Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtii Mungu Ili Ufaidike Kutokana Na Ahadi Zake Zenye Kiapo

Mtii Mungu Ili Ufaidike Kutokana Na Ahadi Zake Zenye Kiapo

“Kwa kuwa [Mungu] hangeweza kuapa kwa yeyote aliye mkubwa zaidi, aliapa kwa nafsi yake mwenyewe.”​—EBR. 6:13.

1. Neno la Yehova linatofautianaje na neno la wanadamu wenye dhambi?

YEHOVA ni “Mungu wa ukweli.” (Zab. 31:5) Wanadamu wenye dhambi hawategemeki sikuzote, lakini “Mungu hawezi kamwe kusema uwongo.” (Ebr. 6:18; soma Hesabu 23:19.) Mambo anayokusudia kwa faida ya wanadamu hutimia sikuzote. Kwa mfano, kila jambo ambalo Mungu alisema angefanya mwanzoni mwa kila kipindi cha uumbaji, ‘lilikuwa hivyo.’ Kwa hiyo, kufikia mwishoni mwa siku ya sita ya uumbaji, “Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.”​—Mwa. 1:6, 7, 30, 31.

2. Siku ya Mungu ya pumziko ni nini, na kwa nini ‘aliifanya kuwa takatifu’?

2 Baada ya kutazama kazi zake za uumbaji, Yehova Mungu alitangaza kuanza kwa siku ya saba, ambayo si siku ya saa 24, bali ni kipindi kirefu cha wakati. Katika kipindi hicho, amepumzika kwa kutofanya kazi zaidi za uumbaji duniani. (Mwa. 2:2) Siku ya Mungu ya kupumzika bado haijakwisha. (Ebr. 4:9, 10) Biblia haitaji wakati hususa ilipoanza. Siku hiyo ilianza miaka 6,000 hivi iliyopita, wakati fulani baada ya Hawa, mke wa Adamu kuumbwa. Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu Kristo utaanza hivi karibuni, na utahakikisha kwamba unatimiza kusudi la Mungu la kuiumba dunia ili iwe paradiso milele itakayojaa wanadamu wakamilifu. (Mwa. 1:27, 28; Ufu. 20:6) Je, unaweza kuwa na hakika kwamba utaishi wakati huo ujao wenye furaha? Bila shaka! Kwa sababu ‘Mungu aliibariki siku ya saba na kuifanya takatifu.’ Huo ulikuwa uhakikisho wa kwamba hata matatizo gani yatokee bila kutarajiwa, kusudi la Mungu lingetimia kwa hakika kufikia mwishoni mwa siku yake ya kupumzika.​—Mwa. 2:3.

3. (a) Baada ya siku ya Mungu ya kupumzika kuanza, ni uasi gani uliotokea? (b) Yehova alielezaje nia yake ya kuukomesha uasi?

3 Hata hivyo, baada ya siku ya Mungu ya kupumzika kuanza, msiba ulitokea. Shetani, mwana wa kimalaika wa Mungu, alijifanya kuwa mungu mpinzani. Alisema uwongo wa kwanza na kumdanganya Hawa na hivyo kumfanya asimtii Yehova. (1 Tim. 2:14) Naye Hawa alimshawishi mume wake ili ajiunge naye katika kuasi. (Mwa. 3:1-6) Hata wakati huo wenye kuhuzunisha zaidi katika historia ya ulimwengu mzima, wakati sifa ya Yehova ya kusema ukweli ilipotiliwa shaka, Yehova hakuona uhitaji wa kuthibitisha kwa kiapo kwamba kusudi lake bado litatimia. Badala yake, Mungu akitumia maneno ambayo yangeeleweka kwa wakati wake, alisema tu jinsi ambavyo uasi huo ungekomeshwa: “Nitaweka uadui kati yako [Shetani] na yule mwanamke na kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye [Uzao ulioahidiwa] atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.”​—Mwa. 3:15; Ufu. 12:9.

KIAPO RASMI​—NJIA MUHIMU YA KISHERIA

4, 5. Abrahamu alitumia njia gani ya kisheria pindi fulani?

4 Katika kipindi hicho cha kwanza cha historia ya wanadamu, inaelekea kwamba Mungu hakuhitaji kuwafundisha Adamu na Hawa kuapa ili kuthibitisha ukweli wa jambo fulani. Viumbe wakamilifu wanaompenda Mungu na kumwiga hawahitaji kuapa; sikuzote wanasema ukweli na wanaaminiana kabisa. Lakini mambo yalibadilika wanadamu walipotenda dhambi na kupoteza ukamilifu. Hatimaye, uwongo na udanganyifu ulipoenea miongoni mwa wanadamu, walilazimika kuapa ili kuthibitisha kwamba mambo fulani muhimu ni ya kweli.

