mimba naye akazaa mwana.’ Wanawake wa huko Bethlehemu walimubariki Naomi na kumusifu Ruthu kwa sababu alikuwa bora kwa Naomi kuliko watoto saba. Mwishowe, mutoto wa Ruthu akawa tate ya Mufalme Daudi. (Ruthu 4:11-22) Na Daudi akaja kuwa katika vizazi ambamo Yesu alizaliwa.​—Mathayo 1:1. *

Ruthu naye alibarikiwa kama Naomi, ambaye alimusaidia kumulea mutoto kama mutoto wake mwenyewe. Maisha ya wanawake hao wawili yanatukumbusha kama Yehova Mungu anapendezwa na wale wote wanaomutumikia kwa ushikamanifu pamoja na watu wake na kufanya kazi kwa bidii ili kushugulikia familia zao. Yehova hatakosa kuwabariki watu waaminifu wanaojikaza kuwa watu wazuri, kama Ruthu.

[Maelezo ya chini]

^ Kama Naomi alivyosema, Yehova anaonyesha wema wake kwa watu wanaoishi na hata kwa wale waliokufa. Naomi alikuwa amefiwa na bwana yake na watoto wake wote wawili. Ruthu pia alikuwa amefiwa na bwana yake. Bila shaka, wanaume hao watatu walipendwa sana na wanawake hao. Wema wowote ambao Naomi na Ruthu walionyeshwa, ni kama vile ulionyeshwa kwa wanaume hao ambao walikuwa wamekufa kwa sababu walipenda wanawake hao washugulikiwe.

^ Sheria ya Mungu ilionyesha kama ndugu ya mwanaume aliyekufa ndiye aliyekuwa na haki ya kumuoa mujane huyo ao wanaume wengine wa jamaa yake ya karibu, ndivyo ilivyokuwa pia juu ya haki ya kuriti.​—Hesabu 27:5-11.

^ Boazi alimupatia Ruthu vipimo sita vya shayiri ambavyo uzito haujulikane​—Labda alifanya hivyo kwa sababu kulikuwa siku ya Sabato kisha siku sita za kazi, kisha kufanya kazi ya nguvu kwa siku sita akiwa mujane, siku ya Ruthu ya “kupumuzika” ilikuwa inakaribia, pumuziko ambalo angetolewa na nyumba ya bwana yake. Tena, labda ni vipimo sita tu vya shayiri ndivyo Ruthu angeweza kubeba kichwani.

^ Ruthu ni mumoja kati ya wanawake ambao Biblia inaonyesha kama walikuwa katika vizazi vya Yesu. Mwanamuke mwengine ni Rahabu, mama ya Boazi. (Mathayo 1:3, 5, 6) Kama Ruthu, yeye pia hakuwa Muisraeli.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Ruthu alitumika kwa bidii ili kujilisha na kumulisha Naomi

[Picha katika ukurasa wa 21]

Ruthu na Naomi walisaidiana na kutiana moyo

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ruthu hakuwa mutu mwenye kutafuta faida yake mwenyewe na hakuwa na nia mbaya alipomuendea Boazi

[Picha katika ukurasa wa 24]

Yehova alimubariki Ruthu kwa kumupa pendeleo la kuwa katika vizazi ambamo Masiya alizaliwa