Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, ni lazima ufunge ndoa ili uwe na furaha?

Je, ni lazima ufunge ndoa ili uwe na furaha?

Je, Biblia inafundisha kwamba ni lazima ufunge ndoa ili uridhike na uwe na furaha? Unapoangalia kijuu-juu, huenda ikaonekana kwamba Neno la Mungu linaunga mkono jambo hilo. Jinsi gani?

Kulingana na simulizi la kitabu cha Mwanzo, Mungu aliona kwamba haikuwa “vema” kwa mwanamume wa kwanza Adamu kukaa peke yake. Hivyo Mungu akamuumba Hawa ili awe “kikamilisho” cha Adamu. (Mwanzo 2:18) Neno “kikamilisho” linamaanisha kitu kinachofanya kitu kingine kiwe kamili. Kutokana na simulizi hilo, tunaweza kukata kauli kwamba mtu hawezi kuwa kamili ikiwa hajafunga ndoa. Kwa kuongezea, masimulizi mengi ya Biblia huonyesha ndoa kuwa chanzo cha baraka na shangwe. Mfano mmoja ni hadithi ya Ruthu.

Hata hivyo, je, ni kweli masimulizi hayo yanakusudiwa kutufundisha kwamba leo Wakristo hawawezi kuwa na furaha, kuridhika, au kuwa kamili isipokuwa wawe wamefunga ndoa na wapate watoto? Hiyo si kweli. Kati ya wanadamu wote, Yesu Kristo ndiye mwanadamu ambaye alikuwa kamili na mwenye kuridhika zaidi. Hata hivyo, alibaki mseja mpaka kifo. Yesu, mwanamume mwenye hekima zaidi ambaye aliwahi kuishi, alikuwa mfano mkamilifu wa “Mungu mwenye furaha,” Yehova. (1 Timotheo 1:11; Yohana 14:9) Yesu alifunua mambo yanayoweza kuleta furaha, au baraka, katika ulimwengu huu. (Mathayo 5:1-12) Hakutaja ndoa katika orodha hiyo.

Hivyo basi, je, Biblia inajipinga yenyewe kuhusiana na jambo hilo? Sivyo hata kidogo. Maoni yetu kuhusu ndoa yanapaswa kutegemea kusudi la Mungu. Ingawa alikusudia ndoa iwe chanzo cha shangwe, urafiki wa karibu, na faraja kifungo hicho kimetimiza pia daraka muhimu katika kutimizwa kwa sehemu fulani za kusudi lake. Kwa mfano, Mungu alikusudia Adamu na Hawa ‘wazae, wawe wengi, na wajaze dunia.’ (Mwanzo 1:28) Adamu wala Hawa hangeweza kutimiza kusudi hilo akiwa peke yake. Badala yake, kila mmoja alimhitaji mwenzake na walikamilishana kwa njia ya kipekee.

Vivyo hivyo, Yehova alikuwa na makusudi ya kipekee kuhusiana na ndoa na maisha ya familia alipokuwa akishughulika na taifa la kidunia la Israeli. Alitaka taifa lake liwe na watu wengi ili lisishindwe na adui zao. Pia, alikusudia kwamba kabila la Yuda litokeze Masihi, ambaye angewakomboa wanadamu waaminifu kutoka kwa matokeo ya dhambi na kifo. (Mwanzo 49:10) Hivyo, wanawake waaminifu Waisraeli, waliliona kuwa pendeleo la pekee kuolewa na kuzaa watoto na kama chanzo cha aibu na huzuni ikiwa hawangeolewa na kuzaa.

Namna gani leo? Je, agizo la Mungu la ‘kuijaza dunia’ linawalazimisha Wakristo wanaoishi katika ulimwengu huu uliojaa watu wafunge ndoa na kuzaa watoto? Hapana. (Mathayo 19:10-12) Leo, Mungu hahitaji tena kulinda na kuhakikisha ukoo wa Masihi wala kulinda taifa ambalo litatokeza Mkombozi. Hivyo basi, Wakristo wanapaswa kuonaje ndoa na useja?

Kwa kweli, useja na ndoa unaweza kuonwa kuwa zawadi kutoka kwa Mungu. Kama unavyojua, zawadi ambayo inaweza kumfaa mtu fulani huenda isimfae mwingine. Ndoa ni mpango mtakatifu ambao unaweza kuwa chanzo cha upendo, urafiki, na msingi mzuri wa familia. Wakati huohuo, Biblia inataja kwamba wale wanaofunga ndoa katika ulimwengu huu usio mkamilifu watakabili pia matatizo, au “dhiki katika mwili wao.” Kuhusu useja, Yehova hauoni kuwa chanzo cha aibu na huzuni. Badala yake, Neno lake linasema kwamba useja una faida fulani zisizopatikana katika ndoa.​—1 Wakorintho 7:28, 32-35.

Hivyo, Biblia inatoa maoni yanayofaa kuhusu ndoa na useja. Yehova, ambaye ndiye Mwanzilishi wa ndoa na familia, anataka watumishi wake wote wawe na furaha na uradhi, iwe ni waseja au wamefunga ndoa.