5 Kufanya viapo ilikuwa njia ya kisheria ambayo mzee wa ukoo Abrahamu aliitumia vizuri katika angalau pindi tatu. (Mwa. 21:22-24; 24:2-4, 9) Kwa mfano, alifanya hivyo baada ya kumshinda mfalme wa Elamu pamoja na wafalme waliomuunga mkono. Mfalme wa Salemu na wa Sodoma walikuja kumlaki Abrahamu. Melkizedeki, mfalme wa Salemu, alikuwa pia “kuhani wa Mungu Aliye Juu Zaidi.” Kwa hiyo, alimbariki Abrahamu na kumsifu Mungu kwa sababu ya kumwezesha Abrahamu kuwashinda adui zake. (Mwa. 14:17-20) Kisha, mfalme wa Sodoma alipotaka kumpa Abrahamu zawadi kwa sababu ya kuwaokoa watu wa mfalme huyo kutokana na majeshi yaliyowavamia, Abrahamu aliapa hivi: “Nainua mkono wangu katika kiapo kwa Yehova Mungu Aliye Juu Zaidi, Mtokezaji wa mbingu na dunia, kwamba, wala uzi wala kamba ya kiatu, sitachukua kitu kutoka kwa chochote kilicho chako, usije ukasema, ‘Ni mimi niliyemtajirisha Abramu.’”​—Mwa. 14:21-23.

AHADI YA YEHOVA YENYE KIAPO KWA ABRAHAMU

6. (a) Abrahamu alituwekea mfano gani? (b) Tutafaidikaje kwa sababu ya utii wa Abrahamu?

6 Kwa faida ya wanadamu wenye dhambi, Yehova Mungu ameapa pia kwa kutumia maneno, “‘Kama ninavyoishi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” (Eze. 17:16) Biblia inataja pindi zaidi ya 40 ambazo Yehova Mungu alifanya viapo rasmi. Huenda mfano unaojulikana zaidi ni kiapo ambacho Mungu alifanya aliposhughulika na Abrahamu. Kwa miaka mingi, Yehova alimpa Abrahamu ahadi kadhaa za maagano ambazo kwa ujumla zinaonyesha kwamba Uzao ulioahidiwa ungetokana na Abrahamu kupitia kwa mwana wake Isaka. (Mwa. 12:1-3, 7; 13:14-17; 15:5, 18; 21:12) Kisha Yehova akampa Abrahamu jaribu gumu kwa kumwamuru amtoe mwana wake mpendwa. Bila kukawia, Abrahamu alitii na alipokuwa karibu kumtoa Isaka kama dhabihu alizuiwa na malaika wa Mungu. Kisha Mungu akaapa hivi: “Naapa kwa nafsi yangu mwenyewe . . . kwamba kwa sababu ya uhakika wa kwamba wewe umefanya jambo hili nawe hukuzuia mwana wako, mwana wako wa pekee, hakika nitakubariki nami nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni na kama chembe za mchanga zilizo kando ya bahari; na uzao wako utamiliki lango la adui zake. Na kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki kwa sababu wewe umeisikiliza sauti yangu.”​—Mwa. 22:1-3, 9-12, 15-18.

7, 8. (a) Mungu alimwapia Abrahamu kwa kusudi gani? (b) “Kondoo wengine” wa Yesu watafaidikaje kutokana na ahadi ya Mungu yenye kiapo?

7 Kwa nini Mungu alimwapia Abrahamu kwamba ahadi Zake zingetimia? Alifanya hivyo ili kuwapa uhakikisho wale ambao wangekuwa warithi pamoja na Kristo na kuimarisha imani yao, yaani, wale wanaofanyiza sehemu ya pili ya ule “uzao” ulioahidiwa. (Soma Waebrania 6:13-18; Gal. 3:29) Kama mtume Paulo alivyoeleza, Yehova “aliingilia kati kwa kiapo, ili, kupitia mambo mawili yasiyobadilika [ahadi yake na kiapo chake] ambayo katika hayo Mungu hawezi kamwe kusema uwongo, sisi . . . tupate kuwa na kitia-moyo chenye nguvu kushikilia tumaini lililowekwa mbele yetu.”

8 Si Wakristo watiwa-mafuta tu wanaofaidika kutokana na ahadi yenye kiapo ambayo Mungu alimpa Abrahamu. Yehova aliapa kwamba kupitia “uzao” wa Abrahamu, watu wa ‘mataifa yote ya dunia wangejibariki.’ (Mwa. 22:18) Watu hao ambao wangejibariki wanatia ndani “kondoo wengine” wa Kristo walio watiifu, wanaotumaini kupata uzima wa milele katika paradiso duniani. (Yoh. 10:16) Iwe una tumaini la kuishi mbinguni au duniani, ‘shikilia’ tumaini hilo kwa kuendelea kumtii Mungu maishani.​—Soma Waebrania 6:11, 12.

VIAPO VINGINE VYA MUNGU

9. Ni kiapo gani rasmi alichofanya Mungu wakati wazao wa Abrahamu walipokuwa utumwani huko Misri?

9 Karne nyingi baadaye, Yehova aliapa tena kuhusiana na ahadi zilizotajwa katika mafungu yaliyotangulia alipomtuma Musa azungumze na wazao wa Abrahamu, waliokuwa utumwani huko Misri. (Kut. 6:6-8) Akirejelea pindi hiyo, Mungu alisema hivi: “Katika siku ile nilipochagua Israeli, . . . niliuinua mkono katika kiapo kwao ili kuwatoa katika nchi ya Misri mpaka katika nchi niliyokuwa nimeipeleleza kwa ajili yao, yenye kutiririka maziwa na asali.”​—Eze. 20:5, 6.

10. Mungu aliwapa Waisraeli ahadi gani baada ya kuwakomboa kutoka Misri?

10 Kisha, baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka Misri, Yehova alitoa ahadi nyingine yenye kiapo: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu, ndipo hakika mtakapokuwa mali yangu ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu, kwa sababu dunia nzima ni yangu. Na ninyi wenyewe mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.” (Kut. 19:5, 6) Mungu aliwapa Waisraeli pendeleo kubwa kama nini! Ilimaanisha kwamba ikiwa wangetii, watu mmoja-mmoja kutoka katika taifa hilo wangepata tumaini la kutumiwa na Mungu wakiwa ufalme wa makuhani ili kuwabariki wanadamu wengine. Baadaye, Yehova alieleza hivi kuhusu jambo alilokuwa amewafanyia Waisraeli pindi hiyo: ‘Nilikutolea ahadi yenye kiapo na kuingia katika agano pamoja nawe.’​—Eze. 16:8.

11. Waisraeli waliitikiaje mwaliko wa Mungu wa kuwa na uhusiano wa agano pamoja naye wakiwa watu wake aliowachagua?

11 Wakati huo, Yehova hakuwashurutisha Waisraeli waahidi kwa kiapo kwamba wangetii; wala Mungu hakuwalazimisha Waisraeli wawe na uhusiano wa pekee pamoja naye. Badala yake, walisema hivi kwa hiari: “Yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.” (Kut. 19:8) Siku tatu baadaye, Yehova Mungu aliwaambia Waisraeli matakwa ambayo alitaka watimize wakiwa taifa lake alilolichagua. Kwanza, walisikia Amri Kumi zikisomwa, kisha Musa akawapa amri zaidi ambazo zimeandikwa katika kitabu cha Kutoka 20:22 hadi 23:33. Waisraeli waliitikiaje? “Watu wote wakajibu kwa sauti moja na kusema: ‘Maneno yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.’” (Kut. 24:3) Kisha Musa akaziandika katika “kitabu cha agano” na kuzisoma kwa sauti ili taifa lote lisikie tena sheria hizo. Baada ya hapo, kwa mara ya tatu, watu wakaapa hivi: “Yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya na kuyatii.”​—Kut. 24:4, 7, 8.

12. Kuhusiana na agano ambalo Yehova alifanya pamoja na watu aliowachagua, yeye alitendaje, na watu wake walitendaje?

12 Yehova alianza mara moja kutimiza sehemu yake katika agano la Sheria kwa kufanya mipango ili kuwe na hema la ibada na ukuhani uliowawezesha wanadamu wenye dhambi kumfikia. Lakini Waisraeli walisahau haraka wakfu wao kwa Mungu na “wakamtia uchungu Mtakatifu wa Israeli.” (Zab. 78:41) Kwa mfano, Musa alipokuwa akipokea maagizo zaidi juu ya Mlima Sinai, Waisraeli walikosa subira na kuanza kupoteza imani katika Mungu wakifikiri kwamba Musa alikuwa amewaacha. Kwa hiyo, walitengeneza sanamu ya ndama wa dhahabu na kuwaambia hivi wenzao: “Huyu ndiye Mungu wako, Ee Israeli, aliyekuongoza kutoka nchi ya Misri.” (Kut. 32:1, 4) Kisha wakafanya sherehe huku wakisema ni “sherehe kwa ajili ya Yehova” na kuiinamia na kuitolea dhabihu sanamu hiyo iliyotengenezwa na wanadamu. Yehova alipoona jambo hilo alimwambia Musa hivi: “Wamegeuka kando haraka kutoka katika njia niliyowaamuru waende.” (Kut. 32:5, 6, 8) Inahuzunisha kwamba kuanzia wakati huo na kuendelea walikuwa na zoea la kuweka nadhiri kwa Mungu na kuzivunja baadaye.​—Hes. 30:2.

VIAPO VINGINE VIWILI

13. Ni ahadi gani yenye kiapo ambayo Mungu alimpa Mfalme Daudi, na inahusianaje na Uzao ulioahidiwa?

13 Wakati wa utawala wa Mfalme Daudi, Yehova alitoa ahadi nyingine mbili zenye kiapo kwa faida ya wote wanaomtii. Kwanza, alimwapia Daudi kwamba kiti chake cha ufalme kingedumu milele. (Zab. 89:35, 36; 132:11, 12) Hilo lilimaanisha kwamba Mzao aliyeahidiwa angeitwa “Mwana wa Daudi.” (Mt. 1:1; 21:9) Kwa unyenyekevu, Daudi alimwita mzao wake wa wakati ujao “Bwana” kwa sababu Kristo angekuwa na cheo kikubwa zaidi.​—Mt. 22:42-44.

14. Yehova alitoa ahadi gani yenye kiapo kuhusu Uzao ulioahidiwa, nasi tunafaidikaje kutokana nayo?

14 Pili, Yehova alimwongoza Daudi kwa roho takatifu kutabiri kwamba Mfalme huyo wa pekee angekuwa pia Kuhani Mkuu wa wanadamu. Katika Israeli, ufalme ulitenganishwa kabisa na ukuhani. Makuhani walitoka katika kabila la Lawi, na wafalme walitoka katika kabila la Yuda. Lakini kuhusu mrithi wake mwenye utukufu, Daudi alitabiri hivi: “Neno la Yehova kwa Bwana wangu ni: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke adui zako kuwa kiti cha miguu yako.’ Yehova ameapa (naye hatajuta): ‘Wewe ni kuhani mpaka wakati usio na kipimo kwa mfano wa Melkizedeki!’” (Zab. 110:1, 4) Katika utimizo wa unabii huo, ule Uzao ulioahidiwa, yaani, Yesu Kristo, anatawala sasa akiwa mbinguni. Pia, anatumikia akiwa Kuhani Mkuu wa wanadamu kwa kuwasaidia wanaotubu wawe na uhusiano mzuri na Mungu.​—Soma Waebrania 7:21, 25, 26.

TAIFA JIPYA LA ISRAELI WA MUNGU

15, 16. (a) Ni mataifa gani mawili ya Israeli yanayorejelewa katika Biblia, na ni taifa gani lililobarikiwa na Mungu leo? (b) Yesu aliwapa wafuasi wake amri gani kuhusu viapo?

15 Kwa sababu ya kumkataa Yesu Kristo, hatimaye taifa la Israeli lilipoteza uhusiano wa pekee pamoja na Mungu na likapoteza tumaini la kuwa “ufalme wa makuhani.” Kama Yesu alivyowaambia viongozi Wayahudi: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” (Mt. 21:43) Taifa hilo jipya lilizaliwa wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. wakati roho ya Mungu ilipomiminwa juu ya wanafunzi 120 wa Yesu waliokusanyika Yerusalemu. Taifa hilo liliitwa “Israeli wa Mungu” na punde si punde likawa na maelfu ya watu kutoka katika kila taifa lililokuwapo katika ulimwengu wa wakati huo.​—Gal. 6:16.

16 Tofauti na Israeli wa kiasili, taifa jipya la kiroho la Mungu limeendelea kuzaa matunda mazuri kwa kuendelea kumtii Mungu. Mojawapo ya amri ambazo washiriki wa taifa hilo hutii inahusu kufanya viapo rasmi. Viapo vilitumiwa vibaya wakati Yesu alipokuwa duniani, watu walikuwa wakiapa kwa uwongo au wakiapa kuhusu mambo madogo-madogo. (Mt. 23:16-22) Yesu aliwafundisha hivi wafuasi wake: “Msiape hata kidogo . . . Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo; kwa maana linalozidi hayo linatoka kwa yule mwovu.”​—Mt. 5:34, 37.

Ahadi za Yehova hutimia sikuzote

17. Ni maswali gani yatakayozungumziwa katika makala inayofuata ya funzo?

17 Je, hilo linamaanisha kwamba ni vibaya sikuzote kuapa? Swali muhimu zaidi ni hili: Ni nini kinachohusika katika kuacha Ndiyo yetu imaanishe Ndiyo? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata ya funzo. Tunapoendelea kutafakari kuhusu Neno la Mungu, na lituchochee kuendelea kumtii Yehova. Tukifanya hivyo, Yehova atafurahi na kutubariki milele kulingana na ahadi zake zenye kiapo zilizo na thamani.